Rais wetu Jakaya Kikwete anaangushwa na wateule wake!

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,268
33,040
1256624937_jk1111.jpg


WIKI chache zilizopita rafiki yangu wa muda mrefu, mtumishi wa Mungu, Dk. Norman Sigalla ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Hai, Mkoani Kilimanjaro alinitembelea ofisini kwangu kwa lengo la kutaka kufahamu nilikuwa naendeleaje! Binafsi naamini, kijana huyu ni miongoni mwa Watanzania wachache wanaofikiria sana kuhusu nchi yao, hivyo hupenda sana kukutana naye ili tupate nafasi ya kujadili hatima yetu...

Nakumbuka siku Mheshimiwa Sigalla anakuja ofisini kwangu ndio siku ambayo magazeti karibu yote nchini yalikuwa yameandika juu ya hali ya Rais wetu, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, kuwa mbaya akiwa Jukwaani huko Mwanza alikokuwa amealikwa kwenye sherehe za Kanisa la African Inland Church kutimiza miaka mia moja.

Asubuhi hiyo nikiwa na Mkuu wa Wilaya ofisini kwangu, miongoni mwa maswali niliyomuuliza Mheshimiwa Norman wakati wa mazungumzo yetu lilikuwa ni la anaionaje hali ya nchi yetu tulipotoka, tulipo na tunakokwenda! Hili ndilo swali ambalo mara nyingi napenda kuwauliza watu wanaofikiria sana kuhusu nchi.

"Kama kila mmoja wetu atatimiza wajibu wake, badala ya kumwachia Rais wetu kila kitu, basi nchi yetu itaendelea na tutafanya mambo ambayo watu watakoishi baada ya sisi watasema ni bora sisi tuliishi kabla yao…" hilo ndilo lilikuwa jibu la Norman.

Kauli hii ya Norman ndio ilikuwa chachu ya mimi kuandika makala haya unayosoma leo, nakubaliana na Mwanasiasa huyu kijana kwa asilimia mia moja kwamba kama sote tutatimiza wajibu wetu, hakika hatutahukumiwa na vizazi vitakvyokuja baada yetu na hapo ndipo hasa tatizo kubwa lililopolala, hiki ndicho kiini cha matatizo yote tuliyonayo kama nchi; watu kutotaka kutimiza wajibu wao na kutafuta watu wa kulaumu katika kila jambo.

Nchi yetu ni kubwa, lakini imegawanywa katika mikoa, wilaya, tarafa, kata na hatimaye mashina! Juu ya mgawanyiko wote huo kuna mtu mmoja mkubwa kuliko wote, huyu anaitwa Rais wa Jamhuri, huyu ndiye baba, huyu ndiye mtunzaji wa Watanzania wote milioni zaidi ya arobaini! Kwa sababu ni mtu mmoja aliyepewa mamlaka na watu wote milioni arobaini kuwaongoza, Rais hulazimika kuteua watu wa kumsaidia kuzifanya kazi zake zote, sababu hawezi kuwepo kila mahali na hatuwezi sote kumfuata Ikulu kumweleza shida zetu.

Huu si utamaduni mpya, umekuwepo duniani kwa miaka maelfu, hata enzi za Musa na safari yake ya Wana wa Israel kwenda Kanan, alilazimika kuteua wazee wa kumsaidia kazi! Uamuzi huu ulifikiwa baada ya Musa kuzidiwa na kazi, maana kila mtu alimfuata yeye, akahisi kuchanganyikiwa akili. Wazee aliowateua walimsaidia kusikiliza shida za watu na baadaye kumwakilishia yeye, huko ndiko mfumo wa serikali na wa Baraza la Mawaziri ulikozaliwa.

Kwa utaratibu huu, Rais wa Jamhuri ambaye ndiye baba wa watu wote milioni arobaini kulazimika kuteua watu wa kumwakilisha, ambao hufanya kazi ambazo angetakiwa kuzifanya yeye kwenye eneo husika; hawa huitwa Mawaziri, Makatibu Wakuu, Wakuu wa Majeshi, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya nk. wote hawa humwakilisha Rais kwenye maeneo waliyoteuliwa kuongoza.

Kama watu hawa walioteuliwa, wakimwakilisha Rais vizuri kwenye maeneo yao, Mawaziri wakajiepusha na tamaa za kujitajirisha, Majaji wakatoa haki sawa kwa wananchi, Wakuu wa Mikoa na wilaya nao wakafanya hivyo, Mkuu wa Jeshi la Polisi akatimiza wajibu wake vizuri kwa kuteua Makamanda wa polisi wa Mkoa na Wilaya wenye sifa zinazostahili badala ya upendeleo au kutoa vyeo zawadi, nchi yetu itatulia amani itadumu na maendeleo yatakuja tena kwa kasi ya ajabu. Kiini cha maendeleo ya nchi yoyote duniani ni watu kutimiza wajibu wao, hakuna jingine.

Mfano, kama Wilaya moja tu katika nchi yetu ambako mkuu wa wilaya hiyo anafanya kazi kama Rais, Mkuu wa polisi wa wilaya (OCD) ambaye katika wilaya hiyo humwakilisha Mkuu wa jeshi la polisi nchini, itakuwa na matukio mengi ya ujambazi na mauaji kwa sababu tu viongozi hawa wawili watashindwa kutimiza wajibu wao vizuri, sifa ya nchi nzima ya Tanzania na Rais wa Jamhuri ya Muungano itachafuka! Hapa ni suala moja tu linalofanya kazi, Uwajibikaji (Accountability)

Tunaposikia mauaji ya Albino yamekithiri nchini Tanzania mpaka dunia nzima inatushangaa, hili si tatizo la Tanzania nzima, limetokea katika wilaya fulani tu, lakini sifa hiyo imechafua nchi yetu kila mahali tunakopita tunaulizwa "Wewe unatoka kwenye nchi wanakouza viungo vya albino?." Hii ni aibu, lakini imetokea kwenye wilaya moja ambako inawezekana kabisa Mkuu wa wilaya husika na Mkuu wa polisi wa wilaya yake hawakutimiza wajibu wao, mwisho wa siku Rais wa nchi anaonekana hafai.

Duniani hakuna mafanikio ya mtu mmoja, kila unapoona mafanikio sehemu fulani lazima ujue kuna timu iliyohusika kuyaleta mafanikio hayo! Kuna watu wapo nyuma ya Bill Gates, wengine wala hawatajwi, kuna watu wapo nyuma ya Barrack Obama lakini hakuna anayewaongelea, kila Rais huyu anapopata mafanikio sifa zote zinamwendea yeye! Kuna watu walikuwepo nyuma ya Rais Bush, waliomshauri vibaya mpaka akaondoka madarakani kwa aibu.

Nimeamua kuandika makala hii leo kuwakumbusha viongozi wa nchi yangu, kuanzia Ikulu mpaka kwenye Shina kwamba, kama kuna kosa kubwa kiongozi anaweza kufanya ni kutoa vyeo kama zawadi au shukrani kwa mema aliyofanyiwa! Kama kuna kosa Marais wa Afrika wanafanya ni hili na ndilo limezamisha Bara la Afrika katika matatizo.

Kama tunataka kufanikiwa, inabidi tubadilike mara moja na kuanza kuteua watu kutokana na sifa zao, wanaostahili kushikilia nyadhifa wanazopewa na kumwakilisha Rais vizuri kwenye maeneo yao! Tujiepushe na kutoa vyeo au mamlaka kama zawadi, ndio maana katika nchi za wenzetu wanaofanya vizuri, hata mtu akiteuliwa na Rais ni lazima apitishwe na Bunge ili kuthibitishwa kama kweli ana sifa za kushika wadhifa huo, wengi waliteuliwa lakini baadaye uteuzi wao ukabatilishwa na Bunge.

Ningetamani sana mfumo huu siku moja uingie katika nchi zetu za Kiafrika, itatuepusha kuwa na watu waliopewa vyeo kama zawadi, mwisho wa siku wakashindwa kutimiza wajibu wao kwenye maeneo waliyopelekwa kumwakilisha kiongozi wa nchi na kuharibu sifa au kuiingiza nchi kwenye matatizo! Hili si jambo jema, inabidi liepukwe mara moja.

Juzi tu Rais ameteua mwanasheria Mkuu mpya, Makatibu wakuu, wakuu wa wilaya na kuhamisha baadhi kutoka sehemu moja kwenda nyingine. Naamini uamuzi huu ni kwa nia ya kuboresha utendaji, hajatoa vyeo zawadi na anafahamu anachokifanya ni vyema tukampa nafasi, lakini jambo moja anatakiwa kulifahamu ni kwamba mwisho wa siku wananchi watapima utendaji wake na kufanya maamuzi yao kwenye boksi la kupigia kura!

Walioteuliwa ni lazima watimize wajibu wao, lazima wamwakilishe kiongozi wa nchi vizuri kwenye maeneo yao ya kazi, uzembe kidogo ndio utamfanya Rais wetu afanye kazi nyingi kupita kiasi sababu anataka kufanikiwa, yeye ni miongoni mwa watu ambao akimtuma mtu kitu na mtu huyo badala ya kukimbia akatembea polepole, yeye huondoka akikimbia na kwenda kukichukua hicho kitu! Naamini hili ndilo limemfanya asipumzike, asipate usingizi wa kutosha, akiuke hata ushauri wa madaktari wake na kujikuta akijisikia vibaya jukwaani.

Yote haya ni kwa sababu ya watu wengi wanaomzunguka kushidwa kutimiza wajibu wao, jambo la hatari kabisa katika uongozi wa nchi, wengi wa wateuliwa huwa ni watu wa kuwaitikia viongozi "Ndio mzee" halafu kiongozi akiondoka hawafanyi lolote, mfumo wa funika kombe mwanaharamu apite, ndio hutumika zaidi katika serikali nyingi za Kiafrika.

Ninachosema mimi ni kwamba mpaka siku wateule wa Rais watakapotimiza wajibu wao ndipo maendeleo katika nchi yetu yatakuja, ni wateule wake ndio wanaomwangusha. Jipu limepasuka, siwezi kuwa adui kwa kusema ukweli.


Chanzo: Global Publishers
 
CCM kuweni makini, Paka amekubali kulala chali!

Namshukuru Mungu,

Ni mwaka mpya wa 2010, mwaka ambao Watanzania wamejiandaa kwa Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge. Ni mwaka ambao nafasi ya mtu wa kawaida kumwadhibu mtu wa juu imewadia, mwaka ambao Watanzania wengi watauza haki yao ya Kikatiba na kuchagua viongozi wasiofaa kwa sababu tu wamepewa kitu fulani na kuteseka kwa miaka mingine mitano...

Ni mwaka huu wa 2010 ndipo nalazimika kuwakumbusha ndugu zangu wa Chama Cha Mapinduzi juu ya kufungua macho pale wanapomwona Paka amekubali kulala chali, si kawaida hata kidogo kwa Paka kukubali kulala chali, akikubali basi ujue kuna jambo analolitaka na si muda mrefu sana atakuparua usoni kwa kucha zake.

Katika hili naiongelea Zanzibar na Serikali yake, Siasa zake, viongozi wake na mambo ambayo yamekuwa yakijitokeza siku za hivi karibuni. Hata ungeziba masikio vipi, ukajifungia mahali fulani eti hutaki kuwasiliana na watu kabisa, bado habari za Maalim Seif Sharif Hamadi kukubali kulala chali zitakufiki, utake usitake.

Hivi sasa minong’ono inaendelea kila kona ya nchi yetu, Watanzania nikiwemo mimi, tukijadili mabadilio ya ghafla ya Maalim Seif, Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi CUF, Mwanasiasa mwenye msimamo asiyetaka kuyumbishwa, yanalenga kwenye kitu gani? Hivi hana moja kichwani kweli? Kuna maswali mengi sana yasiyo na majibu ambayo bila shaka wenye kuyatolea ufafanuzi ni Rais Amani Karume na Seif waliokutana kwenye kikao chao Ikulu ya Zanzibar na baada ya hapo mabadiliko haya makubwa kama homa yakaanza kujitokeza.

Seif? Ndiye leo hii anasimama jukwaani na kusema Karume, Hasidi wake mkubwa katika Siasa, ambaye kwa muda mrefu alishindwa kumtambua, aongezewe muda wa kuitawala Zanzibar? Hata kama mtu akili zako hazikutoshi lazima utasema kimoyomoyo “Hapa kuna kitu!” Kuna jambo ambalo Paka anapoamua kulala chali analitaka, Seif anataka nini? Je, kweli ni maslahi ya Zanzibar peke yake au ana ajenda ya siri?

Sijui kilichoongelewa Ikulu kati ya Rais Karume na Maalim Seif, lakini ukweli mabadiliko ya Seif yamezua maswali mengi sana nchini Tanzania, Bara na Visiwani! Maswali haya yanahitaji majibu, ndio maana watu kama mimi tumeanza kuchukua hatua ya kukitahadharisha Chama Cha Mapinduzi (CCM) ili kiwe makini sana na mabadiliko haya ya Maalim Seif, kisifurahie tu Paka kulala chali, kikumbuke pia kwamba Paka ana makucha, akiamua kuyatumia atasababisha majeraha makubwa, hivyo wanapaswa kushughulika naye kwa umakini akiwa chali.

Sisemi haya kumaanisha kwamba siitakii mema Zanzibar, naipenda Tanzania kwa ujumla wake na ningefurahi iendelee kuwa nchi ya amani siku zote. Kuna uwezekano mkubwa sana kweli Maalim Seif akawa amefikia mahali wa kuweka Maslahi ya Zanzibar mbele na kupuuza maslahi yake binafsi ya kuutafuta Urais wa Visiwa hivyo, kama hiyo ndiyo nia yake, bila moja kichwani, namuunga mkono kwa nguvu zote.

Historia yake ndio itakayompa wakati mgumu sana kukubalika, watu kama mimi watakuwepo wengi ambao watataka kuwa makini naye kabla hawajathibitisha kwamba nia yake ni thabiti, hana ajenda nyingine. Ni kweli hatutakiwi kuwa watu tunaoangalia ubaya tu kwa kila jambo, ni vizuri wakati mwingine kukubali mabadiliko ya watu, lakini ni vyema zaidi kuwa makini na watu wa aina hii. Huu ndio ujumbe wangu leo kwa Chama Cha Mapinduzi.

Inawezekana Seif anaposema Rais Karume aongezewe muda ana nia njema, lakini historia yake itamponza, wengi watahisi nyuma yake kuna jambo, muda si mrefu atalipua! Kwanini leo? Kwanini miezi michache tu kabla ya Uchaguzi Mkuu? Au ndiye mtarajiwa wa kumrithi Karume atakaporejea Chama Cha Mapinduzi? Si jambo la ajabu, kama Maalim Seif yule yule aliyempinga Rais Karume kwa nguvu zote leo hii anaweza akadai aongezewe muda, sishangai akirejea Chama Cha Mapinduzi na baadaye kugombea Urais wa visiwa vya Zanzibar kupitia chama hicho.

Nayasema haya kwa sababu sijui undani wa maongezi ya Seif na Karume Ikulu, lakini jambo moja muhimu ninalota kulisema leo ni kwamba mabadiliko haya ya ‘ghafla’ ya Maalim Seif yamezua maswali mengi sana yanayohitaji majibu, Watanzania wamegoma kabisa kumwelewa, wanahisi kuna jambo, Paka hawezi kukubali kulala chali hivi hivi kama hakuna anachokitaka.

Kama mawazo ya Watanzania wengi ndio hayo, basi sina budi kuwatahadharisha waasisi wa CCM wawe makini sana na mabadiliko haya ya Seif yasije yakakiingiza Chama kwenye dhoruba ambayo mwisho wa siku itakuwa ngumu kuitanzua.

Lakini kama, Insahallah, nia ya Maalim ni njema na CCM wakijiridhisha kwa hilo, basi ni vyema kuunga mkono juhudi zake za kuwaunganisha Wazanzibar na hatimaye kuwaunganisha Watanzania wote na nchi yetu ikaendelea kuwa na amani ya kudumu na mrithi wa Karume akipatikana kwenye uchaguzi mkubwa mwezi Oktoba mwaka huu, aendeleze mema yote yatakayoachwa na aliyemtangulia.

Jipu limepasuka siwe kuwa adui kwa kusema kila ninachoamini ni ukweli.

Mungu ibariki Afrika,
Mungu ibariki Tanzania,
Mungu wabariki Watanzania,
Ahsanteni kwa kunisoma.
 
Ukitaka kumtawala mtu kirahisi muibie kila kitu, lakini mtu akishaibiwa kila kitu hatawaliki


Namshukuru Mungu

Ingawa watu wengi wanadai kwamba chanzo cha vurugu na mtafaruku ambao umekuwa ukitokea ndani ya Chama Cha Mapinduzi siku za hivi karibuni ni matokeo ya majeraha ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005, binafsi bado sijaelewa vizuri undani wa dhoruba hii, ila bado naifanyia kazi kwa nguvu kubwa ingawa sababu iliyotajwa pia inaweza kuwa na ukweli...

Ninachofahamu na ambacho ni ukweli kabisa ni kwamba, ndani ya Chama Cha Mapinduzi, chama Tawala, mambo si shwari, watu wanaparurana kwa makucha marefu! Hata kama tutakanusha kwamba mgonjwa wetu hana malaria, lakini sote tunashuhudia homa, maumivu ya kichwa na viungo nk. hivyo ni vyema kumuona daktari.

Makundi yameibuka ndani ya chama kimoja, tena Chama Tawala! Watu wameanza kukoseana adabu na hata kutukanana mbele ya hadhara, wazee wenye ushawishi katika nchi ambao siku zote Watanzania waliwaheshimu na kuwaona kama taa, nao wamegeuka! Huku wakifahamu kabisa kauli zao zina nguvu na zinaweza kuwagawa wananchi, wamefikia mahali pa kutamka hadharani maneno ya kumbeza mpaka Mwenyekiti wa chama chao, ambaye ni Rais wa nchi yetu.

Suala ambalo watu wengi wanajiuliza hivi sasa ni kwamba hivi tunakwenda wapi? Nchi yetu itakuwa na hali gani miaka kumi ijayo kama hali iitaachwa iendelee kuwa hivi? Nini lengo la watu hawa wenye ushawishi wanapochagua njia hii ya mawasiliano wanapokosoa? Kwa kweli sina jibu, bila shaka wazee kama Salim Ahmed Salim, Joseph Butiku, Mzee Joseph Sinde Warioba na wengineo wengi wanaelewa maana ya wanachokifanya.

Sijawataja majina wazee hawa kwa maana ya kuwabeza, la hasha! Ni wazee wanaoheshimika sana katika nchi yetu, mimi pia nawaheshimu mno maana historia ya nchi yetu haiwezi kuandikwa bila majina yao kutajwa! Zaidi ya hayo wanayo haki ya Kikatiba ya kuongea chochote ndani ya nchi yao ili mradi hawavunji sheria, hivyo basi, walichokifanya, kwa mtazamo wa Kikatiba si kosa na hakuna mtu anayeweza kuwashtaki kwa hilo.

Lakini ninachokiongelea hapa ni Hekima, kitu ambacho mtu hawezi kukisomea shuleni, ambacho Mfalme Suleiman alilazimika kukiomba kutoka kwa Mungu. Kitu ambacho mtu ukiwa nacho hakika utakuwa na kila kitu, kuanzia amani mpaka utajiri lakini ukikikosa mabaya yote ya dunia yatakuwa mali yako. Hiki ndicho ninachokiongelea ambacho naamini kabisa, kwa hapa tulipo, hakitumiwi vizuri sana na viongozi wenye ushawishi katika nchi yetu na kama kikiendelea kutokutumika, hakika nchi yetu itaingia kwenye machafuko muda si mrefu ujao.

Ndugu zangu,

Picha ninayoiona nchini mwetu hivi sasa, naifananisha kabisa na wazazi wanapoondoka nyumbani na kumwachia kaka mkubwa madaraka, heshima hupungua kwani mara nyingi watoto hawamwogopi mtoto mwenzao kama wanavyomwongopa baba! Watu huanza kuchelewa kurudi nyumbani, hakuna utaratibu tena, kila mtu huanza kuongea anachojua na mabishano mengi hujitokeza, huyu anataka nyanya mbili kwenye mboga, mwingine tatu ili mradi kila mtu anasema la kwake.

Naomba nijibiwe swali langu, hivi enzi zile za Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere migororo ndani ya TANU na hatimaye CCM haikuwepo? Bila shaka Salim Ahmed Salim, mzee Warioba, Butiku na wengineo wanaweza kujibu swali hili! Siamini hata kidogo kuwa wakati wa Mwalimu watu wote ndani ya chama walikuwa na mawazo ya aina moja, lazima kulikuwa na utaratibu wa kukosoana ndio maana tulikuwa hatuwezi kusikia watu wakitupiana maneno kiasi hiki, inakuwaje leo mambo yanakuwa hivi?

Naomba nielezwe kama kuna ajenda ya kutugawa Watanzania na kuifanya nchi isitawalike, jambo ambalo Watanzania walio wengi hawataki hata kulisikia! Kwanini tunacheza na amani yetu kiasi hiki? Kwanini wazee wetu wanaoheshimika ndiyo wanataka kuwa majemadari wa mgawanyiko huu? Kipi kimewasibu ambacho walikuwa hawawezi kukifanya enzi zile za Mwalimu?

Kwa maoni yao wanadai nchi haiendeshwi vizuri, hawaridhishwi na mambo yanavyokwenda, hii ina maana wanamdharau Rais aliyeko madarakani, kwa maana nyingine ameshindwa kuongoza nchi! Kauli hizi zinapotolewa na wazee wenye ushawishi, ni za hatari sana, zinatakiwa kushughulikiwa kwa nguvu kubwa ili kuhakikisha haziendelei kuvuruga nchi, kwani kila mmoja wetu anaelewa kwamba kama tunataka amani ya kudumu, vurugu sio njia ya kuipata bali mazungumzo ndani ya vikao halali vya chama au serikali.

Nini ajenda ya watu hawa? Nini kiko nyuma ya kauli zao? Siamini hata kidogo kwamba wanasema tu, lazima kuna jambo, lazima wanawasiliana na lazima wanapanga! Nani mlengwa? Rais Kikwete? Kakosea nini? Kawasahau katika utawala wake?

Wakati umefika wa kurejesha ‘oda’ katika nchi, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano anatakiwa kulielewa jambo hili, akumbuke alipoingia madarakani aliapa kuwalinda Watanzania kwa gharama yoyote ile kwa kutumia katiba, lazima sasa atimize wajibu wake! Aweke maslahi ya Watanzania mbele badala ya maslahi ya watu binafsi, akatae kuburuzwa na ikibidi awakumbushe watu kwamba yeye ni Rais na Ikulu ni mahali patakatifu. Hili likifanyika, hata kama baba hatarudi, atakuwa amerejea kupitia kwa mwanae na nchi itatawalika.

Naongea haya kama Mtanzania, mtu anayependa nchi yake kama ambavyo watu wengine pia wanavyoipenda! Na ninawasihi vijana wa nchi hii, kamwe wasikubali kutumiwa na wajanja wachache, bali waelewe Tanzania ni zaidi ya sisi na kuna vizazi vitakavyofuata baada ya sisi kuondoka, hivyo tusimame kidete kuilinda na kuitetea nchi yetu badala ya kuyumbishwa na wachache wenye moja kichwani.

Wakati nikiyasema haya nikumbushe tena jambo langu la kila siku mahali popote, walioko madarakani wawatendee haki waliowaweka kwenye nafasi zao, nawaongelea wananchi wa Tanzania! Haipendezi hata kidogo, wachache wanapoiba, kula na kushiba huku wengi wakilala na njaa na kufa kwa maradhi kwa kukosa vidonge. Kama hili litafanyika, basi juhudi zote tunazozifanya hazina maana, tusiusahau msemo usemao; Ukitaka kumtawala mtu kirahisi, mwibie kila kitu, lakini mtu akishaibiwa kila kitu hatawaliki.

Hata kama hili ndilo tatizo kubwa la wazee wetu, wanaona wachache wanashiba huku wengine wakilala na njaa, nawaomba watafute njia nzuri zaidi ya kuwasiliana iliyokuwa ikitumika siku za nyuma badala ya wanavyofanya sasa, vinginevyo kauli zao zitageuka petroli kwenye moto na mwisho wa siku tutajikuta mahali fulani tukiulizana “Tumefikaje hapa?” Na lawama nyingi zitawafuata wao, bila shaka hili wanalijua.

Jipu limepasuka, siwezi kuwa adui kwa kusema kile ninachoamini kwamba ni ukweli.

Mungu ibariki Afrika,
Mungu Ibariki Tanzania,
Ahsanteni kwa kunisoma.
 
Ni aidha tusameheane, sheria ichukue mkondo wake au tuendelee kuchafuana!

KUMRADHI: Wiki tatu zilizopita tulikuwa tukichapisha mfululizo wa maneno kutoka hotuba iliyotoka kwenye kitabu cha Nyerere kilichoitwa ‘TUJISAHIHISHE’ kilichotolewa Dar es Salaam Mei 1962, tulipomaliza, kwenye sehemu ya kutambua kazi hiyo, hatukueleza kwamba ndani ya machapisho hayo tulibadili maneno TANU, WanaTANU na wasio WanaTANU kwenda CCM na WanaMtandao na wasio WanaMtandao. Tunaomba radhi kwa usumbufu wowote uliojitokeza katika hilo.Mhariri...

Namshukuru Mungu,
Kwa maoni yangu mimi nikiwa raia wa nchi hii, mwenye haki na uhuru wa kutoa mawazo yangu, naamini mambo matatu tu niliyoyataja hapo juu ndiyo yatakayoliokoa Taifa hili na moto mkubwa unaokuja mbele yetu.

Juma na rafiki yake Martin walikuwa wameketi chini ya mti mkubwa wa Mwembe, wote wakiwa na njaa kali. Katika mazungumzo yao wakaanza kujadili ingekuwaje kama ingetokea siku moja Juma akawa tajiri na kumwajiri Martin kuwa Mhasibu wake? “Yaani wewe uniajiri mimi? Utanilipa shilingi ngapi?”

“Kwanza nilikuwa natania tu, wewe siwezi kukuajiri kama mhasibu wangu, mjanja mno, lazima utaniibia” “Naona unanitukana, yaani mimi nikuibie? Unanifananisha na mwizi?” Tayari vijana hao wawili walianza kupandisha hasira, wakafikia hatua za kutukanana wao wenyewe na kuendelea mpaka kutukaniana wazazi wao matusi ya nguoni, ugomvi mkubwa sana ukaibuka, Martin akamchoma Juma kisu cha kifuani, akafa!

Pamoja na Martin kushtakiwa kwa mauaji na baadaye kuhukumiwa kunyongwa, bado ndugu wa familia hizi zilizoishi jirani walibaki kwenye mgogoro mkubwa sana, kila siku wakawa wanagombana na kutishiana kuuana! Familia zikaingia kwenye fitina, amani ikapotea na haikujulikana ingerejea kwa njia gani.

Baadaye wazee wa kijiji waliingilia kati na kuzikalisha familia zote mbili wakizikumbusha kuwa, Juma alishakufa na asingerudi tena, Martin naye angenyongwa! Hivyo kikubwa kilichokuwepo ni kusameheana na kuendelea na maisha badala ya kuendeleza uhasama usiokuwa na tija.

Kwa kauli hiyo ya wazee, familia zikashikana mikono na ugomvi ukaisha na juhudi za kutafuta maendeleo zikachipuka tena upya, kwani kwa kipindi kirefu familia hizi zilijiingiza katika ugomvi mkubwa, jambo lililofanya zisijiingize katika mipango yoyote ya maendeleo, kazi ilikuwa ni kupandikiza chuki kwa vizazi vilivyofuata kiasi kwamba uhasama huo ungedumu mpaka milele kama wazee wasingeingilia kati.

Hebu tuangalie chanzo cha ugomvi wa Juma na Martin, ni kazi ya uhasibu ambayo kwanza haikuwepo! Ikasababisha mmoja kuitwa mwizi, baadaye wakaanza kutukanana wao na wazazi wao, suala likahama kutoka kwenye mfano wa Uhasibu na kuwa “Kwanini unanitukania wazazi wangu?”, bila shaka matusi hayo, si kazi ya Uhasibu, ndiyo yaliyompandisha hasira Martin na kujikuta akimchoma mwenzake kisu.

Kwanini nimeutoa mfano huu? Ndugu zangu, mambo yanaendelea nchini kwetu kwa hivi sasa yananitisha, yananifanya nielewe tulikotoka na tulipo lakini nisipate jibu la tunakokwenda! Hakuna asiyefahamu kwamba kuna ugomvi mkubwa unaendelea miongoni mwa watu wenye nguvu na sauti kubwa katika nchi yetu, wanaoweza kuipeleka nchi huku ama kule kama wapendavyo wao.

Ugomvi huu wa wenye nguvu ulianzia kwenye suala la Ufisadi, kwamba kulikuwa na kikundi cha watu wenye tamaa waliochota mabilioni ya fedha za wavuja jasho wa nchi hii ambao wengi ni masikini na kujitajirisha wao, hapo ndipo ugomvi huu ulipoanzia, wakapatikana wapambanaji na wapigwaji ambao nao baadaye walibadilika na kuwa wapambanaji, vita vya chini chini vikajitokeza, Watanzania wakaanza kugawanyika, Bunge letu Tukufu likagawanyika katika makundi mawili; waliounga mkono mapambano hayo na waliowaunga mkono walioitwa mafisadi kupambana na mashujaa wa vita.

Sitaki kumtaja jina mtu hapa, wanaoitwa Mafisadi wametajwa sana, nyote mnawafahamu, ni watu wenye nguvu na ushawishi mkubwa sana katika nchi yetu na wapambanaji pia mnawafahamu kwa majina, ni watu wasiokata tamaa wala kurudi nyuma katika mapambano yao, wamedhamiria kabisa kuhakikisha wanawazamisha majini wote waliojipatia utajiri kwa kuchota mali za wavuja jasho wa nchi hii, wanafanya hivi wakiamini wanazo baraka za walio wengi.

Ndugu zangu, Lazima tukubali sasa kwamba mapambano haya yanaigawa nchi yetu, unapoligawa Bunge katika makundi mawili, tayari umegawa nchi! Kwani Bunge ni chombo chenye uwakilishi wa kila mtu katika nchi hii. Jambo hili ndilo limenifanya niandike makala haya leo, sitaki kuona tunazidi kutokomea tunakotaka kwenda, ndugu zangu, kuna hatari kubwa sana mbele yetu kama hatutasimama na kujiuliza tunakwenda wapi? Na tukiona tumekosea njia ni vyema kugeuza na kurejea mwanzo wa safari yetu kujipanga upya.

Kama nilivyosema hapo juu mambo matatu yanaweza kufanyika, badala ya kuendelea na linalofanyika hivi sasa ambalo wanaoitwa mafisadi wanajaribu kwa njia zote kuwaeleza wapambanaji dhidi ya ufisadi kwamba: “Kwani wewe ni msafi?” Wanalifanya hili kwa kuibuka na mambo mbalimbali ya kuonyesha hata wanaopambana nao ni wachafu, kila mtu sasa anajaribu kumtukana mwenzake kama ilivyotokea kati ya Juma na Martin hatimaye wakachomana kisu.

Swali ninalojiuliza kichwani mwangu ni kwamba: mwisho wa siku wapambanaji na mafisadi wakishachafuana na wote kuonekana kumbe ni wachafu, ndiyo itakuwa mwisho wa vita yetu? La hasha! Wananchi wa nchi hii, ambao ndiyo waajiri wa wote waliopo madarakani, hawatakubali kufanywa wajinga, hata kama wapambanaji na mafisadi watachafuana mpaka wasionekane nyuso bado vita dhidi ya ufisadi itaendelea, ni lazima ufisadi upigwe vita kwa nguvu zote.

Nionavyo mimi la kwanza tunaloweza kufanya ni kuangalia ukweli, kamwe tusipoteze dira ya vita yetu kwa wapambanaji na mafisadi kuchafuana, ukweli ubaki pale pale, nani ni fisadi na ashughulikiwe kwa mujibu wa sheria kama itathibitika bila mashaka kwamba alifanya jambo hilo, hii itatusaidia sana kukomesha mgawanyiko na minong’ono inayoendelea ndani ya nchi yetu ambayo mwisho wa siku itakuja kuichoma petroli iliyotawanyika na nchi kulipuka katika hali ambayo hatutakuwa na uwezo wa kuuzima moto huo.

La pili ni kusema, kila mmoja wetu hajatimia, makosa yalifanyika, kama ilivyotokea kwa familia mbili nilizoziongelea hapo juu ni kusema Juma alikufa na Martin kuhukumiwa kunyongwa, hivyo tusameheane na tufungue ukurasa mpya wa maisha yetu, tuendelee na mapambano dhidi ya umasikini na asiwepo mtu wa kurudia tena makosa yaliyofanyika!

Hii ina maana ni lazima tusameheane, Mafisadi na wapambanaji dhidi ya ufisadi wapunguze hasira zao, badala ya kuendelea kuchafuana tutafute suluhisho la matatizo yetu, kwani hali ikiendelea hivi ipo siku tutauana kwa sababu ya jambo hili na tukiwa nchini Zaire, Uganda au Kenya kama wakimbizi tutasikitika sana ni kwanini hatukukaa chini na kutafuta suluhisho.

La tatu ni kuacha mambo yaendelee kama yanavyokwenda, asiwepo mtu wa kukemea, kuanzia Ikulu mpaka kijijini kwangu watu wawe kimya na Watanzania waendelee kutukanana na kuchafuana, iwe nchi ya mtu ukiamka unaweza kumwita mwenzako vyovyote vile na kumchafua utakavyo kama inavyotokea hivi sasa.

Lakini ni vizuri kukumbuka kuwa matusi haya yanayorushwa kutoka kwa makundi makubwa mawili katika nchi yetu, yanazidi kutugawa, yanazidi kututenganisha na kutufanya si wamoja tena! Nashindwa kuelewa kama kweli viongozi wa juu wa nchi yangu hawalioni suala hili na kuamua kulichukulia hatua kwa maslahi ya nchi yetu na vizazi vijavyo, amani yetu ni kitu cha muhimu sana kuliko Urais wa mwaka 2015.

Naomba niishie hapo, wakati wa kufanya maamuzi sahihi ni sasa siyo kesho, Mungu ibariki Tanzania, Jipu limepasuka siwezi kuwa adui kwa kusema ninachoamini kwamba ni ukweli. TANZANIA KWANZA.

Ahsanteni kwa kunisoma.
http://www.globalpublisherstz.com/pasua_jipu/
 
by "anaangushwa na wateule wake" what did u mean from that statement?
chukulia katika familia, kama wewe baba huimizi wajibu wako, utamwambia mtoto atimize wajibu wake?
nyie mbona mnaongea mambo ambayo hata hamfikirii? kama baba ni mwizi, atawezaje kumkataza mtoto wake asiwe mwizi wakati mtoto ana evidence ya baba kuwa ana tabia hiyo?
think clear before you just put your word like that!!
 
Kwani alilazimishwa kuteua hao watendaji wabovu?

Tanzania nayo inaangushwa na wachambuzi wenye upeo mbovu,wanaokurupuka na makala ndeeefu lakini zisizotoa majibu hata kwenye maswali mepesi.Kwa kifupi,na straight to the point,JK ni kiongozi dhaifu asiye na uwezo wa kuongoza.Kuwalaumu aliowateua ni kuwaonea kwa vile hata wangekuwa na uwezo wa aina gani wasingeweza kufanikiwa chini ya uongozi wa kiongozi.
 
aah jamani,

habari zenu wanajamii wenzangu,
kweli ninakereka na haya maneno kua JK rais wa JMT anaangushwa na wasaidizizi wake ambao yeye mwenyewe kawateua na ni yeye mwenyewe ndio mwenye mamlaka na uwezo wakuwaondoa kama hawatendi kama matarajio yake.

Rais amekua akitetewa na watu wenye fikra duni, dhaifu na dhalili.....rais ni nani alimtuma ateua marafiki zake jeshini kua wakuu wa wilaya na mikoa hapa TZ, ni nani alimtuma ateua marafiki zake wa mitaani kuwa wasaidizi wake, rais nani alimtuma ateua rafiki wa familia yake kuwa watendaji wakuu wa serikali, rais nani alimuomba ateua vizee kuwa wasaidizi wake na wabunge wakuteuliwa wakati uwezo wao wakufikiri unalingana na mtoto wa miaka tisa, ni huyu huyu rais anadaiwa kuwateuwa sijui hata aliosoma nao shule kwa sifa ya kizuri kula na rafikio kwenye utawala wa nnchi.

Rais huyu anasifika kwa kutowaangusha mapatna wake.

Kama ulijuana nae katika harakati za maisha atakupa hata Ubalozi ama ukuu wa wilaya ukale japo kwa kipindi chake.

Kifupi JK ana walakini, uteuzi wake una walakini, fikra zake zinatia shaka.....hakuna anae mwangusha ila anatuangusha Watanzania, anawaangusha waliompigia kura, anawaangusha waliomwamini..natamani asirudi tena madarakani kwa sababu ni rais dhaifu, anauza nchi na ameifanya Tanzania kurudi nyuma.
 
ni ngumu sana kuweka urafiki na udugu kwenye maswala ya kitaifa.
watu walishitushwa sana na uteuzi wake wabaraza lile la awali, na wakashangaa, akawajibu kua kelele za mlango hazimzuii mwenye nyumba kulala....kejeli na bezo zake zingelipa kama aliowakabidhi mamlaka ya uongozi kwa niaba yake wasingefanya mambo ya hovyo....
niliamini baada ya kuanguka kwa Lowassa na baraza lake la mawaziri angekuja na baraza la uhakika, angewang'oa majizi wote, asingerudia kosa...mara akawarudisha kina Kawambwa , Chiligati, Makongoro, akamleta mtu mmoja anaitwa Malima..ooh madudu matupu , akachanganya na damu ya mwanamipasho Sophia Simba..aibu kwake. angalia utendaji wa Masha na Ngeleja...hayo yote ni matusi dhidi yake, hakuna uwajibikaji, hakwepi lawama a kushindwa kuifanya nnchi kupiga hatua.
 
Na huyu ni mtumishi wa mungu na huku ni mwana siasa! atajigawa vipi? kumtumikia Mungu na jamii kama mwanasiasa?

Nadhani huyu mchungaji ndiye wa kwanza anatakiwa ang'atuke, sababu hawezi kumtumikia bwana na siasa
 
aaaah,

Hapa sio tu hao Mashosti aliowateua katika Serikali yake wanamwangusha, bali pia hata ninyi mliompa kura yeye na hao jamaa zake ana waangusha zaidi kwa kuendesha Serikali "kishikaji na ujomba mwingi" kuliko matarajio yenu!.
 
Kwani alilazimishwa kuteua hao watendaji wabovu?

Tanzania nayo inaangushwa na wachambuzi wenye upeo mbovu,wanaokurupuka na makala ndeeefu lakini zisizotoa majibu hata kwenye maswali mepesi.Kwa kifupi,na straight to the point,JK ni kiongozi dhaifu asiye na uwezo wa kuongoza.Kuwalaumu aliowateua ni kuwaonea kwa vile hata wangekuwa na uwezo wa aina gani wasingeweza kufanikiwa chini ya uongozi wa kiongozi.
you are righty, watu wengine ni kama wanatafuta, pa kutokea na mtindio wa bongo zao, huwezi ukaongea kauli kama hizo kikwete anaangushwa na wateule wake huu ni ushahidi tosha kuwa mtoa makala hii serikali ya kichwani kwake ina matatizo makubwa
 
tangu lini mpemba kwa asili yake akawa mshauri wa raisi? siyo kwamba nawabagua wapemba lakini ukweli ndo huo, siwezi kuwakumbatia pale nionapo wana kasolo, hawana asli ya uchapa kazi, zaidi kukaa mabarazani kunywa kahawa huku wakijifari kwa kilimo cha mihogo na uvuvi wa pweza, na ndiyo nchi ilitawaliwa mahakama ya kadhi mara OIC hayo hayakuwa mambo muhim kuyapa nafasi kujadiliwa wakati nchi i katika hali mbaya kiuchumi na maisha ya mwananchi mmoja mmoja
 
Kama rais anaangushwa na wateule wake, then by proxy anajiangusha mwenyewe.

Rais kama CEO wa nchi anahitaji kile kibao cha Harry Truman kilichoandikwa "The Buck Stops Here".

Ukiteua watu wanaokuangusha ina maana either hujui kuteua au huna feedback mechanism nzuri.

Either way, the final responsibility rests with the president.No excuses.
 
Ukiteua watu wanaokuangusha ina maana either hujui kuteua au huna feedback mechanism nzuri.Either way, the final responsibility rests with the president.No excuses.

Asante sana mwana JF, Kiranga, umenigusa kwa mstari huu niliounakili.

Ni kweli kabisa raisi wa Tanzania ni issue....nadhani kila mtu anamshangaaa...hata USWIS aliko....alikoenda na agenda kuwa AFRICA INAWEZA KUILISHA DUNIA...jamani hivi alisomaga kitabu cha KUSADIKIKA?

Anyway, nirudi kwenye mada. ninakubaliana na wachangiaji waliotangulia kuwa "RAISI AMEJIANGUSHA MWENYEWE". Hakuna namna ya kumtetea, hakustahili kuwepo madarakani hadi hii leo....lakini kwa sababu ya huruma ya watanzania wenzangu na haswa wale waliokaribu nae (I mean viongozi) ambao wangetakiwa wamwajibishe, hawawezi maana lengo lao ni KUSHIBA and nothing more....Kwani hadi leo

1. JK hajui kuwa anawapambe nuksi....Simba and others?

2. JK hajui kuwa wateule wake hawana qualification walizojipachika....Dr?????? Nchimbi and his counterparts?

3. JK hajua kuwa wateule wake ni "lip-service politicians"...naweza kutaja wote hapa......

4. JK hajui kuwa corruption is hard to fight in Tanzania kwa sababu his government has made it to be "functional Corruption"...kwa nini hawezi kuwashughulikia Rostamu na wengine....

Wana JF tutakao weza kwenda home TZ kupiga kura, twendeni ili tusaidie kupunguza ile degree ya kuwa submissive to our corrupt politicians.

I submit!
 
Asante sana mwana JF, Kiranga, umenigusa kwa mstari huu niliounakili.

Ni kweli kabisa raisi wa Tanzania ni issue....nadhani kila mtu anamshangaaa...hata USWIS aliko....alikoenda na agenda kuwa AFRICA INAWEZA KUILISHA DUNIA...jamani hivi alisomaga kitabu cha KUSADIKIKA?

Anyway, nirudi kwenye mada. ninakubaliana na wachangiaji waliotangulia kuwa "RAISI AMEJIANGUSHA MWENYEWE". Hakuna namna ya kumtetea, hakustahili kuwepo madarakani hadi hii leo....lakini kwa sababu ya huruma ya watanzania wenzangu na haswa wale waliokaribu nae (I mean viongozi) ambao wangetakiwa wamwajibishe, hawawezi maana lengo lao ni KUSHIBA and nothing more....Kwani hadi leo

1. JK hajui kuwa anawapambe nuksi....Simba and others?

2. JK hajui kuwa wateule wake hawana qualification walizojipachika....Dr?????? Nchimbi and his counterparts?

3. JK hajua kuwa wateule wake ni "lip-service politicians"...naweza kutaja wote hapa......

4. JK hajui kuwa corruption is hard to fight in Tanzania kwa sababu his government has made it to be "functional Corruption"...kwa nini hawezi kuwashughulikia Rostamu na wengine....

Wana JF tutakao weza kwenda home TZ kupiga kura, twendeni ili tusaidie kupunguza ile degree ya kuwa submissive to our corrupt politicians.

I submit!


Nashukuru AmaniKatoshi,

Kifupi, JK hana nguvu ya kupingana na uozo huu kwa sababu uozo huu ndio uliomuweka madarakani.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom