Ndugu zangu,
Ni Jumatatu usiku. Siku inaelekea ukingoni. Naandika nikiitafakari siku ya leo. Kwangu haikuja na jipya. Ni yale yale. Moja kubwa ni dhahiri, kuwa Watanzania bado tuna safari ndefu sana kufikia hatua ya kuitwa taifa la kisasa.
Tuyafanyayo mengi bado ni mambo ya hovyo hovyo, na wenye kuongoza kuyafanya hayo ya hovyo hovyo ni viongozi wetu. Lakini hatuna jinsi, hatua tunayopitia sasa ni lazima tuipitie. Hakuna njia nyingine ya kupita na kutufikisha kwa haraka tunakotaka kwenda. Tusisahau tu , kutunza kumbukumbu. Tufanye hivyo ili Watanzania wa vizazi vijavyo waje wajifunze kutokana na matendo yetu.
Tulikuliku ni aina ya ndege. Viongozi wetu wanaweza kujifunza kutoka kwa ndege huyu. Tulikuliku ana kanuni inayomwongoza. Mara ile tulikuliku anapotaga mayai, basi, hufanya maamuzi magumu ya kujinyonyoa manyoya yake.
Kwa pamoja, tulikuliku dume na jike watafanya tendo hilo.
Kwanini?
Wanajiwekea wenyewe mazingira ya kushindwa kuruka. Wanafanya hivyo ili waatamie mayai yao hata atakapotokea nyoka mpenda mayai wapambane nae hapo hapo. Kwamba wangebaki na manyoya, huenda wangemwogopa nyoka. Hivyo, wangeruka na kuacha mayai yakiliwa na nyoka.
Kwa kiongozi kujinyonyoa manyoya ina maana ya kukubali kushuka chini kwa watu. Kuyaelewa matatizo ya watu anaowaongoza. Kuwa tayari kupambana kuyatatua matatizo ya watu akiwa na watu.
Ilivyo kwa viongozi wetu wengi wa leo, ni kuwa, katikati ya dhiki kubwa ya wanaowaongoza, si tu wamefuga manyoya mengi, bali, hata pale wananchi wanapokabiliwa na adui maradhi, wao, viongozi, wana mbawa za kuwawezesha kuruka juu angani huku wakiwaimbia watu wao nyimbo za kejeli. Na bado watafanya hila ili kuwachonganisha na kuwagawa watu wao walio kwenye dhahma ya umasikini.
Na kuna mawili ambayo yaliwezekana kutumiwa na yakafanya kazi miaka ya sitini hadi themanini, na mawili hayo hata yanapotumika sasa, hayafanyi kazi tarajiwa. Maana, wakati umebadilika. Ni yepi hayo?
Naam, ni kwa kiongozi kutumia Uongo na kutishia nguvu za mamlaka. Kiongozi anayetaka kufanikiwa katika zama hizi ni yule aliye tayari na kuachama na mambo ya zama hizo; kuwaongopea watu wako na kutishia nguvu za mamlaka. Badala yake, kuwa tayari kufanya maongezi hata na wale ambao huko nyuma haikuwezekana kukaa nao meza moja.
Vinginevyo, Watanzania tungali na safari ndefu sana. Njia ina miba mingi, lakini ni lazima tuipite. Hakuna njia nyingine. Na hili ni neno la leo.
Maggid Mjengwa
0788 111 765
Mjengwa Blog::Habari,Picha,Matangazo
Ni Jumatatu usiku. Siku inaelekea ukingoni. Naandika nikiitafakari siku ya leo. Kwangu haikuja na jipya. Ni yale yale. Moja kubwa ni dhahiri, kuwa Watanzania bado tuna safari ndefu sana kufikia hatua ya kuitwa taifa la kisasa.
Tuyafanyayo mengi bado ni mambo ya hovyo hovyo, na wenye kuongoza kuyafanya hayo ya hovyo hovyo ni viongozi wetu. Lakini hatuna jinsi, hatua tunayopitia sasa ni lazima tuipitie. Hakuna njia nyingine ya kupita na kutufikisha kwa haraka tunakotaka kwenda. Tusisahau tu , kutunza kumbukumbu. Tufanye hivyo ili Watanzania wa vizazi vijavyo waje wajifunze kutokana na matendo yetu.
Tulikuliku ni aina ya ndege. Viongozi wetu wanaweza kujifunza kutoka kwa ndege huyu. Tulikuliku ana kanuni inayomwongoza. Mara ile tulikuliku anapotaga mayai, basi, hufanya maamuzi magumu ya kujinyonyoa manyoya yake.
Kwa pamoja, tulikuliku dume na jike watafanya tendo hilo.
Kwanini?
Wanajiwekea wenyewe mazingira ya kushindwa kuruka. Wanafanya hivyo ili waatamie mayai yao hata atakapotokea nyoka mpenda mayai wapambane nae hapo hapo. Kwamba wangebaki na manyoya, huenda wangemwogopa nyoka. Hivyo, wangeruka na kuacha mayai yakiliwa na nyoka.
Kwa kiongozi kujinyonyoa manyoya ina maana ya kukubali kushuka chini kwa watu. Kuyaelewa matatizo ya watu anaowaongoza. Kuwa tayari kupambana kuyatatua matatizo ya watu akiwa na watu.
Ilivyo kwa viongozi wetu wengi wa leo, ni kuwa, katikati ya dhiki kubwa ya wanaowaongoza, si tu wamefuga manyoya mengi, bali, hata pale wananchi wanapokabiliwa na adui maradhi, wao, viongozi, wana mbawa za kuwawezesha kuruka juu angani huku wakiwaimbia watu wao nyimbo za kejeli. Na bado watafanya hila ili kuwachonganisha na kuwagawa watu wao walio kwenye dhahma ya umasikini.
Na kuna mawili ambayo yaliwezekana kutumiwa na yakafanya kazi miaka ya sitini hadi themanini, na mawili hayo hata yanapotumika sasa, hayafanyi kazi tarajiwa. Maana, wakati umebadilika. Ni yepi hayo?
Naam, ni kwa kiongozi kutumia Uongo na kutishia nguvu za mamlaka. Kiongozi anayetaka kufanikiwa katika zama hizi ni yule aliye tayari na kuachama na mambo ya zama hizo; kuwaongopea watu wako na kutishia nguvu za mamlaka. Badala yake, kuwa tayari kufanya maongezi hata na wale ambao huko nyuma haikuwezekana kukaa nao meza moja.
Vinginevyo, Watanzania tungali na safari ndefu sana. Njia ina miba mingi, lakini ni lazima tuipite. Hakuna njia nyingine. Na hili ni neno la leo.
Maggid Mjengwa
0788 111 765
Mjengwa Blog::Habari,Picha,Matangazo