Ni CCM mpya au gunia la misumari? CCM Zanzibar tunakabiliwa na kazi Nzito-Vuai - RAI

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797



*Kaulimbiu mpya sasa ni ‘Towards New CCM’
*Nape: Mapinduzi makubwa yaja, viongozi wajiandae
*Vuai: CCM Zanzibar tunakabiliwa na kazi nzito
*Cheche za mrithi wa Makamba ni nguvu ya soda?

Na Innocent Munyuku


SIKU chache baada ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kufanya mabadiliko makubwa ndani ya chama hicho, watendaji wapya wamekuja na mikakati mipya ya kukipaisha chama hicho katika medani za kisiasa Tanzania, huku wakija na kauli mbiu mpya inayosema; Towards New CCM.

RAI imefanya mahojiano na viongozi kadhaa wapya akiwamo Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, Katibu wa Idara ya Fedha na Uchumi, Lameck Mwigulu Nchemba na Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Zanzibar, Vuai Ali Vuai.

Nape, ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Masasi mkoani Mtwara anasisitiza uwajibikaji wa moja kwa moja wa wanachama na kuacha mtindo wa zamani ambapo viongozi walikuwa wakiangalia wingi wa wanachama badala ya kufanya tathmini kujua ni wangapi kati yao wapo tayari kukitetea chama wakati wote.

“Hatutarajii kuwa na vision (mtazamo) wa mtu mmoja mmoja lakini cha msingi ni kwamba lazima chama kirudi kwa wanachama wenye uchungu na chama. Hii maana yake ni kwamba tuachane na utaratibu wa kusomba watu bila kuwatathimini kama wana full commitment kwa CCM.

“Nitakupa mfano. Katika Uchaguzi Mkuu uliopita, majimbo ambayo CCM imepoteza si kwamba hatuna wanachama, wanachama wetu ni wengi kuliko wa upinzani lakini wana-CCM hawakuji-commit kukipa chama chao ushindi,” anasema Nape na kisha kuongeza:

“Hatua kubwa tutakayoichukua ni kuhakikisha tunakuwa na wanachama wenye uchungu na chama chao.

“Lakini pia kule Dodoma tumetoka na maazimio kadhaa lakini kubwa ni kwamba tunaelekea katika mambo mapya, tumesema ‘Towards New CCM.’ Kwa hiyo tutakiimarisha chama kuanzia ngazi ya chini kabisa. Kama nilivyosema awali kwamba tunaboresha mfumo wa kuwapata wanachama wapya.”

Nape anasema kwa mfumo wa siasa uliopo leo, CCM haikuwa na njia nyingine zaidi ya kukubali mabadiliko hayo makubwa kuwahi kufanyika ndani ya chama hicho kwa maslahi ya chama na Tanzania kwa ujumla.

“Kuna mapinduzi makubwa yanakuja. Viongozi wetu wajipime upya. Maadili kwa wengi wao yamepotea. Kwa hiyo basi nawaomba wajipime upya kama kuna mtu anajiona ni mchafu na hataki kubadilika basi ajiondoe kabla ya kuondolewa,” anasema Nape aliyechukua nafasi hiyo kutoka kwa John Chiligati. Chiligati kwa sasa ni Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Tanzania Bara.

Naye Katibu wa mpya wa Idara ya Fedha na Uchumi ya chama hicho, Lameck Mwigulu Nchemba, aliyechukua nafasi hiyo kutoka kwa Mbunge wa Mvomero, Amos Makalla, alipozungumza na Rai, alisema msimamo wa chama kwa sasa ni kujiimarisha kiuchumi.

Nchemba ambaye ni Mbunge wa Iramba Mashariki mkoani Singida, kitaaluma ni mchumi aliyepata pia kuitumikia Benki Kuu ya Tanzania (BoT) miaka ya nyuma kabla ya kuingia katika siasa.

“CCM hii mpya lazima ijiimarishe kwa kiasi kikubwa katika uchumi, chama sharti kijitegemee kiwe na vyanzo vingi vya fedha.

“Kuna miradi mingi imekufa au inaendeshwa isivyo…kwa hiyo lazima mabadiliko ya kiuchumi yapewe msukumo wa haraka.

“Kwa upande wa idara yangu, nitaboresha pia maslahi ya watumishi mbalimbali wa chama. Maslahi yao kwa kweli lazima yaangaliwe upya kulingana na hali halisi ya maisha kwa kuwa ni kidogo mno na hayatoshelezi mahitaji katika hali ya sasa,” anasema Nchemba.

Alipoulizwa ni miradi ipi ataipa kipaumbele, Nchemba alisema atatoa kauli baada ya kukabidhiwa rasmi nyaraka za ofisi leo Alhamisi.

“Ni mapema kusema nitaanza na mradi gani. Kama ni suala la miradi ya zamani au kuanzisha mipya nitajua kesho (leo) baada ya kukabidhiwa rasmi nyaraka za ofisi. Mimi na watu wangu tutakaa na kufanya tathimini,” anasema.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai changamoto kubwa inayomkabili visiwani ni kuyaunganisha makundi ya wanachama yaliyotokana na mpasuko katika kura za maoni kuhusu Serikali ya Umoja wa Kitaifa, Uchaguzi Mkuu na wengine waliokosa imani na chama kutokana na chama kuteleza katika masuala mbalimbali.

Anasema: “CCM tumefanya mabadiliko haya makubwa kwa sababu kuna ni kweli kuna maeneo tuliyokuwa tumeteleza na kupoteza imani kwa wananchi wa Tanzania Bara na Tanzania Visiwani.

“Lakini pia kuna mambo mengi ambayo yamewagawa wanachama wetu. Kwa mfano Zanzibar tulikuwa na mambo mengi kwa wakati mmoja. Tulikuwa na kura ya maoni kuhusu Serikali ya Umoja wa Kitaifa. Tulikuwa na kura za maoni katika uteuzi wa Rais, tulikuwa na kura za maoni katika uteuzi wa wagombea wa ubunge, uwakilishi na udiwani.

“Yote hayo yamesababisha wanachama kugawanyika katika makundi na ni vugumu sana kuyaunganisha makundi haya yote kwa wakati mmoja. Lakini sasa mimi nimehemewa, nimepata meseji nyingi za kunipongeza kote nchini, lakini nyingi zaidi kutoka Unguja na Pemba.

“Nadhani sasa wananchi wana matarajio makubwa na chama chetu. Kinachotakiwa sasa ni sisi viongozi tukidhi matarajio ya wanachama wetu na hiyo ndiyo changamoto yangu katka nafasi hii mpya niliyokabidhiwa. Nawashukuru niongozi wangu kwa kuniamini na kunipa nafasi hii nzito,” anasema Vuai.

CCM kupitia kikao chake cha Halmashauri Kuu (NEC) mjini Dodoma siku chache zilizopita, kimefanya mabadiliko makubwa kwa kuchagua wajumbe wa Kamati Kuu (CC) na Sekretarieti ya chama hicho, huku vigogo kadhaa wakitupwa nje.

Kada wa siku nyingi wa chama hicho, Wilson Mukama, ndiye Katibu Mkuu mpya anayechukua nafasi ya Yusuf Makamba ambaye alijiuzulu pamoja na wajumbe wengine wa Sekretarieti ya chama hicho.

Akizungumza na waandishi wa habari juzi mjini Dodoma, Mukama anasema chama hicho sasa kinajipanga upya kukabiliana na changamoto zinazokikabili, ikiwamo nia yake ya dhati ya kjisafisha mbele ya wananchi.

Mukama anatoa ahadi kwamba kazi kubwa inayomkabili yeye na timu yake katika sekretarieti mpya ni kurudisha imani ya wananchi kwa chama ambayo ilianza kupotea kwa kasi kubwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.

Pamoja na kukiri kwamba chama chake kina wanachama wengi na hivyo hakiwezi kuepuka migogoro, ambayo baadhi ni ya kiafya, Mukama alisisitiza kuwa makundi ambayo yamechangia kukidhoofisha chama hicho hayatapata nafasi katika kipindi cha uongozi wake.

“Tunakabiliwa na changamoto kubwa ya kuijenga CCM mpya na tutafanikiwa katika hili iwapo tu tutakuwa na wanachama wenye nia safi. Ni lazima tukijenge upya chama chetu, watu wenye kashfa watalazimika kujiondoa wenyewe kabla hatujawafukuza,” anasema Mukama.

Lakini wachunguzi wa siasa za Tanzania wanasema inawezekana kabisa kwamba kauli hizo zenye ari kubwa zinatolewa na viongozi hawa wa sekretarieti zinatolewa kutokana na moto uliowashwa na mageuzi hayo ambao joto lake litazidi kupungua kwa kadri siku zinavyokwenda.

Hata hivyo, baadhi ya watu wanaomfahamu Katibu Mkuu huyo mpya kwa karibu wanasema siku zote amekuwa na msimamo katika mambo anayoyaamini na wanaamini kwamba atayasimia yote aliyoyasema katika siku zote za uongozi wake.
Wajumbe wengine wapya wa Sekretarieti hiyo ni pamoja na Januari Makamba anayesimamia Idara ya Siasa na Mambo ya Nje, Kapteni John Chiligati ambaye anakuwa Naibu Katibu Mkuu Tanzania Bara na Asha Abdallah Juma anayesimamia oganaizesheni ya chama.
 
Utekelezaji utakuwa mgumu kwani waasisi wa chama hiki kwa sasa ndiyo wanaonyooshewa vidole. Michango yao hasa ile ya kujitoa na kufanikisha hata ushindi wa wanachama katika ngazi mbalimbali za uongozi. Kama hawataenziwa ila watatoswa basi busara itakuwa ime ................. (Nilikuwa likizo Jinja)
 

Similar Discussions

0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom