Neno La Leo: Kwanini Simba Awinde Panya Pori?

maggid

JF-Expert Member
Dec 3, 2006
1,084
1,246
Na Maggid Mjengwa



INATUHUSU sisi Watanzania. Mnyama simba ana uwezo wa kumfukuza, kumkamata na kumla panya pori. Lakini, simba huyu atakuwa si mwenye busara kwa kutumia muda na nguvu zake nyingi kuwinda panya pori siku nzima. Na simba mwenye tabia hiyo hatma yake ni kufa kwa njaa.
Maana, simba huyo ana uwezo wa kumwinda swala, huo ni mlo toshelezi na mtamu. Swala ni mnyama mkubwa kuliko panya pori. Kwa simba kuwinda, kukamata na kula swala, si tu ni furaha kwake, bali ni chakula anachostahiki na ni heshima kwake.
Nitaendelea na mfano mwingine wa picha ili hoja ninayotaka kuijenga ipate kueleweka zaidi kwako msomaji. Maana, kuandika makala ya kichambuzi ina maana moja kubwa; kufanya tafsiri ya matukio, habari, kauli ya mwanasiasa na hata kimya cha mwanasiasa. Ndiyo, hakuna kimya cha mwanasiasa kisichoongea. Ni uvivu wetu tu wa kutafakari na kutafuta tafsiri.
Ndiyo, kama mzazi unaweza kumwamrisha mwanao “ acha, si hivyo, fanya hivyi”. Na ikawa hivyo. Hata kama mtoto anahisi mzazi amekuwa na hulka ya kutomshirikisha, bali kutoa amri tu, basi, tumaini analo; Kuwa hali hiyo itakuja kwisha mara ile mtoto atakapokua na kuhama mji wa mzazi wake.
Lakini , kiongozi hawezi kuwaongoza watu wake kwa staili hiyo. Anaowaongoza ni watu wazima wenye akili zao. Wanaweza kuwa na upumbavu wa muda lakini si ujinga wa milele. Na watu wazima hawa hawana siku za kuhesabu kabla ya kuhama mji wa ‘baba/mama kiongozi wao’. Ni wana wa nchi, hawana pa kukimbilia. Wakizidiwa, watapiga kelele, wataingia mitaani.
Ndiyo, inahusu maendeleo ya kiuchumi kwa nchi yetu. Na hii ingekuwa ndio ajenda kuu katika miaka mitano ijayo. Kwa nchi, kuwa na kasi ya maendeleo ya kiuchumi ni sawa na mwendesha baiskeli.
Kwa mwendesha baiskeli, anapokuwa kwenye mwendo wa kasi, si rahisi kumsimamisha. Lakini , kama ndiyo kwanza anaipanda baiskeli na kuanza kuvuta kasi, ni rahisi hata kumvuta kwa mkono. Na tuwe na nguvu na kasi kama ya simba. Kasi itakayotufanya tuachane na kuwinda panya pori , na kutazama zaidi wanyama wakubwa. Inawezekana. Na hilo ni Neno La Leo.
Kwa kazi zaidi za Maggid, tembelea; mjengwa http://www.kwanzajamii.com
 
Back
Top Bottom