Ndugu zangu,
Ni Jumapili nyingine. Nina neno. Askofu Msaidizi wa Jimbo Katoliki la Kagera , Dk. Methodius Kilaini ameongea na mwandishi wa gazeti la Mwananchi leo Jumapili, Februari 5, 2012.
Askofu Kilaini ameulizwa juu ya kauli yake ya miaka ya nyuma alipokaririwa akitamka, kuwa Kikwete ni chaguo la Mungu. Je, Kikwete ni chaguo la Mungu?
Askofu Kilaini anajibu; Nilichosema ni kwamba, sauti ya watu ni sauti ya Mungu. Anajibu Askofu Kilaini na kufafanua; kwa vile Rais alichaguliwa na asilimia 80 ya watu, hivyo, amekubalika na watu. Anasema Askofu Kilaini.
Askofu Kilaini anatuleta kwenye mantiki hii; kuwa Kikwete ni kama Mungu, na hapa kwa vile Katiba yetu ya sasa nayo inampa nguvu nyingi Rais, basi, ni nguvu zinazoweza kufanana na za Mungu.
Na Askofu Kilaini anatamani tutawaliwe na dikteta ili mambo yetu yanyooke. Ndio, Askofu Kilaini amekaririwa na gazeti la Mwananchi la leo Jumapili akitamka; kuwa ili nchi isonge mbele, inahitaji kiongozi atakayeongoza kwa mkono wa chuma. Amemtaja Rais Paul Kagame kama mfano wa aina hiyo ya kiongozi.
Natumaini Askofu amenukuliwa vibaya na mwandishi, lakini, kama alichosema ndicho, basi, natumaini hakumaanisha alichosema. Na kama amemaanisha alichosema, basi, napingana vikali na mafundisho hayo ya Baba Askofu Kilaini.
Maana, nchi yetu inachohitaji ni kiongozi na si mtawala. Anayetumia mkono wa chuma- Iron Feast huyo anatawala, haongozi. Huyo atakuwa ni dikteta na si kitu kingine.
Ndio, mtawala anayetumia mkono wa chuma hutumia pia risasi za shaba kuwanyamazisha wanaopingana nae, hata kwa hoja tu. Samahani Askofu Kilaini, Watanzania tungependa tupate kiongozi na si mtawala. Na tunamshukuru Mungu kwa kutuepusha kuwa na mtawala anaendesha nchi kwa ' mkono wa chuma'.
Na Kikwete huyu tuliye naye walau ameonyesha uongozi kwa kutamani Tanzania ije kupata kiongozi. Ni kwa kupitia mabadiliko haya ya Katiba tunayokwenda kuyafanya. Na ndio maana, hata ndani ya chama chake kuna wanaojipanga kupingana nae ili azma ya Kikwete kufanikisha mabadiliko makubwa ya Katiba ya nchi ishindikane.
Na ni matumaini yetu, kuwa Rais Jakaya Kikwete atatumia nguvu hizi za mfano wa Mungu alizopewa na Katiba ya sasa katika kuhakikisha Bunge linapitisha marekebisho ya sheria ya kuanzisha mchakato wa Katiba kama alivyoshauriwa na wadau nje ya CCM na akaafikiana nao.
Hakika, Rais Kikwete atakuwa mtu wa ajabu kama ataendekeza matakwa ya wachache wasiotaka mabadiliko ndani ya chama chake na hivyo basi, kujinyima mwenyewe nafasi yake katika historia ya nchi hii. Maana, Kikwete huyu anaweza kuacha nyuma yake, kumbukumbu ya kudumu Legacy ya kuwa ndiye Rais wa nchi, baada ya miaka 50 ya uhuru, aliyefanikiwa kuwafanya Wazanzibar kuendesha siasa zisizo na chuki miongoni mwao, lakini, aliyefuta pia ubaguzi wa kisiasa kwa Tanzania bara. Ni kwa kuwezesha kuwepo kwa Katiba mpya ambayo, bila shaka, itasafisha njia ya kuwepo , mbali ya mambo mengine, kipengele kitachoruhusu kuundwa kwa Serikali ya Mseto kama ilivyo kwa visiwani.
Naam, Kikwete wa sasa amekuwa ni kiongozi anayejitahidi sana kupima upepo. Huenda ameshabaini , kuwa Watanzania walio wengi, ni wale asilimia 80 anaosema Askofu Kilaini, kuwa ni wenye kutaka mabadiliko. Ndio, sauti ya watu ni sauti ya Mungu. Anasema Askofu Kilaini.
Hivyo basi, na Kikwete bila shaka anajua , kuwa CCM ni mkusanyiko wa wanachama milioni tano tu kati ya Watanzania milioni 40. Na kama Mungu, kama wananchi walio wengi wanataka mabadiliko ya kimfumo kupitia Katiba. Basi, anapaswa kusikiliza sauti za wengi, hata kama wako nje ya chama chake.
Na kama walio wengi wanatoa sauti za kupinga ongezeko la posho za wabunge. Rais anapaswa kusikiliza sauti za wengi. Kwamba anaweza kuacha kubariki ongezeko la posho na umma ukabaki nyuma yake. Maana, sauti za wananchi zapaswa kuwa sauti ya Rais, kwa mantiki ya Askofu Kilaini. Ndio, Rais asipobariki ongezeko la posho za wabunge bado atabaki na waumini wengi tu.
Na je, wenzake ndani ya chama wakiamua kupiga kura ya kukosa imani na Kikwete?
Astaghafillulahi! Hebu tema mate chini usije fikwa na laana. Hilo haliwezekani kamwe. Si tulimsikia Beatrice Shelukindo akipendekeza hilo kwa wabunge wenzake wa CCM juzi kule Dodoma. Akasimama Mbunge Ole Sendeka na kumtamkia Shelukindo; Futa kauli yako! Na Shelukindo akasimama haraka na kukubali kufuta kauli yake. Naam. Kikwete ni kama Mungu. Na yawezekana hataki Rais ajaye awe kama yeye. Kama hivyo ndivyo, basi, Mwenyezi Mungu ashukuriwe.
Kuna wakati , miaka ya mwanzoni mwa uhuru, Julius Nyerere alipata kumwambia mwandishi wa habari wa Kimagharibi; Rais Afrika n i mtu mwenye nguvu sana. Akikohoa tu. Waliomzunguka watashtuka na kunongonezana kwa kusema; Bwana mkubwa amekohoa!.
Ndio, Rais Afrika anaweza kuamka asubuhi na kuamua kufanya chochote anachotaka, hata kama kutaifisha mashamba na nyumba za watu. Rais yuko juu ya kila kitu.
Na Katiba yetu ya sasa inasema , mbunge anapovuliwa uanachama wa chama chake anapoteza sifa ya kuwa Mbunge. Lakini, hakuna mahali popote kwenye Katiba panaposema , kuwa Rais anapovuliwa uanachama wa chama chake, kuwa anapoteza sifa ya kuwa Rais. Hivyo basi, kimsingi, Rais anaweza kuhama chama chake, akaingia chama kingine na akabaki kuwa Rais, kwa mujibu wa Katiba ya sasa.
Naam, haiyumkini kwa waumini kumvua Mungu mamlaka yake. Lakini, waumini wanaweza kujitenga au kutengwa na Mungu wao. Mungu hawezi kukosa waumini wapya . Na waumini wale waliojitenga au kutengwa na Mungu wao wanaweza kuzibiwa njia ya kwenda peponi, na Mungu wao.
Hakika, tunahitaji Katiba Mpya itakayotunusuru na balaa la siku moja kuamka na kukuta tuna mtawala anayetumia mkono wa chuma. Ni Katiba mpya itakayotusaidia kumpata kiongozi mkuu na viongozi wa kumsaidia kiongozi mkuu katika kuliongoza taifa letu n a si kulitawala. Na hilo ni Neno la Leo.
Mungu Ibariki Afrika, Mungu Ibariki Tanzania.
Maggid Mjengwa
Dar es Salaam,
Jumapili, Februari, 5, 2012
Mjengwa Blog::Habari,Picha,Matangazo