Ndugu wa waziri mkuu pinda wapata kikombe cha babu loliondo

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,720
21,779
Ndugu wa Pinda wapata kikombe Send to a friend Thursday, 12 May 2011 22:05 0diggsdigg

Mussa Juma, Samunge
UJUMBE wa watu zaidi ya kumi ambao ni ndugu wa karibu wa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, jana walifika kijijini Samunge wakiwa na ulinzi mkali ili kupata kikombe cha tiba, kinachotolewa na Mchungaji Ambilikile Mwasapila.
Ndugu hao wa Pinda, walifika Samunge saa saba mchana na magari matatu aina ya Toyota Land Cruiser, VX na Prado yenye namba binafsi na walikuwa wamewekewa ulinzi usiokuwa wa kawaida.

Mara baada ya kufika Samunge, ndugu hao wa Waziri Mkuu walipokelewa na maofisa wa Serikali na wale wa usalama ambapo walipelekwa moja kwa moja kwa Mchungaji Mwasapila kupata kikombe.

Ofisa wa Serikali, ambaye alishiriki katika mchakato wa mapokezi ya ndugu hao, alisema ni ndugu wa karibu wa Waziri Mkuu Pinda, ambao wametoka nyumbani kwake na ndio sababu wamepewa upendeleo maalumu katika kupata tiba hiyo.

"Ni kweli, hawa ni ndugu wa Waziri Mkuu, wamo kaka yake aliyeambatana na mkewe pamoja na watoto, pia wamo wajomba na wadogo zake na tangu asubuhi tumekuwa tukiwasubiri ili wapate huduma ya kikombe kutoka kwa Babu,"alisema ofisa huyo.

Hata hivyo, haikuwa rahisi kupata picha zao wakati wakinywa dawa baada ya maofisa wa usalama kuzuia wasipigwe picha kwa maelezo kwamba safari yao hiyo ni ya binafsi.Ujio wa ndugu hao, unafanya iwe familia ya pili ya vigogo wa Serikali kutua Samunge, familia nyingine iliyofika ni ya Rais Mstaafu, Ali Hassan Mwinyi ambapo watoto wake na wake zao walifika Samunge kupata kikombe cha Babu.

Bugudha kwa wageni
Mchungaji Mwasapila ameomba maofisa wa Serikali na Jeshi la Polisi kuacha kuwabugudhi wagonjwa kutoka nje ya nchi wanaokwenda Samunge kupata tiba.

Akizungumza na mamia ya watu kijijini Samunge jana kabla ya kuanza kutoa tiba, Mchungaji Mwasapila alisema amepata taarifa za kubughudhiwa kwa raia wa kigeni ambao wanakwenda Samunge. "Jamani watu wanapokuja hapa Samunge ni kwa shida, hivyo muwatendee mambo mema, wafike salama na kupata tiba,"alisema Mwasapila.

Hata hivyo, mchungaji huyo aliwataka wageni wanaofika Samunge kufuata taratibu za nchi ikiwa ni pamoja na vibali vinavyowaruhusu kuingia nchini.

Serikali na njia za panya
Serikali wilayani Ngorongoro imesema itaimarisha udhibiti wa matumizi ya njia za panya ikiwa ni pamoja na wale wanaotumia njia hizo, hasa wageni kutoka nchi jirani.
Mkuu wa wilaya hiyo, Elias Wawa Lali, alisema tayari Serikali imepiga marufuku magari kutoka nchi jirani kufika Samunge bila kupitia mipaka inayotambuliwa kisheria.

Akizungumza na Mwananchi jana, Lali alisema hatua hiyo, imechukuliwa ili kudhibiti wimbi kubwa la magari yanayofika Samunge kutoka nchi jirani kwa kupitia njia za Panya."Ili kukabiliana na wimbi hili baadhi ya wajumbe wa Kamati za Ulinzi na Usalama tumewatuma kuchunguza hiyo mipaka na kuona ni jinsi gani tutadhibiti,"alisema Lali.

Ushuru wachunguzwa
Katika hatua nyingine, Serikali imeanza kuchunguza ushuru wa Sh500 za Kenya ambazo, hutozwa madereva wa magari yanayotoka nchi hiyo jirani kupitia mpaka wa kijiji cha Soitsambu.Lali, alithibitisha kuanza uchunguzi huo jana na kutumwa kwa maofisa wa Serikali katika Kijiji hicho.

"Ni kweli tumepata taarifa za ushuru huo na tunafuatilia kujua uhalali wake,"alisema Lali.Kwa mujibu wa diwani wa Kata ya Soitsambu, Ngoitika Daniel, wao wanakusanya ushuru huo kwa kufuata taratibu na wamekuwa wakigawana fedha nusu kwa nusu na Halmashauri ya Ngorongoro.

"Fedha ambazo tunakusanya, zinatumika katika masuala ya usafi na ulinzi kama unavyojua kule ni mpakani na mazingira yameanza kuchafuliwa sana,"alisema Daniel.

Hata hivyo, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Ngorongoro, Dominick Lusasi alipotakiwa kuelezea ushuru huo wa magari kutoka nchi jirani ya Kenya, alisema yeye sio msemaji na anayepaswa kuulizwa ni Mkuu wa Wilaya.
 
Back
Top Bottom