Polisi yaanza kuhoji wahusika Richmond

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,011
Date::9/28/2008
Polisi yaanza kuhoji wahusika Richmond

Na Ramadhan Semtawa
Mwananchi

MWEZI mmoja baada ya serikali kutangaza uchunguzi wa Jeshi la polisi kuona kama kampuni ya ufuaji umeme ya Richmond (LLC) ilighushi nyaraka kupata zabuni ya kufua umeme wa dharura, tayari baadhi ya watu wenye uhusiano na kampuni hiyo wamehojiwa.

Uchunguzi huo ni sehemu ya hatua za serikali kutekeleza maazimio 23 ya Bunge la Jamhuri ya Muungano. Azimio la 17 kati ya hayo 23 linataka mhimili huo wa dola uchunguze kuona kama LLC ilighushi nyaraka kupata zabuni hiyo ya mkataba wa Sh179 bilioni, ambao ulisainiwa Juni 23, 2006 .

Taarifa za kina kutoka serikalini, zinasema kuwa kitu cha kwanza ni kuona uhusiano wa watu hao (majina tunayo) na LLC na pia kama walihusika katika jinai hiyo ya kughushi nyaraka.


Kwa mujibu wa duru hizo za kiserikali, watu hao, baada ya baadhi ya kuhojiwa, wameanza kuonekana kuwa na uhusiano na LLC.

Alipoulizwa kuhusu uchunguzi huo, mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Kamishina Robert Manumba alisema kwa sasa unaendelea vizuri.

Kamishna Manumba alisema polisi inafanya uchunguzi wa kina wa kijinai kwa ajili ya kupeleka kesi mahakamani.

"Uchunguzi wetu ni wa kina," alisema Manumba. "Tunafanya uchunguzi kwa ajili ya kesi, hivyo lazima tupate taarifa za kutosha.

"Hatufanyi uchunguzi wa kisiasa. Uliofanyika awali ulikuwa wa kisiasa tofauti na wa kwetu. Huu ni wa kijinai kwa ajili ya kesi mahakamani."

Alipoulizwa kuhusu baadhi ya watu kuhojiwa, alijibu: "Sasa, huwezi kuzungumzia hadharani uchunguzi unaondelea, kumbuka huu bado ni uchunguzi."

Alipoulizwa kama polisi wake wameenda Marekani kufanya uchunguzi kutokana na LLC kuhusishwa na watu kutoka nchi hiyo, Kamishna Manumba alijibu: "Nafikiri sasa tukisema tutaharibu uchunguzi, elewa tunafanya uchunguzi na unakwenda vizuri."


DCI Manumba alifafanua kwamba, uchunguzi huo ni mpana na unagusa maeneo mengi ya msingi, hivyo lazima uwe wa kina.

Hata hivyo, alipoulizwa zaidi ni lini hasa uchunguzi huo unatarajiwa kukamilika na watuhumiwa kuburuzwa mahakamani, alifafanua: "Ni mapema mno kuanza kuzungumzia hilo, fahamu tu uchunguzi uko katika hatua nzuri."

Wakati Kamishna Manumba akitoa majibu hayo, taarifa zaidi kutoka duru hizo za serikali zinasema baadhi ya watu hao waliohojiwa ni kutoka Richmond Tanzania LTD.

Richmond Tanzania LTD tayari imepoteza sifa za kuwa kampuni hai baada ya kubakiwa na mwanahisa mmoja. LLC ilibainika kuwa si kampuni bali ilikuwa na baadhi ya watu wachache matapeli ambao wanaotuhumiwa kuwa walikughushi nyaraka kupata zabuni kubwa ya ufuaji umeme.

"Baadhi ya watu tayari wamekwishaanza kuhojiwa, wengine ilikuwa kipindi kifupi baada ya kauli ya Waziri Mkuu (Mizengo Pinda) bungeni," kilisema chanzo huru.

Chanzo kingine kilifafanua kwamba, baadhi ya wafanyakazi wa Richmond Tanzania Limited ambayo itafutwa rasmi wakati wowote iwapo hakutawasilishwa madai kwenye Ofisi ya Wakala wa Usajili wa Makampuni na Majina ya Biashara (Brela), katika notisi yake ya siku 15, wamehojiwa.

"Ukiangalia Brela, utakuta kumbukumbu zinaonyesha LLC ilikuwa na uhusiano wa kihisa na Richmond Tanzania Limited, ingawa mkataba ulisainiwa miezi karibu miwili baadaye baada ya usajili, lakini inaonekana kuna uhusiano kwa hiyo baadhi yao lazima wahojiwe," kilisema.

Sakata la Richmond lilitikisa nchi kuanzia Juni mwaka 2006, miezi michache baada ya serikali ya awamu ya nne kuingia madarakani na nchi kukabiliwa na ukame uliokuza tatizo la uhaba wa nishati, na kulazimu serikali kutafuta mitambo ya dharura ya kukodi kwa ajili ya kufua umeme.

Hata hivyo, mpango huo uliingiza serikali ya awamu hiyo ya nne katika kashfa nzito ambayo ililifanya Bunge kuunda tume yake chini ya Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe.

Katika mkutano wa 10 wa Bunge la Februari, tume hiyo ilitoa matokeo yake ambayo yalimuhusisha Edward Lowassa katika sakata hilo la utoaji zabuni na kumlazimisha kuachia kiti chake cha Waziri Mkuu.

Mawaziri wengine, Nazir Karamagi na Dk. Ibrahim Msabaha pia walifuata mkondo.

Baada ya kujadili ripoti hiyo ya tume ya Mwakyembe, bunge lilitoa mapendekezo saba ambayo pamoja na ya kamati yalifanya jumla kuwa maazimio 23 yaliyokwenda serikalini kwa utekelezaji, ikiwa imepewa miezi sita.
 
Je Polisi wanatakiwa wafanye kazi kufuatana na uamuzi wa Bunge au wanatakiwa wawe pro-active. i.e walitakiwa kufanya uchunguzi tukio lillpo tokea
 
Majibu ya officer wa polisi yapo very intresting amekuwa antumia maneno haya (fahamu tu uchunguzi uko katika hatua nzuri.)" hii nikama vile hadisi ya Abunuwasi na sungura .mpaka lini jamani viumbe sie wa nchi hii tutaendelea kuwa MADUBU na kukubaliana na hada hada kama hizi??
 
Je Polisi wanatakiwa wafanye kazi kufuatana na uamuzi wa Bunge au wanatakiwa wawe pro-active. i.e walitakiwa kufanya uchunguzi tukio lillpo tokea

Huyu DCI Manumba anataka kupanda mgongoni mwa watu, si kweli kwamba polisi wanafanya uchunguzi peke yao bali kuna timu
 
Hosea mwenyewe alisema mkataba ulikuwa safi sasa hawa polisi hawamwamini au? au wanachunguza walikosea wapi mpaka tume ya bunge ikagundua ukweli!!! lol
 
Mie nilidhani nitaona majina ya hao wanao hojiwa kumbe bado ni kama EPA mwishowe Rais aseme hakuna la zaidi ?
 
Back
Top Bottom