Salamu za mwaka mpya kutoka iringa!

maggid

JF-Expert Member
Dec 3, 2006
1,084
1,246
Ndugu Zangu,

Naandika nikiwa Iringa.
Ndio, tunaumaliza mwaka huu na mjadala wa Katiba mpya. Nami, katika siku hii ya mwisho wa mwaka, nimeona umuhimu wa kuzungumzia suala hili lililo ndani ya wakati.

Mapema kabisa nataka niweke wazi , kuwa lililo muhimu kabisa katika mjadala wowote uwao ni kujiuliza; nini shabaha na malengo yetu? Nionavyo, shabaha na leo letu liwe kudumisha Umoja wetu wa Kitaifa, amani na utulivu tulio nao. Kama swali ni je, Katiba yetu ya sasa, na kwa wakati uliopo, inakidhi matakwa ya shabaha na malengo yetu kama taifa? Jibu langu ni HAPANA. Na ndio maana naunga mkono juhudi za kufanya marekebisho makubwa ya Katiba yetu.

Na katika hili hatuna sababu za kugombania fito ilihali nyumba tunayojenga ni moja na ni yetu sote.
Ieleweke, kuwa madai ya Watanzania kupata Katiba mpya ni madai muhimu na ya kihistoria. Kuna wanaojidanganya, wakidhani, kuwa madai haya yanatokana na ‘ Njama za mabeberu!’. Hizi ni propaganda za miaka ya 70, zimepitwa na wakati.

Ni busara kutambua, kuwa wakati umebadilika. Mtanzania wa mwaka 1977 si Mtanzania wa mwaka 2010. Hoja hii ya Katiba si kama nzi anayetua na kuruka. Hoja ya Katiba kwa sasa inaongozwa na kundi kubwa la vijana wanaotaka mabadiliko. Hawa si nzi wanaotua na kuruka, ni siafu wanaokuja kwa kuongezeka idadi yao.

Na madai ya marekebisho ya Katiba si madai mapya. Si madai ya chama au kikundi kidogo cha ’wapinzani’ wasioitakia mema nchi hii. Ni madai ya msingi ya Watanzania, bila kujali tofauti zao za kiitikadi, kidini, rangi na makabila.

Kama ni shauri mahakamani, basi, lilishafunguliwa. Kinachofanyika sasa ni mwendelezo wa shauri. Ndio, tunapongia mwaka 2011, madai ya Katiba mpya yatatimiza miaka 20. Yalianza tangu mwaka 1991.

Ndio, si wengi, miongoni mwa vijana wa sasa, wenye kumbukumbu ya ukweli huu. Tayari mwaka 1991 vuguvugu la kudai vyama vingi na Katiba mpya lilishaanza. Ndio, wakati huo madai makubwa yalikuwa mawili; vyama vingi na Marekebisho ya Katiba. Kuna mnaokumbuka ’ KAMAKA’- Kamati ya Marekebisho ya katiba iliyondwa na wanaharakati. Hayo yalikuwa ni madai ya Watanzania ndani ya mfumo wa chama kimoja.

Marehemu Chifu Abdalah Fundikira aliongoza Kamati iliyoundwa, si na Serikali, bali wanaharakati, kuratibu mchakato wa kudai vyama vingi na Katiba mpya. Hata wakati huo Mzee Mwinyi, kama Rais,

Aliweka ‘ mkwara’, kuwa madai hayo yasiendeshwe na watu au makundi ya watu bila kibali cha Serikali. Presha ya madai ilipoongezeka, tunakumbuka, kuwa Mzee Mwinyi aliweza kusoma alama za nyakati. Aliongea pale Chuo Kikuu Mlimani na kuweka bayana dhamira ya Serikali ya kuunda ‘ Tume ya Nyalali’ . Tume hiyo ilizunguka nchi nzima kuwauliza Watanzania kama wanataka kuendelea na Chama kimoja au Vyama vingi.

Itakumbukwa, Chifu Fundikira alipata kutamka; kuwa huko ni kupoteza muda na fedha za wananchi. Itakumbukwa pia, Mabere Marando alikuwa Katibu wa Kamati ile ya wanaharakati ya kuratibu mchakato wa madai ya kuwepo na vyama vingi na marekebisho ya Katiba. Marando alipata kutamka na kunukuliwa na Daily News, April, 12, 1991; “ We have a bad political system because our Constitution embraces political discrimination. What we want is that all of us should shout out that our Constitution is bad.” ( Mabere Marando, Daily News, April 12, 1991)

Ndio, Marando aliyasema hayo katika Semina ya kwanza ya Kamati ya kuratibu mchakato wa madai ya vyama vingi na Katiba mpya iliyoongozwa na Chifu Fundikira. Semina hiyo iliudhuriwa na watu wapatao 800 kwa mujibu wa taarifa ya Daily News la April 12, 1991.

Na akina Chifu Fundikira waliandamwa sana. Kwa mujibu wa Daily News la April 26, 1991, Mbunge wa Shinyanga, Ndugu Paulo Makolo alimshambulia Fundikira kwa kusema kuwa , katika hilo la kuwa na vyama vingi na katiba mpya , Chifu Fundikira hawasilishi mawazo ya Wasukuma na Wanyamwezi wenzake; “ This is not a Wanyamwezi and Wasukuma movement. It is the selfish interests of Fundikira and his ten colleagues. Our people are not after parties. They want food, water, education and health care.” ( Paulo Makolo, MP, Shinyanga, Daily News, April 26, 1991). Mwenyezi Mungu umrehemu Chifu Abdalah Fundikira.

hili na nalirudia, kuwa, enyi Watanzania wenye mapenzi mema na nchi yenu, msikae mkafikiri, kuwa madai ya kupata Katiba mpya ni kazi nyepesi. Ni kazi ngumu sana, hata kama mnaowataka wawasaidie kupata Katiba hiyo ni Waafrika wenzenu na si wakoloni.


Ilivyo Afrika, kwanza mtaletewa na walio kwenye mamlaka, ’Katiba mpya’ iliyofanyiwa marekebisho madogo kwa maana katiba iliyoongezewa viraka. Haitawapitisha kwenye chaguzi kwa salama. Kuna kuandamana na hata raia kupoteza maisha. Kuna akina Ocampo wa Mahakama za Kimataifa watakaokuja kuwanyofoa wahusika wa vurugu zitakazozua mauaji ya raia.


Kisha itakuja Katiba mpya. Ni njia mbaya na ya kusikitisha, lakini inaepukika, kama kuna utashi wa kisiasa. Ndiyo, Afrika kudai Katiba mpya yaweza kuwa ni kazi ngumu kuliko kudai uhuru kutoka kwa mkoloni.


Wahenga walinena; "Kazi ngumu ianze!" Si kupiga domo tu, akina Chifu Fundikira wameonyesha mfano. Na nani ajuaye, kwa vile madai ya Katiba mpya ni madai ya haki, kama sauti za wenye kudai zitakuwa nyingi, upo, uwezekano wa kufanyika kwa marekebisho makubwa ya Katiba ndani ya miaka mitano ijayo. Na hapa ielekewe, Katiba iliyofanyiwa mabadiliko makubwa nayo ni Katiba mpya, na ndiyo yenye kuhitajika kwa sasa. Ndiyo, kuipata ni kazi ngumu. Kufanikisha kuipata ni kuianza kazi hiyo, sasa.

HERI YA MWAKA MPYA KWENU NYOTE!
Maggid
Iringa
Desemba 31, 2010.
mjengwa
 
maggid eeh kula tano mjita wangu
nime copy nika ku paste vilivyo kichwani babuu
mkatiba lazima ueleweke tuu mwaka huu
happy mwaka mpya babuu.
 
Vipi na huko kuboma ulasi unawafikieni ikiwa fleshi bado?????????? Heri ya Mwaka Mpya Mnyalukolo wangu.
 
Heri ya Mwaka mpya Maggid! salaam zangu zifike kwa dada Neema ( kama upo karibu naye ) na Wakazi wote wa block P
 
Back
Top Bottom