Panya wakila ghalani.... hula na kukonyezana?

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,476
39,995
rats.jpg

Nawasalimu watani, wa bara na visiwani,
Ninalo la kuwapeni, lanitoka mtimani,​
Linatokea mijini, mpaka kwetu kijijini,​
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Ni kama hawajuani, wanapokuwa ghalani,
Ni washirika makini, kupita mchwa porini,​
Lao ni moja jamani, kweli nawaambieni,​
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Panya hawaulizani, "umefikaje ghalani?"
Ati "jina lako nani", "unatoka nyumba gani"
"Wewe panya panya gani?", "mbona kama fulani?"​
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Panya hawakatazani, wanachokula ghalani,
Kamwe hawakamatani, hata panya fataani,​
Wanapokuwa ghalani, kwao ni kama Kanaani,​
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Panya akiulizani, wale vipi cha ghalani,​
Watamuuliza namnani, huyu panya panya gani,​
Anayejali cha ghalani, panya huyo mpinzani​
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Panya hawanyang'anyani, wanachokula ghalani,​
Kula huku kula gani, wanakula kama fani,
Si nafaka si jibini, hawachagui asilani,
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Wakiwa nje ghalani, waweza gombana njiani,
Wakishaingia ndani, panya hawafukuzani!
Watabishani ghalani, huku wakila jamani,!
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Panya hawasakamani, wakisakama utani,
Ukweli hawaambiani, wakiambiana uhuni,
Wakiwa kwao shimoni, wengine hawapatani,​
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Watakatazwa na nani, wanapokula ghalani,
Kiranja afanye nini, naye ni panya makini,
Pingu ziwashike lini, panya wapo vituoni?
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Paka huyo paka gani, na atoke mji gani
Ataogopwa na nani, ghalani aletwe lini,
Kama ni kura za nani, tume ya panya jamani!
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Wamejazana Bungeni, bunge la panya watani,
Bajeti imesheheni, mambo ya kula ghalani,
Ukiwauliza mtani, utafukuzwa ukumbini!
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Panya ndani mjengoni, lao ni moja jamani,
Madongo yao mitaani, kutuhumiana magazetini,
Kamwe usiwaamini, chama chao cha ghalani!​
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Wanapokuwa ghalani, hukonyezana kwanini?
Wenye kujibu jibuni, hawa panya wana nini?
Ni nini tena kwanini, na sisi tufanye nini?
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Hata nipewe milioni, kamwe panya siamini,
Siwaamini ghalani, hata walishwe yamini,
Panya hawana ubini, ushemeji wala dini,
Panya wakila ghalani, hukonyezana kwanini?

Na. M. M. Mwanakijiji (Sauti ya Kijiji)
 
Ukizingatia li-paka letu chongo, na red-cat ime-expire....
 
Nikiwa A Level, nilinunua panya kwa ajili ya kufanyia mazoezi ya upasuaji nyumbani, panya fulani weupe sana pale medical research Mwanza, nikamuweka chumbani kwangu na kumuacha huru azunguke anavyotaka mle ndani, chakula chake biscuit; alikuwa na tabia tofauti kabisa na panya waharibifu, hakimbii watu, hakimbii mwanga, hajifichi, ukimuaproach anatulia tuliii.

cha ajabu baada ya kama wiki mbili hivi, akabadilika, ukiingia ndani huyo anakimbilia chini ya uvungu, na ndio ukawa mwisho wa mahusiano yetu, nadhani yale mapanya buku yalimconvice.

Naomba hawa panya wetu weupe na wao wasibadirike haraka huko bungeni
 
Panya ni viumbe mischevious sana. Watafanya wafanyalo wapate access ya ghalani, ikibidi hata kusiliba their kind lakini once wakiona cheese wanafanya sherehe na kugonganisha viganja kabisa achilia mbali kukonyezana.
Wanasiasa wetu ni panya na tabia ya panya ndio hizo hapo. Ni unafiki na ulafi ndio uongoza hisia za watu hawa
 
Mkuu Mwanakijiji, Swali ninakuuliza,
Panya hao wa majiji, huwa wanajiuliza?,
Au wale wa vijiji, kazi yao kujiliza?
Panya hao wa ghalani, wote ni aina moja?

Wote ni aina moja, Panya hao wa ghalani?
Au wote lao moja, kila wawapo ghalani?
Mbona kuna moja moja, wapatani asilani?
Panya hao wa ghalani, wote ni aina moja?

Panya hao ni samaki?, na ghalani ndio tenga?
Akioza ni samaki, limeoza lote tenga?
Nimepatwa na hamaki, msije mkanitenga,
Panya hao wa ghalani, wote ni aina moja?

Yaani kazi yao kula, kila wawapo ghalani,
Wote ni makula kula, kila kona ya ghalani
Hakuna wasio kula?, humo walimo ghalani?
Panya hao wa ghalani, wote ni aina moja?

Hata wale wa chadema, nao kazi yao kula?
Hata wa mwembe madema, nao pia kula kula?
Hebu tafasiri "dema", ni mambo ya kula kula?
Panya hao wa ghalani, wote ni aina moja?

Kaditama nimefika, beti sita namaliza
Ujumbe nimeufika, maswali nimemaliza
Mwisho wangu nimefika, naomba jibu maliza
Panya hao wa ghalani, wote ni aina moja?

Pasco.
 
Mkuu Mwanakijiji, Swali ninakuuliza,
Panya hao wa majiji, huwa wanajiuliza?,
Au wale wa vijiji, kazi yao kujiliza?
Panya hao wa ghalani, wote ni aina moja?

Wote ni aina moja, Panya hao wa ghalani?
Au wote lao moja, kila wawapo ghalani?
Mbona kuna moja moja, wapatani asilani?
Panya hao wa ghalani, wote ni aina moja?

Panya hao ni samaki?, na ghalani ndio tenga?
Akioza ni samaki, limeoza lote tenga?
Nimepatwa na hamaki, msije mkanitenga,
Panya hao wa ghalani, wote ni aina moja?

Yaani kazi yao kula, kila wawapo ghalani,
Wote ni makula kula, kila kona ya ghalani
Hakuna wasio kula?, humo walimo ghalani?
Panya hao wa ghalani, wote ni aina moja?

Hata wale wa chadema, nao kazi yao kula?
Hata wa mwembe madema, nao pia kula kula?
Hebu tafasiri "dema", ni mambo ya kula kula?
Panya hao wa ghalani, wote ni aina moja?


Kaditama nimefika, beti sita namaliza
Ujumbe nimeufika, maswali nimemaliza
Mwisho wangu nimefika, naomba jibu maliza
Panya hao wa ghalani, wote ni aina moja?

Pasco.

ahaaaaaaaaaaaaaaa hahaha ha ha aha ha mha mha haa
 
Back
Top Bottom