Serikali imefikia kilele cha uzembe; hata TBC haina bodi ya wakurugenzi!!

Dark City

JF-Expert Member
Oct 18, 2008
16,253
11,598
Bunge latupa taarifa za mashirika ya umma

na Deogratius Temba

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali Mashirika ya Umma, imekataa kupokea taarifa za mashirika matano ya umma kutokana na kutokuwa na bodi za kuyasimamia.

Imewataka mawaziri wanaohusika na taasisi hizo kujieleza mbele ya kamati sababu za kuchelewa kuteua bodi hadi sasa.

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana baada ya kukataa kupokea taarifa ya Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Estarina Kilasi, alisema hawawezi kupokea taarifa na mashirika ambayo hayana bodi ambazo kisheria ndizo zinazowajibika katika utendaji na usimamizi.

Tumewarudisha hawa wa Mwalimu Nyerere, juzi tuliwarudisha wengine, tutawaandikia mawaziri husika barua waje hapa watueleze ni kwanini hawajateua bodi siku zote hizo, alisema.

Aliyataja mashirika mengine ambayo hayana bodi kuwa ni Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), Taasisi ya Ustawi wa Jamii, Veta na Shirika la Tija la Taifa.

Mashirika mengine matatu ambayo taarifa zake zimekataliwa na wahusika wataitwa bungeni ili kutafutiwa muda wa kuzijadili ni Kampuni ya kusimamia mali za lililokuwa Shirika la Reli Tanzania TRC (RAHCO), Shirika la Utangazaji (TBC) na Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB).
 
"Tahariri: Mawaziri Hawa Wawajibike

Moja ya habari zilizotawala kwenye vyombo vya habari jana ni kuhusu Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali Mashirika ya Umma kukataa kupokea taarifa za mashirika sita ya umma.

Kamati hiyo, inayoongozwa na Mbunge wa Jimbo la Mbarali, Estarina Kilasi (CCM), iliamua kuzitupa taarifa hizo kutokana na mashirika hayo kutokuwa na bodi za wakurugenzi wa kuyasimamia wala wenyeviti wao.

Mashirika hayo ambayo hayana bodi za kuziongoza ni pamoja na Tume ya Vyuo Vikuu (TCU), Ustawi wa Jamii, Veta, Tumbaku, Shirika la Tija Taifa, na Mfuko wa Hifadhi ya Taifa ya Jamii (NSSF).

Mbali na mashirika yasiyo na bodi, mengine matatu ambayo taarifa zake zimekataliwa na wahusika wataitwa bungeni ili kutafutiwa muda wa kuzijadili baada ya kubainika kuwa zina utata ni Kampuni ya kusimamia mali za lililokuwa Shirika la Reli – TRC (RAHCO), Shirika la Utangazaji (TBC), na Bodi ya Mkopo ya Elimu ya Juu (HESLB).

Kimsingi, wanaopaswa kuteua bodi za wakurugenzi za mashirika hayo ya umma ni mawaziri husika, lakini hawakufanya hivyo tangu walipochaguliwa kwa sababu wanazozijua.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kamati imewataka mawaziri wanaohusika na taasisi hizo kujieleza mbele ya kamati, kueleza sababu za msingi za kuchelewa kuteua bodi hizo hadi sasa.

Tanzania Daima tumepokea taarifa hiyo ambayo tunaamini inadhoofisha utendaji wa mashirika hayo kwa masikitiko makubwa, hasa tukizingatia umuhimu wa kuwapo kwa bodi za wakurugenzi na wenyeviti wao.

Lakini si tu kwamba bodi hizo ni muhimu kwa ufanisi wa mashirika hayo, bali pia kutoteuliwa kwake kumesababisha ukosefu wa ajira kwa baadhi ya Watanzania wenye sifa ambao wangepaswa kuwamo.

Ikumbukwe kwamba bodi za wakurugenzi za mashirika ya umma ndizo zinazowajibika katika utendaji na usimamizi wa mashirika hayo, hivyo kukosekana kwake kunatoa hata mwanya wa kuwapo ufisadi kwani maamuzi mazito ambayo wakati mwingine yanahitaji fedha, yanaweza kufanywa na mtu mmoja na hakuna wa kumpiga hata kama maamuzi hayo yanamnufaisha mtu binafsi.

Tunajiuliza, kwa muda wote huu mashirika hayo yalijiendeshaje? Na je, mawaziri walioshindwa kuteua bodi za mashirika hayo hawakuwa na ajenda binafsi ya kujinufaisha?

Tunachukua nafasi hii kuwataka mawaziri hao wawajibike na hata ikibidi wawajibishwe kama hawatakuwa na sababu za msingi kwani tunaamini athari zozote zitakazotokea kwenye mashirika hayo kwa kukosa bodi za wakurugenzi kwa muda wote huo zinapaswa kubebwa na mawaziri husika.

Tunaungana na mwenyekiti wa kamati hiyo kutaka kuwaita mawaziri husika ili wajieleze na tunaongeza kuwa mawaziri hao wasiishie kuitwa na kujieleza tu, bali pia wachukuliwe hatua kwa kuzembea na kushindwa kuchukua hatua.

Tunasisitiza mawaziri hao wachukuliwe hatua kwani kuna uwezekano wa kuwapo mashirika na taasisi zingine za umma zinazopaswa kuendeshwa na bodi za wakurugenzi, lakini hazina kwa sababu tu mawaziri wenye dhamana ya uteuzi hawajafanya hivyo.

Mawaziri hao wakiwajibishwa, bila shaka watakuwa somo kwa mawaziri wengine waliopo na watakaoteuliwa siku zijazo kufanya uteuzi wa bodi za wakurugenzi mara baada ya wao kuteuliwa na rais."

Source: Tanzania Daima
 
Back
Top Bottom