Polisi Watumika kuiba kura Z'bar-Shamsi Nahodha upo?

Junius

JF-Expert Member
Mar 11, 2009
3,181
139
Asha Bani,

IMEBAINIKA kuwa, baadhi ya askari polisi visiwani Zanzibar, walipiga kura zaidi ya mara moja katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005.
Taarifa za uhakika zilizolifikia Tanzania Daima Jumatano kutoka kwa viongozi mbalimbali wa kambi ya upinzani visiwani Zanzibar, zinaeleza kuwa, wamenasa ushahidi wa shahada za kupigia kura za polisi waliopiga kura zaidi ya mara moja katika uchaguzi mkuu uliopita.
Taarifa hizo ambazo kwa mara ya kwanza zinaonyesha ushahidi wa polisi kujihusisha na vitendo vya udanganyifu na kuvuruga uchaguzi visiwani humo, zinaeleza kuwa katika Jimbo la Magogoni, wanasiasa wa kambi ya upinzani wamenasa vielelezo vya vitambulisho vya kupigia kura zaidi ya 210 ambavyo vina upungufu, ukiwamo ule wa mpiga kura mmoja kujiandikisha mara tatu katika vituo tofauti pamoja na wapiga kura wapya kuandikishwa wakiwa na umri chini ya miaka 18.
Baadhi ya wanasiasa wa visiwani humo wameeleza kuwa, kubainika kwa njama hizo za polisi ndicho chanzo cha kuibuka kwa mgogoro wa hivi karibuni baina ya Chama cha Wananchi (CUF) na Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC).
Wanasiasa hao walilieleza gazeti hili kuwa, baada ya tume kubaini kuwa baadhi ya shahada zilizotumiwa na polisi kupiga kura zaidi ya mara moja zimetua mikononi mwa wapinzani, maofisa wa tume hiyo walikataa kutoa daftari la wapiga kura ili kuhakiki majina ya wapiga kura kama sheria ya uchaguzi namba 64 ya Zanzibar inavyoeleza.
Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Juma Duni Haji, akizungumzia hali hiyo, alieleza kuwa chama chake kimenasa majina ya askakri hao na vipande vya nakala ya vitambulisho vyao kwenye daftari la kupiga kura baada ya kuitilia shaka ZEC ilipokataa kutoa madaftari ya wapiga kura kabla ya zoezi la upigaji kura kuanza.
Duni alisema majina yaliyoonekana kuwa na makosa, ambayo kwa juhudi zao walifanikiwa kuyanasa ni zaidi ya 210 na 24 kati ya hayo ni ya askari wa Jeshi la Kujenga Uchumi (JKU) ambao wamejiandikisha mara tatu.
“Inashangaza sana kuona askari wa JKU ndio walioongoza katika kujiandikisha mara tatu, na kwamba aibu hii ndiyo imekifanya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwatuma ZEC kutunyima daftari hilo ingawa sheria ya Zanzibar inaruhusu kufanya hivyo,” alisema Duni.
Alisema kuwa, anamshangaa Waziri Kiongozi wa Zanzibar, Shamsi Vuai Nahodha kwa kuwaita wao ni wakorofi, huku uhalali na ukweli wa uozo wa ZEC ukiwa unajulikana na kuwa wametumwa na CCM kufanya njama hizo ili waweze kuiba kura katika chaguzi mbalimbali.
Duni alisema kuwa, kuna sheria katika kifungu cha 64 ambayo inaruhusu wakala wa chama chochote kinachoshiriki uchaguzi aweze kumuona mpiga kura ili aweze kulinganisha kama aliyekuwamo kwenye daftari ndiye ambaye ana kadi ya kupigia kura ya kudumu katika uchaguzi.
“Hii sheria sasa inadharaulika, lakini ni kwamba wanashindwa kufahamu utakapomnyima daftari wakala au chama chake, atawezaje kujua wapiga kura? Buku la ZEC ni bovu na ZEC wanaona aibu kulionesha, kwani limejaa uchafu wa uharamia walioufanya mwaka 2005 katika wizi wa kura na wanaoufanya sasa katika uandikishaji huo,” alisema Duni.
Alisema katika uandikishaji wa sasa wa kura hizo katika Jimbo la Magogoni, wapiga kura 20 (majina tunayo) wamenyimwa shahada mpya ya kupiga kura huku wakiwa na cheti kinachoonyesha kuwa ni wazawa wa jimbo hilo.
Alisisitiza kwa kupinga kauli ya Waziri Kiongozi kwa kuwaita kuwa wao ni watu wenye vurugu, na kwamba kama wakihitaji wajitoe katika uchaguzi, alisema kuwa wao wanafuata sheria na kwamba si watu wenye vurugu huku akihoji ni sababu ipi inayowafanya ZEC washindwe kuwapatia daftari hilo kama si kuficha maovu yao wanayofanya na waliyozoea kuyafanya katika chaguzi mbalimbali zilizopita.
“Hayo ndiyo mambo ambayo ZEC wanatufanyia, hatuna vurugu wala nini, sasa sijui hii serikali yetu itakuwa lini na demokrasia, kila kukicha ni dhuluma katika chaguzi zetu mbalimbali, ndiyo maana tunataka tume huru ya uchaguzi, ama uchaguzi uweze kusimamiwa na Umoja wa Mataifa na si ZEC kwa kuwa ni wezi na wamejaa maovu,” alisema Duni. Jimbo la Magogoni lipo katika kipindi cha uchaguzi mdogo ambapo vyama vitatu vimejitokeza kusimamisha wagombea. Wakati CUF imemsimamisha Ahmad Ally Ahmad, CCM inawakilishwa na Asha Mohamed na Hamis Mselemu wa Sauti ya Umma amesimamishwa na SAU kugombea kiti cha jimbo hilo.

http://www.freemedia.co.tz/daima/habari.php?id=5130#top
blank.gif
 
Back
Top Bottom