Nchi ya Kitu Kidogo

Dingswayo

JF-Expert Member
May 26, 2009
4,019
2,923
Nimeipenda hii:

[video=youtube_share;Sr7_OI7QmVk]http://youtu.be/Sr7_OI7QmVk[/video]
 
NI dhahiri kwamba nchi inaweza kuwa ndogo lakini watu wake wakawa wakubwa, wakati ambapo nchi inaweza kuwa kubwa na watu wake wakawa wadogo. Hapa nazungumzia nchi yenye ukubwa wa ardhi na ukubwa wa idadi ya watu. Wakati mwingine sifa hizi zinaweza pia kuambatana na nchi kuwa na rasilimali kubwa na nyingi za kutosha.

Ziko nchi kubwa kwa maana ya ukubwa wa ardhi na watu na pia rasilimali maridhawa, lakini ambazo watu wake wamebakia kuwa wadogo, na mataifa yaliyoundwa na watu hao yakawa ni madogo pia. Hizi ni jamii na nchi za watu wapuuzi. Nchi ambazo kwa ukubwa wa maili za mraba na ukubwa wa idadi ya watu ni ndogo lakini zikawa na watu wakubwa na mataifa yake yakawa makubwa ni nchi za watu walio makini.

Napenda kuvitaja vielelezo kadhaa vinavyodhirisha kiwango cha juu cha upuuzi ndani ya jamii au nchi ambayo inakuwa kubwa kwa eneo la maili za mraba, wingi wa watu na rasilimali kubwa. Mojawapo ya vielelezo vikubwa vya upuuzi unaoweza kufanywa na jamii au nchi ni pale nchi au jamii inaposhindwa kutumia rasilimali zake kwa manufaa ya watu wake na badala yake ikaziruhusu zikaendelea kuwanufaisha wageni wakati watu wake wanaendelea kudhalilika.

Aina hii ya nchi kimsingi ni nchi iliyokosa uongozi na ikawa inaendeshwa na watawala ambao ama hawana uwezo ama hawana utashi wa kuwaongoza watu wao kuelekea katika maendeleo ya kweli. Mara nyingi hawa ni watawala wanaotawaliwa na uroho wa utajiri binafsi na ambao muda wao mwingi watakuwa katika shughuli za kujikusanyia mali wasiweze kufikia masuala magumu ya maendeleo ya watu wao.

Aghalabu pia watawala wa aina hii watakuwa ni wapagazi wa mabwana wao kutoka nje, hawa wakiwa ni watu binafsi, serikali, makamupuni ya biashara na asasi za kiulinzi na kijasusi. Watawala wa aina hii wanawatumikia wageni na hawana haya kuonyesha hali hiyo. Ndio wale ambao kila wakishutumiwa kwa hili au lile wanakuwa wepesi kusema, "Mbona huko nje wanatushangilia?" Kana kwamba "huko nje' ndiko kulikowachagua.

Mwisho wa siku watawala kama hawa hupoteza haiba (kama waliwahi kuwa nayo), huonekana zaidi wakijipendekeza kwa wageni, na huanza pole pole kuwaogopa watu wao kwa sababu hawana majibu kw maswali wanayoulizwa na watu wao ambao hawawezi kuelewa ufukukara wao unasababishwa na nin katika mazingira ya utajiri mkubwa. Na wala hawawezi kuelewa ubadhirifu unaofanywa na watawala ambao maelezo yao ya siku zote ni hali ngumu ya uchumi duniani.

Hawa ndio watawala wa nchi kama Zaire/Kongo niliowajadili majuzi, na ndio watawala wa nchi kama Nigeria. Zote hizi mbili ni nchi kubwa zenye watu wadogo zinaotawaliwa na watawala walafi. Haziwezi hata kidogo kuwa mataifa makubwa hata zingekuwa na utajiri mkubwa kiasi gani.

Nje ya bara la Afrika, ni nchi kama Urusi ambayo baada ya kusambaratika kwa himaya ya Sovieti (ambayo nayo ilikwisha kupoteza pumzi mapema) imekuwa ikijikokota chini kabisa ya utajiri ilio nao na uwezo wa watu wake. Leo Warusi ni watu wadogo, na taifa lao ni dogo likilinganishwa na ‘potensho' yake. (Vijana wa Kenya waliimba: "Nchi ya kitu kidogo, nchi ya watu wadogo").

Upande mwingine tunaona mataifa makubwa yaliyojengeka ndani ya nchi ndogo, kama Botswana na Mauritius, nchi zenye rasilimali kidogo lakini zenye uongozi makini ambazo zimeweza kuwafanya watu wake wawe wakubwa na watambulike hivyo duniani.

Katika historia ya dunia ya karne kadhaa zilizopita tunajifunza kwamba ‘kijinchi' kama Uingereza, ambacho hakikuwa na lo lote wakati huo, kikiwa kimefungwa katika kisiwa ambacho kwa nusu ya mwaka kimeganda na barafu, kiliweza kutawala nusu ya dunia ya wakati ule na kuwaweka mamilioni ya wanadamu chini ya himaya yake kutoka mashariki hadi magharibi, kaskazini hadi kusini.

Ni jambo gani liliifanya Uingereza iweze kuitawala dunia, kutawala Bara Hindi pamoja na watu wengi wale, tena wenye mapokeo na utamaduni wa fahari? Ni nguvu ya kujiamini, kuamini katika uwezo mkubwa wa jamii na uongozi wake na kuamini katika uwezo usiotishika wala kutikisika mbele ya adui au mpinzani ye yote.

Imani hii katika uwezo wa Uingereza ilipandikizwa akilini na mioyoni mwa watoto wa Uingereza tangu wakiwa ‘nkeremeke' (neno la Kihaya linalomaanisha kichanga) na imani ambayo walikuwa nayo ikawa ni silaha kubwa kila walikokwenda kupora nchi za watu wengine ili kuiletea fahari himaya ya Uingereza.

Hawakuendekeza watawala wala rushwa na wasaliti wa watu wao, na angalau mara moja mfalme wao alipodhihirika kutaka kuwakandamiza walizua uasi na wakamkamata na kumkata kichwa. Katika msukumo wa kutafuta fahari ya Uingereza hawakuvumilia upuuzi.

Mzee mmoja wa Uingereza aliyewahi kufanya kazi kama mtawala wa kikoloni nchini Tanganyika aliniambia kuwa siku ya kwanza shuleni walikusanywa kwenye gwaride la shule nzima na mkuu wa shule akawaambia:
‘Nyie watoto mna bahati kwani mmezaliwa mkiwa Waingereza. Hiyo ina maana mmeshinda bahati nasibu ya kwanza katika maisha yenu."

Nani anaweza kuwaambia watoto wa Tanzania kitu kama hicho leo hii? Katika mazingira mengi watoto wanaweza hata kumzomea kwa sababu hawaoni ni nini hasa kiwafanye waone fahari ya kuwa Watanzania, watu wenye mashaka katika kila idara ya maisha yao, wanaoongozwa na watawala ambao wanaelekea bado wanatafuta kuelewa ni nini hasa maana ya uongozi?

Jamii au nchi inakuwa ya kipuuzi iwapo ina kila aina ya rasilimali lakini rasilimali hizo haziisaidii jamii wala nchi kuendelea wala kuwa jamii au nchi ya furaha. Furaha ndani ya jamii si lazima itokane na maendeleo makubwa ya kiuchumi na ujenzi wa vitu kama barabara na majumba. Hivi ni muhimu, lakini si kila kitu. Zipo jamii duniani ambazo kwa vigezo hivi zinaitwa jamii masikini, lakini viwango vyake vya furaha viko juu sana.

Hizi ni jamii ambazo zimeridhika na hali ya maisha kwa sababu zimeweza kujenga utangamano kati ya rasilimali zilizopo na mafanikio ya kimaisha ya watu wake. Mathalan, jamii inaingiza kipato cha shilingi kumi, kila mwanajamii analijua hilo, halafu jamii inanufaika kwa kiwango cha shilingi kumi, na kila mwanajamii analijua na kulielewa hilo, na wanajamii wote, isipokuwa mwendawazimu, wanaridhika.

Jamii inajihatarisha yenyewe iwapo itafanya kinyume cha hilo, iwapo, mathalan, itaingiza kipato cha shilingi kumi kisha ikaruhusu shilingi moja tu itumike kwa manufaa ya jamii halafu jamii isijue shilingi tisa zilizobaki zimetumika vipi. Hata kama hakuna wizi au ubadhirifu katika matumizi bado misingi ya vita itakuwa imekwisha kujengwa kutokana na nakisi ya taarifa, uwazi, uelewa na maridhiano.

Maridhiano ni tunda la maelewano na maelewano ni tunda la kueleweshana katika uwazi. Uwazi unapopungua na sehemu ya jamii ikahisi kwamba inadhulumiwa au haitendewi haki unakuwa ndio mwanzo wa chokochoko na mfarakano.

Uwezo wa kuchagua umo ndani yetu. Tunaweza kuchagua kuwa nchi kubwa kwa maana ya eneo la maili za mraba na idadi kubwa ya watu (na rasilimali nyingi na kubwa) lakini papo hapo tukawa taifa la wapuuzi, tukajulikana hivyo duniani, au tukachagua kuwa taifa dogo kwa vigezo vya ukubwa wa ardhi, idadi ya watu na rasilimali lakini tukatumia rasilimali hizo ndogo, udogo wa idadi ya watu wetu na udogo wa eneo la mraba la nchi yetu kuwa (na kutambulika kama) taifa kubwa.
Ni kuchagua baina ya kuwa kama Uingereza ama kuwa kama Zaire/Kongo.


Source: Jenerali Ulimwengu: Raia Mwema - Nchi ya kitu kidogo, nchi ya watu wadogo
 
Analysis nzuri sana. Swali ni je nini kifanyike ili tuweze kujinasua kutoka hapa tulipo ili at least tunapozaa watoto tusisikitike kwamba tumewaleta kwenye nchi ambayo hawatakuwa na matumaini.
 
asante kwa somo zuri ila tatizo letu haya yanabaki hapa tu wala hayaendi popote ndio tatizo kubwa la watanzania
 
Mkuu jenerali, Mzee wangu huwa nakukubali sana. lakini pamoja na uchambuzi wako, bado Tanzania na watanzania wanalirudisha madarkani hili li CCM bovu. Binafsi safari hii nimedhamiria kuipinga CCM hata kwa kukampenia chama kingine tu hasa CHADEMA, kwa sababu nimeona Tanzania haiwezi kupata mabadiliko ya kweli kama CCM bado ipo madarakani.

Ni kwa kuiondoa CCM madarakani tu, ndio watanzania tutakuwa tumewapa fundisho wanasiasa watuheshimu na siku zote wafuate matakwa ya wananchi. Naamini CHADEMA wakiingia madarakani watakuwa wamejifunza kuwa wananchi hawataki mchezo, ukicheza, wanachagua chama kingine.

CCM nao watakuwa wamejifunza kuheshimu matakwa ya wananchi, ili kama ikitokea siku nyingine wakapewa tena serikali wakumbuke mtanzania sio wa kuchezea.
 
tz.jpg
This still happens today in this richly and blessed land. We need to do something for sure, but we first need to be tired with this.
 
View attachment 64277
This still happens today in this richly and blessed land. We need to do something for sure, but we first need to be tired with this.

Yasikitisha! Tanzania imerogwa na nani? Halafu rais wa nchi kama hii ndiye anayeshikilia rekodi ya dunia kwa safari za nje! Amekwenda hadi Jamaica kununua casette za Reggae! Yasikitisha, Hata Chad hawako namna hii na walikuwa vitani tangu 1964!
 
Back
Top Bottom