Neno Fupi La Usiku Huu: Ng'ombe Aliyekonda Haoni Aibu, Bali Ni Mwenye Ng'ombe!

maggid

JF-Expert Member
Dec 3, 2006
1,084
1,246
Ndugu zangu,

Ng'ombe aliyekonda haoni aibu, bali aibu ni ya mwenye ng'ombe.

Wenye asili ya ufugaji wanalielewa hili vizuri sana. Kijijini inapoonekana ng'ombe wamekondeana watu huuliza; hawa ni ng'ombe wa nani?

Msemo huu una maana kubwa katika dhana nzima ya uongozi. Unaposhindwa kuongoza usisingizie unaowaongoza, maana, kiongozi ana wajibu wa kuonyesha njia ya kufuatwa.

Nakumbuka mwaka juzi nilipokuwa kijijini kwetu Nyeregete. Jioni moja kabla ya giza kuingia nilifuatwa na mama mwanakijiji. Akaniomba nimsomee kadi yake ya hospitali. Hajui kusoma. Ana HIV/ AIDS na anatumia dawa za kurefusha maisha.

Hakujua ni lini tarehe aliyopangiwa kwenda kuchukua vidonge vingine hospitalini. Nikamwambia, kuwa ni tarehe kama ya siku hiyo kwa mwezi mmoja uliopita. Kwamba alichelewa kwa mwezi mzima.

Nikamwangalia anavyoinamisha kichwa chini kwa huzuni. Hakukumbuka tarehe, hakujua kusoma. Nami nikapatwa na huzuni. Niliona aibu pia. Nilifahamu, kuwa si kosa lake. Wako Watanzania wengine wengi kama mama yule wa kijijini Nyeregete. Hawajui kusoma na kuandika.

Niliona aibu kwa vile tumeshindwa kuelewa, kuwa asilimia 39 ya Watanzania hawajui kusoma, kuandika na kuhesabu. Na kama taifa, hatuna mikakati tahabiti kwa sasa ya kupambana na adui ujinga.

Naam, ng'ombe aliyekonda haoni aibu, bali ni mwenye ng'ombe! Na hili ni Neno Fupi la usiku huu. Alamsiki!

Maggid Mjengwa,

Dar es Salaam.

0788 111 765
Mjengwa Blog::Habari,Picha,Matangazo
 

Similar Discussions

0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom