Polisi sasa watikiswa

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,267
33,039
headline_bullet.jpg
IGP Mwema aunda timu kuchunguza mauaji ya Dar
headline_bullet.jpg
Itabainisha kama ulikuwa ni utekaji nyara au la
headline_bullet.jpg
Kamanda Kova kuitangaza hadharani ripoti hiyo leo



IGP%200.jpg

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Said Mwema, akizungumza jana na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusu raia aliyeuawa na polisi Kinondoni, jijini Dar es Salaam.



Jeshi la Polisi nchini, limeshtushwa na mauaji ya raia yanayofanywa na askari wake na sasa limeunda timu kuchunguza mauaji ya raia Octavian Kashita, ambaye alipigwa risasi na askari polisi wa kituo cha Oysterbay, mkoani Dar es Salaam.
Timu hiyo ambayo imeanza kazi muda mfupi baada ya mauaji hayo kutokea jijini Dar es Salaam, inahusisha watu kutoka ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Makao Makuu ya jeshi hilo na Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam.
Mkuu wa Jeshi hilo, IGP Said Mwema, aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam na kuongeza kuwa maamuzi ya tukio hilo yatatolewa leo na Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam.
Mwema alisema timu hiyo pamoja na mambo mengine, inachunguza mazingira halisi ya tukio hilo kama yalikuwa ya utekaji nyara au la. Pia alisema timu hiyo inachunguza askari polisi waliokwenda kwenye tukio hilo kama walitumia nguvu kupita kiasi ama la.
“Tunataka kujua kama askari wetu walitumia nguvu kupita kipimo, busara au walitumia wito katika ukamataji wa watuhumiwa hao. Ikiwa uchunguzi utaonyesha wametumia nguvu kupita kipimo, watashitakiwa kwa mujibu wa sheria za kijeshi, lakini ikionekana watuhumiwa hao walikuwa katika mazingira ya utekaji, nao sheria itachukua mkondo wake,” alisema Mwema.
Mauaji ya raia huyo yalitokea Jumapili ya wiki iliyopita usiku muda mfupi baada ya askari watano wa kituo cha polisi Oysterbay kupata taarifa za kuwepo kwa watekaji eneo la Victoria karibu na nyumba za viongozi wa serikali.
Askari hao ni Koplo Ahamad, Detective Cyprian, DC Kombo, DC Kasa na DC Charles ambao kwa sasa wanashikiliwa kwa mahojiano zaidi.
Taarifa za utekaji nyara ziliwasilishwa polisi na Sia Minja (28) ambaye aliwaeleza polisi kuwa kaka yake Bariki Minja alikuwa ametekwa na watu hao.
Awali, akizungumza na waandishi wa habari Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, alisema baada ya askari hao kupata taarifa walielekea eneo la tukio na kuwakuta watu hao wakiwa na mtu aliyetekwa.
Alisema Kashita alipigwa risasi na mmoja wa askari hao baada ya kuzuka vurugu zilizohusisha polisi hao na watuhumiwa ambazo zilikuwa zikipinga kupelekwa kituo cha polisi.
Hata hivyo miongoni mwa watuhumiwa hao inadaiwa kuwa alikuwepo mtoto wa familia ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Celina Kombani, ambaye inadaiwa kuwa alikuwa dereva kwenye gari lililotumika katika utekaji.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Elias Kalinga aliliambia gazeti hili jana kuwa, mtoto huyo ambaye ni Goodluck Mlinga, siku ya tukio alikuwa ni dereva wa gari lenye namba za usajili T 864 BHC aina ya Toyota Land Cruiser Prado ambalo walilitumia katika utekaji.
Alisema uchunguzi wa kina juu wa mtoto huyo pamoja na wenzake walioshirikiana unaendelea kufanyika.
“Tunachunguza kama mtoto huyo kweli anatoka katika familia ya waziri pamoja na wenzake, pia askari waliohusika katika tukio hili wanaendelea kushikiliwa kwa mahojiano zaidi,” alisema
Aidha, utekaji huo ulidaiwa chanzo chake ni ugomvi wa muda mrefu wa kifamilia kati ya Minja na Martha ambaye amezaa naye mtoto mmoja na kwamba kesi hiyo ipo mahakamani.
Katika hatua nyingine, gazeti hili jana lilipofika nyumbani kwa marehemu Kashita ili kujua taratibu za mazishi, mwandishi aliwakuta watu wachache ambao walikuwa wamejifungia ndani ya geti.
Nyumbani kwa marehemu ni miongoni mwa nyumba wanazoishi viongozi wa serikali.
Mmoja wa walinzi wa nyumba hiyo ambaye alifungua geti kwa ajili ya kumsikiliza mwandishi, alipoulizwa kama kuna mtu atakayeweza kueleza utaratibu wa maziko ya marehemu Kashita, alidai kuwa, ndugu wote hawapo na kwamba msiba haupo hapo.
Kabla mlinzi huyo hajatoa kauli hiyo, alifungua geti na mwandishi kujitambulisha na kumuomba amuite mhusika.
Hata hivyo, mlinzi huyo aliporudi, alidai kuwa wahusika hawapo na msiba hajui ulipo kwa wakati huo.
Nipashe lilipomtafuta Waziri Kombani kuzungumzia tukio hilo, alisema hawezi kuzungumza kwa maelezo kuwa hakuwa na taarifa zozote kwa kuwa alikuwa maeneo ya vijijini katika huko Mahenge, mkoani Morogoro. Waziri Kombani alimshauri aulizwe Mlinga.
Mlinga alipotafutwa kwa simu, alikataa kutoa maelezo kwa kuwa suala hilo liko polisi.
Polisi wamehusishwa na matukio kadhaa ya mauaji ya raia katika maeneo mbalimbali nchini.
Katika kipindi cha miaka mitano jeshi la polisi nchini limejikuta likikumbwa na kashfa mbalimbali za askari wake kujihusisha na vitendo vya mauaji ya raia, hali ambayo imesababisha baadhi ya wananchi kulilalamikia.
Kashfa ya kwanza ni ile ya mauaji ya wafanyabiashara watatu wa madini ambao walikuwa wakazi wa Mahenge, mkoani Morogoro na dereva teksi wa Dar es Salaam. Askari polisi kadhaa walishitakiwa kwa kuwaua, akiwemo aliyekuwa Kaimu Kamanda wa Polisi na Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Mkoa wa Dar es Salaam, Abdallah Zombe, mwaka 2006.
Tukio lingine ni lile la mauaji ya vijana wawili mkoani Arusha yaliyofanywa na askari polisi kwa madai kuwa ni majambazi.
Katika mkoa wa Dar es Salaam, matukio yaliyojitokeza ni lile la Kimara Stop Over ambapo askari polisi walimpiga risasi dereva teksi kwa madai kuwa ni jambazi na matukio mawili ya mauaji yaliyotokea kwenye vituo vya polisi moja lilitokea Stakishari na lingine kituo cha polisi Chang'ombe.



CHANZO: NIPASHE
 
Sasa ndio tujue vizuri kesi hii ili ishia wapi maana yawezekana huyu Mlinga alibebwa kwenye kesi hii kama alivyobebwa kwenye ubunge kwa vile alizaliwa na Kombani.
Hatutakiwi kulea uhalifu, kesi za mauaji ya binadamu sio za kuletea mchezo ndio huwa zinaleta visasi
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom