Nini maana ya kuwa msomi na mtaalamu wa fani husika

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
266
Nini maana ya kuwa mhitimu katika fani au sekta husika? Je Watanzania wasomi tunaelewa maana halisi ya kujishughulisha na fani/utaalamu fulani au kusomea fani hizo kama ijulikanavyo na wengi wa wanafunzi katika Vyuo na taasisi mbalimbali za elimu ya juu hapa nchini? Ionekanavyo ni bado hatujaweza kuzitumia fani/taaluma hizo kwa maendeleo ya nchi yetu, Je tatizo liko wapi na ni kwanini basi kuwepo na hali hiyo? Fuatilia makala hii ili tusaidiane mawazo katika kueleweshana na kujaribu kupata ufumbuzi wa tatizo hili ndani ya jamii ya watanzania.

Ni wangapi walioko katika fani mbalimbali hapa nchini wanaweza kujivuna kuwa wamechangia kwa kiwango cha kupigiwa mfano au hata kiwango cha chini kabisa katika fani zao? Kama ni kuwataja basi itakuwa ni wachache sana ikilinganishwa na idadi ya waliosomea fani/taaluma hizo husika. (Najua sio wengi kama ipasavyo kuwa). Ni katika siasa tu ambako kwa matazamo wangu kuna mengi lakini mimi sitazungumzia huko. Sina maana kuwa sithamini mchango wa wanasiasa, la hasha ila katika makala hii sikusudii kuangalia masuala ya wanasiasa.




Tumekuwa na watu wachache sana katika nchi yetu ambao wamewajibika kiukweli na kupigiwa mfano katika fani/taaluma zao, wengi wetu tumekuwa tukibabaisha na tunaingia humo zaidi kwa kutafuta maslahi binafsi tofauti kabisa na wenzetu katika nchi zilizoendelea. Zaidi sisi tunatafuta pesa na ulwa kwa ajili ya maslahi binafsi. Tunachangia kwa sababu tutapata maslahi binafsi, kama hakuna maslahi basi tunaacha na tunajifanyia mambo yetu binafsi, kinyume na maana halisi ya kuingia katika fani/taaluma husika.

Kwa kupitia ripoti na vitabu tofauti nilivyosoma nimeweza kujifunza kidogo na kwa kiasi ambacho nasema ninaweza kuandika na watu wakasoma tukaelewana ni nini nakusudia kuwasilisha kwa wasomaji wangu kuhusu dhana ya fani katika maisha yetu ya kila siku humu duniani. Kuna msemo mmoja maarufu sana ambao kwa tafsiri yangu binafsi unajulikana kama “Mtu hawezi kuwa wa fani zote”.

Katika kugawana majukumu na ili kuweza kupata maendeleo, jamii inatakiwa iwe na watu wa fani mbalimbali katika sekta nyingi zilizomo ndani ya jamii husika. Na kadri siku zinavyokwenda mbele na kugunduliwa kwa vitu vipya, fani mpya nazo zinaibuka kutokana na wakati na mabadiliko ya muda huo uliopo. Yote hayo ni katika kugawana majukumu, haiwezekani mtu mmoja akawa na utaalamu katika sehemu mbalimbali, nakubali kuwa wapo watu wa aina hiyo lakini ni wachache na mchango wao unakuwa sio wenye ufanisi.

Kuna baadhi ya fani zipo tokea maisha ya mwanaadamu yalivyoanza kama vile matabibu wa afya ya binaadamu na wanyama, wanafizikia, wanachemia au kwa ujumla wao tunawaita wanasanyansi, waalimu na kadhalika. Hii yote inaonyesha kuwa wanahitajika katika kusaidiana kuendesha maisha ya kila siku katika jamii husika. Hakuna jamii/nchi isiyotegemea wataalamu katika fani mbali mbali kwa maisha ya kila siku.

Kinachonisikitisha ni mtazamo wa wengi (sina takwimu kamili) kupitia mazungumzo ya kawaida kwa wanaosoma hivi sasa, kutokana na mfumo mbovu na uongozi usio na dira ya wapi na nini kinatakiwa kwa maendeleo ya nchi hii, wengi wa vijana na wanaosomea fani mbalimbali katika Tanzania hii hawana mpango wa kuzitumikia fani hizo mara baada ya masomo yao.

Wanachokisema ni kuwa “nasoma ili niweze kuishi katika ulimwengu huu wa wasomi, maana bila ya elimu ya Chuo kikuu sitoweza kupata kazi”, hii ni hatari na wahusika hawana budi kulifanyia kazi suala hili. Hali ilivyo inajionesha dhahiri wala haihitaji utafiti wa kina kama unaweza ulizia tu wanafunzi wachache unaowafahamu halafu utaona majibu yao. Tuangalie tu mfano mdogo wa wahitimu waliotoka katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine katika kipindi cha miaka ishirini iliyopita wako wapi, je ni kweli wote wako katika fani mbalimbali za kilimo? Na kama hawapo, wako wapi na kwanini iwe hivyo? Kuna sababu gani ya kusomesha wataalamu wote hao halafu hawatumiki katika fani husika?

Haya ni baadhi tu ya maswali ambayo walioko madarakani na jamii inapaswa kujiuliza na kuyapatia suluhisho na bila ya kufanya hivyo hatuwezi kupata maendeleo hata siku moja. Haiwezekani mtu asomee kilimo miaka mitatu kwa ajili ya shahada ya kwanza halafu mtu huyo aende akahesabu fedha benki, hivi inaingia akilini kweli? Halafu tunasema tuna viongozi wako madarakani na wanafanya kazi na mishahara wanapata kutokana na kodi za wananchi?

Sikatai kama mtu huyo atatumia utaalamu wake aliosomea katika kuboresha mazingira ya kazi hiyo nyingine anayoifanya, mfano kama vile aliyesomea kilimo halafu akaamua kuwa mwandishi wa habari. Huyu anaweza kusaidia sana kuandika kwa ufanisi kama atapata misingi ya uandishi. Lakini inapokuja mtu huyu akaenda kufanya shughuli ambayo kwa muda wote hatumii kabisa kile alichojisomea ni hatari kwa maendeleo ya nchi yetu.

Lakini mbali ya kulaumu na kuwashangaa viongozi tunamfikiria na kumuweka wapi yule ambaye amekaa darasani miaka mitatu mpaka mitano kwa fani husika na kufanya japo kazi ndogo ya kiuchunguzi/kitaaluma katika fani hiyo husika halafu anaiacha fani hiyo na kwenda katika fani ambayo sio yake kabisa ila kutokana na kupata elimu ya Chuo Kikuu ameweza kuwa na uwezo wa kufanya kazi nyingine. Je ni haki kweli?

Nasema ni haki kweli sio kwa mhusika bali kwa fani husika kutendewa hayo yanayotendwa hivi sasa na wengi wetu tunaopata bahati ya kusoma. Kwa ujumla maswali ni mengi kuliko majibu. Na yote hii ni kutokana na hali halisi ya mfumo mzima wa nchi ulivyo na narudia tena kusisitiza kupitia makala zangu mbalimbali hii yote ni kutokana na viongozi walioko madarakani kutokuwa na dhana ya ujasiriamali katika utendaji wao wa kila siku.

Wengi wanaweza kusema sio tatizo kubwa hili suala la kutofanya kazi au kuwa katika fani ambayo mtu amesomea, sina tatizo ni uamuzi binafsi wa mtu kuchagua anachotaka kufanya, lakini kwanini tutumie fedha chungu nzima ya walipa kodi halafu watu wasiwalipe hao walipa kodi kile ambacho wanapaswa kuilipa jamii kutokana na mchango waliopewa? Kama ulijua awali hutofanya kazi katika fani husika kwanini utumie fedha nyingi kiasi hicho bila ya faida?

Fikiria kama wanafunzi wa shahada ya kwanza wapatao 2,698 (1996-2005) ambao wamehitimu katika fani mbalimbali za kilimo na ufugaji wangeingia katika fani zao na kufanya kile ambacho kimewapelekea kuingia katika fani hizo na kufanikiwa kutunukiwa shahada katika fani husika hakika hii nchi leo isingekuwa hapa ilipo. Wenzetu wanaendelea kwa sababu ya kutumia fani zao katika sekta mbalimbali, lakini hapa kwetu ni kinyume cha hapo sasa na tujiulize tunafanya nini?

Wajibu hauko sehemu moja tu, serikali kama mtendaji na mwezeshaji mkuu inapaswa kukaa chini na kujipanga upya, hatutoweza kufika popote kwa kudharau wataalamu katika fani mbalimbali ndani ya Taifa hili, na jinsi hali ilivyo inaonesha ni dharau kwao, kwani mishahara na mazingira ya kazi ya waliosomea hayaridhishi na hilo ndio mojawapo ya tatizo la watu kukimbia walichokisomea na kufanya shughuli nyingine katika maisha.

Haiwezekani kama ni daktari anahitaji chombo au mazingira fulani ya kazi ili kuweza kutoa huduma husika kwa ufanisi asiwe na hicho kitendea kazi au mazingira yasimruhusu. Matokeo ya hayo ni kutokuwa na ari na furaha ya kazi yake. Lakini cha ajabu na kusikitisha, mkubwa wake yuko katika ofisi yenye thamani ya mamilioni ya fenicha pamoja na magari ya gharama kubwa kabisa. Inashangaza lakini ndio hali halisi tuliyonayo ndani ya nchi hii. Hatujui au tunafanya kusudi kutosheleza maslahi binafsi na kusahau jamii kwa sehemu kubwa. Tunapaswa tubadilike kama kweli tunataka maendeleo.

Lakini pia mfumo wa elimu ulivyo nafikiri hautoi nafasi pana kwa wanaosomea taaluma mbalimbali kuelewa maana halisi ya wao kuwa katika taaluma hizo. Kwani naamini kama watafundishwa umuhimu wa wao kuwa katika hizo fani na miiko na maadili ya fani hizo, ni vigumu kwao kuweza kuzikimbia mapema kama ilivyo sasa. Hata ukiangalia jinsi ya vitabu vya utambulisho vya vyuo na taasisi zetu za elimu ya juu hazichambui na kuelezea fani husika kama ambavyo ukiangalia vitabu kama hivyo katika vyuo vya wenzetu hao wanojulikana wameendelea.

Mapema mwanafunzi anajetaka kujiunga na fani husika anakuwa na mwelekeo halisi wa nani atakuwa ndani ya jamii pamoja na maeneo yote ambayo yeye baada ya kumaliza shahada yake anaweza kuyafanyia kazi. Leo jaribu kupitia wanafunzi walioko Vyuoni uwaulize utakapomaliza hapo anategemea kuwa nani au nini mipango yako ya baadae usikie atakachokuambia, zaidi ni kuwa na gari, nyumba nzuri na maisha ya starehe, lakini sio kuchangia maendeleo kupitia fani yake au kuifanya hivyo fani ikubalike zaidi ndani ya jamii.

Hii inajionesha wale walioko katika fani husika wanakiuka miiko na maadili ya kazi zao. Naamini kama msisitizo ungelikuwepo tokea mapema ni vigumu kwa kiasi kikubwa wataalamu hawa kukiuka miiko na maadili hayo. Na kama wanafundishwa hayo maadili na miiko basi sio kwa dhati na kwa ufanisi. Walio vyuoni hawana budi kuangalia upya ufundishaji wao kwani hakutokuwa na faida ya kusomesha wataalamu halafu wasomi hao hawaonekani wakitoa mchango wowote katika fani na taaluma husika.

Kuwepo kwa jumuia za fani husika kama vile madaktari, mafamasia, wahasibu, na kadhalika nako kwa kiasi kikubwa kunachangia kuboresha na kuzungumzia maslahi na matatizo yanayozikumba fani husika. Lakini cha ajabu ni kwamba hatujasikia wakilalamika juu ya hali ilivyo sasa ya watu kutofanyia kazi fani zao jambo ambalo linazidi kushika kasi miongoni mwa vijana na wasomi wa sasa.

Hakika tunapaswa kuelewa kuwa dunia ya leo ni utaalamu hakuna ubabaishaji katika sekta yoyote ile kama kweli tunataka kuwa na maendeleo kama ya hao wenzetu. Inaeleweka kuwa waliosoma wako wachache sana katika Tanzania hii, kwani asilimia karibu themanini ya wakazi wako vijijini na ambako ndiko wasomi wanatakiwa kufika ili kufikisha utaalamu wao kwa maendeleo.

Sasa kama hawa wachache wanaopata bahati ya kusoma na kushindwa kutumia utaalamu wa fani zao kusaidia huo umati ulioko vijijini ni lini tutapata maendeleo? Ubaya zaidi unakuja pale wachache hao wanapokimbia kuajiriwa au kujiajiri katika fani zao na vile vile kukimbilia nje ya nchi kwa ajili ya kujiridhisha kitaaluma na pia kwa maslahi binafsi huku waliochangia yeye kuwa katika kiwango hicho alichofikia wakiachwa hoi na kushindwa kujua nini wafanye.

Ni jukumu la pamoja wachache waliopata bahati ya kuwa katika fani husika kuweka mikakati na kuangalia wapi watu walipojikwaa na kutafuta suluhisho badala ya kukaa na kulaumiana. Lawama hivi sasa hazitoweza kusaidia tutafute suluhisho kwa maendeleo ya Taifa hili sasa na kwa kizazi kijacho. Tuache kuweka maslahi binafsi mbele haitosaidia nchi hii, tufikirie na wengine walioko ndani ya jamii kwani wanatuhusu wote.

Wizara na taasisi husika zinapaswa kuona kuwa wale wote waliosomea fani husika wanapata ajira. Haiingii akilini kwa kuwa katika nchi hii bado tuko nyuma kwa idadi ya wataalamu katika fani mbalimbali lakini wataalamu hao katika fani husika kukosa ajira?! Sitaki kuamini kuwa nafasi za kazi zimeshajaa kiasi hicho hadi tunafikia mahali watu wanakimbia fani zao na kwenda kufanya kazi ambazo ziko nje ya taaluma zao.

Kama tumefikia hapo basi hakika tuna tatizo katika ajira, tatizo ambalo naweza kusema la kuajiri watu wasio na utaalamu katika kazi zao. Hii ni hatari, hutuwezi kuwa na wataalamu halafu wasipate kazi kama ambavyo hali ilivyo sasa. Haiingii akilini hawajawa wengi kiasi hicho cha kukosa ajira, tutafute suluhisho.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom