Serikali yasalimu masharti Udom

Rutashubanyuma

JF-Expert Member
Sep 24, 2010
219,470
911,173
Serikali yasalimu masharti Udom
Wednesday, 22 December 2010 19:49

nahodha.jpg
Habel Chidawali na Masoud Masasi, Dodoma

HATIMAYE Serikali imesalimu amri kwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom), baada ya kuridhia madai yao na kukubali kulipa gharama za uharibifu wa mali zao zilizotokana na vurugu kati yao na polisi.

Hatua hiyo imefikiwa baada ya mawaziri wawili; Shukuru Kawambwa wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi na Waziri wa Mambo ya Ndani, Shamsi Vuai Nahodha kufika chuoni hapo juzi mchana kwa ndege ya kukodi kwa ajili ya kusuluhisha mgogoro huo uliodumu kwa siku mbili.

Mawaziri hao wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma , Dk James Msekela na maafisa wengine wa Serikali mkoani Dodoma, walifika Udom saa 9 alasiri na kwenda moja kwa moja katika ukumbi kwa ajili ya kikao hicho kilichomalizika saa 8:00 usiku wa kuamkia jana.

Wakati mawaziri hao wakifika chuoni hapo kwa msafara, viongozi wa serikali ya wanafunzi waliwasili kwa basi dogo wakitokea polisi walikokuwa wamewekwa rumande na baadaye kumlaki kiongozi wa Kitivo cha Sayansi ya Jamii aliyekuwa kinara wa mgomo huo, Leonard Singo.

Baadaye Singo alikutana kwa faragha na Rais wa serikali ya wanachuo wa chuo hicho, Saimon Baisi na kuteta jambo kabla hawajaingia kwenye ukumbi wa mkutano.

Baada ya kikao hicho kumalizika, Dk Kawambwa alienda kuzungumza na wanachuo na kuwaeleza kuwa Serikali imesikia kilio chao na sasa inaenda kuyafanyia kazi madai yao.

Dk Kawambwa alizungumza na wanachuo hao saa 12:00 asubuhi wakati anajiandaa kwenda Uwanja wa Ndege Dodoma kwa ajili ya safari ya kurejea jijini Dar es Salaam.

"Serikali imekubali matatizo yenu baada ya kuyaona kuwa ni ya msingi kwani hakuna watu wanaosoma bila kwenda field (mazoezi kwa vitendo)," alisema Dk Kawambwa na kuongeza:

"Tunaorodhesha majina yenu ili wanafunzi wa mwaka wa pili waende field mapema iwezekanavyo na wale wa mwaka wa tatu waende kabla ya kumaliza chuo."

Awali Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Idris Kikula alieleza kuwa Serikali inakwenda kutengeneza bajeti ya kuwalipa wanafunzi hao baada ya kuorodhesha majina yao na kuwasilishwa Tume ya Vyuo Vikuu na Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu.

Profesa Kikula aliwasihi wanafunzi hao kurejea madarasani ili waendelee na masomo kwa kuwa mgomo huo sasa umekwisha.

Alisema kilichotokea hata chuo hicho kikashindwa kuwapeleka kwenye mafunzo kwa vitendo baadhi ya wanafunzi hao ni ufinyu wa bajeti ya serikali.

Kabla kulitokea hali ya kutoelewana baada ya wanachuo hao kumkataa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk Msekela katika mazungumzo hayo kwa madai kuwa yeye ni moja ya chanzo cha vurugu zilizotokea juzi.

Baisi ambaye juzi alitangaza mgomo wa wanafunzi wote jana endapo Serikali isingekubali kuyatekeleza madai hayo alithibitisha kumalizika kwa mgomo huo.

Hata hivyo, kiongozi huyo wa serikali ya wanafunzi alitahadharisha kuwa wanafunzi hao wamekubali kusitisha mgomo ili kuipa muda Serikali kutekeleza madai hayo, lakini hawatasita kuuitisha tena kama kauli hiyo ya Serikali ni danganya toto.

“Tumeingia madarasani baada ya kuambiwa kuwa mambo yetu yanashughulikiwa. Kimsingi tulikubaliana na mawaziri hao waende kwa Waziri Mkuu na baada ya siku tatu watuletee majibu ya kutosha lini tutaanza mafunzo hayo kwa vitendo. Nasema wasipofanya hivyo bado tutaingia katika mgomo, tena mkubwa,” alisema Baisi.

Juzi wanachuo wapatao 500 wa Kitivo cha Sayansi walifanya maandamano ambayo yalisababisha polisi kutumia nguvu ya kuwatawanya kwa mabomu ya machozi hali iliyosababisha baadhi yao kuumizwa na kukimbizwa katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma kwa matibabu.

Lakini jana Waziri Kawambwa alisema pamoja na kutekeleza madai hayo, Serikali pia italipa gharama za mali za wanafunzi hao zilizopotea au kuharibika katika vurugu hizo.

Wanafunzi wengi wamekuwa wakieleza kuwa wamepoteza simu na kompyuta ndogo (laptop).


 
wanajidanganya hao wanafunzi...nani awalipe simu na laptop.Jaribuni kuwa serious kidogo...
 
Hongera wanaelimu wa UDOM na poleni na kisago cha polisi. Ninawapa hongera na kutuonesha njia kuwa katika nchi hii bila migomo wala maandamano hakuna anayesikilizwa, ijapokuwa kuwa kwa kufanya hivyo yanaweza kutokea kama yaliyowafika nyinyi kwa kupigwa mkiwa mnatetea sio maslahi yenu tu bali maslahi ya taifa. Lakini hii ni gharama tunayopaswa kulipa wakati tunatetea haki zetu, bila ya uoga wala kusaliti imani zetu.
Ufinyu wa bajeti ya serikali? Kila ninaposikia kauli hii hunifanya nicheke kwa uchungu.
 
Back
Top Bottom