BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,790
- 288,009
Sakata la Richmond lalipuka tena bungeni
Mwandishi Wetu Februari 11, 2009
Raia Mwema~Muungwana ni Vitendo
Mwandishi Wetu Februari 11, 2009
Raia Mwema~Muungwana ni Vitendo
LILE sakata la mradi wa umeme wa dharura uliokabidhiwa kampuni ya Richmond Development LLC limeibuka tena kwa kasi bungeni huku baadhi ya wabunge wakionyesha kutoridhishwa jinsi Serikali inavyolishughulikia, imefahamika.
Baadhi ya wabunge waliozungumza na Raia Mwema wiki hii wanasema wanasubiri kwa hamu taarifa ya utekelezaji wa maazimio ya Bunge kuhusu kashfa ya kampuni ya kufua umeme wa dharura ya Richmond, itakayowasilishwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Miongoni mwa hatua ambazo zimeelezwa kutowaridhisha wabunge ni uamuzi wa kumfikisha mahakamani mtu mmoja pekee, Mkurugenzi wa Richmond Development Tanzania, Naeem Gire.
Wabunge hao wamekejeli uamuzi huo wa kumfikisha mahakamani, Mkurugenzi wa Richmond Development Tanzania, Naeem Gire, ilihali ikitambulika kuwa kampuni iliyoingia mkataba na TANESCO si hiyo bali ni Kampuni ya Richmond Development LLC ya Huston, Marekani.
Lakini mbali na ukweli huo kwamba mkataba uliokuwapo ni kati ya TANESCO na Richmond Development LLC ya Huston, Marekani (na si Richmond-Tanzania), wabunge hao wamesema inashangaza kumshitaki Naeem Gire, ambaye hana hisa katika kampuni hiyo ya Marekani.
Wamesisitiza kuwa aliyepaswa kushitakiwa ni yule aliyeingia mkataba na TANESCO, yaani Richmond ya Marekani na si Richmond ya Tanzania , ambayo haipo.
Wamesema utata mwingine upo katika aina ya mashitaka yanayomkabili Gire ambayo ni kusema uongo kuwa anayo ridhaa ya kisheria ya kuendesha shughuli za Richmond ya Huston nchini Tanzania.
Wabunge hao wamefafanua kuwa wanachotarajia kitakachotokea katika mwenendo wa kesi hiyo ni Richmond ya Huston kuwasilisha barua itakayothibitisha kuwa Gire aliruhusiwa kuendesha shughuli za Richmond ya Huston, nchini Tanzania na huo ndiyo unaotarajiwa kuwa mwisho wa kesi hiyo.
Wameidokeza Raia Mwema kuwa kama Serikali ilikuwa na dhamira ya dhati ya kuchukua hatua za kimahakama dhidi ya wahusika, basi aliyestahili kukamatwa ni mkurugenzi wa Richmond ya Huston-Texas, Marekani ambayo ndiyo iliingia mkataba na TANESCO, mkataba ambao ilishindwa kuutekeleza kikamilifu na kwa wakati.
Lakini mbali na wabunge hao kutoridhishwa na taarifa ya Serikali, imebainika pia kwamba bodi ya wakurugenzi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), imetumbukia katika utata kuhusu kashfa ya Kampuni ya Richmond Development LLC, kutokana na hatua yake ya kutoa taarifa inayopingana na ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).
Katika ripoti yake, BoT iliwahi kutoa taarifa kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kuwa mrithi wa mkataba wa Richmond, kampuni ya Dowans Holdings S.A ililipwa kihalali malipo ya ziada ya $4,865,000 za Marekani (zaidi ya Sh bilioni 4.9), ikiwa ni gharama ya usafirishaji wa mitambo ya kufua umeme.
Lakini wakati taarifa hiyo ya BoT ikisema hivyo, ripoti ya CAG ya ukaguzi wa hesabu za Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa mwaka unaoshia Desemba 2007, inabainisha kuwa fedha hizo hazikustaili kulipwa Dowans na kusisitiza kuwa zinapaswa kurejeshwa.
Ripoti ya CAG inabainisha kuwa mara baada ya Dowans kulipwa fedha hizo ilipaswa kuzirejesha serikalini lakini haikufanya hivyo hadi mkataba iliorithi kutoka Richmond ilipovunjwa na TANESCO, Agosti mosi, mwaka 2008.
Mbali na Dowans, ripoti ya CAG inabainisha pia kwamba Richmond iliondoka na kitita kingine cha Serikali cha takriban Sh bilioni 23, fedha ambazo zilitolewa kwa kampuni hiyo ili pamoja na mambo mengine kufanikisha ufunguaji wa hati ya muamana (letter of credit).
Fedha hizo zilitolewa kwa Richmond kutoka serikalini ili baadaye zirejeshwe kwa awamu. Fedha za jumla zilizotolewa katika makubaliano hayo ni takriban Sh bilioni 30, lakini Richmond ilifanikiwa kurejesha Sh bilioni saba pekee.
Wabunge wengi walionekana kutoridhishwa na utekelezaji maazimio kadhaa, hususan azimio namba 10. Matakwa ya Azimio hilo yalitaka Gavana wa Benki Kuu pamoja na Bodi ya Wakurugenzi wachunguze kwa makini uhalali wa malipo ya ziada ($4,865,000) yaliyofanywa kwa Dowans Holdings A.S, iliyorithi majukumu ya Richmond Development Company na kuwachukulia hatua waliohusika na uzembe huo.
Kwa kuzingatia azimio hilo , Waziri Mkuu Pinda, Agosti mwaka jana aliwasilisha taarifa yake ikielezea kuwa malipo hayo yalikuwa halali, taarifa inayopingana na ile ya CAG.
Pinda aliwaeleza wabunge (Agosti, 2008) kuwa Wizara ya Fedha na Uchumi na Benki Kuu ya Tanzania walichunguza na kuona kuwa malipo ya Sh bilioni 4.9 ($4,865,000) yaliyolipwa kwa Kampuni ya Dowans Holdings S.A. iliyorithi majukumu ya Richmond Development Company LLC ni halali.
Akabainisha kuwa malipo hayo yalilipwa Februari 2, mwaka 2007 ikiwa ni gharama za ndege za usafirishaji wa mitambo ya kukodi ya umeme wa dharura, baada ya kupokea Invoice Namba EFD786675. Lakini wakati taarifa hiyo ikisema malipo ni halali, CAG anasema fedha hizo zinapaswa kurejeshwa serikalini.