'Rais adhibitiwe katika uteuzi'

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797




Na Mwandishi Wetu, Mbeya

IMESHAURIWA kuundwa kwa chombo maalumu kitakachomshauri Rais wa Tanzania hasa katika uteuzi wa viongozi ikiwa ni hatua inayotakiwa kujumuishwa
katika katiba mpya ijayo kwa lengo la kudhibiti mamlaka hayo ya uteuzi.

Hayo ni moja ya mapendekezo yaliyotolewa na Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Mzumbe Kampasi ya Mbeya, Bw. Ross Kinemo alipokuwa anachangia mada katika kongamano la mchakato wa mabadiliko ya katiba Tanzania lililofanyika katika kampasi hiyo juzi.

Bw. Kinemo ambae pia ni Mkurugenzi wa kampasi hiyo alikuwa anatoa mada kuhusu 'Mgawanyo wa Madaraka ya Vyombo vya Dola katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania: Umuhimu wa kuboresha mfumo wa kudhibitiana'.

Akielezea zaidi, Bw. Kinemo alitoa mfano wa Nchi ya Ghana ambayo imeunda chombo hicho maalumu ambacho kitamshauri na vilevile kumdhibiti rais.
“Hili si pendekezo jipya,” alisema.

Kwa mujibu wa mtaalamu huyo wa sheria, chombo hicho pia kinatoa ushauri kwa mawaziri, bunge na tasisi za umma zilizoundwa kwa mujibu wa katiba.
“Rais anatakiwa kuomba ushauri katika chombo hiki katika uteuzi wa nafasi kubwa kama Jaji Mkuu, Mkuu wa Polisi, Kamishna wa Mapato, Mabalozi na wengineo,” alisema.

Akichangia zaidi mapendekezo yake, aliongeza kuwa mbunge yeyote aliyechaguliwa hapaswi kuteuliwa kuwa waziri maana hii inapingana na dhana nzima ya mgawanyo wa mamlaka na madaraka ya vyombo vya serikali na pia mfumo wa kudhibitiana.

Alipendekeza kwamba katika katiba mpya ijayo, mawaziri wachaguliwe na kupewa wizara kutokana na taaluma zao pamoja na kuangalia sifa za anayechaguliwa kushika wizara husika.

Bw. Kinemo alipendekeza kuwa mamlaka ya kuanzisha uchunguzi dhidi ya chombo cha utawala hayana budi kuwa chini ya bunge.

“Hiki ni chombo pekee kinachoweza kuchunguza na kupendekeza kuwaondoa baadhi ya watendaji kutoka kwenye nyadhifa zao,” alisema.

Jaji Mkuu Mstaafu, Bw. Barnabas Samatta aliyekuwa mzungumzaji mkuu katika kongamano hilo alisema sasa ni muda muafaka kwa Watanzania kujiuliza kama ni sawa kwa katiba ya sasa kutokuweka kiwango cha mawaziri wanaoteuliwa serikalini.

Akitoa mfano wa nchi ya Ghana alisema rais wa nchi hiyo anabanwa na katiba ya kuteua mawaziri wasiopungua kumi na wasiozidi 19 wakati nchini Kenya, rais anaruhusiwa kuteua mawaziri wasiopungua 14 na wasiozidi 22.

“Faida za kuwa na baraza dogo la mawaziri ziko wazi kwa ufanisi wa shughuli za serikali,” alisema na kuongeza kwamba Marekani ni taifa kubwa duniani lenye ufanisi serikalini pamoja na udogo wa idadi ya mawaziri katika serikali yake kwa mujibu wa katiba ya nchi hiyo.

Bw. Samatta ambaye pia ni Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe alipendekeza kutambuliwa kwa Benki Kuu ya Tanzania katika katiba mpya.

“Katiba ya sasa haijataja popote Benki Kuu ya Tanzania ambayo ni muhimu sana katika uhai wa uchumi wetu,” alisema.

Hata hivyo gwiji huyo wa sheria alionya kwamba Tanzania inaweza kuwa na katiba mpya na bado pasitokee mabadiliko yaliyotarajiwa.

“Ili mabadiliko ya kweli yafanyike, viongozi na vyombo vya habari wafanye kazi kwa bidii na ujasiri mkubwa, na wananchi watafute na kujua haki zao kuliko ilivyo hivi sasa,” alisema.

Akitoa mapendekezo yake ya katiba mpya, Mhadhiri Msaidizi wa Sheria chuoni hapo, Bw. Yohana Seme alisema ni vyema majina ya viongozi ya wanaoteuliwa na rais kuongoza Tume ya Uchaguzi yawe kwanza yameidhinishwa na Kamati ya Bunge yenye wawakilishi kutoka vyama vyote vya siasa.

Aliongeza kwamba katiba ijayo pia iruhusu haki ya mtu kupinga matokeo ya uchaguzi katika ngazi ya urais.

Mkuu wa Idara ya Sheria Chuo Kikuu Mzumbe, Dk. Eleuter Mushi alisema ili iwe na manufaa, ni lazima katiba mpya ilenge kunyanyua hadhi ya maisha ya Watanzania na kwamba kuna uhusiano mkubwa kati ya katiba, utawala bora na ubora wa maisha.

Kongamano la Mbeya lilifuata lile lililofanyika kampasi kuu ya Mzumbe wiki iliyopita.

Kongamano hilo mjini Mbeya lilihudhuriwa na viongozi wa serikali, viongozi wa vyama vya siasa, viongozi wa dini, viongozi wa vyama vya wafanyakazi, asasi zisizo za kiserikali, wanazuoni, vyombo vya habari na wananchi wote kwa ujumla.

Washiriki walipata nafasi ya kuchangia maoni yao kuhusiana na mada husika lengo kuu likiwa ni kuelimisha na kujadili changamoto mbalimbali zilizopo katika katiba ya sasa na kupendekeza mambo ya kuzingatiwa.
 
Ingekuwa bora pia wateule wowote wa Rais lazima waende kwenye Vikao Vya Wabunge na kuulizwa Maswali
1. Rushwa
2.Ubaguzi wa Aina yoyote
3.Uwezo wa kufanya kazi (Qualification)
 
Hata iweje hilo ni lazima tulitolee maoni mengi kwenye mchakato wa katiba ili tuweze kumuondolea rais madaraka ya kuchagua watendaji wakuu wa serikali na taasisi za umma. Kama mkuu wa majeshi, ijp, gavana, mwana sheria mkuu, jaji mkuu na wakurugenzi na watendaji wa malaka za umma
 
..hebu ona uteuzi kama wa WASSIRA sijui hasira ni hovyoooooooooooooooooooooooo mtupu
 
Back
Top Bottom