Elections 2010 Rostam aipasua CCM; Yahaha kulibakisha jimbo

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
• Yahaha kulibakisha jimbo

na Tamali Vullu


SPIKA wa Bunge, Anne Makinda, amemwandikia barua Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Lewis Makame, kumjulisha juu ya kuwa wazi kwa kiti cha ubunge katika Jimbo la Igunga.

Makinda alisema alifikia hatua hiyo baada ya kupokea barua ya kujiuzulu kwa aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Rostam Aziz, ambaye alijiuzulu Julai 13, mwaka huu nafasi hiyo na nyadhifa alizokuwa nazo ndani ya Chama Cha Mapinduzi na kubaki mwanachama wa kawaida .

Akizungumza jana na waandishi wa habari bungeni, Kaimu Katibu Mkuu wa Bunge, John Joel, alisema Spika Makinda alipokea barua ya Rostam Julai 19 akimjulisha rasmi kujiuzulu nafasi hiyo.

Alisema kuwa kwa mujibu wa barua ya Rostam aliyoiandika Julai 15 mwaka huu ilipokewa na Spika Julai 20, hivyo kwa utaratibu wa Bunge ni lazima wapitie vifungu vyote vya sheria ili kubaini kuwa alijiuzulu kwa hiari yake na hapakuwa na shinikizo.

Joel alisema baada ya kupitia vifungu hivyo na kujiridhisha, waliona kuwa Rostam alifikia uamuzi huo kwa ridhaa yake pasipo kushawishiwa.

Alisema kuwa katika nukuu ya barua hiyo, Rostam alisema alifanya uamuzi huo kwa kuzingatia Ibara ya 71 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Taratibu za mbunge kujiuzulu zimefafanuliwa katika Katiba na Sheria ya Uchaguzi Ibara ya 149 inayoelekeza kwamba mtu yeyote mwenye dhamana ya kazi yoyote iliyoanzishwa na Katiba ikiwa ni pamoja na kazi ya waziri, naibu waziri au mbunge, isipokuwa mbunge ambaye ni mbunge kwa mujibu wa madaraka ya kazi yake,” alisema na kuongeza kuwa:

“Anaweza kujiuzulu kwa kutoa taarifa iliyoandikwa na kutiwa sahihi kwa mkono wake, Ibara hiyo inafafanua zaidi kuwa kwa mbunge anayetaka kujiuzulu atawasilisha taarifa yake ya kujiuzulu kwa Spika.”

Alisema Ibara ya 149 (2) inafafanua zaidi kuwa mtu anayetoa taarifa ya kujiuzulu atahesabiwa kujiuzulu tangu siku taarifa yake ilipopokewa katika ofisi ya Bunge.
Joel alisema kuwa mishahara pamoja na posho nyingine husimamishwa mara baada ya Spika kupokea barua hiyo, na kwamba mafao atakayolipwa ni yale ambayo alikaa ndani ya Bunge.

Rostam alijiuzulu nafasi hizo kwa maelezo ya kuwa aliona ni afadhali awape nafasi wale wanaoendesha siasa uchwara na zisizo na tija, ambazo yeye hana muda nazo na hawezi kuwa sehemu yake.

Alisema haoni sababu ya kuendelea kuvutana na viongozi wa chama chake na wanachama wenzake katika mambo ambayo yanaweza kumalizwa kwa njia muafaka.

“Uamuzi wangu wa kuachia nafasi zangu zote za uongozi nilizopata kwa tiketi ya CCM, haukutokana na wala haumaanishi kukubaliana na shinikizo lililopotoshwa kuhusu azima ya utekelezaji wa dhana ya kujivua gamba.

“Nimeuchukua kwa dhamira ya dhati uamuazi wa kuachana na siasa hizi uchwara na kutumia muda wangu kushughulika na biashara zangu,” alisema.

Wakati huo huo, BARAZA la Vijana wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (BAVICHA), limeanza harakati za kuwania Jimbo la Igunga mkoani Tabora, kesho wanatarajia kufanya maandamano yatakayohitimishwa na mkutano wa hadhara wilayani humo.

Mwenyekiti wa baraza hilo taifa, John Heche, alisema wataendesha operesheni maalumu itakayofahamika kama ‘Chukua Jimbo la Igunga kwa siku 12’.

Alisema hatua hiyo itaambatana na mkakati wa kukiimarisha chama hicho jimbo humo.
“Hii ni awamu ya kwanza kufanywa na BAVICHA, na kubwa ambalo napenda kulisema kazi tuliyonayo ni kuchukua Jimbo la Igunga ambayo imekabidhiwa kwa vijana, na tunaamini tutaonyesha umahiri kadiri ya uwezo wetu na kamwe hatutawaangusha Watanzania,” alisema Heche.

Akifafanua juu ya tatizo la umeme linaloendelea nchini, alisema serikali inapaswa kuwajibika hasa kupitia Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ambaye ameonyesha wazi kushindwa kusimamia shughuli za serikali kama mtendaji mkuu.

“Tunasema Waziri Pinda hafai kutokana na udhaifu wake kiutendaji na hawezi kuchukua maamuzi yoyote yenye tija kwa wananchi, ipo mifano kadhaa ambayo inadhihirisha kuwa ni mwoga au hajui nini cha kufanya katika mamlaka yake aliyokabidhiwa,” alisema Heche.
Alisema BAVICHA inaamini kupitia nguvu ya umma itawaamsha Watanzania ili wakubali kwa wingi siasa za mageuzi, hasa kwa kuunga mkono harakati za mabadiliko kupitia chama hicho.

 
Back
Top Bottom