Rais Kikwete akutana na UNDP Administrator Bibi Helen Clark Ikulu jijini Dar es salam

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,268
33,040
Rais Kikwete akutana na UNDP Administrator Bibi Helen Clark Ikulu jijini Dar es salaam




Rais Jakaya Mrisho Kikwete akikutana na UNDP Administrator Bibi Heken Clark ikulu jijini Dar es salaam leo asubuhi
(Picha na Freddy Maro - Ikulu)

Mwenyekiti wa Kundi la Maendeleo la Umoja wa Mataifa na Mtawala Mkuu wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Bi. Hellen Clark amesema kuwa uchaguzi wa kweli kweli wa kidemokrasia siyo lazima ubadilishe chama tawala kwa sababu maana halisi ya demokrasia siyo kubadilisha vyama tawala, bali ni kuwawezesha wananchi kuwa na haki ya kuchagua baina ya vyama vinavyowania madaraka.

“Linalotakiwa ni kuwa na uchaguzi wa amani, ulio huru na wa haki kwa sababu maana halisi ya demokrasia siyo kubadilisha chama kilichoko madarakani, bali kutoa nafasi kwa wananchi kuchagua chama wanachokitaka,” amesema Mama Hellen Clark.

Bi. Clark alikuwa anazungumza na Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wakati mama huyo alipokwenda Ikulu, Dar es Salaam, kumwona Rais Kikwete leo, Jumanne, Mei 11, 2010.

Katika mazungumzo hayo, Rais Kikwete ametumia muda kumweleza Bi. Clark hali ya kisiasa na kiuchumi ilivyo nchini, na jinsi Tanzania inavyojiandaa kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika mwishoni mwa Oktoba mwaka huu.

Katika mazungumzo hayo, Bi. Clark amemweleza Rais Kikwete kuwa ipo mifano mingi hata katika nchi zilizoendelea na za kidemokrasia ambako chama kimoja kimebakia madarakani kwa miaka mingi tu.

“Chukua mfano hata wa Marekani ambako chama kimoja kinaweza kubakia madarakani kwa vipindi hata vitatu…ama chukulia mfano wa Japan ambako chama kimoja kilibakia madarakani kwa miaka mingi sana. Suala siyo kubadilisha vyama bali kutoa nafasi kwa wananchi kuchagua chama wanachokitaka,” amesema mama huyo.

Viongozi hao wawili pia wamejadili hali ya kisiasa ya Zanzibar na maendeleo ya mchakato wa maridhiano Visiwani humo, Rais Kikwete akisisitiza kuwa hali ya sasa ya kisiasa katika Zanzibar ilihitaji majawabu ya makubaliano na maridhiano.

Kuhusu hali ya uchumi nchini, viongozi hao wamekubaliana kuwa umasikini katika Bara la Afrika utapungua tu baada ya kuanza kukua kwa sekta zinazogusa moja kwa moja wananchi na hasa kilimo.

Rais Kikwete amesema kuwa katika Tanzania, sekta ambazo zinakuwa kwa haraka zaidi, yaani sekta za mawasiliano, ujenzi na madini ni sekta muhimu lazima haziwagusi wananchi wengi zaidi moja kwa moja kwa karibu zaidi kama kilivyo kilimo.

Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.

11 Mei, 2010
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom