Odinga alikuja Mlimani na Makatambuga!

Sumaku

Member
Feb 17, 2009
53
1
Odinga Alikuja Mlimani Na Makatambuga!


Ya Miaka Kumi ya Kuanzia 1960: Msimamo Mkali wa Vijana wa Mlimani (11)

Born Again Pagan

Bado tunajenga muktadha wa matukio ya ki-mataifa, ki-ukanda (regional) na ki-taifa (Tanzania) uliozalisha msimamo mkali wa baadhi ya wanafunzi vijana wa Mlim,anai miaka ya 1960-hadi 1970.

Thelathini na tisa, uongozi na udamisi (joviality) wa Mwalimu Nyerere: Mwalimu Nyerere naye alikipenda Chuo Kikuu Mlimani! Alikuwa "a regular visitor", kulingana na maneno ya Mkuu wa Chuo Dr. Wilbert Kumalija Chagula. Kuna wakati alitumia kama juma moja hivi hapo Mlimani tukifundishana ya Ujamaa (A Teach-in Week on Socialism). Lakini akina Mwinyi-Mkapa-Kikwete wanawasaga tu bila kuwafundisha wananchi ya u-Bepari wauelewe!

Akina Mwinyi-Mkapa-Kikwete wanawaambia wananchi ni lazima wafuate utandawazi wa soko huria kwa sababu kila nchi inuafuata, mithili ya ngoma ya mdundiko! Hii si kweli. Utandawazi ni sera za vyama tawala na serikali zao za mkono wa kulia, hasa wakati wa Reaganomics-Thatcherism na mabaki yake.
Kuyumba kwa uchumi wa dunia leo hii kumeyafanya hayo ya Reaganomics-Thatcherism kupitwa na wakati, penda, tusipende! Kuyumba kwa uchumi kunarudisha pole pole ya vyama na serikali za mkono wa kushoto, penda, tusipende!

Wakati mwingine Mwalimu Nyerere alipendelea kuwaleta wageni wa taifa hapo Mlimani kukutana na jamii ya Chuo Kikuu na kubadilishana mawazo, kwa mfano, Rais Josip Tito wa Yugoslavia na Indira Gandhi wa India.

Mwalimu alivutwa na wanafunzi wa Mlimani. Lakini alivutwa zaidi na wana-TYL, Tawi la Mlimani. Alipokuwa na nafasi, hakusita kuwakaribisha alasiri Jumapili wana-TYL nyumbani kwake Msasani kwa vinywaji (bia na soda) na korosho za kukaangwa ili kubadilishana mawazo.

Nakumbuka siku moja alitukaribisha kwa mazungumzo. Walikuwepo wasaidizi wake: Paul Sozigwa, Joseph Butiku, Philemon Mgaya na wengineo. Mkutano ulianza kwa ukimya. Mara Mwalimu aliamuru tuletewe vinywaji kwa kuamuru, "Waleteeni vijana wangu vinywaji. Najua wakinywa bia moja au mbili wataanza kuzungumza. Wewe unakunywa nini? Na wewe?"

Vijana walioulizwa walikuwa wameketi karibu naye. Lakini sijui kwa kuogopa, waliomba soda. Mwalimu alishangaa na kuendelea, "Mwenye kutaka kunywa bia asiogope, ‘feel at home'.

Mwalimu alikoshwa sana na baadhi ya michango kutoka kwa kundi letu. Akiwa amejawa na furaha, huku naye ameshikilia glasi kubwa ya bia na kutafuna korosho, Mwalimu alitamka maneno yafuatayo (si neno kwa neno – verbatim - ila maneno haya yapo karibu karibu sana na yale aliyotamka):

Vijana, nimesikia sifa zenu! Wakati mwingine mnaacha kumalizia "homework" zenu alasiri za Jumatano zisizo na madarasa mkisaidia wananchi katika kisomo cha watu wazima na kuokota korosho hapo Mlimani kutunisha mfuko wa Tawi lenu. Na wakati mwingine nasikia kwamba mnaacha raha za wikiendi. Mnakwenda huko Ruvu kuvuna mpunga na kutoa misaada mingineyo kwa wanavijiji huko Bagamoyo! Mnawakumbuka wanyonge!

Mwalimu Nyerere alisita kidogo kabla ya kuongezea: Vijana, mnafanya kazi hizi za kujitolea hata kuwashinda viongozi wangu. Lau kama viongozi wangu wanaonisaidia wangekuwa na nia na moyo, kama ninyi, nchi yetu ingekuwa mbali katika maendeleo yake!

Huku tukipiga makofi, tuliguswa sana na tamko hilo la Mwalimu. Lakini kusoma furaha zetu na makofi tuliyopiga, mara Mwalimu alitoa changamoto kali:

Ninyi vijana ni ‘progressive'. Lakini cha kunishangaza ni kwamba mnapomaliza miaka ya ujana wenu na masomo yenu, mnabadilika; mnakuwa ma-‘reactionary, per excellence!"

Hakuna hata mmoja wetu aliyediriki kutoa mchango mchango kujibu hiyo hoja na changamoto ya Mwalimu Nyerere!

Labda, hiyo kauli ya Mwalimu Nyerere ilikuwa na utabiri unaoweza kujibu kidogo baadhi ya kero za msomaji Rugeiyamu Kahwa, kuhusu vijana akina Yoweri Kaguta Museveni na Issa Shivji wa zamani na sasa.

Makamu wa Kwanza Rais Abed Karume alikuja pia Mlimani kuimarisha umoja wa vijana wa Tanzania. Binafsi alitoa mwaliko rasmi kwa wana-TYL Tawi la Mlimani kuitembelea Zanzibar wajionee maendeleo huko Tanzania Visiwa, ikiwa ni pamoja na kukutana na vijana wenzao.

Arubaini, mtafaruki baina ya Ma-Rais Kwame Nkrumah na Julius Nyerere: Wote wawili walikuwa na malengo sawa ya ukombozi na umoja wa Afrika. Lakini kidogo walihitilafiana katika mbinu za kufikia ukombozi na umoja huo.
Rais Kwame Nkrumah alipendelea Afrika ijikomboe kwa mkupuo ili kuleta umoja huo mara moja. Zaidi, alitaka Ghana iongoze katika ukombozi wa kumaliza u-Koloni, kama ilivyoongoza katika kuanza kuutoa na kuleta uhuru.

Rais Julius Nyerere alipendelea Afrika ifikie umoja wake kwa rejareja, au ki-makundi. Zaidi, alitaka mojawapo ya nchi huru zilizokuwa karibu ya kusini mwa Afrika ndio ishike hatamu za ukombozi.

Dar es Salaam ilishinda hilo la wapi yawe makao makuu ya African Liberation Committee (Kamati ya Ukombozi).

Arubaini na moja, Tanzania ikawa ni kimbilio la wapigania uhuru kutoka kusini mwa Afrika na Komoro: Afrika Kusini: Pan-African Congress of Azania (PAC) na African national Congress (ANC); South West Africa (Namibia): South West African People's Organisation (SWAPO); Angola: Movimento Popular de Libertação de Angola - MPLA), União Nacional para a Independência Total de Angola) – Unita na Frente Nacional de Libertação de Angola; Rhodesia/Zimbabwe: ZANU-Patriotic Front (Zimbabwe African National Union -Patriotic Front) na ZAPU (Zimbabwe African People's Union) na Comoro National Liberation Movement (Komoro).

Arubaini na mbili, vyama vya ukombozi dhidi ya tawala za walowezi wabaguzi wa-Ulaya wachache wa ma-Koloni ya Kusini mwa Afrika (licha ya chama cha ukombozi cha wa-Komoro), vilibadilisha mikakati ya mapambano; vilitegemea mtutu wa bunduki, kama maadui wao walikifanya.

Kusini mwa Afrika kukawaka moto! Vita ya ukombozi vikakaribisha maprofesa wengine wenye kutaka kuandika juu ya ukombozi wa Afrika, kwa mfano, Prof. John Saul. Tanzania ikaanzisha Idara maalumu ya vipindi vya redio kwa nchi za nje (external service) iliyotumiwa na vyama hivyo vya ukombozi katika kuzikomboa sehemu hizo za Afrika zilizokuwa bado zikitawaliwa.

Arubaini na tatu, Tanzania kusaidia na kuwasetri wapigania uhuru wa Msumbiji kuliwakera sana wa-Ureno kiasi cha kushambulia kwa ndege sehemu za Tanzania huko Nachingwea. Hii ilisababisha Tanzania kujikita zaidi katika vita hiyo.

Arubaini na nne, kujitangazia uhuru wa maguvu kwa Rhodesia kuliitenga nchi hiyo, ki-mataifa, na ikawekewa vikwazo vya uchumi. Kutokana na Zambia iliyozingirwa bila bandari, ikabidi Afrika itafute njia ya kuisadia. Tanzania na Zambia zilijikita katika kupambana na vita hiyo ya uchumi ili kuikwamua Zambia. Wa-China wakajenga Reli ya Tazara (Reli ya Uhuru). Barabara ya lami kutoka Dar es Salaam hadi Zambia. Wa-Italiano wakasaidia kujenga bomba la mafuta hadi Zambia.

Arubaini na tano, Weusi wa Amerika walivutwa na Tanzania na kutaka kuja kuona mapinduzi yaliyokiendelea. Nyerere akawa ni jina tamu miongoni mwabaadhi ya Weusi hao. Kwa mfano, akina Charlie Cobb na Prexy Nesbitt walikuja kuishi kwa muda Tanzania. Wakati huo huo Stokely Carmichael "blew our minds" alipokuja hapo Mlimani na kupokelewa kwa makaribisho ya ajabu. Baada ya kuzungumza na wanafunzi na walimu, alibebwa na baadhi ya wanafunzi juu juu toka Nkrumah hadi Mess No. 1 kwa chakula cha jioni na wanafunzi.

Hapo Mlimani, kiongozi mwingine aliyewahi kupata makaribisho kama hayo ya Bwana Stokely Carmichael alikuwa ni Jaramogi Odinga Oginga – aliyewakosha wanafunzi kwa kuvaa viatu vya magurudumu ya gari (matairi) au "toka Arusha mpaka Moshi", kama viatu hivyo vilikijulikana zamani huko Arusha/Moshi.

Arubaini na sita, njama za wa-Ureno hazikuishia kuwashambulia wapigania uhuru na wakati mwingine kulipua mabomu sehemu za Tanzania mpakani na Msumbiji. Kupitia shirika lake la ki-jasusi, PIDE, lilimwua aliyekuwa kiongozi wa chama cha wapigania uhuru wa Msumbiji - Frente de Libertação de Moçambique (FRELIMO) – Dr. Eduardo Chivambo Mondlane. Kifo hicho kilisababishwa na zawadi ya kitabu alichotumiwa kwa posta kumbe lilikuwa ni bomu lililomlipua wakati alipoifungua hapo nyumbani kwake mjini Dar es Salaam.

Arubaini na saba, Tanzania ikawa ni kimbilio la wakimbizi wa-Tusi kutoka Rwanda. Ki-demokrasia, huko Rwanda, kura ya mtu mmoja mmoja iliondoa utawala wa ki-falme na unyarubanja, chini ya wa-Tusi na kuwapa wa-Hutu, nchini na kuunda dola inayotawaliwa na wananchi wenyewe (jamhuri). Wa-Tusi wengine wakawa wakimbizi kutokana na kutokutaka kuwa chini ya wa-Hutu waliokuwa wakiwaona kama ni watu duni!

Arobaini na nane, Tanzania ikawa ni kimbilio la wakimbizi wa-Hutu kutoka Burundi mpaka hivi majuzi. Ki-demokrasia, huko Burundi, wa-Tusi waliogopa ya Rwanda yasiwafike. Wanajeshi wa sehemu za Kasikazini waliamua kuingilia kati na kumtoa Mfalme wao. nchi hiyo ikawa chini ya utawala wa kijeshi, ambapo wa-Tusi wa Kasikazini walijikita kupambana na kundi la wanajeshi wa-Tusi wa Kusini, kutoka sehemu za Bururi, walifanikiwa kuendelea kuitawala nchi hiyo ki-jeshi.

Arubaini na tisa, serikali za nchi za kasikazini mwa Ulaya Magharibi, zenye msimamao wa mkono wa kushoto, zilimwaga misaada mingi sana nchini Tanzania bila ya viongozi kutembeza mabakuli ya ombaomba! Mashirika yake binafsi pia yakafanya hivyo: NORDIC, DANIDA, SIDA na Tanzania tukajikuta tunasaidiwa sana kinyume cha Siasa ya Kujitegemea!

Ujamaa ulipozidi kuzika mizizi, Nchi za Magharibi zilianza kumshutumu Rais Nyerere kwa kuchomekeza wana-harakati wake wa ki-soshalisti katika nchi tulivu za Ukanda wa Joto wa Afrika ("unleashing his guerrilla socialist locusts in the otherwise tranquil savannah landscape"). Lakini Nyerere alipona kupinduliwa na ma-Bepari wenye kuchukia mwingilio wa Ujamaa!

Hamsini, mgogoro wa Mashariki ya Kati ulijikita katika ukombozi wa wa-Palestina kutoka kuwafikiria kuwa ni wakimbizi tu kwenda katika suala la ukombozi wao. Msimamo huo uliingilia uhusiano wetu na serikali ya Israel, hususan, kufuatia vita ya mwaka 1967 ambapo Israel iliteka sehemu ya Afrika ya Sinai (Misri). Tanzania ilivunja uhusiano na Israel.

Hadi kufikia wakati huo, Israel ilikuwa imewekeza katika kuanzisha Jeshi la Kujenga Taifa, misaada mingine ya ki-Jeshi la Ulinzi na usalama, utalii (ikiwa ni pamoja na kutujengea Hoteli za ki-talii, kwa mfano, Kilimanjaro kupitia Kampuni ya Uendeleaji wa ma-Hoteli ya Molonot), biashara ya Karadha, na miradi mingine ya kilimo cha kiangazi (kumwagilia mashamba).

Uhusuiano huo ulihusu serikali. Lakini kuna watu walionufaika binafsi, pia. Kwa mfano, Mama Maria Nyerere alipata nafasi ya kwenda huko kusomea Mambo ya Nyumbani (Domestic Science) pamoja na utaalamu wa kufuga kuku hapo Kigamboni.

Makala yajayo yatamalizia matukio haya.

Mwandishi anapatikana kwa barua pepe: romuinja@yahoo.com

CHANZO: kwanzajamii.com
 
Yaani First lady alikwenda kusoma domestic science na ufugaji kuku Israel. Kweli safari ndefu.
 
Labda sababu ya utawawazi....ndio maana siku hizi wanaogopa kwenda UD na vyuo vingine kujadili .mada mbali mbali zenye manufaa kwa jamiii na mifumo ya siasa uchumi na utawala duniani.............hawajiamini au wanaogopa vivuli vyao??
 
Back
Top Bottom