M
MegaPyne
Guest
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Na Mwandishi Maalum, Pritoria
MWENYEKITI wa Umoja wa Afrika (AU), Rais Jakaya Kikwete, amesema umoja huo hautawavumilia viongozi wanaoingia madarakani kwa njia zisizo za kidemokrasia.
Amesema nchi za Afrika lazima ziheshimu na kulea njia ya kidemokrasia katika kupata viongozi wake.
Rais Kikwete alisema hayo jana alipokuwa akifungua rasmi kikao cha 10 cha Bunge la Afrika, kwenye ukumbi wa Bunge hilo ulioko Midrand, hapa.
Msimamo wa zamani wa kutoingilia mambo ya ndani ya nchi mwanachama hauna nafasi tena katika bara letu. Afrika sasa haiwezi kuendelea kukaa pembeni na kuangalia maadili ya kidemokrasia ikivunjwa, au serikali inapokandamiza raia wake., alisema na kusisitiza kuwa ni lazima AU ichukue hatua dhidi ya tawala za aina hiyo.
Alisema bara la Afrika siyo tena bara la kuendekeza tawala zisizoheshimu demokrasia, haki za binadamu na utawala wa sheria, na ni muhimu suala la kupata viongozi wake kwa njia za demokrasia ziheshimiwa na kulinda.
Serikali yoyote itakayoingia madarakani kwa njia zisizo za kidemokrasia haitakubalika na itasimamishwa uanachama wake kwenye Umoja wa Afrika. Uamuzi huu umeshaanza kutekelezwa kwa baadhi ya nchi (ambazo viongozi wake wamejitwalia madaraka), Mauritania ikiwa mfano wa karibu, alisema.
Mwenyekiti huyo wa AU alisema Afrika ni lazima ilinde misingi ya kidemokrasia, utawala wa sheria na haki za binadamu zinazoonekana sasa katika bara hilo kwa kuheshimu uchaguzi wa kidemokrasia na matokeo yake.
Utamaduni wa nchi kufanya uchaguzi muda unapofika alisema, umeimarika na kutekelezwa na nchi kadhaa za Afrika, ambapo alisema tokea kuanzishwa kwa Bunge hilo la Afrika mwaka 2004, uchaguzi wa kidemokrasia na wa wazi umefanywa katika nchi 45, ambapo mwaka huu pekee nchi tano zimefanya uchaguzi.
Alisema wakati Afrika inafurahia maendeleo hayo ya kidemokrasi, bado kuna matukio machache yasiyofurahisha, na amelitaka Bunge la Afrika kuunga mkono juhudi za kulinda demokrasia, haki za binadamu na utawala wa sheria.
Rais Kikwete amesema analitarajia Bunge hilo kuwa chachu na nguvu ya kulinda misingi hiyo, kwa kujadili na kuwasukuma viongozi wa Afrika juu wa wajibu wao wa kuheshimu utawala bora, kulinda haki za binadamu na kuwajibika kuhakikisha utawala wa sheria katika nchi wanazoziongoza.
Akizungumzia uchumi, alisema bara la Afrika linaimarika kutokana na hatua za kufufua uchumi zilizochukuliwa na nchi mbalimbali ambapo ukuaji wake wa uchumi umevuka asilimia tano katika miaka michache iliyopita.
Ikiwa hali hii itadumishwa na ukuaji huo kudumishwa, hali ya uchumi barani Afrika itakuwa bora zaidi katika uongozi ujao, alisema.
Akitoa mfano alisema, mwaka 2007 pato la taifa (GDP) la nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara lilikuwa kwa asilimia 6.5, ambalo liliwafanya hata wale wanaoiangalia Afrika kama bara lisilofanya vizuri, kukiri kuwa sasa lina mustakabali mzuri zaidi kiuchumi.
Hata hivyo, ametoa wito kwa nchi za Afrika kujiimarisha kiuchumi kwa kuunganisha na kuuimarisha ushirikiano wa taasisi za kiuchumi za kikanda, kama zilivyofanya Jumuia ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SDAC), COMESA na Jumuia ya Afrika Mashariki, mjini Kampala , Uganda , hivi karibuni.
Rais Kikwete amesema ili Afrika iendelee na kasi ya mabadiliko hayo yenye mafanikio inapaswa kutekeleza mambo matano, ambayo ni kuunganisha mafanikio ya kiuchumi yaliyopatikana katika miaka ya karibuni ili kudumisha mazingira bora ya kukuza uchumi, kuheshimu demokrasia na utawala bora kwa kuimarisha taasisi zinazoisimamia, kuimarisha vyombo vya kusuluhisha migogoro na vifanye kazi, kuepuka mambo yanayozusha machafuko, na kuimarisha taasisi ya amani na usalama ya AU ili ifanye kazi kwa ufanisi.
Mapema akimkaribisha Rais Kikwete kufungua kikao hicho cha Bunge, Rais wa Bunge hilo , Dk. Getrude Mongela, alisema lina wabunge 245 kutoka nchi 47 zinazowakilishwa.
Rais Kikwete aliondoka hapa jana jioni (tarehe 27Oktoba, 2008) kurejea nyumbani.
MWISHO.