Elections 2010 Natamani Mpendazoe atumie hoja hizi kuimaliza CCM Segerea

tempo_user1

Senior Member
Sep 7, 2010
134
15
Wapiga debe na hoja zisizojaa mkononi

Godfrey Dilunga Septemba 22, 2010 (Raia Mwema)

WILLIAM Penn Adair, maarufu kama Will Rogers, mwigizaji na mtunzi wa filamu wa Marekani wakati fulani aliwahi kuelezea majuto yake kuhusu wanasiasa.

Hakuna sababu za kina zilizoainishwa kufafanua kwa kina kwa nini alionyesha majuto. Itoshe tu kusema, Rogers alichukizwa na baadhi ya matendo ya wanasiasa.

Chuki yake dhidi ya baadhi ya matendo hayo ya wanasiasa ni kutumia mfano mgumu na pengine wenye kukera wanasiasa husika.

Alidhihirisha namna anavyokerwa na wanasiasa wa aina hiyo. Katika mazingira yasiyo ya kawaida, Rogers alidiriki kusifu tabia ya mbwa dhidi ya baadhi ya wanasiasa.

Alisifu tabia ya mbwa dhidi ya wanasiasa wanafiki, wasio na haya. Wanasiasa walioko tayari kujidhalilisha au kudhalilisha washindani. Wako tayari kufanya hivyo kwa sababu za kisiasa, tena siasa chafu.

Katika kueleza kwa namna gani wanasiasa hao walivyo kero, mtunzi huyo wa filamu, aliyefariki dunia mwaka 1935, akiishi duniani kwa miaka 36 tu, hakusita kusema anampenda sana mbwa kitabia dhidi ya wanasiasa hao.

Akabainisha sababu za kumpenda na kumheshimu mbwa kuliko wanasiasa wa aina hiyo. Akasema ni kutokana na ukweli kuwa, chochote anachofanya mbwa hafanyi kwa sababu za kisiasa.

Will Rogers, ananukuliwa akitamka; “I love a dog. He does nothing for political reasons.” Ni kweli, pale mbwa anapobweka, basi, hufanya hivyo si kwa sababu ya kisiasa.

Mbwa anabweka kwa taratibu zake, kwa mazingira anayokabiliana nayo kwa wakati husika. Hafanyi hivyo eti tu kuhemea tumbo.

Hajipendekezi kwa anayemmiliki, kubweka kwa mbwa ni matokeo ya matumizi ya kiwango cha juu cha maarifa yake. Anatoa ishara kwa kupiga kelele (kubweka) bila kujali ni wakati gani.

Mbwa anapiga kelele bila kujali ni usiku wa manane. Hajali uwezekano wa kumkera anayemlisha. Anasimamia ukweli. Kwamba kama kuna hatari anatoa ishara. Haogopi kumkera yeyote kwa kelele zake.

Hamwogopi hata adui. Mbwa ni mkweli kwa kuzingatia hali halisi. Anatoa ishara kulingana na mahitaji ya wakati. Na kwa hiyo, kwa mujibu wa Rogers, ni kiumbe cha kuaminika zaidi ya baadhi ya wanasiasa.

Mbwa anatimiza wajibu wake kikamilifu si kinafiki. Anawajibika. Wakati mwingine inapobidi, mbwa hufanya shambulizi dhidi ya adui (kwa kuzingatia tafsiri yake).

Kwa hiyo, mbwa kwanza anatoa ishara lakini ikimlazimu anafanya shambulizi. Matukio haya mawili yanalenga kulinda maslahi ya anayemtunza, si kwa masharti au amri ya mtunzaji bali kwa kuzingatia mtazamo wa mbwa.

Msimamo huu wa mbwa umemjengea heshima kubwa sana. Bosi aliyekuwa akikoroma usiku na kuamshwa kwa kelele za mbwa, hatachukia. Badala yake, atajiandaa kwa kuwa anaamini ishara za mbwa wake kuwa kuna hatari nje.

Mantiki ya maelezo haya ya Will Rogers, ni muhimu kwetu hususan wakati huu wa kuelekea Uchaguzi Mkuu.

Kwa kuzingatia mantiki ya mfano wa Rogers, nitajadili tabia ya baadhi ya wapambe au wapiga debe wa wagombea hasa nafasi ya ubunge.

Kwa kadri kampeni za Uchaguzi Mkuu zinavyoelekea ukingoni, ni dhahiri baadhi ya wapiga debe wa wagombea hawapaswi kuaminika.

Baadhi ya wapiga debe hao wameibua kauli zenye udhalilishaji dhidi ya viongozi wenzao. Wamedhihirika kutenda ubaguzi kwa kujaribu kubomoa msingi wa utu.

Kimsingi, hatupaswi kujiruhusu kushawishika kupiga kura kwa kuzingatia baadhi ya kauli zao jukwaani. Na kwa mazingira haya tuungane na Rogers, kupenda tabia fulani za mbwa kuliko watu hawa.

Ipo mifano ya wanasiasa wasiopaswa kuaminika jukwaani. Kati ya mifano hiyo ni waliokuwa viongozi wa kilichokuwa Chama Cha Jamii (CCJ), hususan aliyekuwa Mwenyekiti wake, Richard Kiyabo.

Huyu amejiunga na CCM. Ni haki yake. Hata hivyo, ikumbukwe ndiye aliyekuwa mwenyekiti - kiongozi wa juu wa CCJ. Inawezekana kuna mambo aliamini pamoja na wenzake wanaweza kufanya.

Kama nilivyoeleza, sina tatizo na uamuzi wa Kiyabo kuanzisha au kuhama chama. Au kutokuwa mwanachama wa chama chochote. Ni haki yake kushiriki shughuli za siasa.

Tatizo langu ni aina ya upigaji debe wake hasa alipokuwa akimnadi mgombea ubunge wa jimbo la Segerea-Dar es Salaam kwa tiketi ya CCM, Dk. Makongoro Mahanga, dhidi ya mgombea wa CHADEMA, Fred Mpendazoe.

Katika mkutano wa kampeni, alinukuliwa akisema alimuomba Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba kujiunga na chama hicho. Akakubaliwa.

Lakini pia alikuwa na ombi jingine. Aliomba kazi ya kuinadi CCM jimbo la Segerea. Kwa mujibu wa maelezo yake, aliomba kazi maalumu (sijui kama malipo yake pia ni maalumu).

Akiwa jukwaani, akabainisha kuwa yeye na Mpendazoe ni ndugu. Huu ni ukweli alioamua kuuweka hadharani kwa mara ya kwanza tangu atoke CCJ.

Lakini mbali na ukweli huo, ukweli mwingine ni kwamba, kwa kushirikiana wao ndiyo waliofanikisha uanzishwaji wa CCJ.

Bila shaka, wote waliridhika kuwa ni watu makini katika harakati zao CCJ. Hawakutiliana shaka historia zao binafsi na hata za kiuongozi. Walikuwa viongozi wa kitaifa CCJ. Mmoja mwenyekiti, mwingine msemaji wa chama hicho.

Hata hivyo, katika uzinduzi wa kampeni za ubunge za CCM, Segerea, Kiyabo ambaye ameomba kazi ‘maalumu’ kwa Makamba, alimtaja Mpendazoe si mtu makini.

Sitaki kuingilia kati mashambulizi kati ya Kiyabo na Mpendazoe. Kilichonikera ni Kiyabo kuhusisha mashambulizi yake na watu wasiokuwamo, tena katika mwelekeo wa kuwadharau.

Akiwa jukwaani Kiyabo alisema kwamba kazi anayostahili Mpendazoe ni ubalozi wa nyumba 10 tu na si vinginevyo. Hii ndiyo kauli iliyonikera. Kauli hii ndiyo kiini cha mjadala.

Madhara ya kauli hii yamegawanyika katika maeneo mengi lakini nitabainisha machache. Kwanza, pengine kwa kukosa maarifa ya kutosha, Kiyabo ameshindwa kutambua au kujitambua kuwa mbele ya wana-CCM amedhihirisha hakijui chama hicho.

Makamba na wenzake CCM pamoja na udhaifu wao wa kimaadili na kiutendaji, wakati fulani wamekuwa na ndoto zenye mantiki kwamba mabalozi wa nyumba 10 ndiyo nguzo ya ushindi wa chama chao.

Kwa maana nyingine, wanaheshimu mabalozi wa nyumba 10. Ni mtaji wao wa ushindi. Ni jeshi lao la ushindi. Mabalozi ni askari wa mstari wa mbele CCM. Mabalozi si kundi la watu wasiojua kuongoza, wachovu wa kufikiri.

Kwa hiyo, kitendo cha Kiyabo kutumia mabalozi kama mfano unaotoa tafsiri kuwa ni viongozi wasio na maana mbele ya jamii, ni kosa kubwa kwenye jukwaa la kampeni, na hasa Segerea.

Pili, uwezo wa Kiyabo kujitambua na kutambua kauli gani itolewe wapi, kwa wakati gani na kwa malengo gani si wa kiwango kikubwa.

Kitendo cha kusema mtu asiye na sifa za kiuongozi, basi, anastahili ubalozi wa nyumba 10, kinadhihirisha kuwa hana imani na wasio na madaraka makubwa nchini.

Mtazamo wake ni tofauti na mtazamo wa waasisi wa CCM ambao waliamini katika uongozi shirikishi ngazi za chini, wakabuni mabalozi wa nyumba 10.

Tukio hili ni sehemu ya matokeo ya CCM kugeuka kokoro la kubeba kila anayedhaniwa anaweza kutamka chochote dhidi ya uypinzani bila kujali kinaweza kuumiza chama hicho kwa kiwango gani.

Kama nilivyoeleza, wakati wa waasisi wa CCM wakiwa kwenye hatamu za uongozi mabalozi ndiyo waliokuwa msingi wa chama hicho.

Hata hivyo, haishangazi pengine alichosema Kiyabo ndicho wanachofikiri na kuamini hata viongozi wengine waandamizi CCM.

Dharau ya Kiyabo kwa mabalozi pengine imefanana na ile waliyokuwa nayo baadhi ya vigogo wa CCM, na ndiyo maana wamempokea haraka na baada ya dakika kadhaa wakamteua mpiga debe, tena jukumu zito la kunadi CCM.

Tafakari: Kiyabo ametamka hayo mbele ya Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, John Guninita ambaye kwa nafasi yake alipaswa kunusuru chuki inayoweza kujitokeza miongoni mwa mabalozi wa nyumba 10 kutokana na kauli husika. Huyu hakuona tatizo.

Lakini si Guninita pekee, Makongoro Mahanga ambaye ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM, kama ilivyo kwa Guninita, naye hakuona tatizo. Hakutafakari madhara ya kauli hiyo. Huku ndiko kuporomoka kwa maadili ya viongozi tunakopigia kelele kila kukicha.

Viongozi wakubwa (kitaifa) katika CCM leo hii wamejiwekea daraja. Wanaamini ni tofauti na viongozi wadogo (mabalozi). Wasiyemtaka au anayewakera basi wanamfananisha na mabalozi wa nyumba kumi.
 
Dilunga, huu uchambuzi wako umetulia, nimeukubali..nimesoma x2.
Natumaini pia ujumbe umewafika wengi..
 
Back
Top Bottom