Rose Kamili awalipua Anna Abdallah, Mudhihir Mudhihir na mke wake kwa ufisadi

Tumaini Makene

JF-Expert Member
Jan 6, 2012
2,642
6,070
HOTUBA YA MSEMAJI MKUU WA KAMBI YA UPINZANI MHESHIMIWA ROSE KAMILI SUKUM (MB) WIZARA YA KILIMO, CHAKULA NA USHIRIKA KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013



  1. UTANGULIZI.
Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kwangu mimi na kwa niaba ya wabunge wenzangu wote wa Kambi Rasmi ya Upinzani kutoa rambirambi kwa ndugu, jamaa na marafiki kwa msiba mkubwa uliolikumba taifa wa kuzama meli ya abiria iyokuwa inatoka Zanzibar kuja Dar es Salaam. Mwenyezi Mungu atupe wote roho ya subira na ustahimilivu. Amina

Mheshimiwa Spika,
Nachukua fursa hii kwa mujibu wa kanuni za Bunge kanuni ya 99 (7) toleo la 2007 kuwasilisha maoni ya Kambi ya upinzani kuhusu makadirio ya Mapato na matumizi ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kwa mwaka wa Fedha 2012/2013.

Mheshimiwa Spika,
Kwa moyo wa dhati napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema na fadhila kwa kunijalia uhai, afya njema na kwa upendo wake anaotujalia kila mmoja wetu kwa nafasi yake.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee napenda kumshukuru Kiongozi wa Kambi ya Upinzani na Mwenyekiti wa Chama makini cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Makamanda wenzangu wa chama hiki makini cha watu. Aidha napenda kuwashukuru Watanzania wote wenye mapenzi mema na nchi yetu.

2.
HALI YAKILIMO NA CHAKULA NCHINI

Mheshimiwa Spika,
Hali ya kilimo nchini si nzuri, kwani, sekta ya kilimo nchini kwa mwaka 2011 imezorota kwa asilimia 0.6% ikilinganishwa na mwaka 2010, aidha, mchango wa sekta ya kilimo kwenye pato la Taifa (GDP) umeshuka kwa asilimia 0.4% kwa mwaka 2011/2012 ukilinganishwa na mwaka 2010.

Mheshimiwa Spika,
hali ya chakula nchini hairidhishi, kwani uzalishaji wa mazao ya chakula kwa msimu wa 2010/2011 umepungua ukilinganishwa na mahitaji ya chakula kwa mwaka 2011/2012. Kwa mujibu wa Taarifa ya Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika kwenye Kamati ya Bunge ya Kilimo, Maji na Mifugo ya tarehe 8 Juni, 2012 ni kwamba kuna upungufu wa jumla ya tani 204,821 kwa mazao ya nafaka . Kati ya upungufu huo mahindi yakiwa ni tani 160,917 na ngano upungufu wa tani 111,717.

Mheshimiwa Spika,
kambi ya Upinzani, inaitaka Serikali kueleza mbele ya bunge hili kuwa imechukua hatua gani hadi sasa katika kukabiliana na upungufu wa chakula nchini, hasa ikizingatiwa kuwa nchi hii ina mabonde mengi yanayofaa kwa kilimo na maji ya kutosha.

3.
HALI YA KILIMO NA HATMA YAKE KATIKA UCHUMI

Mheshimiwa Spika, Kilimo ni sekta ambayo ni tegemeo na ni kimbilio la watanzania wengi katika kuendeleza maisha yao. Kwa mujibu wa Taarifa Fupi ya Benki ya Dunia (2011) kuhusu uchumi wa Tanzania, ni kwamba takriban asilimia 80 ya kaya za kitanzania hutegemea kilimo kama shughuli zao za msingi za kiuchumi. Taarifa hiyo inaeleza kwamba kitendo cha watanzania wengi kiasi hiki kutegemea kilimo, kinauweka uchumi wa Tanzania katika hali ya hatari kutokana na kilimo kuwa na tabia ya kuathiriwa sana na mabadiliko ya hali ya hewa pamoja na kupanda na kushuka kwa bei za mazao katika masoko ya Kimataifa.

Mheshimiwa Spika,
hali hii ya hatari tayari imeanza kutokea kwani kwa muda wa miaka kumi iliyopita kilimo kimekuwa kinashuka nafasi katika uchangiaji wa uchumi wa Taifa. Kwa mujibu wa taarifa fupi ya Benki ya Dunia (2011) kuhusu uchumi wa Tanzania ni kwamba sekta zinazoongoza kwa kuchangia uchumi wa Taifa katika miaka kumi iliyopita ni madini, ujenzi, mawasiliano, huduma na sekta ya fedha.

Mheshimiwa Spika,
si jambo baya kupata mapato kutoka katika Sekta nilizozitaja, ila ni hatari sana uchumi kutegemea rasilimali zinazoisha (non-renewable resources) kwa mfano madini. Ni hatari vilevile uchumi kutegemea sekta ndogo kama ujenzi, mawasiliano huduma na fedha kwa kuwa hazina wigo mpana wa ajira kwa wananchi. Hali kama hii husababisha uchumi kuwa ni wa kitendawili kwa maana kwamba; wakati hali ya uchumi wa taifa inaonekana kwenda vizuri, idadi ya watu wasio na ajira inaongezeka na umasikini wa mtu mmoja mmoja unaongezeka pia. Hii ina maana kwamba sekta zinazoongoza katika kuchangia uchumi wa taifa kwa sasa hazina mchango wa moja kwa moja kwa uchumi wa mtu mmoja mmoja. Hivyo kuna umuhimu mkubwa sana wa kuwekeza katika kilimo kwani kinaajiri watu wengi zaidi hapa nchini (80% kwa sasa) na msingi wake ni rasilimali ardhi ambayo ni endelevu.


4.
MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA BAJETI ILIYOPITA 2011/2012

Mheshimiwa Spika, Taarifa ya Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika kwa kamati ya Bunge (uk.26) ni kwambafedha iliyoidhinishwa kwa ajili ya Wizara hii fungu 43 mwaka 2011/2012 ni shilingi bilioni 258.35 Kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 152.41 ni fedha za matumizi ya kawaida na shilingi bilioni 105.94 zikiwa ni fedha za maendeleo. Mheshimiwa Spika, hadi tarehe 31 Mei, 2012 fedha za matumizi zilizopelekwa wizarani kutoka hazina ni shilingi bilioni 103.06 sawa na asimia 67.62 ya kiasi kilichoidhinishwa. Kwa upande wa fedha za maendeleo hadi kufikia tarehe 31 Mei, 2012 fedha zilizokuwa zimepelekwa wizarani kutoka hazina ni shilingi bilioni 72.63 sawa na asilimia 68.56 ya fedha zilizoidhinishwa.

Mheshimiwa Spika, katika muktadha huohuo, fedha zilizoidhinishwa kwa wizara hii fungu 24 kwa mwaka 2011/2012 zilikuwa ni shilingi bilioni 6.612 kwa matumizi ya kawaida. Hata hivyo fedha iliyokuwa imetolewa na hazina hadi kufikia tarehe 31 Mei, 2012 ni shilingi bilioni 4.63 sawa na asilimia 70 ya kiasi kilichoidhinishwa.

Mheshimiwa Spika, kwa takwimu hizi, ni kwamba bajeti ya Wizara hii katika fungu 43 haikutekelezwa kwa zaidi ya theluthi moja. Huu ni uthibisho kamili kwamba malengo yaliyopangwa kufikiwa katika mwaka wa fedha 2011/2012 hayakufikiwa.

Mheshimiwa Spika,
Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali itoe maelezo mbele ya Bunge hili Tukufu kwa nini tuipatie fedha inazoomba kwa Wizara hii, wakati mwaka jana haikutekeleza bajeti iliyoidhinishwa na bunge na hivyo kuzorotesha malengo ya Wizara hii. Aidha, kambi ya upinzani inaitaka Serikali kueleza itatekeleza vipi viporo vya malengo ambayo hayakutekelezwa kwa mwaka uliopita.

5. UCHAMBUZI WA BAJETI YA WIZARA YA KILIMO CHAKULA NA USHIRIKA KWA MWAKA 2012/2013

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya utekelezaji ya Wizara hii (uk.62), (fungu 43) bajeti imepungua kutoka shilingi bilioni 258.35 mwaka 2011/2012 hadi shilingi bilioni 237.624 sawa na punguzo la asimia 8.7 Mheshimiwa Spika, pamoja na kupungua kwa jumla kwa bajeti, matumizi ya kawaida yameongezeka kutoka shilingi bilioni 152.41 mwaka 2011/2012 hadi kufikia shilingi bilioni 170.364 sawa na ongezeko la asilimia 11.78

Mheshimiwa Spika, wakati matumizi ya kawaida yameongezeka kwa takriban asilimia 12, bajeti ya maendeleo katika wizara hii imepungua kutoka shilingi bilioni 105.94 mwaka 2011/2012 hadi kufikia shilingi bilioni 67.260 ikiwa ni anguko la asilimia 57.5 Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kueleza, Hivi kitendo cha kupunguza fedha za maendeleo kwa asilimia 57.5 katika wizara ya Kilimo ndio mkakati wa kutekeleza kauli mbiu ya “Kilimo Kwanza?”

Mheshimiwa Spika, pamoja na fedha hizi za maendeleo kupungua kiasi hiki, bado bajeti ya maendeleo imeendelea kuwa tegemezi kwa fedha za nje kwa asilimia 77.7. Tafsiri ya utegemezi huu ni kwamba sasa Serikali imeamua kukiweka kilimo chetu rehani.

Mheshimiwa Spika, Ukiangalia kwa makini Jedwali namba 7 lenye mchanganuo wa bajeti ya matumizi ya maendeleo katika taarifa ya utekelezaji ya wizara hii uk. 65 utagundua kuwa miradi ambayo inaweza kuendeleza kilimo chetu kwa mfano utafiti na maendeleo, umwagiliaji, mpango wa matumizi ya ardhi, kilimo cha kisasa imetengewa fedha ndogo sana za ndani.

Mheshimiwa Spika, kinachoshangaza kabisa ni kwamba kasma 5001 inayohusu Usalama wa Chakula wa Taifa, hakuna hata senti moja kutoka ndani. Hii ina maana Usalama wa Chakula wa Taifa uko mikononi mwa wahisani ?

Mheshimiwa Spika
, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali isifanye mzaha kabisa na masuala ya usalama wa chakula nchini kwa kuwa usalama wa chakula ndio uhai wenyewe wa wananchi. Kutotenga fedha za ndani kwa ajili ya usalama wa chakula ni kuweka rehani maisha ya watanzania, na huku ni kuudhalilisha utu na uhuru wa mtanzania na kamwe hatutakubaliana na hali hii.

Mheshimiwa Spika
, Kambi ya Upinzani kwa mara nyingine inaitaka Serikali kulieleza bunge hili ina mpango gani wa kuwahakikishia watanzania usalama wa chakula ikiwa fedha zote za usalama wa chakula zinatoka nje? Pili, Serikali ieleze njia nyingine mbadala za kuendeleza kilimo iwapo wahisani/wafadhili watakoma kutoa misaada katika sekta ya kilimo.

Mheshimiwa spika
, Hayati mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliwahi kusema, “Tunakipuuza kilimo; kama tungekuwa hatukipuuzi, basi Wizara zote, mashirika ya umma yote na mikutano yote ya chama ingekuwa inafanya kazi kushughulikia mahitaji ya wakulima. Ni lazima sasa tuache kukipuuza kilimo. Ni lazima tukifanye kilimo kiwe ndio shina na mwanzo wa mipango yetu yote ya maendeleo. Kwani kwa hakika, Kilimo ndio msingi wa maendeleo yetu” (Nyerere, 1982).

Mheshimiwa Spika, kwa kupunguza bajeti hii ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika ni dhahiri kwamba Serikali hii ya CCM inapuuza kilimo. Hivyo Kambi ya Upinzani inaiasa Serikali ya CCM kuzingatia wosia wa Baba wa Taifa ambaye tangu mwaka 1982 alishagundua kuwa CCM inapuuza Kilimo ambacho ndio tegemeo la watanzania wengi. 5.1 Uwiano wa Mgawanyo wa Bajeti na Usalama wa Chakula Nchini Mheshimiwa Spika, mojawapo ya malengo ya Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika ni kuhakikisha usambazaji na uwepo endelevu wa chakula katika kila kaya. Kwa maneno mengine lengo hili likifikiwa, kutakuwepo na usalama wa chakula katika kila kaya.

Mheshimiwa Spika, kwa Mujibu wa utafiti wa Gabagambi (2011) Tanzania haizingatii hali ya usalama wa chakula katika mgawanyo wa bajeti ya kilimo. Katika utafiti huu ilibainika kwamba Mikoa 10 ya Tanzania Bara ambayo ni Arusha, Kilimanjaro, Lindi, Manyara, Mara, Mwanza, Mtwara, Shinyanga, Singida, na Tabora haina usalama madhubuti wa chakula. Utafiti uliofanywa, unaonesha kuwa mikoa hii haipatiwi kipaumbele maalum cha kibajeti ili kuhakikisha kuwa kuna usalama wa chakula katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, matokeo ya utafiti wa Gabagambi (2011) unaonesha kwamba mikoa kumi iliyotajwa ambayo ni karibu asilimia 50 ya mikoa yote ambayo ni asilimia 46.2% ya idadi ya watu wote nchini, ilipewa asilimia 30.2 tu ya bajeti ya kitaifa ya District Agricultural Development Plans(DADPs) kwa mwaka 2009/2010. Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kueleza ni vigezo gani vinatumiwa katika kugawa fedha za DADPs. Pili Serikali ina mkakati gani maalumu wa kuhakikisha kuwa kuna usalama wa chakula hasa katika mikoa yenye upungufu mkubwa wa chakula nchini? 6.

PEMBEJEO NA ZANA ZA KILIMO


Mheshimiwa Spika, katika kufanikisha lengo la kukuza kilimo nchini, serikali imepunguza bei ya trekta za Suma JKT ili kuwawezesha wakulima kumudu bei, mfano Farmtrac 60 (yenye horse power 50, 2 wheel drive) iliyokuwa inauzwa shilingi milioni 25.64 na baada ya punguzo sasa inauzwa shilingi milioni 16.5 kiwa ni punguzo la asilimia 35.71%.

Mheshimiwa Spika,
Kambi ya upinzani inaitaka Serikali kuweka wazi ni kwanini punguzo hili halikufanywa mapema ili kuwawezesha wananchi kufaidi punguzo hili mapema? Na pia vifaa kwa ajili ya matrekta haya kama harrow, majembe, planters, nk kwanini havikupunguzwa bei ili wananchi waweze kunufaika na punguzo hili?

6.1 Ruzuku ya Pembejeo za Kilimo
Mheshimiwa Spika, ruzuku ya pembejeo za kilimo kwa mkulima inalenga kupunguza gharama za kuendesha kilimo kwa wakulima wadogo. Hata hivyo mfumo wa ruzuku ya pembejeo kwa wakulima umekuwa na matatizo mengi. Moja ya matatizo yaliyojitokeza katika mfumo wa vocha za ruzuku ya pembejeo kwa wakulima ni pamoja na baadhi viongozi wa serikali kula njama na mawakala kuiba vocha kwa kutumia majina hewa na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu huku wananchi wakibaki bila pembejeo.

Mheshimiwa Spika,kwa mujibu wa Gazeti la Mwananchi la Machi 6, 2011 shilingi 5,004,169,500/=zilikuwa zimeibwa na wajanja kutoka katika Mfuko wa Pembejeo. Upotevu huo unawahusisha baadhi ya watendaji wa Serikali na baadhi ya Wakuu wa Wilaya ambao ndio wasimamizi wakuu wa Mfuko wa Pembejeo. Aidha Gazeti la Habari Leo la Juni 21, 2012 lilimnukuu Mkuu wa Mkoa wa Arusha akiamuru wakala wa pemejeo Ndugu Selestine Magati kupelekwa Mahakamani kwa kuwaibia wakulima mbolea ya ruzuku.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mfumo huu wa kusambaza pembejeo za kilimo kwa njia ya vocha umegubikwa na wingu la rushwa, wizi, ulanguzi na hata uchakachuaji wa pembejeo (kwa mfano mbolea kuchanganywa na saruji), Serikali imebuni njia gani mbadala ambayo itasaidia wakulima kupata pembejeo bila usumbufu wanaoupata sasa?

Mheshimiwa Spika,
kuwa kuwa sera ya Kilimo ya mwaka 1997 inasema kilimo kiwe cha kisasa na endelevu, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kuacha mtindo wa kuzifanya pembejeo kama mbolea na mbegu kuwa bidhaa za msimu na badala yake bidhaa hizo ziwe kwenye soko muda wote wa mwaka. Hii ndiyo njia pekee itakayoondoa rushwa na ulanguzi katika usamabzaji wa pembejeo.

6.2 Mfuko wa Pembejeo


Mheshimiwa Spika, upo mfuko wa pembejeo wa Taifa ambao hutoa mikopo ya vifaa vya kilimo kama trekta, power tiller, mikopo ya kukarabati trekta, mashine za umwagiliaji na usindikaji nk.

Mheshimiwa Spika,
mikopo hii huwa ni mikubwa kiasi kwamba wanaoweza kumudu marejesho ni wakulima wakubwa ambao ni wachache. Hii ina maana kwamba wakulima wadogo wadogo ambao ndio wengi hapa nchini hawanufaiki na mfuko huu, na hivyo kilimo chao kinazidi kuzorota.

Mheshimiwa Spika, masharti ya mfuko huu yarekebishwe ili na wakulima wadogowadogo waweze kunufaika na mfuko huu ambao kwa sasa si rafiki wa wakulima wadogo. Aidha Kambi ya Upinzani inapendekeza kuwe na mfuko mmoja wa pembejeo ili kutowachanganya wakulima wakati wa ufuatiliaji wa pembejeo za kilimo.

6.3
Mikopo kwa Wakulima

Mheshimiwa Spika,
katika utoaji wa mikopo kwa wakulima hapa nchini kumekuwa na matatizo kama · Mikopo kufika bila kuzingatia misimu ya kilimo. · Urasimu na mlolongo mrefu katika kuchukua mikopo · Urejeshaji wa mikopo mara kwa mara bila kuzingatia msimu wa mavuno. · Taasisi chache za mikopo na zisizokuwa na matawi mengi nchini hivyo kusababisha wakulima kusafiri umbali mrefu katika kufuatilia mikopo. · upendeleo katika utoaji wa mikopo

Mheshimiwa Spika,
Kambi ya upinzani inapenda kutoa mapendekezo yafuatayo ili kuondokana na matatizo yatokanayo na mikopo kwa wakulima: · Mfuko wa pembejeo wa Taifa na zana za kilimo ufungue ofisi katika kila wilaya na kutoa mikopo moja kwa moja kwa wakulima bila kupitia katika uongozi wa mikoa au wilaya, hili litasaidia kupunguza urasimu mrefu wanaokutana nao wakulima wakati wa kuchukua mikopo. · Taasisi za fedha zipunguze masharti ya upatikanaji wa mikopo kwa wakulima hasa wadogo ikiwemo kupunguza riba zinazotozwa wakati wa urejeshaji wa mikopo, tunapendekeza kupunguza kiwango cha malipo ya mwanzo kutoka asilimia 50 ya sasa hadi asilimia 25 ili kuwawezesha wakulima wadogo kumudu kupata mikopo hiyo. · Muda wa marejesho ya mkopo uongezwe na uzingatie msimu wa mavuno tofauti na sasa ambapo msimu wa mavuno hauzingatiwi na mkopaji hutakiwa kurejesha mkopo muda mfupi tu baada ya kukopa.

7. MATUMIZI MABAYA YA MASHAMBA YA NAFCO Mheshimiwa Spika, mashamba ya NAFCO yaliyo chini ya mwekezaji NGANO Ltd yanatumika chini ya kiwango na hivyo kwenda kinyume na sera ya uwekezaji. Mheshimiwa Spika, katika ekari 30,000 za mashamba ya Murjanda, Gidamowd na Setchet, ni ekari 9,000 tu zinazolimwa. Kutokana na hali hii, takriban watu 600 wamekosa ajira kutokana matumizi ya mashamba haya chini ya kiwango.

Mheshimiwa Spika,
aidha shamba la ‘Bassotu Plantation’ halijapata mwekezaji. Shamba hili lina vifaa kama Matrekta, Combine Harvesters, Boom Sprayers na vifaa vingine ambavyo vinaharibika kwa kutu, kuungua, na vingine kuibiwa.

Mheshimiwa Spika
, Serikali inasemaje kuhusu hasara inayotokana na uharibifu wa vifaa inayoendelea kutokea katika Shamba la Bassotu Planatation? Aidha Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kurudisha mashamba haya kwa wanachi kwa kuwa kwa sasa yanatumika chini ya kiwango na hivyo kutowanufaisha wananchi kwa maana ya ajira.

8. UZALISHAJI, UAGIZAJI NA USAMBAZAJI WA MBEGU BORA

Mheshmiwa Spika, Serikali ilitunga sheria inayoitwa “Protection of New Plant Varieties (Plant Breeders Rights) Act, 2002”, inayotambua haki miliki za wazalishaji wa mbegu na mimea mipya na itakayokidhi mabadiliko ya kijamii na kiuchumi kulingana na soko huria la uzalishaji na usambazaji wa mbegu nchini. Haki hizo zinawawezesha wazalishaji wa mimea na mbegu mpya kunufaika na utafiti wao kutokana na malipo watakayopata kwa kutoa leseni au kuruhusu mbegu zao zitumiwe na wazalishaji wengine kwa ajili ya biashara (“seed multiplication”).

Mheshimiwa Spika, hadi mwaka 2011 kuna jumla ya makampuni 53 ambayo yamesajiliwa kisheria nchini. Aidha, mwaka 2006, Serikali ilianzisha Wakala wa Mbegu za Kilimo (Agricultural Seed Agency) kwa lengo la kuongeza uzalishaji na upatikanaji wa mbegu bora nchini.

Mheshimiwa Spika,
Mbegu zilizozalishwa na taasisi za Serikali za utafiti zitalindwa chini ya Sheria hii na kuiwezesha Serikali kupata mapato kutoka kwa wazalishaji wa kibiashara watakaoomba na kupewa leseni za kuzalisha au kuuza mbegu na mimea mipya iliyogunduliwa na watafiti wa Serikali. Aidha, kwa kutumia njia ya kuwasajili wazalishaji wa mbegu na mimea mipya Serikali itaweza kudhibiti ubora wa mbegu mpya, ikiwa ni pamoja na kuwadhibiti wazalishaji holela.

Mheshimiwa Spika, mahitaji ya mbegu bora yamefikia tani 120,000 kwa mwaka iwapo kila mkulima atatumia mbegu bora. Hata hivyo, upatikanaji umeongezeka kutoka tani 6,781 mwaka 1980 hadi tani 17,000 mwaka 2011. Lengo la Serikali ni kuongeza upatikanaji pamoja na matumizi ya mbegu bora ili yafikie tani 60,000 za mazao ya nafaka, mikunde na mbegu za mafuta ifikapo mwaka 2015. Miaka ya 2000 hadi 2003 Mashamba ya mbegu ya Serikali yalichangia tani 594, sawa na asilimia 4, zikiwa ni mbegu za msingi. Chini ya utaratibu wa uzalishaji wa mbegu kwa kutumia wakulima wadogo, tani 553 zilizalishwa. Makampuni ya mbegu yaliingiza nchini tani 10,878 za mbegu.

Mheshimiwa Spika
, kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa katika maonyesho ya Kilimo Nane nane 2010 hapa Dodoma alisema “tumekuwa tukiagiza mbegu kwa asilimia 75 kutoka nchi za nje, lakini hazitufai kutokana na aina ya mbegu hizo na mazingira yetu mbegu inatakiwa ifanyiwe utafiti katika eneo husika inapopandwa,” Mheshimiwa Spika, kutokana na takwimu tajwa hapo juu za mahitaji ya mbegu na asilimia ya mchango wa makampuni ya nje ni dhahiri kuwa kama nchi kilimo chetu kiko mashakani, haiwezekani kwa nchi ambayo zaidi ya asilimia 70 ya wananchi wake wanapata riziki zao kutokana na sekta hiyo na pale pale aslimia 75 ya mbegu zinazotegemewa kwa mazao ya chakula zinatoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, kutokana na ubinafsishaji na ufilisikaji kwa Kampuni ya Mbegu Tanzania (TANSEED), mfumo wa uzalishaji na usambazaji wa mbegu nchini nao ulisambaratika sambamba na kampuni hiyo ya Mbegu. Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali ilieleze Bunge hili ni mkakati gani mahususi wa kuyafufua mashamba yote yaliyokuwa yanazalisha mbegu hapa nchini. Kwani kama hatutaweza kuwa na uwezo wa kutosheleza mahitaji ya mbegu bora kwa wakulima wetu ni dhahiri kauli mbiu ya Kilimo Kwanza haitakuwa na maana kwa maendeleo ya wakulima wa nchi hii.

9. BODI ZA MAZAO YA BIASHARA NA MAENDELEO YA KILIMO

Mheshimiwa Spika, kilimo cha mazao ya biashara hapa nchini kwa sasa kina changamoto nyingi. Changamoto hizo ni pamoja kukosa soko na bei za uhakika za mazao hayo.

Mheshimiwa Spika, malengo ya kuwa na bodi hizi za mazao ilikuwa ni kuwasaidia wakulima kupata masoko na bei nzuri kwa mazao yao. Ila cha kusikitisha bodi hizi badala ya kupigania haki za wakulima, zimekuwa zikijali maslahi ya wajumbe wake huku wakulima wakiachwa bila msaada wowote.

Mheshimiwa Spika, kwa kuonesha jinsi bodi za mazao haziwatendei haki wakulima wa nchi hii naomba kunukuu sehemu ya hotuba ya Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni aliyoitoa hapa Bungeni mapema tarehe 25/06/2012. Nanukuuu “Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa tuliyonayo ni kwamba mfumo wetu wa Kilimo cha mazao ya biashara kimehodhiwa na Bodi za Mazao ambazo kazi yake kubwa ni kunyonya (extractive behaviour) wakulima badala ya kuwaendeleza. Bodi za Mazao yote hapa nchini kama zilivyoundwa baada ya kuvunja Mamlaka za Mazao zimeonyesha kushindwa kabisa kusimamia Mazao yao. Mkulima ndio anaathirika na Bodi za Mazao kutokana na maamuzi yao ambayo hayazingatii haki za Wakulima na bodi hizi kuongozwa kisiasa zaidi na makada wa CCM wakiwamo Wabunge kuliko utaalam. Ni hakika basi kuwa Chama cha Mapinduzi hakiwezi kukwepa lawama ya kilio cha wakulima nchi hii kwa kushindwa kuongoza bodi hizi na kuzigeuza vitegauchumi”.Mwisho wa kunukuu.

9.1 Bodi ya Korosho na Matumizi Mabaya ya Fedha za Wakulima


Mheshimiwa Spika, kwa kukazia hoja ya Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, naomba nitoe mfano wa Bodi ya Korosho jinsi inavyowanyonya wakulima wa Korosho katika Mikoa ya Lindi, Mtwara,Pwani na Ruvuma kwa kujilipa posho nyingi na marupurupu mengine huku wakiwaacha wakulima wa korosho wakiteseka na kuhangaika huku na huko kama kondoo wasio na mchungaji bila kutatua matatizo yao.

Mheshimiwa Spika, bodi ilipokea kiasi cha shilingi bilioni 2 kati ya mwezi Oktoba 2011 na Januari 2012 kutokana na ushuru wa mazao ya nje(Export levy) ya korosho kwa msimu wa 2010/2011. Kiasi hicho kilikuwa ni kwa ajili ya shughuli za kuendeleza tasnia ya Korosho nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa masikitiko makubwa fedha hizo hazikutumika kufanya shughuli kama ilivyotarajiwa na badala yake zilitumika kugharamia vikao vya bodi ya wakurugenzi na safari za viongozi (management ya bodi) ambazo hazijaleta tija kwa tasnia nzima kama ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, hayo yanapata ushahidi kutokana na matumizi ya kulipa posho kwa wajumbe wa bodi wanaounda Kamati ya ajira na uwekezaji ambayo wajumbe wake ni wanne, lakini aliwekwa na mke wa mjumbe katika malipo.

Mheshimiwa Spika,
kwa kikao cha siku moja kilichofanyika tarehe 29/11/2011 wajumbe wa bodi hiyo walilipwa posho kama ifuatavyo:

1.
Mh. J. Bwanausi – Mjumbe wa Bodi: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 1,550,000/=, ikiwa shilingi 750,000/= ni posho ya kawaida (Per diem) na shilingi 800,000 ni “working session” kama ilivyoandikwa kwenye fomu ya malipo.

2.
Mh. Anna M. Abdallah – M/Kiti wa Bodi ya Wakurugenzi: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 1,800,000/= kwa mchanganuo ufuatao: Posho ya kikao shilingi 500,000/=, Usafiri shilingi 300,000/= Posho ya kawaida (Per diem) shilingi 900,000/= na Usafiri Dar es Salaam shilingi 100,000/=

3.
Mh. Jerome Bwanausi – Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi: Huyu alilipwa kwa mara nyingine tena kwenye kikao hicho hicho jumla ya shilingi 1,550,000/= ikiwa posho ya kikao ni shilingi 400,000/=, Usafiri wa Ndege shilingi 300,000/=, Posho ya kawaida(Per diem) shilingi 750,000/= na Usafiri Dar es Salaam shilingi 100,000/=

4.
Mh. Mudhihir M. Mudhihir – Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 1,550,000/= ikiwa posho ya kikao ni sh. 400,000/=, Usafiri wa Ndege sh. 300,000/= Posho ya Kawaida(Per diem) sh. 750,000/=, Usafiri Dar es Salaam sh. 100,000/=

5.
Mrs. Mudhihir M. Mudhihir – Mke wa Mh. Mudhihir M. Mudhihir: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 875,000/= kwa mchanganuo ufuatao: Posho ya kikao sh. 200,000/=, Usafiri sh. 300,000/= Posho ya kawaida (Per diem) sh. 375,00/=

Mheshimiwa Spika,
Jumla ya fedha zote zilizolipwa (kwa watu watano) katika kikao hiki cha wakurugenzi wa Bodi ya Korosho cha tarehe 29/11/2011 ni shilingi 7,325,000/=

Mheshimiwa Spika, licha ya matumizi ya fedha hizi kuwa hayana tija kwa kuwa matatizo ya wakulima wa korosho hayajapatiwaufumbuzi hadi sasa, utaratibu walioutumia wajumbe hawa kujipatia fedha hizi una dalili za kifisadi ndani yake. Hii ni kwa sababu mke wa Mh. Mudhihir M.Mudhihir ambaye si mjumbe wa kikao aliingia kwenye kikao na kulipwa posho. Utaratibu uliotumika kumlipa mke wa Mudhihir haueleweki na hata viwango vilivyotumika kukokotoa malipo yake pia havifahamiki.

Mheshimiwa Spika,
dalili ya ufisadi mwingine katika bodi hii, ni kwa Mjumbe wa bodi Mh. Jerome Bwanausi kulipwa posho hiyo mara mbili. Katika fomu za malipo kwa Mh. Bwanausi, fomu moja ameandika jina lake kwa kifupi yaani J. Bwanausi na tarehe ya kuchukua fedha ameandika ni tarehe 28/11/2011 wakati katika fomu ya pili ya malipo ameandika jina kamili yaani Jerome Bwanausi na tarehe ya kuchukua fedha kaandika 29/11/2011.

Mheshimiwa Spika,
mazingira kama hayo, yanaibua hisia kuwa Mh. Bwanausi alijipatia fedha hizo kwa njia ya udanganyifu na hivyo kuwaaminisha watu kuwa alitumia nafasi yake kama mjumbe wa bodi ya korosho kuchukua fedha za wakulima wanyonge wa korosho. Kambi ya upinzani, tunaitaka serikali kutoa majibu juu ya bodi hizi za mazao na utaratibu wa kulipana posho ukoje?Aidha tunamtaka mkaguzi na mthibiti Mkuu wa serikali kufanya ukaguzi maalum (special audit) kwenye matumizi ya bodi hii .

9.2 Bodi ya Pamba na Mgogoro wa Kilimo cha Mkataba na Bei ya Pamba Nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Pamba namba 2 ya mwaka 2001, majukumu ya Bodi ya Pamba ni pamoja na kukuza na kuendeleza sekta ya pamba kwa kujenga mazingira ya ushindani wa haki, kuongeza uzalishaji na uchambuaji wa pamba pamoja na kuboresha masoko ya pamba na kusimamia na kudhibiti ununuzi wa pamba, mbegu na nyuzi kuanzia ngazi ya gulio, kiwandani na masoko.

Mheshimiwa Spika, kutokana na hali mbaya inayokikumba kilimo cha pamba na biashara ya pamba kwa sasa, ni dhahiri kwamba Bodi ya Pamba imeshindwa kutekeleza majukumu yake ya kisheria kama nilivyoyataja hapo awali.

Mheshimiwa Spika,
hadi sasa hivi kuna mgogoro mkubwa na malalamiko makubwa miongoni mwa wakulima wa pamba kutokana na bei ya pamba kushuka sana lakini pia kuna hali ya sintofahamu juu ya kilimo cha pamba kwa mkataba kwa wakulima wa pamba.

Mheshimiwa Spika,
mwanzoni kulikuwa na hisia kuwa kilimo cha pamba cha mkataba kingekuwa mkombozi kwa mkulima wa pamba. Lakini kwa hali inayoendelea ni kwamba kilimo cha mkataba sasa kimekuwa mwiba na kikwazo kikubwa kwa maendeleo ya kilimo cha pamba nchini.

Mheshimiwa Spika, msingi wa nadharia ya kilimo cha mkataba ni kwamba mkataba unafanyika baina ya mkulima na mnunuzi na kwamba bei hupangwa kwa makubaliano kabla ya uzalishaji kufanyika. Tofauti na mwongozo huu wa kinadharia ni kwamba kinachofanyika sasa hivi kwenye kilimo cha pamba ni kwamba makampuni ya kibiashara ndiyo yanapanga bei tena baada ya pamba kuvunwa na bila makubaliano na mkulima.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wakulima wa pamba wana chombo cha uwakilishi yaani Bodi ya Pamba, ilitakiwa mkataba ufanyike baina ya makampuni hayo na bodi kwa niaba ya wakulima. Tofauti na hivyo Makampuni hayo yanaingia mkataba na wakulima moja kwa moja na wakulima ambao hawana uelewa wa sheria za mikataba na hivyo kuwalaghai na kuwanyonya.

Mheshimiwa Spika, tatizo jingine ni kwamba wakulima hawa wanasainishwa fomu kuwa tayari wamepokea pembejeo ambapo wakati mwingine pembejeo hizo haziletwi kwa idadi ambayo imesainiwa kwenye fomu na vilevile mkulima hajui gharama ya pembejeo na hivyo kutojua kama anapata faida au anapunjwa. Wakati mwingine pembejeo nyingine kama dawa na mbole huwa zimechakachuliwa na hivyo kutofanya kazi. Pia mkulima analazimishwa kumuuzia mnunuzi kwa mkataba, hata kama kuna makampuni mengine au viwanda vyenye bei nzuri. Mkulima pia hana hiari ya kutouza pamba yake kusubiri bei nzuri ingawa mnunuzi anaweza kuwasubirisha wakulima bila kununua pamba yao akisubiri bei nzuri.

Mheshimiwa Spika, Kuna malalamiko pia kwamba Bodi ya pamba ambayo ina mamlaka kisheria kusimamia kilimo na biashara ya pamba inafanya biashara kwa kuwauzia wakulima mbegu kupitia makampuni ya biashara. Bodi hii inalalamikiwa pia kuwa imeyaacha huru makampuni haya kwenda kuwalaghai wakulima juu ya kilimo cha mkataba. Hili limejidhihirisha pale ambapo makampuni haya ya biashara yalipowauzia wakulima mbegu zilizoharibika ambazo hazikuota, madawa na mbolea zilizochakachuliwa na Bodi kukaa kimya bila kuyachukulia makampuni haya hatua yoyote.

Mheshimiwa Spika, mambo yote haya yenye utata yanatoa picha kwamba Bodi ya Pamba inahusika kwa kiwango kikubwa na mgogoro wa biashara ya pamba kwa sasa. Kwa sababu hiyo, Kambi ya Upinzani inataka kujua Serikali inachukua hatua gani dhidi ya bodi ya pamba ambayo imewageuka wakulima wa pamba kwa maslahi yake binafsi.

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inataka Serikali ya CCM ielewe kwamba kuongoza dola ni pamoja na kuwa uwezo kuingilia kati migogoro ya kiuchumi kama huu unaowakabili wakulima wa pamba sasa hivi na kuupatia ufumbuzi. Kitendo cha Serikali kukaa kimya na kuwaacha wakulima hawa wakiteseka na kutojua cha kufanya ni udhalimu mkubwa dhidi ya juhudi za wakulima katika kuujenga uchumi wa Taifa. Aidha kushindwa kusimamia kilimo ambacho kinaajiri asilimia 80% ya watanzania wakiwemo wakulima wa pamba ni kukosa sifa kabisa ya kuongoza dola. Hii ni kwa sababu msingi wa dola ni watu. Na kama watu hawa wanapuuzwa na Serikali basi moja kwa moja Serikali inakosa sifa ya kuwaongoza watu hawa.

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali itoe maelezo ya utata wa kilimo cha pamba cha mkataba na imechukua hatua gani hadi sasa kutatua mgogoro wa bei ya pamba ambayo ni kikwazo kikubwa kwa wakulima wa pamba kwa sasa. Aidha, tunataka kujua zimechukuliwa hatua gani kuhusiana na kupatikana kwa wanunuzi wa pamba ambao pamoja na bei kuwa ndogo baadhi ya maeneo hakuna wanunuzi mpaka sasa.

9.3 Bodi ya Kahawa na Kuzorota kwa Kilimo cha Kahawa Nchini

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa katika mwaka 2011 ni kwamba uzalishaji wa zao la kahawa ulipungua kutoka tani 60,575 mwaka 2010 hadi tani 32,304 mwaka 2011 sawa na upungufu wa asilimia 88. Sababu zilizotolewa kwa kushuka kwa uzalishaji ni pamoja na kupungua kwa mvua za vuli katika mikoa ya Kagera na Mbeya na matumizi duni ya Pembejeo.

Mheshimiwa Spika,
sina hakika kama Tume ya Mipango hutembelea mikoa husika na kubaini sababu mahsusi za kushuka kwa uzalishaji wa zao la kahawa. Hii ni kwa sababu, inatoa sababu za jumla mno kiasi cha kushindwa kujua kiini cha tatizo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na sababu za tume ya Mipango, ni kwamba uzalishaji wa kahawa umepungua kwa sababu baadhi ya wakulima wamejitoa kwenye kilimo cha kahawa. Ukweli ni kwamba wakulima wengi wa kahawa katika jimbo la Vunjo na hasa katika eneo la Kilema Mkoani Kilimanjaro ambapo ndipo kilimo cha kahawa nchini kilipoanza, wamekatishwa tamaa ya kuendelea na uzalishaji baada ya vyama vya ushirika na vya msingi kufilisiwa na hivyo kushindwa kuwapatia pembejeo na pia kushindwa kununua kahawa ya wakulima kwa bei nzuri.

Mheshimiwa Spika, kutokana na hali hii wakulima hasa katika vijiji vya Kilema Pofo na Masaera katika jimbo la vunjo wameng’oa miti ya kahawa na badala yake wameanza kilimo cha nyanya, kabichi, hoho na matango ambapo kwa maoni yao kina tija zaidi kuliko kahawa. Aidha wananchi wengi wa mkoa wa Kilimanjaro wamejikita zaidi kwenye kilimo cha Ndizi na hivyo kupunguza kasi ya kilimo cha kahawa. Tatizo hili linaweza kuwa ni kubwa kwa maeneo mengine yanayolima kahawa nchini kama mkoa wa Kagera. Kama Serikali itaendelea kutokuwa makini na zao la kahawa kama ilivyo sasa, kuna hatari kubwa ya zao la kahawa kuondoka kwenye safu ya mazao ya biashara yanayoliingizia taifa hili fedha nyingi za kigeni.

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani itaka Serikali kutoa maelezo katika bunge hili, kuwa bodi ya Kahawa imechukua hatua gani katika kuhakikisha kilimo cha Kahawa kinafufuliwa hapa nchini ambacho kwa sasa kimezorota ?

Mheshimiwa Spika, Kambi ya upinzani inaitaka Serikali kutoa tamko sasa kama kuna haja ya kuendelea kuwa na bodi hizi za mazao wakati zimeshindwa kutatua matatizo ya wakulima, Pili, Serikali inatoa kauli gani kuhusu matumizi ya kifujaji yanayofanyika katika bodi hizi .

10. VITUO VYA UTAFITI VYA KILIMO

Mheshimiwa Spika, utafiti wa kilimo ndio msingi wa mapinduzi ya kilimo endelevu chenye tija kwa mkulima na kwa Taifa. Kambi ya Upinzani, inaitaka Serikali kuviendeleza vituo vya utafiti wa kilimo kwa kuvipatia fedha na vifaa ili viweze kukamilisha tafiti za kilimo kwa maendeleo ya kilimo chetu.

Mheshimiwa Spika, tunasema hivi kwa sababu baadhi ya vituo vya utafiti viko katika hali mbaya kwa sababu ya kukosa fedha za kuendeshea tafiti na kuwalipa watumishi. Kwa mfano, Kituo cha Utafiti cha Mikocheni, Dar es Salaam hakikupatiwa fedha kilizoomba katika bajeti ya 2011/2012 kwa ajili ya utafiti wa minazi, huku wafanyakazi wakilalamikia maslahi duni na magari chakavu. Aidha, kituo hiki kimekuwa hakifanyi kazi (dormant) kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inashangazwa na uwepo wa kituo hiki na Serikali inaendelea kuwalipa watumishi wakati haipeleki fedha za maendeleo na hivyo kufanya kituo hiki kushindwa kufanya kazi. Hali kama hii imesababisha kilimo cha minazi kufa.

Mheshimiwa Spika,
Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kueleza Bunge hili, inawalipa watumishi wa kituo hiki kwa kazi gani?
Mheshimiwa Spika,
kambi ya upinzani inaitaka Serikali kueleza hali ya maendeleo ya vituo vingine vya utafiti wa kilimo nchini na mikakati ya kuviboresha ili kuleta mapinduzi ya Kilimo hapa nchini.

11. KILIMO CHA UMWAGILIAJI

Mheshimiwa Spika,
mwaka 2010 Serikali ilijiwekea lengo la kufikia hekta milioni moja za eneo la umwagiliaji kufikia mwaka 2015, mpaka kufikia julai mwaka 2011 jumla ya hekta 345,690 zilikuwa zimekamilika na serikali ikajiwekea lengo la kuongeza hekta 40,000 ili kufikia hekta 385,690 kufikia mwaka 2012, mpaka sasa jumla ya hekta 17,824 zinatarajiwa kukamilika ikiwa ni tofauti ya hekta 22,176 ya lengo la serikali lililoombewa fedha mwaka wa fedha 2011/2012.

Mheshimiwa Spika, kutokana na kasi ndogo ya ukamilishaji wa skimu mbali mbali za umwagiliaji ni dhahiri kuwa lengo la serikali la kufikia hekta milioni 1,000 ,000 ifikapo mwaka 2015 ni ndoto . Aidha kambi ya upinzani inapenda kuishauri Serikali yafuatayo ; 1. Juhudi kubwa za Serikali sasa zihamishiwe kwenye kilimo cha umwagiliaji, kwani pamoja na kutolewa kwa pembejeo na zana ni dhahiri kuwa bila juhudi hizo kuhamishwa katika kilimo cha umwagiliaji mapinduzi ya kijani hayataweza kutokea. 2. Serikali itoe mikopo kwa sekta (wakulima) binafsi kwa ajili ya kutafuta vyanzo vya maji, kuchimba visima, kuvuna maji ya mvua na kujenga mabwawa na malambo. 3. Juhudi kubwa ziongezwe katika kutafuta vyanzo vipya vya maji ili kufanikisha kilimo cha umwagiliaji.

11.1 Utekelezaji wa Miradi ya DASIP

Mheshimiwa Spika,
bado miradi kadhaa inayotekelezwa chini ya “District Agricultural Sector Investment Program (DASIP) haijatekelezwa wakati Programu hii inatarajia kumaliza muda wake mwaka huu 2012. Hii ina kwamba, kuna uwezekano mkubwa kabisa wa fedha za mradi kurudishwa na hivyo kutowanufaisha wananchi.

Mheshimiwa Spika,
kwa taarifa zilizopo ni kwamba kukwama kwa utekelezaji huu wa mradi kunatokana na kiburi cha Afisa wa kitengo cha Manunuzi katika Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika, Ndugu Burhani Shabani. Afisa huyu ni mng’ang’anizi wa madaraka na hivyo akitoka ofisini anafunga shughuli zote za kimaamuzi hadi yeye mwenyewe awepo.

Mheshimiwa Spika,
kutokana ukiritimba kiutendaji, kati ya miradi 20 ya umwagiliaji ya DASIP Kanda ya Ziwa ni miradi 3 tu iliyotekelezwa hadi sasa. Miradi ya Masoko Mkakati yaliyokuwa yajengwe katika wilaya za Tarime, Karagwe na Kasulu hayajajengwa hadi sasa. Pikipiki za mradi zilizokuwa zigawiwe kwa wadau wa kilimo kanda ya ziwa hazijagawiwa hadi sasa. Power Tillers za mradi Mwanza hazijigawiwa hadi sasa.

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kulieleza Bunge kwanini miradi hiyo imeshindwa kutekelezwa hadi programu hii inakaribia kumalizika?

12. MIGOGORO KATIKA SEKTA YA KILIMO

Mheshimiwa Spika, tumeshuhudia migogoro mingi katika maeneo mengi nchini baina ya makundi mbali mbali inayohusiana moja kwa moja na shughuli za kilimo, migogoro hiyo ni kama ifuatavyo;

12.1 Migogoro kati ya Wakulima na Wafugaji

Mheshimiwa Spika, Migogoro ya aina hii imetokea katika maeneo kama Kilosa, Kilombero, Ikwiriri, Kiteto,Kagera, na migogoro hii pamoja na sababu nyingine nyingi kwa kiasi kikubwa inasababishwa na sababu hizi; a) Serikali kushindwa kutenga maeneo maalum kwa ajili ya kilimo na ufugaji. b) Serikali kutokufanya maandalizi ya kutosha kabla ya kuwahamisha wafugaji kwenda katika maeneo yaliyotengwa ikiwemo miundombinu kwa ajili ya ufugaji kama vile majosho na malambo. c) Utendaji mbovu wa watendaji wa serikali wakiwemo watendaji wa vijiji na kata na polisi kwa upande mwingine. Watendaji hawa wamekuwa wakipokea rushwa na hivyo kupendelea upande mmoja.

Mheshimiwa Spika,
kutokana na migogoro iliyokithiri kati ya wakulima na wafugaji Kambi ya upinzani inajiuliza hivi mbona tumeweza kutenga maeneo kwa ajili ya wanyama pori tunashindwa nini kuwatengea maeneo wakulima na wafugaji wetu? tunapenda kutoa ushauri kwa Serikali kama ifuatavyo; a) Kutengwa maeneo maalum kwa ajili ya wakulima na wafugaji yanayokidhi mahitaji ya makundi hayo. Aidha, maeneo ya wafugaji yawe na miundombinu muhimu kama majosho, malambo ya maji, maeneo yenye malisho na yasiyo kuwa na wadudu au wanyama hatari kwa mifugo. b) Serikali iwawajibishe viongozi wabovu na wakulima au wafugaji wanaokiuka sheria baada ya kutengewa maeneo.

12.2 Migogoro baina ya Wawekezaji na Wananchi

Mheshimiwa Spika, mgogoro huu kati ya wananchi na wawekezaji katika masuala ya ardhi na kilimo umetokea mara kwa mara tangu nchi yetu ilipopata uhuru. Migogori hii ni kama ili iliyotokea Kiru, Mbarali, Arumeru n.k.Pamoja na sababu nyingine zinazosababisha migogoro hii ni pamoja na ; a) Mikataba mibovu kati ya Wawekezaji na Serikali bila ya kuwashirikisha wananchi wanaoendesha shughuli zao katika maeneo wanayopewa wawekezaji. b) Wawekezaji kuhodhi ardhi bila kuiendeleza na hivyo kuwashawishi wananchi kuvamia kwa nia ya kutaka kufanya shughuli zao ili kukidhi mahitaji yao. c) Uwekezaji katika kilimo kutowanufaisha wananchi wanaozunguka eneo husika kama kuwapatia huduma za kijamii kama vile maji, shule, zahanati, barabara na ajira kwa wazawa. d) Sera au mkataba isiyo wazi kwa pande zote juu ya umiliki wa maeneo husika hivyo kila upande kudai na kuamini kuwa eneo linalobishaniwa ni la kwake.

Mheshimiwa Spika,
kutokana na migogoro hii ya wakulima na wawekezaji kambi ya upinzani inapendekeza yafuatayo; a) Kuwepo na ushirikishwaji mkubwa wa wananchi katika makubaliano na mikataba inayofanywa kati ya wawekezaji na Serikali. b) Serikali itoe fidia ya ardhi yenye thamani sawa na ardhi anayohamishwa mwananchi, fidia ya mali inayopotea na usumbufu unaotokea kutokana na uwekezaji utakaofanywa. c) Uwekezaji uwe ni wa kuwanufaisha wananchi kwa kutoa huduma kwa wananchi kama vile kujenga shule, barabara, zahanati, maji na kutoa ajira kwa wananchi. d) Misimaha ya kodi kwa wawekezaji iondolewe ili kuongeza pato la taifa na halmashauri husika. e) Wawekezaji wanaoshindwa kuendeleza ardhi wanyang’anywe na kurudishiwa wananchi.

13. VYAMA VYA MSINGI NA USHIRIKA

Mheshimiwa Spika, Vyama vya Msingi na Ushirika viliwasaidia sana wakulima hasa wa mazao ya biashara katika kuwapatia wakulima pembejeo na masoko kwa mazao yao. Hata hivyo vyama vya msingi na ushirika kwa ajili ya biashara ya mazao ya kilimo umedhoofika sana hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa utafiti wa Prof. Sam Maghimbi[1] wa mwaka 2010, juu ya Vyama vya Ushirika, ni kwamba vyama vya ushirika vimefilisika kutokana na madeni mengi na kwamba ni vyama wili tu vya Kagera Cooperative Union (KCU) na Karagwe District Cooperative Union (KDC) vyenye afadhali kwa kuwa na fedha kidogo za kununua mazao ya wakulima.

Mheshimiwa Spika, vyama hivi vimefilisika na vingine vimeanza mchakato wa kuuza majengo yake ili kulipa madeni. Kwa mfano Kilimanjara National Cooperative Union (KNCU) kimeanza mchakato wa kuuza majengo yake ili kukinusuru kiwanda cha kukoboa kahawa (TCCCO) kinachodaiwa zaidi ya shilingi milioni 757[2].

Mheshimiwa Spika,
Kambi ya upinzani haioni kama kuuza majengo ya chama hicho ni suluhisho la kudumu la madeni ya chama hicho, na badala yake ni hatua ya kukiua kabisa chama hicho.

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kutoa tamko katika bunge hili kuwa ina mkakati gani juu ya kuvifufua vyama vya ushirika vya msingi vya mazao ya biashara ambapo miaka ya nyuma ndivyo vilivyokuwa mtetezi na msaidizi wa haraka kutatua matatizo ya wakulima?

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inataka kujua ; ni nini mchango wa taaluma ya Ushirika inayotolewa na Chuo Kikuu Kishiriki cha Ushirika na Stadi za Biashara (MUCCOBS) hapa nchini ikiwa ushirika hasa katika mazao ya biashara unazidi kudimia ?

14. MWENENDO WA KIBAJETI KATIKA WIZARA

Mheshimiwa Spika,kwa mujibu wa utafiti wa Dkt. Damian M. Gabagambi[3] (2011) kuhusu Mgawanyo wa Kibajeti katika Sekta ya Kilimo nchini ni kwamba kwa ujumla bajeti ya matumizi ya kawaida katika Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika imekuwa inaongezeka wakati bajeti ya maendeleo katika Wizara hii imekuwa inapungua. Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa utafiti huu, mwenendo huo sio mzuri kwa kuwa unakwenda kinyume na ari ya kuendeleza kilimo. Hata hivyo pamoja na fedha za maendeleo kupungua, asilimia 90 ya bajeti ya maendeleo ni fedha za nje kwa maana ya mikopo na misaada. Hii ina maana kwamba Serikali hutumia fedha kidogo sana kutoka mapato yake ya ndani katika sekta ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika,
kwa mwenendo huu, ni dhahiri kwamba ni vigumu kufanya maboresho endelevu katika Sekta ya Kilimo. Vilevile ni ishara ya wazi kuwa Serikali haijaweka kipaumbele katika Sekta ya Kilimo ambacho zaidi ya asilimia 75 ya Watanzania wanakitegemea. Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kutoa taarifa katika Bunge hili kwamba ina mpango gani na Kilimo cha Tanzania? Pili, endapo fedha za wahisani hazitakuwepo, Serikali ina mikakati gani ya kuendeleza Kilimo nchini kwa kutumia fedha zake za ndani?

15.
HITIMISHO

Mheshimiwa Spika,
ni wazi kuwa nchi yetu haiwezi kupata maendeleo endelevu bila ya kilimo. Kuna umuhimu sasa kilimo kupewa kipaumbele si tu kwa nadharia, kama ilivyo sasa bali kwa vitendo na uwajibikaji. Pamoja na umuhimu wa zana na pembejeo za kilimo katika maendeleo ya kilimo, nguvu zaidi inatikiwa ielekezwe kwenye upatikanaji wa maji ya kutosha ili kuongeza kasi ya kilimo cha umwagiliaji ambacho hakiathiriwi sana na msimu au mabadiliko ya hali ya hewa. Kwa kufanya hivyo, Taifa litajihakikishia usalama wa chakula na pia litajipatia fedha za kigeni kwa kuuza ziada ya mavuno.

Mheshimiwa Spika kwa niaba ya kambi ya Upinzani naomba kuwasilisha.
…………………….
ROSE KAMILI SUKUM (MB)
MSEMAJI MKUU WA KAMBI RASMI YA UPINZANI
WIZARA YA KILIMO, CHAKULA NA USHIRIKA
20 JULAI, 2012

[1] Prof. Sam Maghimbi kwa sasa ni Mkuu wa Kitivo cha Humanitia na Sayansi za Jamii katika Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (DUCE) [2] Habari hii ni kwa mujibu wa Gazeti la Mwananchi la Julai 8, 2012 [3] Dkt. Damian Gabagambi ni Mtafiti na Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine – Morogoro.
 
Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee napenda kumshukuru Kiongozi wa Kambi ya Upinzani na Mwenyekiti wa Chama makini cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Makamanda wenzangu wa chama hiki makini cha watu. Aidha napenda kuwashukuru Watanzania wote wenye mapenzi mema na nchi yetu.


KUMBE YALE YALIYOKO MAHAKAMANI NI HUYO MKUU NDIO ANAYECHEZA NAYO? UBARIKIWE SANA KAMNDA MBOWE KWA UAMUZI WAKO HUU WA BUSARA SILAA HATUFAI ENDELEEN KUMUWEKA UCHI ILI ARUDI KANISANI TUJE KUKEMEA MAPEPO YAKE
 
ingesaidia sana ungechuja yale ya msingi sio kila mtu ana muda wa kusoma taarifa ndefu.

kile uchokiona kina maslahi ya wengi kuliko kingine kwenye taarifa hiyo ungetupa na sisi.

Niko busy sina muda wa kusoma.
 
ingesaidia sana ungechuja yale ya msingi sio kila mtu ana muda wa kusoma taarifa ndefu.

kile uchokiona kina maslahi ya wengi kuliko kingine kwenye taarifa hiyo ungetupa na sisi.

Niko busy sina muda wa kusoma.

Hapo kwenye red kwani wewe ni nani humu?
 
Thanks Kamanda Tumaini Makene, but heading ingekuwa "Bajeti mbadala ya upinzani kuhusu wizara ya kilimo na chakula", hilo la kuwalipua hao vibaka ikawa kama sehemu ya taarifa ya bajeti!
by the way, big up kaka!
 
Last edited by a moderator:
ingesaidia sana ungechuja yale ya msingi sio kila mtu ana muda wa kusoma taarifa ndefu.

kile uchokiona kina maslahi ya wengi kuliko kingine kwenye taarifa hiyo ungetupa na sisi.

Niko busy sina muda wa kusoma.

Na we si upost yako yenye aya mbili kama ile ya ndago? Porojo mingiiiiiiiiiiiii
 
ingesaidia sana ungechuja yale ya msingi sio kila mtu ana muda wa kusoma taarifa ndefu.Kile uchokiona kina maslahi ya wengi kuliko kingine kwenye taarifa hiyo ungetupa na sisi.

Niko busy sina muda wa kusoma.

Kwa sababu ya passion ya kuzalisha, kusambaza na kutoa habari, nitakuwekea hapa chini. Lakini hata hivyo nafikiri kama wewe ni mvivu wa kusoma, basi automatically unakuwa ni mvivu wa kufikiri, conclusion yake ni kwamba umejiondolea sifa ya kuwa Great Thinker. Karibu usome hapa;

9.1 Bodi ya Korosho na Matumizi Mabaya ya Fedha za Wakulima
Mheshimiwa Spika, kwa kukazia hoja ya Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, naomba nitoe mfano wa Bodi ya Korosho jinsi inavyowanyonya wakulima wa Korosho katika Mikoa ya Lindi, Mtwara,Pwani na Ruvuma kwa kujilipa posho nyingi na marupurupu mengine huku wakiwaacha wakulima wa korosho wakiteseka na kuhangaika huku na huko kama kondoo wasio na mchungaji bila kutatua matatizo yao.

Mheshimiwa Spika
, bodi ilipokea kiasi cha shilingi bilioni 2 kati ya mwezi Oktoba 2011 na Januari 2012 kutokana na ushuru wa mazao ya nje(Export levy) ya korosho kwa msimu wa 2010/2011. Kiasi hicho kilikuwa ni kwa ajili ya shughuli za kuendeleza tasnia ya Korosho nchini.

Mheshimiwa Spika,
kwa masikitiko makubwa fedha hizo hazikutumika kufanya shughuli kama ilivyotarajiwa na badala yake zilitumika kugharamia vikao vya bodi ya wakurugenzi na safari za viongozi (management ya bodi) ambazo hazijaleta tija kwa tasnia nzima kama ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, hayo yanapata ushahidi kutokana na matumizi ya kulipa posho kwa wajumbe wa bodi wanaounda Kamati ya ajira na uwekezaji ambayo wajumbe wake ni wanne, lakini aliwekwa na mke wa mjumbe katika malipo.

Mheshimiwa Spika, kwa kikao cha siku moja kilichofanyika tarehe 29/11/2011 wajumbe wa bodi hiyo walilipwa posho kama ifuatavyo:

1. Mh. J. Bwanausi – Mjumbe wa Bodi: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 1,550,000/=, ikiwa shilingi 750,000/= ni posho ya kawaida (Per diem) na shilingi 800,000 ni “working session” kama ilivyoandikwa kwenye fomu ya malipo.

2.
Mh. Anna M. Abdallah – M/Kiti wa Bodi ya Wakurugenzi: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 1,800,000/= kwa mchanganuo ufuatao: Posho ya kikao shilingi 500,000/=, Usafiri shilingi 300,000/= Posho ya kawaida (Per diem) shilingi 900,000/= na Usafiri Dar es Salaam shilingi 100,000/=

3. Mh. Jerome Bwanausi – Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi: Huyu alilipwa kwa mara nyingine tena kwenye kikao hicho hicho jumla ya shilingi 1,550,000/= ikiwa posho ya kikao ni shilingi 400,000/=, Usafiri wa Ndege shilingi 300,000/=, Posho ya kawaida(Per diem) shilingi 750,000/= na Usafiri Dar es Salaam shilingi 100,000/=

4.
Mh. Mudhihir M. Mudhihir – Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 1,550,000/= ikiwa posho ya kikao ni sh. 400,000/=, Usafiri wa Ndege sh. 300,000/= Posho ya Kawaida(Per diem) sh. 750,000/=, Usafiri Dar es Salaam sh. 100,000/=

5.
Mrs. Mudhihir M. Mudhihir – Mke wa Mh. Mudhihir M. Mudhihir: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 875,000/= kwa mchanganuo ufuatao: Posho ya kikao sh. 200,000/=, Usafiri sh. 300,000/= Posho ya kawaida (Per diem) sh. 375,00/=

Mheshimiwa Spika,
Jumla ya fedha zote zilizolipwa (kwa watu watano) katika kikao hiki cha wakurugenzi wa Bodi ya Korosho cha tarehe 29/11/2011 ni shilingi 7,325,000/=

Mheshimiwa Spika, licha ya matumizi ya fedha hizi kuwa hayana tija kwa kuwa matatizo ya wakulima wa korosho hayajapatiwaufumbuzi hadi sasa, utaratibu walioutumia wajumbe hawa kujipatia fedha hizi una dalili za kifisadi ndani yake. Hii ni kwa sababu mke wa Mh. Mudhihir M.Mudhihir ambaye si mjumbe wa kikao aliingia kwenye kikao na kulipwa posho. Utaratibu uliotumika kumlipa mke wa Mudhihir haueleweki na hata viwango vilivyotumika kukokotoa malipo yake pia havifahamiki.

Mheshimiwa Spika, dalili ya ufisadi mwingine katika bodi hii, ni kwa Mjumbe wa bodi Mh. Jerome Bwanausi kulipwa posho hiyo mara mbili. Katika fomu za malipo kwa Mh. Bwanausi, fomu moja ameandika jina lake kwa kifupi yaani J. Bwanausi na tarehe ya kuchukua fedha ameandika ni tarehe 28/11/2011 wakati katika fomu ya pili ya malipo ameandika jina kamili yaani Jerome Bwanausi na tarehe ya kuchukua fedha kaandika 29/11/2011.

Mheshimiwa Spika, mazingira kama hayo, yanaibua hisia kuwa Mh. Bwanausi alijipatia fedha hizo kwa njia ya udanganyifu na hivyo kuwaaminisha watu kuwa alitumia nafasi yake kama mjumbe wa bodi ya korosho kuchukua fedha za wakulima wanyonge wa korosho.

Kambi ya upinzani, tunaitaka serikali kutoa majibu juu ya bodi hizi za mazao na utaratibu wa kulipana posho ukoje?Aidha tunamtaka mkaguzi na mthibiti Mkuu wa serikali kufanya ukaguzi maalum (special audit) kwenye matumizi ya bodi hii .
 
Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee napenda kumshukuru Kiongozi wa Kambi ya Upinzani na Mwenyekiti wa Chama makini cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Makamanda wenzangu wa chama hiki makini cha watu. Aidha napenda kuwashukuru Watanzania wote wenye mapenzi mema na nchi yetu.


KUMBE YALE YALIYOKO MAHAKAMANI NI HUYO MKUU NDIO ANAYECHEZA NAYO? UBARIKIWE SANA KAMNDA MBOWE KWA UAMUZI WAKO HUU WA BUSARA SILAA HATUFAI ENDELEEN KUMUWEKA UCHI ILI ARUDI KANISANI TUJE KUKEMEA MAPEPO YAKE

Ovyo kabisa mkitaka kuombea mapepo wakina nape na kina vasko da gama wana mapepo sugu
 
Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee napenda kumshukuru Kiongozi wa Kambi ya Upinzani na Mwenyekiti wa Chama makini cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Makamanda wenzangu wa chama hiki makini cha watu. Aidha napenda kuwashukuru Watanzania wote wenye mapenzi mema na nchi yetu.


KUMBE YALE YALIYOKO MAHAKAMANI NI HUYO MKUU NDIO ANAYECHEZA NAYO? UBARIKIWE SANA KAMNDA MBOWE KWA UAMUZI WAKO HUU WA BUSARA SILAA HATUFAI ENDELEEN KUMUWEKA UCHI ILI ARUDI KANISANI TUJE KUKEMEA MAPEPO YAKE


Kwani hili ulilozungumzia hapa lipo kwenye maelezo hapo juu au limetoka wapi
 
ingesaidia sana ungechuja yale ya msingi sio kila mtu ana muda wa kusoma taarifa ndefu.

kile uchokiona kina maslahi ya wengi kuliko kingine kwenye taarifa hiyo ungetupa na sisi.

Niko busy sina muda wa kusoma.

Uko busy kutengeneza propaganda za kuichafua CDM na kunyonga haki za walalahoi?
 
Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee napenda kumshukuru Kiongozi wa Kambi ya Upinzani na Mwenyekiti wa Chama makini cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Makamanda wenzangu wa chama hiki makini cha watu. Aidha napenda kuwashukuru Watanzania wote wenye mapenzi mema na nchi yetu.


KUMBE YALE YALIYOKO MAHAKAMANI NI HUYO MKUU NDIO ANAYECHEZA NAYO? UBARIKIWE SANA KAMNDA MBOWE KWA UAMUZI WAKO HUU WA BUSARA SILAA HATUFAI ENDELEEN KUMUWEKA UCHI ILI ARUDI KANISANI TUJE KUKEMEA MAPEPO YAKE


Hii iko kwenye hotuba hapo juu au umeamua kujiandikia tuu kupoteza lengo
 
ingesaidia sana ungechuja yale ya msingi sio kila mtu ana muda wa kusoma taarifa ndefu.

kile uchokiona kina maslahi ya wengi kuliko kingine kwenye taarifa hiyo ungetupa na sisi.

Niko busy sina muda wa kusoma.
Sasa unatuambia sisi ili tufanyeje? Tunajua wazi kuwa huna muda wa kusoma kama walivyo Magamba wenzako wanaopitisha mambo kwa kuitikia "Ndiyooooooooooooooo" baada ya kugutuka usingizini! Bora wenzio huwa wamesinzia kuliko wewe unayekosa muda wa kusoma kwa kumburudisha m.k.w.e.r.e. usiku kucha!
 
Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee napenda kumshukuru Kiongozi wa Kambi ya Upinzani na Mwenyekiti wa Chama makini cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Makamanda wenzangu wa chama hiki makini cha watu. Aidha napenda kuwashukuru Watanzania wote wenye mapenzi mema na nchi yetu.


KUMBE YALE YALIYOKO MAHAKAMANI NI HUYO MKUU NDIO ANAYECHEZA NAYO? UBARIKIWE SANA KAMNDA MBOWE KWA UAMUZI WAKO HUU WA BUSARA SILAA HATUFAI ENDELEEN KUMUWEKA UCHI ILI ARUDI KANISANI TUJE KUKEMEA MAPEPO YAKE

we ni mchungaji wa wachawi au wazinzi mbona upo biased sana
 
Halafu hao watu wa kusini bado tu wanag'ang'ana na magamba! hawajui ukombozi ni nini!
 
ingesaidia sana ungechuja yale ya msingi sio kila mtu ana muda wa kusoma taarifa ndefu.

kile uchokiona kina maslahi ya wengi kuliko kingine kwenye taarifa hiyo ungetupa na sisi.

Niko busy sina muda wa kusoma.
Kama huna muda kilichokuleta kwenye hii thread nini?
 
9.1 Bodi ya Korosho na Matumizi Mabaya ya Fedha za Wakulima

Mheshimiwa Spika,
kwa kukazia hoja ya Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, naomba nitoe mfano wa Bodi ya Korosho jinsi inavyowanyonya wakulima wa Korosho katika Mikoa ya Lindi, Mtwara,Pwani na Ruvuma kwa kujilipa posho nyingi na marupurupu mengine huku wakiwaacha wakulima wa korosho wakiteseka na kuhangaika huku na huko kama kondoo wasio na mchungaji bila kutatua matatizo yao.

Mheshimiwa Spika
, bodi ilipokea kiasi cha shilingi bilioni 2 kati ya mwezi Oktoba 2011 na Januari 2012 kutokana na ushuru wa mazao ya nje(Export levy) ya korosho kwa msimu wa 2010/2011. Kiasi hicho kilikuwa ni kwa ajili ya shughuli za kuendeleza tasnia ya Korosho nchini.

Mheshimiwa Spika,
kwa masikitiko makubwa fedha hizo hazikutumika kufanya shughuli kama ilivyotarajiwa na badala yake zilitumika kugharamia vikao vya bodi ya wakurugenzi na safari za viongozi (management ya bodi) ambazo hazijaleta tija kwa tasnia nzima kama ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika,
hayo yanapata ushahidi kutokana na matumizi ya kulipa posho kwa wajumbe wa bodi wanaounda Kamati ya ajira na uwekezaji ambayo wajumbe wake ni wanne, lakini aliwekwa na mke wa mjumbe katika malipo.

Mheshimiwa Spika,
kwa kikao cha siku moja kilichofanyika tarehe 29/11/2011 wajumbe wa bodi hiyo walilipwa posho kama ifuatavyo:

1. Mh. J. Bwanausi – Mjumbe wa Bodi: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 1,550,000/=, ikiwa shilingi 750,000/= ni posho ya kawaida (Per diem) na shilingi 800,000 ni "working session" kama ilivyoandikwa kwenye fomu ya malipo.
2. Mh. Anna M. Abdallah – M/Kiti wa Bodi ya Wakurugenzi: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 1,800,000/= kwa mchanganuo ufuatao: Posho ya kikao shilingi 500,000/=, Usafiri shilingi 300,000/= Posho ya kawaida (Per diem) shilingi 900,000/= na Usafiri Dar es Salaam shilingi 100,000/=
3. Mh. Jerome Bwanausi – Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi: Huyu alilipwa kwa mara nyingine tena kwenye kikao hicho hicho jumla ya shilingi 1,550,000/= ikiwa posho ya kikao ni shilingi 400,000/=, Usafiri wa Ndege shilingi 300,000/=, Posho ya kawaida(Per diem) shilingi 750,000/= na Usafiri Dar es Salaam shilingi 100,000/=
4. Mh. Mudhihir M. Mudhihir – Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 1,550,000/= ikiwa posho ya kikao ni sh. 400,000/=, Usafiri wa Ndege sh. 300,000/= Posho ya Kawaida(Per diem) sh. 750,000/=, Usafiri Dar es Salaam sh. 100,000/=
5. Mrs. Mudhihir M. Mudhihir – Mke wa Mh. Mudhihir M. Mudhihir: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 875,000/= kwa mchanganuo ufuatao: Posho ya kikao sh. 200,000/=, Usafiri sh. 300,000/= Posho ya kawaida (Per diem) sh. 375,00/=
Mheshimiwa Spika, Jumla ya fedha zote zilizolipwa (kwa watu watano) katika kikao hiki cha wakurugenzi wa Bodi ya Korosho cha tarehe 29/11/2011 ni shilingi 7,325,000/=

Mheshimiwa Spika,
licha ya matumizi ya fedha hizi kuwa hayana tija kwa kuwa matatizo ya wakulima wa korosho hayajapatiwaufumbuzi hadi sasa, utaratibu walioutumia wajumbe hawa kujipatia fedha hizi una dalili za kifisadi ndani yake. Hii ni kwa sababu mke wa Mh. Mudhihir M.Mudhihir ambaye si mjumbe wa kikao aliingia kwenye kikao na kulipwa posho. Utaratibu uliotumika kumlipa mke wa Mudhihir haueleweki na hata viwango vilivyotumika kukokotoa malipo yake pia havifahamiki.

Mheshimiwa Spika,
dalili ya ufisadi mwingine katika bodi hii, ni kwa Mjumbe wa bodi Mh. Jerome Bwanausi kulipwa posho hiyo mara mbili. Katika fomu za malipo kwa Mh. Bwanausi, fomu moja ameandika jina lake kwa kifupi yaani J. Bwanausi na tarehe ya kuchukua fedha ameandika ni tarehe 28/11/2011 wakati katika fomu ya pili ya malipo ameandika jina kamili yaani Jerome Bwanausi na tarehe ya kuchukua fedha kaandika 29/11/2011.

Mheshimiwa Spika,
mazingira kama hayo, yanaibua hisia kuwa Mh. Bwanausi alijipatia fedha hizo kwa njia ya udanganyifu na hivyo kuwaaminisha watu kuwa alitumia nafasi yake kama mjumbe wa bodi ya korosho kuchukua fedha za wakulima wanyonge wa korosho.

Kambi ya upinzani,
tunaitaka serikali kutoa majibu juu ya bodi hizi za mazao na utaratibu wa kulipana posho ukoje?Aidha tunamtaka mkaguzi na mthibiti Mkuu wa serikali kufanya ukaguzi maalum (special audit) kwenye matumizi ya bodi hii .

 
Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee napenda kumshukuru Kiongozi wa Kambi ya Upinzani na Mwenyekiti wa Chama makini cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Makamanda wenzangu wa chama hiki makini cha watu. Aidha napenda kuwashukuru Watanzania wote wenye mapenzi mema na nchi yetu.


KUMBE YALE YALIYOKO MAHAKAMANI NI HUYO MKUU NDIO ANAYECHEZA NAYO? UBARIKIWE SANA KAMNDA MBOWE KWA UAMUZI WAKO HUU WA BUSARA SILAA HATUFAI ENDELEEN KUMUWEKA UCHI ILI ARUDI KANISANI TUJE KUKEMEA MAPEPO YAKE

watanzania wanataka kuona tunajadili hoja za kujenga mitizamo ya kusaidia jamii.je hilli katika wizara ya kilimo na chakula ni jambo la msingi kujadili?watanzania wenzangu na wana jf hebu tujadli hoja zilizoilibiliwa kwenye wizara hii kama ufisadi kwenye bodi za mao wakati wakulima wakiendelea kuteseka kuhusu bei na system za kimasoko zisizoelweka, wakurugenzi wa bodi kuridhia kutoa posho kwa mke wa mudhihir huku si murugenzi au mjumbe wa bodi, na mambo kadha wa kadha mbayo sekta hii ni muhimu kuliko hoja yako isiyo na mashiko.Kwann vijana wa jf nape hamtulii na kuchuja kujibu pumba?
 
Kwa sababu ya passion ya kuzalisha, kusambaza na kutoa habari, nitakuwekea hapa chini. Lakini hata hivyo nafikiri kama wewe ni mvivu wa kusoma, basi automatically unakuwa ni mvivu wa kufikiri, conclusion yake ni kwamba umejiondolea sifa ya kuwa Great Thinker. Karibu usome hapa;

9.1 Bodi ya Korosho na Matumizi Mabaya ya Fedha za Wakulima
Mheshimiwa Spika, kwa kukazia hoja ya Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, naomba nitoe mfano wa Bodi ya Korosho jinsi inavyowanyonya wakulima wa Korosho katika Mikoa ya Lindi, Mtwara,Pwani na Ruvuma kwa kujilipa posho nyingi na marupurupu mengine huku wakiwaacha wakulima wa korosho wakiteseka na kuhangaika huku na huko kama kondoo wasio na mchungaji bila kutatua matatizo yao.

Mheshimiwa Spika
, bodi ilipokea kiasi cha shilingi bilioni 2 kati ya mwezi Oktoba 2011 na Januari 2012 kutokana na ushuru wa mazao ya nje(Export levy) ya korosho kwa msimu wa 2010/2011. Kiasi hicho kilikuwa ni kwa ajili ya shughuli za kuendeleza tasnia ya Korosho nchini.

Mheshimiwa Spika,
kwa masikitiko makubwa fedha hizo hazikutumika kufanya shughuli kama ilivyotarajiwa na badala yake zilitumika kugharamia vikao vya bodi ya wakurugenzi na safari za viongozi (management ya bodi) ambazo hazijaleta tija kwa tasnia nzima kama ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, hayo yanapata ushahidi kutokana na matumizi ya kulipa posho kwa wajumbe wa bodi wanaounda Kamati ya ajira na uwekezaji ambayo wajumbe wake ni wanne, lakini aliwekwa na mke wa mjumbe katika malipo.

Mheshimiwa Spika, kwa kikao cha siku moja kilichofanyika tarehe 29/11/2011 wajumbe wa bodi hiyo walilipwa posho kama ifuatavyo:

1. Mh. J. Bwanausi – Mjumbe wa Bodi: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 1,550,000/=, ikiwa shilingi 750,000/= ni posho ya kawaida (Per diem) na shilingi 800,000 ni “working session” kama ilivyoandikwa kwenye fomu ya malipo.

2.
Mh. Anna M. Abdallah – M/Kiti wa Bodi ya Wakurugenzi: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 1,800,000/= kwa mchanganuo ufuatao: Posho ya kikao shilingi 500,000/=, Usafiri shilingi 300,000/= Posho ya kawaida (Per diem) shilingi 900,000/= na Usafiri Dar es Salaam shilingi 100,000/=

3. Mh. Jerome Bwanausi – Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi: Huyu alilipwa kwa mara nyingine tena kwenye kikao hicho hicho jumla ya shilingi 1,550,000/= ikiwa posho ya kikao ni shilingi 400,000/=, Usafiri wa Ndege shilingi 300,000/=, Posho ya kawaida(Per diem) shilingi 750,000/= na Usafiri Dar es Salaam shilingi 100,000/=

4.
Mh. Mudhihir M. Mudhihir – Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 1,550,000/= ikiwa posho ya kikao ni sh. 400,000/=, Usafiri wa Ndege sh. 300,000/= Posho ya Kawaida(Per diem) sh. 750,000/=, Usafiri Dar es Salaam sh. 100,000/=

5.
Mrs. Mudhihir M. Mudhihir – Mke wa Mh. Mudhihir M. Mudhihir: Huyu alilipwa jumla ya shilingi 875,000/= kwa mchanganuo ufuatao: Posho ya kikao sh. 200,000/=, Usafiri sh. 300,000/= Posho ya kawaida (Per diem) sh. 375,00/=

Mheshimiwa Spika,
Jumla ya fedha zote zilizolipwa (kwa watu watano) katika kikao hiki cha wakurugenzi wa Bodi ya Korosho cha tarehe 29/11/2011 ni shilingi 7,325,000/=

Mheshimiwa Spika, licha ya matumizi ya fedha hizi kuwa hayana tija kwa kuwa matatizo ya wakulima wa korosho hayajapatiwaufumbuzi hadi sasa, utaratibu walioutumia wajumbe hawa kujipatia fedha hizi una dalili za kifisadi ndani yake. Hii ni kwa sababu mke wa Mh. Mudhihir M.Mudhihir ambaye si mjumbe wa kikao aliingia kwenye kikao na kulipwa posho. Utaratibu uliotumika kumlipa mke wa Mudhihir haueleweki na hata viwango vilivyotumika kukokotoa malipo yake pia havifahamiki.

Mheshimiwa Spika, dalili ya ufisadi mwingine katika bodi hii, ni kwa Mjumbe wa bodi Mh. Jerome Bwanausi kulipwa posho hiyo mara mbili. Katika fomu za malipo kwa Mh. Bwanausi, fomu moja ameandika jina lake kwa kifupi yaani J. Bwanausi na tarehe ya kuchukua fedha ameandika ni tarehe 28/11/2011 wakati katika fomu ya pili ya malipo ameandika jina kamili yaani Jerome Bwanausi na tarehe ya kuchukua fedha kaandika 29/11/2011.

Mheshimiwa Spika, mazingira kama hayo, yanaibua hisia kuwa Mh. Bwanausi alijipatia fedha hizo kwa njia ya udanganyifu na hivyo kuwaaminisha watu kuwa alitumia nafasi yake kama mjumbe wa bodi ya korosho kuchukua fedha za wakulima wanyonge wa korosho.

Kambi ya upinzani, tunaitaka serikali kutoa majibu juu ya bodi hizi za mazao na utaratibu wa kulipana posho ukoje?Aidha tunamtaka mkaguzi na mthibiti Mkuu wa serikali kufanya ukaguzi maalum (special audit) kwenye matumizi ya bodi hii .

2015 nagombea ubunge mtwara vujini
 
Back
Top Bottom