Serikali yatangaza kiama kwa wapenda migomo vyuoni

zubedayo_mchuzi

JF-Expert Member
Sep 2, 2011
4,873
1,216
Tuesday, 27 September 2011 19:47

SERIKALI imeonya kwamba haitavumilia na kutishia kufuta udhamini wa mikopo kwa wanafunzi wote wa vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu nchini watakaoshiriki kwenye migomo na maandamano kwa sababu zisizo na msingi.

Msimamo huo ulitolewa juzi na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Dk Shukuru Kawambwa alipozungumza na jamii ya Chuo Kikuu cha Tumaini Makumira wakati wa ziara ya kujifunza shughuli, utendaji na changamoto zinazozikabili vyuo vikuu nchini.

Alisema msimamo huo wa Serikali unatokana na dhamira ya kuboresha mfumo wa elimu ya juu nchini uliosababisha wizara yake kutengewa Sh 300 bilioni kwa ajili ya mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya
juu.

"Katika bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha wa 2011/12, zaidi ya Sh80 bilioni zilinyofolewa kutoka mfuko wa kuendeleza elimu ya ufundi na kupelekwa bodi ya mikopo ili kuhakikisha wanafunzi zaidi wenye kutimiza masharti na vigezo wanakopeshwa. Hatutakubali fedha nyingi kiasi hicho zipotee bure kwa wanafunzi kuendekeza migomo na maandamano yasiyo na tija badala a kusoma," alisema Dk Kawambwa.

Alisema fedha hizo zingeweza kujenga vyuo 50 vya ufundi vyenye miundombinu na vifaa vyote muhimu iwapo zisingehamishiwa bodi ya mikopo hivyo ni wajibu wa wote wanaokopeshwa kutimiza wajibu wao kwa kusoma kwa bidii ili taifa lipate wataalamu wa kada mbalimbali.

Dk Kawambwa alisema kutoka kumegwa kwa fedha hizo, zaidi ya nusu ya wanafunzi 500 watakaohitimu elimu ya sekondari na wenzao zaidi milioni moja waliohitimu elimu ya msingi mwaka huu, hawatafanikiwa kuendelea na masomo au kujiunga na elimu ya ufundi kwa sababu fedha ambazo zingeelekezwa huko zimekopeshwa kwa kaka na dada zao wa vyuo vikuu.

Katika bajeti ya mwaka huu, mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu imetengewa Sh317 bilioni ambazo Dk Kawambwa alidai ni kubwa mara 20 kulinganisha na bajeti ya baadhi ya wizara akaitaja ile ya Jinsia na Maendeleo ya Jamii iliyotengewa fedha isiyozidi Sh17 bilioni.

Kuhusu siasa vyuoni, waziri huyo aliwaagiza wakuu wa taasisi zote za elimu ya juu kuhakikisha hakuna shughuli wala harakati za kisiasa ndani ya maeneo na mazingira ya vyuo vyao ili kuepuka mitafaruku ndani ya jamii zao na kuleta utulivu kwa wahadhiri kufundisha na wanafunzi kujifunza.

MWANANCHI
 
Back
Top Bottom