Serikali yakopa watumishi wake

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
266
SERIKALI imethibitisha kukabiliwa na ukata baada ya sasa kuanza kuwakopa baadhi ya watumishi wake kupitia mishahara ya kila mwezi, MwanaHALISI imegundua.Taarifa za uhakika kutoka vyanzo mbalimbali vya habari, zimesema serikali inakopa wafanyakazi kwa kuwakata mishahara yao kwa njia ya kulipia mikopo ambayo haijawahi kuwapatia.

Imeelezwa kuwa ulikuwepo mpango wa serikali kukopesha magari kwa watumishi wake na kwa wale waliojitokeza kutaka kukopa, wakatakiwa kujaza fomu maalum.
Waliofaulu walijulishwa na kuahidiwa kusubiri waingiziwe fedha lakini kabla ya kuingiziwa fedha hizo ili wanunue magari, watumishi hao walishtukia wakipokea mishahara iliyokatwa makato kwa lengo kulipia mikopo.

Mtumishi mmoja aliyezungumza na MwanaHALISI kwa sharti la kutotajwa gazetini, alisema ni kweli yeye alikopa na kukubaliwa baada ya kutimiza masharti yaliyotakiwa.


Hata hivyo, anasema "Nimekumbwa na mkasa mkubwa maana nimetangulia kukatwa mshahara wangu wakati hata mkopo wenyewe sijatiliwa kwenye akaunti yangu."
"Unajua kuna kipindi Bunge lilipitisha sheria kwamba watumishi wa umma wapatiwe mikopo kwa ajili ya kununulia vyombo vya usafiri pamoja na samani za ndani. Baada ya mjadala mrefu ilipitishwa," alisema.Lakini kilichotokea katika hatua ya serikali kuanza kukopesha, wale watumishi walioomba fedha tuseme Sh. 20 milioni wameambiwa serikali haina fedha, badala yake watapewa milioni 10 tu.

Alisema wapo wengine waliomba Sh. 10 milioni lakini walipojulishwa kukubaliwa kukopeshwa walielezwa watapata nusu ya fedha hizo walizoomba. "Sababu ni hiyohiyo, ‘serikali haina fedha," alisema mtumishi huyo.
Watumishi waliojulishwa kuwa watakopeshwa nusu ya mkopo walioomba, waliridhia huku mmoja akisema, "si unajua sisi watumishi wa umma tunaishi kwa mtindo wa kuungaunga. Maisha ni magumu sasa unavyoambiwa inabidi ukubali ili siku ziende na huna cha kupoteza.

"
"Sasa mwezi uliopita (Oktoba) wizara na taasisi mbalimbali za serikali wakaletewa fomu za mikopo ya serikali kuzijaza kwa kuambatanisha na yote yaliyotakiwa. Tungali tunasubiri kutiliwa fedha zetu, ndio yanatokea haya kwa baadhi yetu," alisema.Mtumishi huyo alisema ameshangazwa kubaini mwezi uliofuata wa (Novemba) walianza kukatwa makato ya mikopo hiyo bila ya hata kupewa fedha yenyewe.

Mkuu wa Idara ya Mawasiliano ya Wizara ya Fedha na Uchumi, Ingiahedi Mduma, amekiri kuwapo mpango wa serikali kukopesha watumishi wake fedha kwa ajili ya kununulia vyombo vya usafiri.
Hata hivyo, alitetea uamuzi wa watumishi kuanza kukatwa mikopo hiyo kwa kuamini kuwa utaratibu wa kupatiwa fedha kwa waliokopa upo tayari."Kama kuna mtumishi ameanza kukatwa ninavyojua mimi tayari hatua za kupata fedha hizo zitakuwa tayari.

Kinachosubiriwa ni fungu tu kutoka kwa Kamishna wa Bajeti. Hivyo ndivyo ninavyolifahamu suala hilo," alisema Mduma.
Gazeti hili limeona hati za malipo ya mshahara ya Novemba za baadhi ya watumishi waliokatwa kulipia mikopo wakati hawajawahi kuingiziwa fedha zao za mikopo."Watu wakaenda mbali zaidi wakauliza Hazina mbona wanakata fedha bila kuwa tumepata mikopo kwanza; wakaambiwa wasubiri mpaka hali itakapokuwa nzuri wataingiziwa fedha zao," alisema mtumishi mwingine.

"Kama serikali haina fedha kulikuwa na uharaka gani wa kutekeleza mpango wa kukopesha watumishi wake. Na je, ni sahihi mtumishi kukatwa mshahara wakati hajapatiwa mkopo alioomba," alihoji mtumishi huyo.
Baadhi ya watumishi waandamizi wameliambia gazeti hili kuwa kitendo hicho ni kielelezo kingine cha serikali kukosa vipaumbele halisi.

Kwa muda wa miezi kadhaa sasa, kumekuwa na taarifa za serikali kukabiliwa na tatizo la fedha kwa ajili ya kugharamia mahitaji yake na hivyo kulazimika kukopa kwenye benki za biashara, mtindo unaopingwa na wachumi kwa kuwa unaongeza mzigo kwa wananchi na kupunguza nguvu ya mabenki kukopesha wazalishaji katika sekta binafsi.


Lakini taarifa hizo zinakuja katika kipindi ambacho serikali imeingia katika kashfa nzito ya kuongezea posho ya wabunge kwa siku wanapokuwa vikaoni kutoka Sh. 70,000 hadi Sh. 2000,000 kwa siku.
Ongezeko hilo limelipwa huku Katibu wa Bunge, Thomas Kashililah akisema ofisi ya bunge haijapokea ruhusa rasmi ya rais kuongeza viwango vipya vya posho kwa wabunge vilivyopendekezwa.

Lakini, Spika Anne Makinda aliarifu siku moja baadaye kuwa wabunge wameanza kulipwa ongezeko hilo katika mkutano uliomalizika katikati ya mwezi uliopita.
Spika alisema posho ya kikao imepanda kutoka Sh 70,000 hadi Sh 200,000 wakati mafuta kwa ajili ya usafiri ni Sh 50,000 kwa siku na fedha ya kujikimu inabaki kuwa Sh 170,000.Alisema ongezeko hilo linafuatia mapendekezo yaliyowasilishwa serikalini kutokana na wabunge kulalamika kukabiliwa na matatizo mengi wawapo kwenye vikao mjini Dodoma na hulazimika kusaidia fedha watu wanaokutana nao bungeni.

Zimefichuka taarifa kuwa ongezeko hilo halikupaswa kulipwa mpaka lipate idhini ya rais ambaye anatarajiwa kusaini sheria ya ongezeko hilo.
Taarifa kutoka serikalini zimethibitisha kuwa Rais Jakaya Kikwete hajasaini sheria hiyo hivyo haikutarajiwa kuwa ongezeko lingelipwa kabla ya hapo.Tatizo la ukata serikalini limekuwepo kwa muda sasa huku vyanzo katika umoja wa wafadhili vikisema serikali inalaumiwa kwa kutumia zaidi ya inavyokusanya.

Zipo taarifa kuwa serikali mwezi uliopita ilikopa fedha kwa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa ajili ya kulipa mishahara ya watumishi wake.
Imeelezwa kuwa baadhi ya wizara na taasisi zake zimekuwa zikicheleweshewa mishahara kiasi cha kupokea ndani ya wiki ya kwanza ya mwezi unaofuata.Kuna fununu kuwa kisingizio kinachotolewa ni cha hitilafu ya mfumo wa mawasiliano ya kimtandao.

Hata hivyo, baadhi ya vyanzo vya taarifa vilisema Serikali ilikubaliana na Benki ya Makabwela (National Micro-Finance, NMB) kuwaingizia watumishi malipo hewa ili waone wamelipwa lakini kila wanakwama wanapotaka kutoa fedha.
Halmashauri nyingi zimekosa fedha walizotaka kutoka serikalini huku serikali ikishindwa kulipa kwa wakati ruzuku kwa vyama vya siasa tangu Oktoba mwaka huu.

Watoa huduma kwa serikali na taasisi zake nao wamekuwa wakilalamikia kitendo cha kucheleweshewa malipo yao baada ya kutoa huduma kwa miezi kadhaa sasa, hivyo kuathiri shughuli zao.
Kila viongozi wanapoulizwa hutamba kuwa matumizi yanawiana na makusanyo hasa kwa kuwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imekuwa ikikusanya zaidi ya lengo lililowekwa.

Mwenendo wa matumizi serikalini unakera nchi wafadhili kiasi cha kumshambulia Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo hivi karibuni wakati wa mkutano wa mashauriano kuhusu utekelezaji ahadi zao kusaidia mfuko wa bajeti ya serikali (GBS) kwa mwaka 2011/12.


Wiki kadhaa zilizopita, mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohamed aliwahi kusema kuwa waziri Mkulo alishindwa kueleza ni wapi serikali imepata mabilioni ya shilingi zilizotumika kwa ajili ya shughuli za maadhimisho ya miaka 50 ya uhuru wa Tanganyika.

source

Serikali yakopa watumishi wake | Gazeti la MwanaHalisi

 
Maisha wa watanzania hasa ya watumishi wa umma yanazidi kuwa magumu kwa sababu mbalimbali ikiwemo kutokuwa na uhakika wa lini watapokea mshahara na kama wataupokea utakuwa umekatwa kwa kiasi gani. Loh poor civil servants!
 
hali ni ya hatari sana na majanga ya kitaifa ndio yanazidi kutukumba chaguzi zinamaliza pesa maafa ya mafuriko na mabomu ya mbagala na gongo la mboto na bado ufisadi na wizi wa mali za umma unatumaliza matatizo ya ajira kwa vijana ndio usiseme
 
Wengine si tu kwamba kazi ni kukosoa tu bali ni kwamba tuliwatahadharisha siku nyingi juu ya ufujaji wa kodi zetu kwa mambo ya anasa sasa ndio kama hivo mshahara mpaka tarehe 68 ikiwahi sana. Ila aliyetoa wazo hilo la kulipa mshahara dirishani KIBOKO!!!!!!!!!!!!

Wale wezi wooote waliozoea kuvuta kodi zetu kama mishahara ya watu 6 hadi 10 msukule safari hii wakale tu mawe.Rais Kikwete kwa hilo umenikuna kidooogo japo kwa kuchelewa na tena baada ya maudhi lukuki!


kuku anakula vifaranga wake
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom