Neno La Leo: Kipande Cha Sabuni Ya Punda!

maggid

JF-Expert Member
Dec 3, 2006
1,084
1,246
Na Maggid Mjengwa,

Nikiwa kijijini kwetu Nyeregete kuna nilichojifunza pale nilipomwomba mmoja wa wenyeji zangu anionyeshe ulipo msala. Nilitaka kwenda haja ndogo. Hatua 20 kutoka tulipokaa tukiongea ndipo ulipokuwa msala. Nikaonyeshwa, nikaenda. Kama wengi wetu tulioishi vijijini tunavyojua; mlango wa kuingia msalani ni wa gunia.

Huku nyuma nikamsikia mwenyeji wangu anavyohangaika kuyatafuta maji. Akayapata akaniletea haraka. Akanijulisha kuwa maji ameyaweka nje, na kipande cha sabuni pia. Kwenye kisahani cha chai.

Nikamaliza haja yangu, nikatoka nje. Nikayakuta maji nusu galoni. Pembeni kisahani cha chai na kipande kidogo kabisa cha sabuni ya punda. Hakika, sabuni ile ilikuwa imetumika ikabaki kipisi sawa na bazoka iliyotafunwa na kubaki.

Nikanawa mikono yangu na kipande kile cha sabuni ya punda. Hata povu lake kulipata ni kwa tabu. Kwa haraka unaweza kuingiwa na mawazo ya kukitupa baada ya kumaliza kunawa. Hapana, niko kijijini, ni lazima nifikiri mara mbili. Nikakirudisha kipande cha sabuni ya punda kisahanini.

Nilipoanza kuondoka kutoka msalani, haraka mwenyeji wangu akaja kukichukua kipande kile cha sabuni punda na kukirudisha ndani. Kwenda kukihifadhi.

Mwenyeji wangu yule alikuwa mkarimu sana. Aliniandalia chakula na hata chai. Alinishangaa sana nilipomwambia chai yangu asiniwekee sukari, kuwa situmii sukari. Nilihofia alidhani kuwa sikufikiri kama ana sukari ya kutosha.

Nilipoaga na kuondoka mahali hapo nilifikiri sana kuhusu kipande kile cha sabuni ya punda. Kwamba sisi tuliotoka kwenye mazingira ya wazazi masikini tuna lazima ya kurudi kwa wananchi, kurudi vijijini na kukaa na wananchi japo kwa siku moja, mara moja kwa mwaka. Si kurudi kuwahutubia, bali kuingia katika maisha yao. Ndipo hapo tutakapoelewa maana ya umasikini. Ndipo tutakapoelewa hali ya watu wetu kwa kuanzia na ‘kipande cha sabuni ya punda'.

Na hilo ni Neno La Leo.
 
Wee mtani wangu wee, hebu kula tano kwa huo ujumbe.

Kumbe sisi Sikonge kweli tuna nafuu. Huo umasikini kwa kweli haupo kwa kiasi kile. Kama huamini, basi njoo na rafiki yako Lugusha sijui (ulimkaribisha kwenu na akakalia kiti cha miguu 3 na ukaweka kwenye blog). Nawashangaa kuwa hata mabadiliko hamtaki na umasikini wote huo. Nyie wa Iringa, kweli inabidi Yesu azaliwe kwenu ili Awaokowe na huu umasikini.

Tukiacha utani, hii ni hali ya kawaida sana Tanzania. Nilishawahi kwenda kumtembelea kaka yangu mmoja kwenye familia. Nilishangaa kuwa aliniachia kitanda na kitandani kuna khanga tu katandika. Watoto wanalala kwenye mkeka na kujifunika khanga pia. Mbu walikuwa wanauma kishenzi na joto kali sana na nikashindwa kulala usiku mzima. Yeye alikaa kwenye kiti usiku mzima karibu na moto (ndani hamna kibatari). Nilitamani tubadilishane ila nikawa naogopa kujenga sura kuwa mie ninajifanta TAJIRI.

Kwa sababu ilikuwa ni kipindi naenda shule basi maada ya miezi sita, nilirudi nyumbani na kuwaambia Baba na Mama kuwa hongereni sana kwa kuwa na mji kama ule maana kwa kweli najisikia kuwa natoka familia Tajiri. Ukweli ni kuwa pamoja na mabadiliko makubwa katika maisha, bado najiona masikini. Sasa leo hii nikienda na kumkuta akiwa na maisha yale bado, sijui ntamuonaje? Mtani sitaki hata kufikiri. Kweli inatisha na ngumu sana. Ila ni heri umesema maana nikienda basi lazima niwe nimejiandaa na vitu kama hivyo na kugawa kama zawadi.
 
Kwa kijijini haya ni maisha ya kawaida. Na bahati mbaya watu wanaona kama ni haki kuishi maisha hayo na katu hawawezi kuachana nayo.

Hivi ulimwuliza mwaka huu kura atampagia nani?
 
Cha kujiuliza zaidi ya hapo ni hatua gani umechukua kuondoa matatizo ya ndani ya jamii.

serikali iliyopo imeonekana kufeli kabisa katika kumkwamua mwananchi wake. Nafikiri ni wakati wa wale waliokwamuka kidogo kuchukua hatua kusaidia wale walioko katika hali duni.

Umechukua hatua gani?
 
Cha kujiuliza zaidi ya hapo ni hatua gani umechukua kuondoa matatizo ya ndani ya jamii.

serikali iliyopo imeonekana kufeli kabisa katika kumkwamua mwananchi wake. Nafikiri ni wakati wa wale waliokwamuka kidogo kuchukua hatua kusaidia wale walioko katika hali duni.

Umechukua hatua gani?

Teacher, ndo maana wengine tunauliza, amemuuliza kama amejiandikisha kupiga kura? Na atampigia nani? Majibu ya maswali hayo ni muhimu kabla hata ya kuangalia jinsi ya kumsaidia.

Ila nina hakika huyo bwana atakuwa alikuwa ametinga t-shirt ya kijani na kofia ya njano. Na kama hatuwezi kuwasaidia watu wetu kwenye mambo kama hayo basi itakuwa vingumu kuwavuta hatua hata moja kuelekea kwenye uhuru wa kweli.

DC
 
"Enyi wagalatia ni nani aliyewaloga?" Namnukuu mtume Paulo. Naamini siku ya kura watawapigia wale wale waliowafanya hali yao iwe vile. WATU HAWA WAMELOGWA!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!
 
DC

Hapo kumuelimisha kuhusu haki na wapi apige kura yangu ni mwanzo tu. Tunahitaji kujenga tabia za 'kujitolea'

Wengi ukiwauliza wamesaidiaje taifa lao, majibu ni kuwa hanawa pesa, hawawezi kutoa misaada, wanasahau kuwa msaada unaweza kuwa katika mfumo wa ujuzi walionao, nguvu au hata mawazo.

Hatua gani umechukua?
 
Back
Top Bottom