Candid Scope
JF-Expert Member
- Nov 8, 2010
- 11,885
- 6,885
Sita washtakiwa kwa ugaidi Arusha
WATUHUMIWA sita wanaodaiwa kurusha bomu katika mgahawa wa Vama Tradition jijini Arusha, Julai 7, mwaka huu, na kusababisha watu wanane kujeruhiwa huku mmoja wao akikatwa mguu, wamepandishwa kizimbani na kusomewa mashtaka manne.
Watuhumiwa hao ambao walikamatwa juzi kwa nyakati tofauti, walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha jana chini ya ulinzi mkali wa polisi, majira ya saa 7:30 mchana.
Baada ya kufikishwa mahakamani hapo, washtakiwa hao, Shabani Mmasa, Athumani Huseini, Mohamedi Nuru, Jafari Lema, Abdul Salum na Saidi Temba, walisomewa mashtaka manne na Mwanasheria wa Serikali, Augustino Kombe.
Mbele ya Hakimu Mkazi, Rose Ngoka, washtakiwa wote walisomewa shtaka la kwaza la kupanga njama za kufanya ugaidi kinyume na sheria ya ugaidi ya nchi.
Washtakiwa hao walidaiwa kuwa Februari na Julai mwaka huu, walipanga njama za kufanya ugaidi katika mgahawa wa Vama uliopo maeneo ya Gymkhana jirani na Mahakama Kuu jijini Arusha na kujeruhi watu wanane waliokuwemo ndani ya mgahawa huo.
Waliojeruhiwa katika kadhia hiyo ni Deepack Gupta aliyekatwa mguu wa kushoto, Manisha Gupta, Prateek Javey, Manci Gupta, Mahish Gupta, Ray Rajin, Ritwik Khandehral na Vinpd Suresh.
Katika kosa la pili, washtakiwa wanadiwa kufanya ugaidi ambapo mwanasheria Kombe alisema mnamo Julai 7, mwaka huu, walirusha bomu katika mgahawa huo na kusababisha
kujeruhi watu wanane waliokuwamo ndani ya mgahawa huo.
Kosa la tatu lilitajwa kwa washtakiwa Lema na Huseini ambao walidaiwa mahakamani hapo kuwa walihusika kutoa silaha ambazo ni bomu zilizohusika katika shambulio hilo.
Shtaka la nne liliwahusisha washtakiwa wote sita wakidaiwa kutoa ushirikiano katika kufanikisha kutendeka kwa kosa la ugaidi na kukiuka vifungu kadhaa vya sheria ya ugaidi vinavyokataza mtu yeyote kujihusisha na masuala ya ugaidi.
Hakimu Ngoka mara baada ya kutajwa kwa mashtaka hayo, aliwazuia wasijibu chochote kwa kuwa mahakama hiyo haina uwezo wa kusikiliza kesi hiyo.
Aidha, mwanasheria wa serikali, Kombe aliiambia mahakama hiyo kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamailika, hivyo kuiomba ipange tarehe nyingine ya kutaja kesi hiyo.
Baada ya maombi hayo, hakimu Ngoka aliahirisha kesi hiyo hadi Agosti 6, mwaka huu, itakapokuja kwa ajili ya kutajwa tena, huku washtakiwa wakipelekwa rumande.