Pdidy
JF-Expert Member
- Nov 22, 2007
- 50,720
- 21,779
Nimeanza kumtamani Lukuvi
PDIDY
PDIDY
SIKUPATA kufikiri hata siku moja kuwa, William Lukuvi, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, anaweza kukifikilisha kichwa changu kiasi cha kupoteza muda wangu kumjadili katika safu yangu ya mchokonozi.
Siku zote nimekuwa nikimuona mwepesi sana licha ya kushikilia nyadhifa mbalimbali katika chama chetu cha maulaji kinachounda serikali ya kufikirika.
Nimekuwa nikimsikia muda mrefu kuwa naye ni kiongozi, kuwa alikuwa waziri, ni mbunge na mkuu wa mkoa, lakini mpaka leo sijui huwa anaongoza nini! Walah naapa, sijui!
Nimewahi kumuona kwa karibu mjengoni huko Dodoma katika vikao vyetu vya kujadili mambo nyeti yasiyotekelezeka yanayolihusu taifa letu, lakini hakunivutia hata kidogo, hivyo sikuona hata sababu ya kumpa salamu yetu ya jeuri ya chama. Nilimpotezea!
Nilimpotezea kwa sababu muonekano wake ulikuwa haufanani na ule wa huyu ni mwenzetu. Nilimuona kama mtu mjivuni asiye na tofauti na staa fulani wa filamu, kama sikosei za Kinaijeria au kibongo na macho yangu ya siri yalimuona kama blaza man fulani ambaye alifika mjengoni kuangalia namna sisi tuliobahatika tunavyoendesha shughuli zetu huko na kuishi maisha bora.
Lakini hata baada ya kubaini kuwa ni kiongozi, tena mbunge na mkuu wa mkoa wakati huo akiwa Dodoma, sikuwahi kumsikia katika duru zetu za siasa za kifisadi au zile za maji taka.
Si hivyo tu, katika uhai wa Bunge hili la viwango na kasi, sijawahi kumsikia akizungumza neno lolote kuchangia mjadala hata wa wizara ya waziri wa nchi asiyekuwa na ofisi maalumu.
Nieleweke jamani, kuwa sijawahi kumsikia akisema hata maneno ya hovyo hovyo mjengoni. Hivyo hata nilipomuona nje ya ukumbi wa mjengoni, sikuwa na habari naye kabisa.
Kwa mara ya kwanza nilianza kumsikia baada ya Jiji la Dar es Salaam kutikiswa na mlipuko wa mabomu yaliyokuwa yamehifadhiwa katika kambi ya jeshi Mbagala.
Kati ya yote aliyozungumza, nilivutiwa na moja tu la kuwataka wakazi wa Mbagala kuwa wavumilivu kama wa Kipawa wanaoumizwa masikio yao kila siku na kelele za midege mikubwa na midogo inayopita karibu sana na makazi yao. Siku hiyo si siri, nilianza kumtamani Lukuvi kwa kauli zake.
Sikushangazwa na kauli yake hii kwa sababu tangu siku ya kwanza nilipomuona sikumkubali kama kiongozi.
Hivyo hata kauli yake hiyo nilijiaminisha moyoni kuwa kama kweli aliitoa, alikuwa sahihi kwa sababu kwangu mimi hana sifa za uongozi hata ule wa ngazi za chini kabisa, yaani kitongoji au kijiji. Kwa maneno mapesi na sahihi, hafai!
Majuzi tena nilisoma habari magazetini zilizomnukuu akieleza wazazi wa watoto watakaochaguliwa kujiungna na kidato cha kwanza mkoani Dar es Salaam, wajiandae kuwanunulia madawati watoto wao.
Yaani kila mzazi wa Dar es Salaam ambaye mtoto wake atafaulu kujiunga na kidato cha kwanza katika shule yoyote ya sekondari jijini, ajiandae kumnunulia mwanawe dawati. Baada ya kuisoma habari hiyo, nilianza kuitilia shaka akili yake ya kawaida na ile ya ziada.
Shauku ya kutaka kujua historia yake ilinijia, nilitamani kujua kiwango cha elimu yake na shule aliyosoma.
Nilipata shauku ya kutaka kuwajua watoto wake, kama anao, wanasoma shule gani na iwapo amekwisha kuwanunulia madawati na kuyapeleka shuleni, na zaidi ni nilitamani kuwaona wazee waliomuona Lukuvi wakati akiwa mwanafunzi ili wanieleze mazingira aliyosomea na maendeleo yake darasani yalikuwaje. Nilitaka pia kuwauliza kama baba yake alikuwa akiichukuliaje michango ya kipuuzi kama huu uliotangazwa sasa na Lukuvi.
Hii ni kwa sababu sikupata kufikiri hata siku moja kama taifa letu linaweza kuwa na kiongozi wa aina ya Lukuvi ambaye wakati anaowaongoza wanaokufa kwa kukosa hata sh 100 ya kununulia dawa ya malaria, yeye anaibuka na kuwataka ambao watoto wao wamechaguliwa kujiunga na elimu ya sekondari kuwanunulia dawati ambalo thamani yake ni maelfu ya shilingi.
Nadhani nilikuwa sahihi kabisa nilipomtizama Lukuvi na kumuona kama mcheza muvi.
Ninaamini hivyo kwa sababu kwa kauli yake hii haina shaka kuwa hafahamu kuwa moja ya tatizo linaloikabili sekta ya elimu ni kushuka kwa kiwango cha ubora kwa elimu ya shule ya msingi na sekondari kwa sababu walimu wamegoma kufundisha.
Lukuvi hajui kuwa wanafunzi wanafundishwa masomo mawili au matatu kwa wiki katika shule nyingi hapa jijini na shule nyingine hawafundishwi kabisa, leo ni miezi kadhaa?
Wazazi wana jukumu la kujikamua ili kulipa gharama za masomo ya ziada kwa sababu bila kufanya hivyo hakuna wenye kuumia ni wao.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam hajui hayo, anapopita katika barabara za jijini akiwa ndani ya gari la kifisadi akivinjari huku na huko na kuwaona wanafunzi wakilandalanda barabarani, anafurahi kwa sababu hajui kuwa shuleni hawasomi, bali wanakwenda kuzurura na kusubiri muda wa kusoma tution.
Lukuvi hajui kama utitiri wa shule za sekondari zilizojengwa sehemu mbalimbali hapa nchini ambazo mimi huzilinganisha na uchafu, kwa sababu zipo maboma tu yasiyokuwa na madawati wala walimu, hazikupaswa kujengwa kwa sababu ni kero nyingine kwa Watanzania?
Yaani baada ya kuwakamua wazazi kuchangia ujenzi wa shule, sasa anataka wakamuliwe tena kununua madawati. Hapo bado michango mingine mingi ya kipuuzi, huku walimu wakiwa hawapo.
Ni mwendawazimu peke yake anayeweza kumchukia Lukuvi, ambaye hajui kuwa Watanzania sasa wanalia kwa jinsi wanavyozidi kusinyaa kwa maisha magumu huku viongozi wao wakizidi kunawili kwa pesa ya kodi wanazolipa maskini hawa.
Ni mwendawazimu tu anayeweza kumchukia badala ya kumpenda mtu wa aina ya Lukuvi ambaye kwa maneno yake anaonyesha hajui kuwa sasa walimu wamekata tama, hivyo hata kama kila shule itanunuliwa madawati mpaka msalani, kamwe kiwango cha elimu hakitapanda kwa sababu hawako tayari kufundisha mpaka watakapolipwa chao.
Pengine nimuombe Lukuvi, kuwa badala ya kuanza kushinikiza wazazi kuwanunuliwa watoto wao madawati, aanze kwanza kupitisha bakuli kwa wazazi kuchangisha fedha zitakazotumika kuwalipa walimu mishahara. Nisichukue muda mrefu kumjadili mtu huyu, William Lukuvi, kwa sababu yeye kama Lukuvi kwa jinsi nilivyomuona tangu siku ya kwanza, alikuwa sahihi kutoa kauli kama hiyo, lakini kama mkuu wa mkoa alikosea. Na alikosea, kwa sababu ninaamini hafai kushikilia wadhifa huo. Tumuombee adumu katika wadhifa wake huu, ili tuzidi kumfahamu vizuri zaidi.