Nyuma ya panzia la mitandao jamii

Kilongwe

JF-Expert Member
Feb 7, 2008
423
115
2uzs683.jpg


Tumeona takwimu zilizotolewa siku za karibuni kuwa moja ya mitandao jamii yaani Facebook wamefikisha watumiaji milioni mia tano,hiki ni kiwango kikubwa mno,sasa tunaweza kujiuliza je ni kwanini watu wengi wamekuwa wakikimbilia huko,sababu kubwa ni kuwa kizuri chajiuza na kibaya chajitembeza.Lakini hizi takwimu kwa upande mwingine zinaweza kutupa changamoto mbalimbali za kuweza kuangalia mengi yake,kwani kila siku zinavyozidi kwenda mbele ndio wana jamii wetu wengi wamekuwa wakijiunga humo,hivyo sisi kama wadau wa ICT management ni kazi yetu kuangalia kwa undani hii mitandao jamii ili tuweke wazi kila kitu ili isije kuathiri jamii yetu ya Kitanzania na Afrika mashariki kwa ujumla.

Kitu kimoja kinachoniumiza kichwa ni kuwa, kwenye mitandao hii,mtu unaweka mambo yako mengi mno wazi,ingawa kuna uwezo wa kuficha ila kwa kufanya hivyo malengo ya matumizi yatakuwa hayajapatikanika,hivyo uamuzi unabaki kwako,weka wazi ili watu waone au usijiunge,kwani katikati yake hakuleti ufanisi.Hofu yangu ni kuwa,wengi wetu tumekuwa tukijaza mambo kibao kwenye hii mitandao jamii,itakuja siku mtu atajikana mwenyewe au kubadilisha jina kwakuwa jina lake limechafuliwa sana kwenye mitandao jamii.Binafsi kuja kwa mitandao jamii kumenifundisha jambo kubwa moja,siri binafsi,nini natakiwa kuwapa watu waone na nini kitaendelea kuwa changu binafsi na watuu wa karibu tu.


Faida zinazopatikani na hii mitandao jamii ni kubwa mno,binafsi nimeweza kukutana na rafiki yangu tuliyekuwa naye tangu vidudu na shule ya msingi halafu kupoteana,kwa kutumia Facebook nimeweza kuonana naye tena tukiwa mbali mno,hii inaonesha umuhimu wa hii mitandao jamii.Mitandao jamii imeleta mapinduzi makubwa mno kwenye tovuti,mfano ni Twitter,unaweza kupata habari iliyotokea dakika chache moja kwa moja,kwa nchi zilizoendelea wamekuwa wakitumia Facebook ama Twitter kama njia mojawapo na thabiti ya kampeni,hivyo ukweli unabaki palepale bado tunaihitaji,ila kwa tahadhari.


Tatizo kubwa la hii mitandao jamii ni kuwa,kwa sekunde moja unaweza kuharibu jina na hadhi yako moja kwa moja,baya zaidi ni kuwa kitu ukishakiweka kwenye mitandao ni ngumu kukifuta tena,kwani hata kama utaondoa kuna wajanja au website zinazohifadhi mafaili hayo,pia kuna watu ambao wapo haraka,ndani ya sekunde akishaona kitu chenye muelekeo hukiifadhi kwenye kompyuta yake kwa amatumizi ya baadae. Ni wangapi wamevunja ndoa zao kwakuwa ameona picha ya mchumba yake yupo na msichana au mvulana mwingine.


Binafsi kipindi nikiwa webmaster wa website ya wanafunzi wa kigeni hapa Wuhan,China,pia tulikuwa na ukurasa wa facebook(facebook page),nilikuwa napokea malalamiko kila kukicha watu wakilalamika kufuta picha kadhaa zilizowekwa na members zikiwaonesha wakiwa kwenye majumba ya starehe kwakuwa nyumbani wakijua ni mwisho wa shule,Niliwahi kujiwa na mdada wa kisomali huku akilia kwakuwa kama ile picha ikionekana kwao basi ana adhabu kali mno.Kumbuka jamabo unaloliona ni la kawaida leo linaweza kuwa ni kizingiti kwako miaka kumi ijayo kwani watu huifadhi kumbukumbu hadi pale itakapokuwa na umuhimu.

Tukiachana na hayo hebu tuangalie mambo mengine yaliyo nyuma ya panzia la hii mitandao jamii.


Kusaka ajira


Siku hizi kuna baadhi ya wajiri hutaka kupata kumbukumbu za mhusika kwenye facebook ama Twitter kwa siku za karibuni,kwani wao wanatambua au kuamini kuwa huko wanaweza kukujua wewe halisi,unaweza kusema njia ni rahisi tu,nitafuta,ila sio kila kitu kinafutika pia sio rahisi kwako kujua kama watahitaji hivyo unajikuta unapambana nayo siku ya siku..


Kwa kutumia mitandao hii unaweza kumjua mtu katika hali halisi na sio majificho ndani ya interview.Nimewahi kuongea na muajiri mmoja kuhusu hili,yeye alisema kuwa jambo muhimu katika kuajiri ni kupata mtu asilia na anayeweza kufanya kazi kwa timu na mahali pa kuzipata hizi ni kwenye mitandao jamii.

Kupoteza ajira


Wangapi wamekuwa wakipoteza kazi kutokana na ujumbe wao walioweka kwente facebook au Twitter,nimewahi kusoma makala moja,jamaa alikuwa na matatizo na Bosi wake,yeye akaamua kuhamishia bifu kwenye facebook,akaweka ujumbe mzito pale,watu bila kuchelewa wakaanza kumalizia asira zao za zamani na yule bosi,basi mpaka bosi anapelekewa taarifa na wapambe wake tayari alikuwa kashavulika nguo,unategemea nini kitafuata? Sio hilo tu,wewe uunaweza kuwa na lengo zuri labda la kutaka kuomba ushauri kwa marafiki zako lakini kila mtu ana uwezo wake wa kupambanua mambo na hao ndio watakaokuweka matatani.


Kutilia mkazo hili,kipindi kimoja nilikuwa manager kwenye sehemu fulani,tukaandaa sherehe,baada ya sherehe kuna member wetu wa ndani alituma picha kwenye facebook kumuonesha mfanyakazi mwingine aliyekuja kwenye sherehe kama anaenda msibani na akaacha kibwagizo,msiba au sherehe?,watu waliacha maoni ya kudharirisha.Ilinibidi nifanye maamuzi magumu pale ya kumuondoa mhusika kwenye kile kitengo.

Marafiki wanaokuzunguka


Sio siri ukweli ni kuwa maranyingi marafiki zako huweza kutoa picha yako kamili,hapa ninamaanisha watu wanaweza kukujua au kukuthaminisha kutokana na kundi la marafiki zako,kipindi nikiwa mtoto nilikuwa napewa mafundisho kuwa ukitembea na mwizi nawe utakuwa mwizi hivyo nilitakiwa kuwa na marafiki wanaofanya vizuri darasani,kuna methali kadhaa za kiswahili zinazotilia mkazo hili(Ukitembea na muuza….[imenitoka kidogo]).


Sasa siku hizi kuna baadhi ya watu hupenda kukuthaminisha kutokana na kundi la marafiki ulionao kwenye mitandao jamii,inawezekanika wewe mwenyewe hujui hili ila lipo.Baadhi ya mabenki ya nchi fulani fulani wamekuwa wakitumia hii kuangalia kipato cha marafiki zako na wewe binafsi kwa kuangalia picha na maisha yako halisi,unatumiaje pesa zako,unamiliki nini nk ili kupitisha mikopo yote haya yanaweza kupatikanika ndani ya mitandao jamii.

Mahusiano


Inawezekana kuwa mpenzi au mchumba wako ni mmoja wa marafiki zako kwenye facebook au twitter,na ataendelea kuwa rafiki,kumbuka wengi wetu tumekuwa tukiona wapenzi wakitoa maoni mbalimbali juu yao yakiambatana na ahadi kemkem,watu wanaangalia na kuyahifadhi,nani anajua nini kitatokea kesho? unaweza kujikuta unajiingiza kwenye msongo wa mawazo.Kuna rafiki yangu aliwahi kuandika maoni ya kwenye picha yake ya harusi kwenye facebook kuwa "Sisi tumechaguliwa na mungu,siku nitapoachana nawe basi kichwa changu kata",ujumbe kama huu unaweza kukusababishia matatizo baadae,oho,watu watataka kuja kukichukua kichwa chao.Kwani mapenzi ni mapenzi,nani anajua nini kitatokea kesho?


Mahakamani


Sina uhakika kwa nyumbani,ila kwa nchi za wenzetu mawakili au mahakimu hutumia sana kumbukumbu za mitandao jamii kupata ukweli wa jambo fulani,ujumbe ulioandika miaka mitatu iliyopita kuhusu kumchukia kwako bwana Kilonge inaweza kusaidia mawakili kukupata kiundani,mfano mzuri tu kuna kipindi nilikuwa nafanya utafiti wa jamaa waliokuwa wanatuma e mail za kashfa kwenye yahoo group letu.Baada ya kupitia njia fulani fulani za Forensic nikaja mwisho kutumia mitandao jamii kumbaini ni nani aliyekuwa anafanya maupuuzi,tangu hapo alikuwa mpole kwani nilimtumia kila kitu kuonesha uhusiano wake.


Hitimisho

Kuna usemi wa kingereza unasema "an elephant never forgets".Sasa kumbuka kuwa Internet nayo haisahau kwenye internet kuna idadi kubwa ya hazina ya kumbukumbu ambayo inaweza kupatikanika ndani ya sekunde ,ahsante mitandao kama Google inayotuwezesha kupata mambo matamu kama haya.

Binafsi sitaki kuwatisha au kuwafanya watu wanze kutumia majina bandia kama kwenye sehemu fulanifulani za udaku,ila napenda ukutilia mkazo, kuwa makini juu ya kitu gani unatuma na kitu gani kitaendelea kuwa kwenye hazina yako,tafakari kwa undani na sio kujitumia kwani ipo siku unaweza kujijutia na kuichukia hii mitandao jamii. Nimeongelea machache tu ili mada isiwaboe
 
Back
Top Bottom