Rasimu ya katiba ya kenya yalenga kuulinda uongozi uliopo!

Rutashubanyuma

JF-Expert Member
Sep 24, 2010
219,422
911,172



Katiba ya Kenya katika Ibara Na. 1 (1) inatoa tamko ya kuwa miliki wake halali ni raia wa Kenya. Je ni kweli? Ukweli upo kwenye hukumu ya Rev. Njoya and others v. Attorney General and others 1 E.A [2004] ambapo ilitamkwa bayana ya kuwa Bunge la Kenya halina mamlaka ya kutunga katiba mpya ila linaweza tu kukarabati katiba iliyopo kwa marekebisho madogo madogo. Katika hukumu tajwa mahakama ya kikatiba ya Kenya ilitamka bayana ya kuwa chombo chenye mamlaka ya kutunga katiba mpya ni Mkutano wa kikatiba ambao pamoja haukutajwa kwenye katiba iliyopo lakini kutokana na Ibara inayowamilikisha wakenya mamlaka ya kujitawala wenyewe basi ndiyo imewapa mamlaka ya kujitungia katiba.

Na ya kuwa, kupitia wawakilishi wao wenyewe waliowachagua moja kwa moja kwa shughuli ya kuiandika katiba upya kupitia mkutano wa kikatiba raia wa Kenya watakuwa wameiandika katiba hiyo mpya. Sasa viongozi wanasiasa wa Kenya kwa vile hawaamini hata kidogo raia wake katika kuiandika katiba mpya kwa kuhofu masilahi ya viongozi yatasurubiwa na wawakilishi wa walalahoi basi wakabuni mkakati wa kuipinga chenga ya mwili hukumu ya kasisi Njoya kwa kuunda sheria batili ya kumilikisha mamlaka ya Mkutano wa kikatiba kwa kamati ya wataalamu! Sasa, je Bunge linayo mamlaka ya kukasimu madaraka ya kuandika katiba kwa kamati ya wataalamu wakati Bunge hilo halina mamlaka hayo? Jibu hili tunalipata katika hukumu ya hivi karibuni ya mahakama ya kikatiba ya Kenya kwenye Hon. Justice Moijo Mataiya Ole Ketwua v. the Attorney general and others Misc. civil Application No. 1298 [2004] ambapo iliamuliwa ya kuwa chombo kitoacho haki hakiwezi kukasimu madaraka kwenye chombo kingine madaraka ambayo hakina.

Hivyo hukumu tajwa, imeharamisha uwezo wa Bunge la Kenya kuunda kamati ya wataalamu ili kubeba majukumu ya Mkutano wa kikatiba kwa sababu Bunge hilo hayo madaraka ya kuandika katiba mpya haikuwa nayo na hivyo isingeweza kukasimu madaraka ambayo haina. Pili, kamati ya wataalamu haikuwa na sifa zilizoainishwa kwenye hukumu ya kasisi Njoya ambayo ni kuchaguliwa moja kwa moja na raia wa Kenya kwa kazi hiyo ya kuiandika katiba hiyo. Bunge haliwezi kujinyakulia madaraka ya kuwachagulia raia wajumbe wa mkutano wa kikatiba kazi ambayo si ya kwake. Matokeo ya Bunge la Kenya kuunda chombo haramu cha kamati ya wataalamu ni kuwa chombo hicho kimekuwa mstari wa mbele kulinda masilahi ya waajiri wao ambao ni Bunge na kutelekeza masilahi ya raia wa Kenya. Mfano Ibara Na. 2 (3) inawazuia raia wa Kenya kuhoji uhalali wa Katiba hiyo kwenye mahakama na hivyo kuwanyima haki ya msingi na ya asili ya kudai haki pale ambapo raia (w)ataoana sheria imetungwa ili kufinya haki zake za kimsingi. Ukienda Ibara Na. 262 - (4), 9, 10 and 12 zihusuzo kipindi cha mpito baada ya katiba mpya kupitishwa kwenye kura ya maoni utaona ya kuwa Bunge na wanasiasa wa ngazi za juu ambao kwa pamoja ndiyo waajiri wa kamati ya wataalamu wamepewa ulaji wa kuhakikisha utekelezaji wa katiba mpya ambayo wao hawakuchaguliwa nayo!

Lakini rasimu ya katiba hiyohiyo imewatoa kafara wanahaki kwenye Ibara 262- (23) (2) ambapo wameambiwa hawana haki ya kwenda mahakamani au kwenye chombo chochote kile kuhoji uhalali wa wao kufutwa kazi kulingana na matakwa ya ibara na. 262 – (23) (1) ambayo inasema wanahaki itabidi wasajiliwe upya au wastaafu kwa lazima…kisa ni katiba mpya ambayo haiwahusu wanasiasa na watendaji serikalini katika kuendelea kuchapa kazi!

Ama kwa uhakika huu ni ubaguzi usio na kifani ambao watunga sheria mpya hii wanauona ila wamezuia usihojiwe kwa kupitia Ibara 2- (3) na 262- (23) (2). Hizi kufuli ni janja za nyani lakini ni kazi bure kwani mantiki muhimu ya hukumu ya Hon. Justice Moijo Mataiya Ole Ketwua v. the Attorney general and others Misc. civil Application No. 1298 [2004] imebainisha ya kuwa uhuru wa mahakama kutekeleza majukumu yake hauwezi kufungwa kwa kukosekana sheria za kuiruhusu kufanya kazi au kuwepo kwa sheria za kuifunga kufuri la kufanya kazi. Rasimu hii inayopigiwa makelele ya kuiunga mkono au kuibeza huko Kenya haitaweza kuzuia machafuko ya vita vya kikabila na ya tofauti za kimapato yaliyotokea mwaka 2008. Mwarobaini wa kero za uonevu wa kijamii ni kuwajengea mazingira mazuri raia wote kuunda katiba waitakayo kupitia mkutano wa kikatiba waliouchagua wenyewe badala ya viongozi wanasiasa kuliteka nyara zoezi hilo kwa masilahi yao binafsi.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom