Bazazi
JF-Expert Member
- Aug 18, 2008
- 2,806
- 3,476
Hivi neno UPENDO linamaanisha nini hasa? Maana yake ni nini hasa ukizingatia kuwa imesemwa/inasemwa/itasemwa kwamba upendo ndio uhitaji mkubwa zaidi wa Wanadamu. Tangu wanapozaliwa hadi kufa, watu hutamani kupendwa, wanaishi kwa furaha wanapopendwa na hata wanadhoofika na kufa wasipopendwa. Bila shaka, watu huongea sana kuhusu Upendo. Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kuwa sio rahisi kuelezea maana ya Upendo. Baadhi ya wachambuzi wamefikia kukata kauli kuwa Upendo unaweza kuonyeshwa tu kupitia matendo.
Tunaweza kupata ufahamu wa ndani wa neno hilo kutokana na maneno ya awali (ya Kiyunani) yaliyotafsiriwa Upendo katika Biblia (ya Kiswahili). Neno UPENDO linatokana na kutafsiri maneno manne (ndio aina nne za upendo) ya Kigiriki cha mwanzo/awali. Maneno hayo ni;
· PHI·LE´O
· STOR·GE´
· E´ROS
· A·GA´PE
PHILEO: Kitenzi kinachomaanisha kuwa na shauku, kuthamini au kupenda (kama mtu anavyompenda rafiki wa karibu au ndugu). Hutumika mara nyingi katika Agano Jipya baada ya neno Agape.
STORGE: Upendo ulio kati ya watu wa familia moja. Huu ndio upendo ambao Paulo mtume alisema una/utakuwa haba katika siku za mwisho (2Tim 3:3).
EROS: Upendo wa kimahaba kati ya watu wa jinsi tofauti. Upendo huu hautajwi katika Agano Jipya bali katika Agano la Kale (Mith 5:15-20).
AGAPE: Upendo unaoongozwa na kanuni na unatia ndani mambo mengi; unahusisha fikira na una kusudi fulani na hauna ubinafsi. Upendo huu sio hisia tunayokuwa nayo bila kufikiri. Mara nyingi huhusisha uhusiano wa karibu wenye upendo. Agape ndilo neno linaloelezea Upendo kwa njia nzuri zaidi. Aidha kati ya maneno hayo yote kuhusu Upendo; Agape limetumika mara nyingi zaidi katika Agano Jipya.
Kwa ujumla (mara nyingi) aina zote zinastahili na zinabidi ziende pamoja. Mfano: Ni kweli upendo wa kimahaba (eros) una sehemu yenye maana sana katika ndoa zenye mafanikio; shauku yenye kina kirefu na urafiki (philia) huongezeka kati ya wanandani na huimarishwa na upendo (agape) ambao hustawishwa kumwelekea Mungu, Kristo na Jirani Yetu (Zetu).
Kwahiyo, neno hilo (Upendo) ni neno ambalo lime/lina/litatumiwa sana na wanadamu. Ni neno ambalo limeandikiwa vitabu, likatungiwa nyimbo riwaya na mashairi mengi mno. Pamoja na hayo mara/ nyakati nyingine halifafanuliwi ifaavyo/ipasavyo. Ni neno ambalo lime/lina/litatumiwa sana hivi kwamba inaonekana (limeanza) kupoteza maana yake halisi (mfano ushoga, usagaji na ukahaba).
NB: Je wajua kuwa Upendo ndio sifa kuu zaidi ya Mwenyezi Mungu?