Na Maggid Mjengwa,
Nikiwa kijijini kwetu Nyeregete kuna nilichojifunza pale nilipomwomba mmoja wa wenyeji zangu anionyeshe ulipo msala. Nilitaka kwenda haja ndogo. Hatua 20 kutoka tulipokaa tukiongea ndipo ulipokuwa msala. Nikaonyeshwa, nikaenda. Kama wengi wetu tulioishi vijijini tunavyojua; mlango wa kuingia msalani ni wa gunia.
Huku nyuma nikamsikia mwenyeji wangu anavyohangaika kuyatafuta maji. Akayapata akaniletea haraka. Akanijulisha kuwa maji ameyaweka nje, na kipande cha sabuni pia. Kwenye kisahani cha chai.
Nikamaliza haja yangu, nikatoka nje. Nikayakuta maji nusu galoni. Pembeni kisahani cha chai na kipande kidogo kabisa cha sabuni ya punda. Hakika, sabuni ile ilikuwa imetumika ikabaki kipisi sawa na bazoka iliyotafunwa na kubaki.
Nikanawa mikono yangu na kipande kile cha sabuni ya punda. Hata povu lake kulipata ni kwa tabu. Kwa haraka unaweza kuingiwa na mawazo ya kukitupa baada ya kumaliza kunawa. Hapana, niko kijijini, ni lazima nifikiri mara mbili. Nikakirudisha kipande cha sabuni ya punda kisahanini.
Nilipoanza kuondoka kutoka msalani, haraka mwenyeji wangu akaja kukichukua kipande kile cha sabuni punda na kukirudisha ndani. Kwenda kukihifadhi.
Mwenyeji wangu yule alikuwa mkarimu sana. Aliniandalia chakula na hata chai. Alinishangaa sana nilipomwambia chai yangu asiniwekee sukari, kuwa situmii sukari. Nilihofia alidhani kuwa sikufikiri kama ana sukari ya kutosha.
Nilipoaga na kuondoka mahali hapo nilifikiri sana kuhusu kipande kile cha sabuni ya punda. Kwamba sisi tuliotoka kwenye mazingira ya wazazi masikini tuna lazima ya kurudi kwa wananchi, kurudi vijijini na kukaa na wananchi japo kwa siku moja, mara moja kwa mwaka. Si kurudi kuwahutubia, bali kuingia katika maisha yao. Ndipo hapo tutakapoelewa maana ya umasikini. Ndipo tutakapoelewa hali ya watu wetu kwa kuanzia na ‘kipande cha sabuni ya punda'.
Na hilo ni Neno La Leo.
Nikiwa kijijini kwetu Nyeregete kuna nilichojifunza pale nilipomwomba mmoja wa wenyeji zangu anionyeshe ulipo msala. Nilitaka kwenda haja ndogo. Hatua 20 kutoka tulipokaa tukiongea ndipo ulipokuwa msala. Nikaonyeshwa, nikaenda. Kama wengi wetu tulioishi vijijini tunavyojua; mlango wa kuingia msalani ni wa gunia.
Huku nyuma nikamsikia mwenyeji wangu anavyohangaika kuyatafuta maji. Akayapata akaniletea haraka. Akanijulisha kuwa maji ameyaweka nje, na kipande cha sabuni pia. Kwenye kisahani cha chai.
Nikamaliza haja yangu, nikatoka nje. Nikayakuta maji nusu galoni. Pembeni kisahani cha chai na kipande kidogo kabisa cha sabuni ya punda. Hakika, sabuni ile ilikuwa imetumika ikabaki kipisi sawa na bazoka iliyotafunwa na kubaki.
Nikanawa mikono yangu na kipande kile cha sabuni ya punda. Hata povu lake kulipata ni kwa tabu. Kwa haraka unaweza kuingiwa na mawazo ya kukitupa baada ya kumaliza kunawa. Hapana, niko kijijini, ni lazima nifikiri mara mbili. Nikakirudisha kipande cha sabuni ya punda kisahanini.
Nilipoanza kuondoka kutoka msalani, haraka mwenyeji wangu akaja kukichukua kipande kile cha sabuni punda na kukirudisha ndani. Kwenda kukihifadhi.
Mwenyeji wangu yule alikuwa mkarimu sana. Aliniandalia chakula na hata chai. Alinishangaa sana nilipomwambia chai yangu asiniwekee sukari, kuwa situmii sukari. Nilihofia alidhani kuwa sikufikiri kama ana sukari ya kutosha.
Nilipoaga na kuondoka mahali hapo nilifikiri sana kuhusu kipande kile cha sabuni ya punda. Kwamba sisi tuliotoka kwenye mazingira ya wazazi masikini tuna lazima ya kurudi kwa wananchi, kurudi vijijini na kukaa na wananchi japo kwa siku moja, mara moja kwa mwaka. Si kurudi kuwahutubia, bali kuingia katika maisha yao. Ndipo hapo tutakapoelewa maana ya umasikini. Ndipo tutakapoelewa hali ya watu wetu kwa kuanzia na ‘kipande cha sabuni ya punda'.
Na hilo ni Neno La Leo.