Raia Mwema: Chura akipigwa teke, amepunguziwa safari!

Zak Malang

JF-Expert Member
Dec 30, 2008
5,404
234
Chura akipigwa teke, amepunguziwa safari!

Na Msomaji Raia


JUMAMOSI ya Juni 4, 2011, kiongozi mkuu wa Upinzani katika Bunge alijisalimisha Kituo Kikuu cha Polisi, Dar es Salaam na kuwekwa chini ya ulinzi.

Mheshimiwa Freeman Mbowe alifanya hivyo baada ya vyombo vya habari kutangaza kuwa hati ya kukamatwa kwake ilikuwa imetolewa na hakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Arusha kwa kosa la kuruka mdhamana.

Sihitaji kujadili undani wa hati hiyo ambayo iliishia kufutwa na Mbowe kuachiwa huru mapema Jumatatu Juni 6, 2011. Habari zinaeleza; ilifutwa bila Mbowe kuulizwa lolote. Sinema ya bure iliyotengenezwa ghafla mwishoni mwa wikiendi iliishia hapo na kuacha mjadala unaoendelea na ambao una sura nyingi.

Wapo wanaodai kuwa tukio zima lilikuwa ni hujuma dhidi ya chama tawala na Serikali iliyofanywa na watu wachache wajanja ndani ya Chama na Serikali. Wanaodai hivi wanalenga kuonyesha madhara ya makundi hasimu ya Serikali na Chama.

Wapo wanaodai hii ni ajali ya kimaamuzi iliyofanywa bila kukusudia na ikaenea na kuviambukiza vyombo vingine vya dola. Nia njema ya kutaka kuonyesha kuwa utawala wa sheria umerudi toka likizo katika Taifa ikageuka kuwa sinema ya kisiasa badala ya mkono mrefu wa sheria.

Kwa kuwa taifa letu linaugua na liko taabani kwa magonjwa yaliyosababishwa na wana siasa, sinema hii ikapata washabiki wengi isivyotarajiwa kwa sababu ipo hamu kubwa miongoni mwa watu wengi kuona tiba ya magonjwa-siasa inapatikana upesi.

Wapo wanaodai kuwa Jeshi la Polisi limeishiwa weledi na uadilifu katika jamii kiasi kwamba linahaha kuwafurahisha watawala, na kwa kufanya hivyo linajikuta linatumia nguvu bila hekima wala akili za kawaida.

Ilitarajiwa kuwa Jeshi la Polisi linajua na kuheshimu kuwa Mbowe ni mtu mashuhuri asiyeweza kutoroka wito wa Mahakama. Kwa jinsi hiyo, Kamanda wa Polisi wa Dar es Salaam angemuelekeza Mbowe aende mwenyewe Arusha na kuripoti kwa Kamanda wa Mkoa wa Arusha na taratibu zifuatwe za kumfikisha Mbowe mahakamani.

Ama kwa kutaka kuwafurahisha watawala au kwa kukosa weledi katika kazi zao, Polisi wakamng'ang'ania Mbowe na hatimaye kumsafirisha kwa ndege ya Jeshi kwenda Arusha. Ukata huu wa mkakati si wa Polisi pekee yake; maana wapo maafisa Usalama wa Taifa, wapo watawala wetu wa Ikulu na mafundi-mchundo (makada) katika chama tawala. Hawa wangeweza kirahisi kuepusha aibu hii iliyojitokeza.

Wapo wanaodai sinema hii iliandaliwa kwa ufundi sana na viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ili kupata umaarufu wa kisiasa. Kwamba, walijua Polisi ina udhaifu unaoendekeza ubaguzi katika masuala ya kufuata sheria za nchi.

Kwamba Polisi imewageuza viongozi wa vyama vya Upinzani kama gunia la kufanyia mazoezi ya kukamata na kuweka ndani. Kwamba, Polisi wanaotetemeka na kudondosha suruali mbele ya wanasiasa wa chama tawala, wanakuwa wepesi wa kuwakamata viongozi wa Upinzani hata bila kufuata taratibu zilizowekwa.

Huku wakijua mtego huo, CHADEMA wakautumia vema na kuwanasa wote; yaani Polisi, CCM, Mahakama na Serikali. Dhana hii inaonekana kuwa tamu mno na kukosa uhalisia, lakini kwa kuwa yametokea yanayotufanya tuhoji hekima ya watawala, tunafikia hitimisho la kusema kuwa kila jambo linawezekana katika mfumo ambao umeruhusu akili ziende likizo na ulevi wa madaraka uwe msingi wa shughuli za kila siku za watawala wetu.

Wapo wanaodai hizi ni njama za Rais Jakaya Kikwete kukihujumu chama chake kwa kuwa yuko katika muhula wa mwisho na hana la kupoteza chama kikiondoka madarakani. Dhana hii inaaminika zaidi miongoni mwa makada wazoefu wanaodai kuwa wanakijua vema Chama cha Mapinduzi (CCM) na utendaji wake.

Watu hawa wanadai Kikwete amekinyima chama nafasi yake katika utawala wa nchi; hasa pale anapoendekeza maamuzi mepesi. Wanaendelea kudai Kikwete ana hasira na baadhi ya wana siasa ndani ya Chama anaodai wanamkera kwa kudai wao wana umaarufu kuliko Chama au kuliko yeye Mwenyekiti.

Walio karibu na Kikwete wanamnukuu akisema; "Chama kiachwe kijitetee chenyewe kuliko kumtegemea yeye kama Rais aweze kukitetea". Kundi hili linapingana na msimamo wake huu kwa madai kama ni kweli Chama kiachwe kujitetea, mbona amewaacha Polisi ndio wanakuwa watendaji wa Chama na kusababisha Chama kichukiwe zaidi?

Mbona Polisi hao hao hawawashughulikii mafisadi ambao Kikwete amedai siku za karibuni kuwa wamekidhalilisha Chama mbele ya wapiga kura.

Wachambuzi wa kundi hili wanazua masuala mengi yenye utata lakini yanayoshawishi akili za watu waliokata tamaa. Wanadai kwa jinsi mambo yanavyokwenda, ghadhabu ya wananchi kwa sasa si juu ya Kikwete; bali juu ya CCM na Serikali. Kimsingi, hata ghadhabu juu ya mafisadi inapungua na kuelekezwa kwa Chama na Serikali ambavyo vinaonekana kuelemewa kabisa na mzigo huu.

Serikali yenyewe imeelemewa na makundi pamoja na kutotabirika kwa Rais Kikwete. Lakini cha ajabu, ghadhabu ya wananchi inaenda kwa mawaziri na watendaji binafsi; huku Kikwete akionekana kupuuzwa hadharani lakini bila chuki kali kama inayoelekezwa kwa Chama chake na watendaji.

Kutokana na muono huu wa kundi la mwisho hapo juu, ni rahisi kutoa hitimisho kuwa kukamatwa kwa Mbowe kumempandisha chati Mbowe na chama chake; huku kukikidhalilisha chama tawala na watendaji wake.

Mbowe na chama chake wamepata umaarufu bila kuulipia wala kuugharimia. Wamepata huruma ya wananchi wanaoona kuwa CHADEMA inaonewa na chama tawala pamoja na vyombo vyake vya dola. Mmoja amesema; hii ni sawa na kumpiga teke chura ukilenga kumuumiza lakini ukaishia kumpunguzia safari yake.

Wenye hekima wanasema Mbowe hakupaswa kusindikizwa na ndege ya Jeshi wala kupata ulinzi mkali namna hiyo. Mbowe hakuwa mhaini wala gaidi; bali kiongozi wa chama aliyekosea taratibu za kisheria.

Matumizi ya ziada ya ulinzi na gharama za safari zimeinufaisha CHADEMA na Mbowe kuliko Serikali iliyoishia kufuta kesi yake na kumwachia huru. Kwa kuwa Serikali hii hii inatuhumiwa sana na ufisadi, si ajabu wapo wanaoweza kudai hizi zilikuwa ni njama maalumu za kujichotea fedha na masurufu ya safari ya kumsindikiza Mbowe kwenda mahakamani.

Mtiririko huu wa harufu ya hujuma unaweza kuleta hasara kubwa kwa Serikali yetu na hata amani yetu. Iwe ni kweli kuwa Kikwete anahujumiwa na watendaji wake; au Polisi inamhujumu Kikwete na Serikali; au Kikwete anakihujumu chama anachokiongoza; na pengine Chama kinahujumu nchi, kuna haja ya Kikwete kukaa chini na kuchora upya mustakabali wake baada ya kustaafu kuliko kufikiri siku zake zilizobaki kabla ya kustaafu.

Ni wazi hawezi tena kubadili hali ya mambo ilivyo ndani ya chama na Serikali. Walio wengi wanaona ni kama anaikabidhi nchi makusudi kwa CHADEMA bila CHADEMA kutumia raslimali zake; bali kwa kutumia mtaji wa udhaifu wa Kikwete na watendaji wake.

Mwalimu na Baba wa Taifa, Julius Nyerere, aliwahi kusema kuwa Kikwete alikuwa bado hajaiva kuwa Rais wa nchi. Mwalimu aliposema hivyo, hakusema atakuwa tayari lini! Yawezekana Mwalimu alikuwa sahihi.


Chanzo: Raia Mwema

 
Hahahahaha imekaa vizuri

Ilikua inahitaji akili kidogo tu, dah kweli poleni wakuu
 
Nimefurehishwa sana na mawazo komavu yasiyo na chembe ya upendeleo zaidi yanahimiza wahusika kufikiri kwa kina Mwalimu hakukosea huyu m kwe re hajakua na hata kua milele
 
Mwalimu Nyerere alikuwa anaona mbali sana ubongo wa kikwete aliuoana haukuwa umekomaa ndio maana alimkataa haya yote ni aibu kwa chama ccm na kuipa cdm umaarufu lakini huo ni ukweli maana hata mimi nilijiuliza kwa nini Mbowe wa simwambie atafute njia yoyote ile aliport Arusha lakini kwa ujinga na upungufu wa maarifa kichaa mwema kaamulisha apelekwe kwa ndege kwani angekimbilia wapi Mbowe?
 
Ilikuwa ni aina nyingine ya ufisadi nini? Kuna mbinu nyingi bana, watu wamechacha ni kutafuta jinsi ya kupona MASURUFU!

Ahsante Malang Hii safu imekaa vizuri!!!!!!!!!
 
(Mahakama+Polisi VS Mbowe) yote ilikuwa potezapoteza ili kupunguza kasi ya CDM ktk mchakato wa kuunganisha wananchi ili kuunda taifa jipya la tanzania yenye maendeleo endelevu.
 
Huyo msomaji raia ni nani? Kweli mtu anaweza kujiita msomaji raia?
 
Ebana kamanda hii kweli si ya kuacha kusoma. nimeisoma imetulia nimeipenda 100%. hakuna kulala mpaka kieleweke
 
Hili suala zima la Mbowe kwa yeyote mwenye akili timamu lazima limfikirishe sana. Hii makala imekaa vizuri na inatufumbua macho zaidi kuwa nini kinaweza kuwa kilikuwa kîkiendelea nyuma ya pazia. Lkn kuna sehemu ina ukakasi kidogo~ ".....bali kiongozi wa chama aliyekosea taratibu za kisheria."

Wabongo tumekuwa na tabia ya kukaririshwa mambo na kuyachukua hata kama kwa uchunguzi kidogo tu ukweli ungetuonyesha vinginevyo. Wasemaji wa Chadema tofauti walisema kuwa Mwenyekiti wao alikuwa na ruhusa ya mahakama ile ile kutohudhuria. Na mahakama haikukanusha hilo hadi sasa!

Na zaidi sana mahakama hiyo hiyo 'imedhibitisha' hilo kwa kutomuhoji, mwadhibu wala kumuonya Mbowe alipopelekwa huko! Inashangaza kwamba bado wengi wetu tunaimba wimbo wa Chagonja kuwa mbowe alivunja sheria, hivi alipewa adhabu gani na mahakama gani kwa huko kuvunja sheria?! Hapo hatujauliza aliyeinjinia kuunganisha jeshi(ndege ya jeshi) na polisi ktk kadhia hii.... UWT? labda.
 
Kaka hapo umenena vyema na haki na kwa ubadhirifu huu nafikiri walitaka kumalizia masazo kabla ya budget mpya.
Ila waelewe CHADEMA ni moto wa petrol hata uingie majini utakusubiri uibuke na si moto wa mabua kama alivyosema katibu wao mstaafu.
 
Back
Top Bottom