bibikuku
JF-Expert Member
- Feb 16, 2011
- 832
- 495
Hii ni kwa mujibu wa gazeti la Mwananchi la leo.
Siri ya JK, madaktari Ikulu yafichuka
Monday, 12 March 2012
Kizitto Noya | Mwananchi
MADAKTARI wametoboa siri ya mazungumzo yao na Rais Jakaya Kikwete wakisema mkuu huyo wa nchi alisita kutoa jibu la moja kwa moja kama atamwajibisha Waziri wa Afya, Dk Hadji Mponda na Naibu wake, Lucy Nkya ama la, badala yake alitaka apewe muda wa kushughulikia suala hilo.
Hata hivyo, walisema pamoja na jibu hilo walikubali kurejea kazini kutokana na imani waliyonayo kwa Rais wakiamini kuwa ujumbe kuhusu madai yao umefika.
Ijumaa iliyopita, Rais Kikwete na viongozi Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), walifanya mazungumzo Ikulu yaliyokuwa na lengo la kutafuta suluhu ya mgomo huo wa pili ulioanza Machi 7, mwaka huu na kutishia kuvuruga utoaji wa huduma za afya nchini.
Rais wa MAT, Dk Namala Mkopi alisema jana kwamba suala la kutaka kuwajibishwa kwa mawaziri hao ili kuwepo imani katika mazungumzo yao na Serikali halikuwekwa bayana... Rais hakuweka bayana kama atawafukuza badala yake alisisitiza apewe muda.
Dk Mkopi aliendelea: Ila alitia shaka katika mambo mawili; alisema kuwafukuza mawaziri hao kutachelewesha utekelezaji wa madai ya madaktari kwa kuwa atakuja waziri mpya ambaye ni mgeni kwa madai hayo na pili alisema ni tabu pia kuwaacha kwa sababu ni vigumu kwao (mawaziri) kutekeleza madai ya watu wasiowaamini.
Hata hivyo, Dk Mkopi alisema mbali na hoja hizo mbili katika kuwawajibisha mawaziri hao, Rais hakuzungumzia jambo jipya zaidi ya kujadili madai ya awali ya madaktari hao na kuomba apewe muda kuyashughulikia.
Kimsingi, kilichofanyika ni imani yetu kwa Rais. Hakutueleza chochote cha ziada zaidi ya kutuomba turudi kazini kwa ahadi kwamba atashughulikia madai yetu ya msingi, alisema Mkopi na kuongeza:
Sisi tukaamua kumwamini kwa sababu yeye ni mtu wa mwisho wa kumfikishia madai yetu. Tukaona hatuna haja ya kubishana naye zaidi ya kumwachia muda alioomba kuyatekeleza madai hayo.
Alipoulizwa endapo walikubaliana na rais madai hayo yatekelezwe katika kipindi gani Dk Mkopi alijibu: Hapana... hatukukubaliana muda kwa sababu kufanya hivyo ni kuondoa imani ya mtu unayemwamini. Tuliamini tu kwamba atatekeleza madai yetu kama alivyoahidi... na hivyo ndivyo ilivyokuwa kwake alivyotuamini sisi kwamba tungerudi kazini.
Kuhusu namna Rais alivyopokea mgomo wa madai yao, Dk Mkopi alisema: Kimsingi alionyesha kusikitika sana. Anasema yeye binafsi (Rais) aliamua kuwekeza sana kwenye sekta ya afya na asingependa kuiona sekta hiyo inavurugwa.
Kabla ya juzi
Kabla ya mgomo huo uliomalizika juzi, tayari madaktari hao waligoma kwa siku 17 kuanzia Januari 20 hadi waliporejea kazini Februari 7 mwaka huu.
Katika mgomo huo, madaktari hao walitaka utekelezaji wa maslahi yao mbalimbali ikiwemo kuongezewa mishahara, kupatiwa nyumba, kuongezwa posho na pia kuwajibishwa kwa watendaji wa wizara ambao walikuwa ni Katibu Mkuu, Blandina Nyoni, Mganga Mkuu, Dk Deo Mtasiwa na mawaziri hao.
Mgomo huo ulitikisa nchi na Januari 29, mwaka huu Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alipanga kukutana na wanataaluma hao katika Ukumbi wa Karimjee, Dar es Salaam lakini waligoma jambo lililomkera na kutoa onyo la kuwafukuza kazi wote watakaoshindwa kuripoti katika vituo vyao vya kazi huku akipiga marufuku mkusanyiko wao popote nchini.
Amri hiyo haikusaidia na badala yake iliongeza makali ya mgomo na ndipo Februari 6, mwaka huu, Pinda alipoamua kuacha shughuli bungeni na kuwafuata katika Hospitali ya Taifa Muhimbili na kufanya nao mazungumzo.
Katika mkutano huo, Pinda alitangaza kuwasimamisha kazi Nyoni na Dk Mtasiwa huku akisema hatma ya Dk Mponda na Dk Nkya ilikuwa mikononi mwa Rais na kwamba angemfikishia ujumbe huku akiwaambia: Kitakachotokea nadhani mnakijua.
Lakini wiki iliyopita, akizungumzia mgomo huo wa pili alisema isingekuwa rahisi kumpa mkuu wa nchi saa 72 kuwawajibisha mawaziri hao.
Siri ya JK, madaktari Ikulu yafichuka
Monday, 12 March 2012
Kizitto Noya | Mwananchi
MADAKTARI wametoboa siri ya mazungumzo yao na Rais Jakaya Kikwete wakisema mkuu huyo wa nchi alisita kutoa jibu la moja kwa moja kama atamwajibisha Waziri wa Afya, Dk Hadji Mponda na Naibu wake, Lucy Nkya ama la, badala yake alitaka apewe muda wa kushughulikia suala hilo.
Hata hivyo, walisema pamoja na jibu hilo walikubali kurejea kazini kutokana na imani waliyonayo kwa Rais wakiamini kuwa ujumbe kuhusu madai yao umefika.
Ijumaa iliyopita, Rais Kikwete na viongozi Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), walifanya mazungumzo Ikulu yaliyokuwa na lengo la kutafuta suluhu ya mgomo huo wa pili ulioanza Machi 7, mwaka huu na kutishia kuvuruga utoaji wa huduma za afya nchini.
Rais wa MAT, Dk Namala Mkopi alisema jana kwamba suala la kutaka kuwajibishwa kwa mawaziri hao ili kuwepo imani katika mazungumzo yao na Serikali halikuwekwa bayana... Rais hakuweka bayana kama atawafukuza badala yake alisisitiza apewe muda.
Dk Mkopi aliendelea: Ila alitia shaka katika mambo mawili; alisema kuwafukuza mawaziri hao kutachelewesha utekelezaji wa madai ya madaktari kwa kuwa atakuja waziri mpya ambaye ni mgeni kwa madai hayo na pili alisema ni tabu pia kuwaacha kwa sababu ni vigumu kwao (mawaziri) kutekeleza madai ya watu wasiowaamini.
Hata hivyo, Dk Mkopi alisema mbali na hoja hizo mbili katika kuwawajibisha mawaziri hao, Rais hakuzungumzia jambo jipya zaidi ya kujadili madai ya awali ya madaktari hao na kuomba apewe muda kuyashughulikia.
Kimsingi, kilichofanyika ni imani yetu kwa Rais. Hakutueleza chochote cha ziada zaidi ya kutuomba turudi kazini kwa ahadi kwamba atashughulikia madai yetu ya msingi, alisema Mkopi na kuongeza:
Sisi tukaamua kumwamini kwa sababu yeye ni mtu wa mwisho wa kumfikishia madai yetu. Tukaona hatuna haja ya kubishana naye zaidi ya kumwachia muda alioomba kuyatekeleza madai hayo.
Alipoulizwa endapo walikubaliana na rais madai hayo yatekelezwe katika kipindi gani Dk Mkopi alijibu: Hapana... hatukukubaliana muda kwa sababu kufanya hivyo ni kuondoa imani ya mtu unayemwamini. Tuliamini tu kwamba atatekeleza madai yetu kama alivyoahidi... na hivyo ndivyo ilivyokuwa kwake alivyotuamini sisi kwamba tungerudi kazini.
Kuhusu namna Rais alivyopokea mgomo wa madai yao, Dk Mkopi alisema: Kimsingi alionyesha kusikitika sana. Anasema yeye binafsi (Rais) aliamua kuwekeza sana kwenye sekta ya afya na asingependa kuiona sekta hiyo inavurugwa.
Kabla ya juzi
Kabla ya mgomo huo uliomalizika juzi, tayari madaktari hao waligoma kwa siku 17 kuanzia Januari 20 hadi waliporejea kazini Februari 7 mwaka huu.
Katika mgomo huo, madaktari hao walitaka utekelezaji wa maslahi yao mbalimbali ikiwemo kuongezewa mishahara, kupatiwa nyumba, kuongezwa posho na pia kuwajibishwa kwa watendaji wa wizara ambao walikuwa ni Katibu Mkuu, Blandina Nyoni, Mganga Mkuu, Dk Deo Mtasiwa na mawaziri hao.
Mgomo huo ulitikisa nchi na Januari 29, mwaka huu Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alipanga kukutana na wanataaluma hao katika Ukumbi wa Karimjee, Dar es Salaam lakini waligoma jambo lililomkera na kutoa onyo la kuwafukuza kazi wote watakaoshindwa kuripoti katika vituo vyao vya kazi huku akipiga marufuku mkusanyiko wao popote nchini.
Amri hiyo haikusaidia na badala yake iliongeza makali ya mgomo na ndipo Februari 6, mwaka huu, Pinda alipoamua kuacha shughuli bungeni na kuwafuata katika Hospitali ya Taifa Muhimbili na kufanya nao mazungumzo.
Katika mkutano huo, Pinda alitangaza kuwasimamisha kazi Nyoni na Dk Mtasiwa huku akisema hatma ya Dk Mponda na Dk Nkya ilikuwa mikononi mwa Rais na kwamba angemfikishia ujumbe huku akiwaambia: Kitakachotokea nadhani mnakijua.
Lakini wiki iliyopita, akizungumzia mgomo huo wa pili alisema isingekuwa rahisi kumpa mkuu wa nchi saa 72 kuwawajibisha mawaziri hao.