Ni kweli balozi zetu nje ya nchi zimeishiwa fedha?

Mwanajamii

JF-Expert Member
Mar 5, 2008
7,063
68
Balozi ziko hoi kifedha. Ni taarifa iliyowekwa wazi na vyombo vya habari leo. Hii taarifa imekaaje?

Tusaidiane kutafuta ufumbuzi, matusi tuweke pembeni. Tujenge hoja namna ya kujinasua na hali hii.


CHANZO: NIPASHE 14 FEBRUARI, 2012


MABALOZI WA TANZANIA HOI

Ni ukata mkali hadi mishahara hakuna
Katibu Mkuu asema hali ni tete mno


Wakati Serikali ikikabwa koo na madaktari juu ya madai ya nyongeza ya posho na mishahara yao, hali kadhalika walimu wakiwa wamekwisha kutoa ilani juu ya nyongeza ya mishahara yao, imethibitika kwamba Ofisi za Tanzania nje ziko hoi kutokana na kukosa fedha za matumizi ya kawaida.

Kama haitoshi, baadhi ya balozi zinadaiwa kuendeshwa bila mishahara kwa kipindi kirefu sasa, hali inayovunja heshima na hadhi za ofisi hizo ughaibuni.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, John Haule, alibainisha hali hiyo jana jijini Dar es Salaam mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC).

Haule alisema kwa mwaka 2011/2012, serikali ilitenga Sh. bilioni 150 kwa ajili ya matumizi ya kawaida, lakini Hazina iliwapa Sh. bilioni 80 na kwamba hatua hiyo imeifanya wizara yake kuwa na wakati mgumu katika kulipa mishahara pamoja na kugharamia uendeshaji wa ofisi za balozi.

Alithibitisha kuwa, kushuka kwa sarafu ya Tanzania kunachangia hali hiyo na kwamba serikali inashindwa kumudu kulipa mishahara kwa kuwa watumishi wa balozi za Tanzania wanaolipwa kwa Dola ya Marekani kutokana na bajeti kutengwa kwa kutumia shilingi.

"Nikiri kwamba hali katika balozi zetu ni mbaya kutokana na ukata unaoikabili wizara yangu ambayo inaziangalia balozi hizi," Haule aliwambia wajumbe wa kamati hiyo ambayo Mwenyekiti wake ni Mbunge wa Bariadi Mashariki (UDP), John Cheyo.

Haule aliongeza kuwa, bajeti ya kuzihudumia balozi za Tanzania inazidi kupungua mwaka hadi mwaka. Ingawa hakutoa takwimu, lakini alisema hali hiyo imekuwepo kwa kipindi cha miaka saba hadi sasa.

Katika kudhibiti matumizi ya fedha kidogo ambazo wizara yake inatengewa na serikali, Haule aliambia kamati hiyo kuwa serikali imezuia mafao ya aliyekuwa Balozi wa Tanzania, Abu Dhabi, Falme za Kiarabu, Mustafa Nyang'anyi, baada ya kubainika kwamba alitumia fedha za huko Dirham 31,000 (Sh. milioni 13, 402,081.20) bila kuzitolea maelezo.

Haule alisema kuwa, zaidi ya shilingi milioni tano alizostahili kulipwa kama mafao zimezuiliwa na kwamba serikali itaendelea kumdai fedha zingine kwani hizo hazitoshi kulipia kiasi anachodaiwa.

Kuhusu mahusiano ya kimataifa, Haule, alisema Tanzania imefunga ubalozi wake nchini Uholanzi kutokana na matatizo mbalimbali yakiwemo ya kupishana mtazamo wa masuala mbalimbali.

Kwa upande wake, Cheyo, alisema anasikitishwa na kitendo cha serikali kushindwa kuwalipa mishahara watumishi wake katika balozi zake.

Cheyo alisema mtumishi akiwa hapa nchini akikosa mshahara angalau anaweza kwenda kukopa kwa ndugu yake, lakini anapokuwa nje ya nchi anapata shida na kuishia kukopa benki.

Alisema ni aibu kwa Tanzania kuendesha ofisi zake za nje kwa kuhaingaika na kwamba lazima serikali ihakikishe inachukua hatua na kumaliza tatizo hilo.

"Kwa miaka 50 ya uhuru wa Tanzania sikutegemea kama balozi za Tanzania zitaendeshwa nama hii kwa kukosa fedha na watumishi wake kuendelea kuhangaika," alisema Cheyo, ambaye aliongozana na Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Zainabu Vulu na wajumbe wengine.

Kamati hiyo ilipitia hesabu za Wizara hiyo na kubaini kwamba katika Ubalozi wa Tanzania nchini Uganda matumizi yake yalizidi na kumuagiza Haule kufuatilia suala hilo na kuwapatia taarifa.

Katika kikao hicho kilichofanyika katika ofisi ndogo za Bunge jijini Dar es Salaam, Haule, alifuatana na maofisa kadhaa wa wizara na taasisi zilizoko chini ya wizara hiyo.

Hivi karibuni madaktari waligoma nchini wakidai nyongeza ya posho na mishara yao, mgomo ambao ulisababisha kukosekana kwa huduma za kitabibu katika hospitali kuu nchini kwa takribani mwezi mmoja.

Mgomo huo ulisitishwa baada ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kukutana nao na kutangaza nyongeza ya posho hizo, huku ikiundwa kamati ya kupitia madai ya nyongeza ya mishahara ikiwa ni pamoja na kuwasimamisha kazi, na kuwachunguza Katibu Mkuu wa Afya na Ustawi wa Jamii, Blandina Nyoni na Mganga Mkuu, Dei Mutasiwa, kwa tuhuma mbalimbali za ufisadi.

Walimu nao wametaka nyongeza ya mishahara kwa zaidi ya asilimia 100 kuanzia Julai mwaka huu, vinginevyo wataanza mgomo.
 
Balozi ziko hoi kifedha. Ni taarifa iliyowekwa wazi na vyombo vya habari leo. Hii taarifa imekaaje?

Tusaidiane kutafuta ufumbuzi, matusi tuweke pembeni. Tujenge hoja namna ya kujinasua na hali hii.
Nitaamini kuwa Hazina wameishiwa pesa kwa kwa kutumia case study ya jimbo la Arumeru!...kama sitaona ugawaji wa fedha na t-shirt na mabango ya 'chagua chama Mama'...basi nitajua hooooi !
Kwa kauli zao za kawaida hawaaminiki hawa!
 
Hatua mojawapo iliyochukuliwa ni kupunguza idadi ya watu wanaoambatana na Mhe. Rais kwenye ziara zake nje ya nchi , hili yeye mwenyewe kaliona na ameshatoa maelekezo kwa wizara ya mambo ya nnje kwa utekelezaji. kwa kuzingatia freq. ya safarari hizi ni kubwa pesa za kuhudumia balozi zetu zitapatikana
 
Hatua mojawapo iliyochukuliwa ni kupunguza idadi ya watu wanaoambatana na Mhe. Rais kwenye ziara zake nje ya nchi , hili yeye mwenyewe kaliona na ameshatoa maelekezo kwa wizara ya mambo ya nnje kwa utekelezaji. kwa kuzingatia freq. ya safarari hizi ni kubwa pesa za kuhudumia balozi zetu zitapatikana

Asante kwa mchango wako. Ni suluhu mojawapo.
 
TFDA wamelipwa mshaara wa January, tarehe 8 February.
 
Magazeti yameripoti, je magazeti yametoa wapi taarifa hii? tujue chanzo kwanza ndiyo tutajadili vizuri... vinginevyo tunaweza kujikuta tunajadili uongo tu hapa.
 
Nitaamini kuwa Hazina wameishiwa pesa kwa kwa kutumia case study ya jimbo la Arumeru!...kama sitaona ugawaji wa fedha na t-shirt na mabango ya 'chagua chama Mama'...basi nitajua hooooi !
Kwa kauli zao za kawaida hawaaminiki hawa!

Hizo zitakuwa fedha za chama sio za serikali
 
Magazeti yameripoti, je magazeti yametoa wapi taarifa hii? tujue chanzo kwanza ndiyo tutajadili vizuri... vinginevyo tunaweza kujikuta tunajadili uongo tu hapa.

Aliyesema hayo ni katibu mkuu wizara ya mambo ya nje, wakati akizungumza na kamati ya bunge ya hesabu za serikali..
 
Hizo zitakuwa fedha za chama sio za serikali
Ha ha haaa!
Mpaka wa chama na serikali uko wapi?...USHAWAHI KUUONA?
Hukuwahi kuona magari ya STK yanatolewa namba na kuwekwa T432 CCM?
Au unaamini chama kiliacha kushika hatamu!
 
Nchi kubwa za ulaya zina matatizo makubwa ya kifedha, ugiriki hali mbaya wanapunguza ajira na mishahara, sasa cha ajabu nini kwa nchi ombaomba kama tanzania?
Hizi mada nyingine hazina kichwa wala miguu, wewe utakuwa umesoma chuo kikuu cha kata tu
 
Muwe mnaangalia na Channel za kidini mambo haya yametabiriwa na si kwa TZ tu,nchi kibao uchumi utaumba to the maximum kiasi kwamba kutakuwa na limit ya kutumia hela.Ole wao waliozoea kutumia hovyohovyo,mtalazimishwa kuwa na nidhamu za matumizi yenu.Matokeo haya ni kutokana na reaction za seikali au mtu binafsi kwa wale wanaonekana wanafanya makosa,baada ya kuwarudisha katika mstari,Tiba tunayowapa ni makosa juu ya makosa! tafakari,Chukua hatua!
 
Magazeti yameripoti, je magazeti yametoa wapi taarifa hii? tujue chanzo kwanza ndiyo tutajadili vizuri... vinginevyo tunaweza kujikuta tunajadili uongo tu hapa.

Kwani hiyo habari umeisoma au umeamuwa kufanya kijamiijamii tu? Naamini ungeisoma basi tungekuwa tunaendelea na mjadala badala ya kurudi nyuma.
 
Nchi kubwa za ulaya zina matatizo makubwa ya kifedha, ugiriki hali mbaya wanapunguza ajira na mishahara, sasa cha ajabu nini kwa nchi ombaomba kama tanzania?
Hizi mada nyingine hazina kichwa wala miguu, wewe utakuwa umesoma chuo kikuu cha kata tu


Unataka kutwambia tusijadili matatizo yetu eti kwa kuwa wengine wanayo kama hayo? Tuendelee na mada yetu na hasa hili la ziara za viongozi zinakula pesa nyingi kiasi kwamba ungekuwa wazi matumizi yanayofanyika kwenye ziara hizo basi tungeemewa sote!
 
Mi sioni ajabu. Walikojazana waumizane huko huko.
Na bado mgomo wa waalimu.
 
Aliyesema hayo ni katibu mkuu wizara ya mambo ya nje, wakati akizungumza na kamati ya bunge ya hesabu za serikali..
Hata kama Balozi zikiishiwa sioni kuwa ni suala la kuniwangisha kichwa hata kidogo. Anayetakiwa asumbuliwe na hili ni jk na serikali yake, sisi wengine tusumbuliwe tu na mawazo ya mlo wa watoto wa jioni.
 
TAARIFA YA WIZARA YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA KUHUSU MALIPO YA MISHAHARA KATIKA BALOZI ZETU.


Tarehe 13/2/2010 Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) ilifanya kikao cha pamoja na Menejimenti ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa. Lengo la kikao hicho lilikuwa ni kujadili taarifa ya Hesabu za Wizara kwa mwaka wa fedha 2009/2010.

Kufuatia kikao hicho baadhi ya vyombo vya habari vilitoa taarifa ambazo siyo sahihi kufuatia masuala yaliyojadiliwa katika kikao hicho.

Wizara inakanusha taarifa hizo zilizotolewa na baadhi ya vyombo vya habari, na sio kweli kwamba Balozi zetu zina matatizo makubwa ya kifedha.

Kilichozungumziwa katika kikao hicho ni kuwa Balozi zetu bado zinatumia viwango vya Posho ya Utumishi wa Nje ambavyo vimepitwa na wakati. Ili kuhakikisha kuwa viwango hivyo vya Posho ya Utumishi wa Nje vinaboreshwa ili kuendana na hali halisi ya maisha; Awali Wizara ilifanya mapitio ya Kanuni za Utumishi wa Nje (Foreign Service Regulations) zinazohusisha Posho ya Utumishi wa Nje na kuziwasilisha katika mamlaka husika. Kwa kuwa mapitio Kanuni hizo ziliandaliwa muda mrefu uliopita, Wizara iliona kuwa upo umuhimu wa kuunda kamati maalum ya kupitia kanuni hizo za Utumishi wa Nje. Kamati hiyo imeshakamilisha kazi yake na kuiwasilisha kwa Menejimenti ya Wizara kwa ajili ya uhakiki na hatimaye kuiwasilisha katika mamlaka husika.

Pamoja na kuwepo kwa changamoto hiyo ya kuwa na viwango vya Posho ya Utumishi wa Nje vilivyopitwa na wakati, Balozi zetu zimeweza kupelekewa mishahara yao ya kila mwezi pasipo kuchelewa. Aidha, tatizo jingine lililoelezwa ni upungufu wa Bajeti unaotokana na kushuka kwa thamani ya shilingi ya Tanzania dhidi ya Fedha nyingine za Kigeni.

Katika kuwezesha kutatua tatizo hili Hazina imekuwa ikilipa kwa wakati fidia inayotokana na kushuka kwa thamani ya shilingi ya Tanzania katika kila kipindi cha robo mwaka.

Kwa ujumla Balozi zetu zimeendelea kutekeleza majukumu yao ipasavyo kwa kutumia rasilimali fedha zilizopo katika Bajeti. Aidha, siku zote Wizara imekuwa ikipata ushirikiano mkubwa kutoka Hazina katika kushughulikia masuala ya fedha Balozini.

IMETOLEWA NA: WIZARA YA MAMBO YA NJE
NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA, DAR ES SALAAM

14/2/2012
 
Back
Top Bottom