Sauti ya Kisonge ni ya KIMA AKIMALIZA MITI! "Wana CCM Mseto ni hatari

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Written by Stonetown (Kiongozi) // 13/10/2012 // Makala/Tahariri // 8 Comments

KISONGE-564x272.jpeg



Moja katika jambo linalorudisha nyuma maendeleo ya nchi au tuseme visiwa vyetu vya Zanzibar ni kuwepo tabia ya ‘USAADATI' wa kijadi kwa baadhi ya wananchi. Usaadati katika muktadha huu ni ile hali ya kuwa mtu ni mzima wa afya, ana uwezo, na nafasi ya kufanya kazi ya kujipatia rizki, na chumo lake halali la kula nyumbani na watoto lakini akawa hataki kufanya kazi wala bazi kwa maksudi.


Masaadati wako wa aina nyingi. Kuna Masaadati ambao kwa kawaida wakiamka tu hukimbilia maskani zao za kucheza bao, karata, na lagh'wi nyengine zilizomo mjini na hukaa hapo mpaka jua likachwa na hurudi nyumbani kama alivyotoka asubuhi.Pia kuna masaadati ambao hawakai maskani mda wote ila hutegemea kazi zisizo za uhakika wala sisizotambulika rasmi kama vile kujitia udalali, kujipendekeza kwa wenye kitu na vyeo mwisho wa siku akagaiwa kilichopo nae huridhika mtu huyo na hali hiyo.


Masaadati hata ukiwapanga kufanya kazi yenye stara na inayotambulika rasmi japo sio ya kiofisi wala serikali basi hawakubali kuifanya au wataishika tu na huku muda mwingi wakitegemea kuishi kwa kupiga magoli na michongo ya huku na huko, mradi tu wasifanye kazi itakayowatoa jasho au itakayowagharaimu akili, nguvu, na muda wao. Jamii ya watu hawa huitwa masaadati.


Utamaduni wa kisaadati hapa Zanzibar umekuwepo kwa siku nyingi. Naweza kusema kuwa tangu enzi za ukoloni na ndio utamaduni huu hasa uliotupelekea wengine kukubali kuvutishwa marikshoo, huku tukiacha kufanya maarifa mengine ya kujitegemea bila kudhalilisha utu wetu. Utamaduni huu ni kiwazo kikubwa kwa maendeleo ya taifa na kwa muda mrefu uliondoka hasa hasa wakati wa Serikali za awali za Mapinduzi. Mzee wetu Abeid Karume, aliwahi kuukemea sana utamaduni huu na kwa kiasi kikubwa aliumudu, na taifa lilisonga mbele ukilinganisha na sasa.


Kwa bahati mbaya, kila masika huja na mbu wake. Mara tu alipoingia madarakani Rais Salimin Amour (Komandoo) aliona njia pekee ya kujipatia umaarufu na ushindi wa kishindo ni wa kulitumia kundi hili kubwa la wanyambi (masaadati) ambao pamoja na kuwa wengi wetu hatuwaoni, lakini wapo wengi mno katika visiwa hivi, na hilo Salmin aliliona na akaamuwa kulitumia ipasavyo kundi hilo.


Alichokifanya Salmin Amour ni kufungua ‘Maskani' nchi nzima ambapo kwa kufanya hivyo aliweza kuwakutanisha masaadati wa nchi nzima pahala pamoja na kuweza kuwatumia atakavyo. Kisha akaifanya Kisonge, maskani kaka, ndio makao makuu ya MASAADATI hapa visiwani. Na hii ndio ngome kuu aliyokuwa akiitumia Salmin Amour kuleta fujo, fitina, machafuko, kejeli na kila aina ya uchafu. Masaadati ni watu wenye kuhusudu sana Utumwa, na mtu anaehusudu kutumiliwa na kutumwa na mtu mwengine kwa hiari yake ni sawa na mbwa wa kufuga. Anafanya lolote lile analoamini litamridhisha bwana wake.


Nae Salmin Amour, aliehitimu vyema somo la soshiolojia ya jamii ya watu masaadati hapa Zanzibar, alihakikisha anawapa kila walichohitaji watu wa maskani ilhali kazi zake ziende vizuri. Maskani zilijazwa mapesa ya bure kila mwezi. Watu wakigawa wakatumia. Kukicha asubuhi, watu wako maskani na ukiangalia nyumbani moshi haukatiki jikoni. Kijungu jiko, wala watu hawaendi kazini. Maskani kuanzia asubuhi hadi jioni. Hivi ndio Salmini alivyowalea masaadati katika masakni za Chama kama hivi ilivyo Kisonge.


Wakati ukuta! Baada ya Salmin kuondoka aliekuja alikuja na yake. Akazitupilia mbali maskani na kuzidharau. Sasa hebu jiulize kama paka au mbwa aliezoea kulishwa bure ukimkatishia huduma bila kutegemea atafanya nini? Wengi wenu mtanijibu kuwa atakuja mwilini au atakamata chochote kitachompitia mbele yake. Atamng'ata yoyote hata awe Sheikh, Mzee, au mtu mwenye utukufu usiomithilika. Haachi kitu. Ataharibu tu na ataudhi bila kujali wala kubuni mbinu ya kujipatia rizki hata akiwa anajuwa kuwa njia niliyoizoea kujipatia rizki imefungwa na sasa nifanye utaratibu mwengine wa kutafuta rizki upande mwengine. Sifa hii ni muhali kwa masaadati.


Mfano nzuri tazama sasa kwa takribani miaka kumi na mbili Serikali zetu zimezifumbia macho maskani zote nchini ikiwemo hiyo Kisonge. Sasa waliotegemea bure pale ndio haipo. Ndio hayo unayoayaona ya kutukana wanaotukaniaka na wasiotukanika. Ni matusi kwenda mbele. Yalianza kumfika Amani Karume alipoambiwa ‘kama wataka mseto kapike nyumbani na mkeo'.


Sifa moja kubwa ya Amani Karume ni ukimya anapoudhiwa, lakini pia ni mtu aliyekuwa na akili pana na uoni wa mbali. Basi Bwana Karume akaupika kweli ule mseto ikulu, lakini akahakikisha umeliwa nchi nzima wakiwemo hao Kisonge, wapungufu wa fadhila. Wakaona haya. Jana na juzi kashikwa Mzee Hassan Nassor Moyo, mtu mzima na heshima zake ametukanwa mpaka alipotokea. Amefujwa na kudhalilishwa kiasi ya kukosa uungwana na kuona aibu sisi tunaosoma maandiko yale yaliyoitwa ‘SAUTI YA KISONGE'.


Lakini pamoja na yote hayo sishangai. Wenzetu wa Kisonge wakitegemea kula kwa kusubiri watu wauliwe, watukanane, amani isiwepo, ugomvi kila siku ilimradi wao mkono uende kinywani. Sasa mambo yamegeuka, hawana pa kushika. Miaka kumi na mbili ya njaa kali si mchezo hata kidogo. Na bado hata Sheni hajaonesha dalili ya kuzitupia jicho Maskani. Na sijui kama atazitupia kamwe. Katika hali kama hii ya njaa kali na kuishiwa, kisonge watamtukana kila mtu, sio Mzee MOYO tu, hata wazazi wao waliowazaa, kwani upeo wa maarifa yao haujui pengine ila hapo Maskani tu hata kama nyufa za Rizki za hapo zimeshafungwa lakini hawana maarifa ya kujuwa hayo.


Kwa hili nawasihi wananchi wote wenye uungwana heshima na utu hapa Zanzibar waliokerwa na matusi yale dhidi yam zee wetu MOYO, kwamba musiwe na pupa, KISONGE walianza kumtukana Rais Amani Karume na ahli yake mama Shadya, wamekuja kwa Mzee MOYO na aila yake yote hadi kumfikishia matusi ya laana. Basi muda si mrefu angalia sauti ya Kisonge tolea lijalo, utakuta wamemtukana mzazi wa Mbaraka Shamte, kisha watamtukana matusi ya nguoni Mzazi wa BoraAfya na kisha wajumbe na wafuasi wote wa Kisonge watatukanana wenyewe kwa wenyewe, wajifunge vibwebwe vya kanga hadaharani iwe kidole machoni, iwe mbwa mbwa wewe, nyoko nyoko wewe. Wakimaliza kutukaniana wazee wao sasa watataja wakunga wa wazazi wao, na kisha ngariba, yaani waliowatahiri wao na wazai wao na ahli zao! Mwisho wataingia majumbani mwao wasasambure ya wake na waume zao. Hapo itakuwa dhambi ya utukanifu wao imefika mwisho kwani, ‘Kima akimaliza miti huja mwilini!'


 
Kwa kusema Ukweli SIJAELEWA Mantiki Wa Habari Hii Hata Kidogo; Ndio Maana Nimeweka kupata WanaJamii Kutoa Maoni yao baada ya kusoma...
 
Hakuna kingine Zanzibar isipokuwa lugha ya visasi, majungu, fitna, lawama, umbeya, nyodo, wivu na ushirikina!!!!
 
Dah kiswahili kipana kwakweli, inabidi uwe na Kamusi pembeni kuelewa anachoongea huyu jamaa
 
Kwa kusema Ukweli SIJAELEWA Mantiki Wa Habari Hii Hata Kidogo; Ndio Maana Nimeweka kupata WanaJamii Kutoa Maoni yao baada ya kusoma...

Wewe mtu wa Tanaganyika huwezi kuelewa, haya ni mambo ya WAZENJ wao wanaelewana jinsi wanavyotukanana!!! Hapo wanamnanga Kamadoo na staili yake ya utawala wakimfananisha na Amani Karume!!
 
Kwa kusema Ukweli SIJAELEWA Mantiki Wa Habari Hii Hata Kidogo; Ndio Maana Nimeweka kupata WanaJamii Kutoa Maoni yao baada ya kusoma...

Anashutumu siasa za Vijiwe zilizoasisisiwa na Salmini Amuri, kijiwe kikubwa, au 'maskani' kama zinavyoitwa ni Kisonge, kuna ubao mkubwa ambao huandikwa ujumbe kila siku.

Mtoa mada anamaanisha hao watu wa maskanini ni masaadati, au mamwinyi, wanaopenda maisha mazuri lakini kazi hawataki kufanya, kwa hiyo wakawa wanakaa vijiweni na kusubiri vya kupewa, sasa Marais waliofuata wakawakataa hao wadananda, matokeo yake wamepaniki, matusi mvua, wakamtukana mpaka Mzee Nasoro Moyo...

Anamaliza kwa kusema watatukana hadi wazazi wao, njaa mbaya sana!

Umepata mwanga?
 
Back
Top Bottom