Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,476
- 39,995
Nawasalimu watani, wa bara na visiwani,
Ninalo la kuwapeni, lanitoka mtimani,
Linatokea mijini, mpaka kwetu kijijini,
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Ni kama hawajuani, wanapokuwa ghalani,
Ni washirika makini, kupita mchwa porini,
Lao ni moja jamani, kweli nawaambieni,
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Panya hawaulizani, "umefikaje ghalani?"
Ati "jina lako nani", "unatoka nyumba gani"
"Wewe panya panya gani?", "mbona kama fulani?"
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Panya hawakatazani, wanachokula ghalani,
Kamwe hawakamatani, hata panya fataani,
Wanapokuwa ghalani, kwao ni kama Kanaani,
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Panya akiulizani, wale vipi cha ghalani,
Watamuuliza namnani, huyu panya panya gani,
Anayejali cha ghalani, panya huyo mpinzani
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Panya hawanyang'anyani, wanachokula ghalani,
Kula huku kula gani, wanakula kama fani,
Si nafaka si jibini, hawachagui asilani,
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Wakiwa nje ghalani, waweza gombana njiani,
Wakishaingia ndani, panya hawafukuzani!
Watabishani ghalani, huku wakila jamani,!
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Panya hawasakamani, wakisakama utani,
Ukweli hawaambiani, wakiambiana uhuni,
Wakiwa kwao shimoni, wengine hawapatani,
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Watakatazwa na nani, wanapokula ghalani,
Kiranja afanye nini, naye ni panya makini,
Pingu ziwashike lini, panya wapo vituoni?
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Paka huyo paka gani, na atoke mji gani
Ataogopwa na nani, ghalani aletwe lini,
Kama ni kura za nani, tume ya panya jamani!
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Wamejazana Bungeni, bunge la panya watani,
Bajeti imesheheni, mambo ya kula ghalani,
Ukiwauliza mtani, utafukuzwa ukumbini!
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Panya ndani mjengoni, lao ni moja jamani,
Madongo yao mitaani, kutuhumiana magazetini,
Kamwe usiwaamini, chama chao cha ghalani!
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Wanapokuwa ghalani, hukonyezana kwanini?
Wenye kujibu jibuni, hawa panya wana nini?
Ni nini tena kwanini, na sisi tufanye nini?
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Hata nipewe milioni, kamwe panya siamini,
Siwaamini ghalani, hata walishwe yamini,
Panya hawana ubini, ushemeji wala dini,
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?
Na. M. M. Mwanakijiji (Sauti ya Kijiji)