X-PASTER
JF-Expert Member
- Feb 12, 2007
- 11,610
- 1,810
Natamani Kuishi Tanzania Na si Tanganyika
Salaam ndugu zanguni wapendwa ndani ya jukwaa hili la JF, ni matumaini mpo na siha njema kabisa. Leo nami nimeonelea kuingia tena kwenye jukwaa la siyasa, maana tangia kipindi kile refa alipo amua kukwatua nami nikaamua kukaa pembeni na kuwa mtazamaji badala ya kuwa mchezaji.
Wengi watashtuka na kichwa cha makala haya, Natamani Kuishi Tanzania Na si Tanganyika Naam ndugu zanguni kwani leo nimewakumbuka ndugu, marafiki, na jamaa zangu, niliokuwa naishi nao nyumbani enzi zile nchi ilipokuwa ikijulikana kwa jina la Tanganyika !
Kumbukumbu zangu kwenye somo la historia, nikichanganya na simulizi toka kwa Marehemu Babu na Bibi yangu walipokuwa wakinihadithia jinsi harakati za ukombozi wa Tanganyika zilivyoanza. Walinihadithia kuwa harakati zilianza pale tu mkoloni wa kwanza Mjerumani alipotia mguu wake kwenye ardhi hii tukufu ya Tanganyika.
Mkoloni alitiwa sana adabu na mababu zetu ambao kwa namna moja ama nyingine ule ushujaa na uhodari wao hakuna aliyeweza kuurithi hata mmoja.
Nakumbuka kuwa harakati zilishika kani zaidi Kadri muda ulivyokwenda harakati hizi ziliongezeka na kuwa maarufu haswa miaka ile ya hamsini na hasa baada ya chama cha TAA kubadili jina kuitwa TANU.
Kipindi kile watu hawakuwa waoga kueleza kweli, vijana kwa wazee walijitolea kwa hali na mali ili kufikia malengo ya kupatikana kwa uhuru kamili katika kujitawala na kujiamulia mambo yetu wenyewe. Matunda ya harakati hizi yalipatikana mwaka 1961 ambapo Tanganyika ilipata uhuru wake Hakika ilikuwa furaha ilioje kwa wazalendo haswa wale wanaharakati, waliojitolea kupigania uhuru wa Tanganyika.
Ni dhahiri kuwa usiku ule wa Desemba 9, 1961 wakati ilipokuwa inashushwa bendera ya Muingereza na kupandishwa ile ya Tanganyika, wengi walitokwa na machozi ya furaha kila aliyeshuhudia alikuwa na yakini kuwa ule ulikuwa ndio mwanzo wa maendeleo ya nchi yetu Tanganyika.
Maendeleo ambayo yangekuja kuonekana katika hali bora zaidi za kiuchumi kwa taifa na mtu mmoja mmoja, nyumba bora zaidi, kilimo cha kisasa zaidi, usafiri bora zaidi na juu ya hayo elimu bora zaidi na kwa wote.
Ni hakika kabisa wale wote ambao leo hii tumewasahau kuwa ndio mashujaa wetu walio kufa shahidi walikufa katika harakati zile nao wamekufa wanaamini vivyo hivyo. (si ajabu wakifufuka leo hii na kukuta hali hii watakufa papo hapo kwa kihoro).
Lahiti tungalijuwa kuwa Uhuru ule ungetuletea mashaka haya nina ukakika kabisa washujaa wetu wasingetumia mali zao na muda wao kuondoa ubaguzi wa kikoloni na hata ingekuwa tumepewa uhuru bila ya harakati basi hakuna ambaye angesheherekea kama ilivyokuwa siku ile ya uhuru.
Lakini basi hakuna mtu yeyote aliyekuwa na mashaka siku ile ya uhuru juu ya uhusiano mkubwa uliokuwepo baina ya kuondoka kwa wakoloni, yaani kupata uhuru na kukaribisha aina mpya ya ukoloni ambao leo tunahuita kwa jina jingine la kizalendo zaidi, yaani ufisadi miongoni mwa watu wachache wakikumbatiwa na watawala wa nchi hii.
Leo hii inakaribia miaka hamsini (50) tangia tupate uhuru wetu, wengi wa wale waliokuwepo na wale waliokuja kuzaliwa nyuma, si ajabu wakawa na wakati mgumu zaidi endapo wataulizwa kubainisha wakati ule wa mkoloni na huu tulio nao upi ni bora kwao. Si ajabu leo mtu akaulizwa uhuru na ukoloni utachagua nini? Si ajabu kwa mtu ambaye amebahatika kuona utawala wa Mjerumani na Muingereza akisema...
Subiri nifikirie!.... Mmmm ukoloniiii... nahisi jina ukoloni kama si jina zuri labda tuite ule utawala wa Mjerumani na Muingereza uzuri ni kuwa haukuwa wa Kifisadi...
Baada ya uhuru mwaka 1961 viongozi (nina maanisha watawala) wa Tanganyika walifanya mengi wakidhani kuwa wanaendeleza nchi hii. Kuna mambo mawili ambayo yalikwisha pangwa na UN (United National) Nayo ni:
Uhuru wa Tanganyika mwaka 1961 na kupatika kwa Jamhuri ya Tanganyika1962.
Haya mawili hayakuwa na shaka, lazima tungeyapata maana yalikuwa ni moja ya maazimio ya Umoja wa Mataifa.
Baadaye Wale watawala wetu wakaamua kuunganisha nchi mbili ambazo kwa simulizi zisizo rasmi inasemekana kabla ya Gharika kuu (enzi ya Nabii Nuhu) hizi nchi zilikuwa ni nchi moja, ila baada ya ile zahma ya gharika, nchi iliyokuwa moja ikajikuta imegawanywa mapande mawili mapande hayo ya ardhi baadae sana yaani baada ya kupita karne nyingi sana zikaja kujulikana kwa majina ya Tanganyika na Zanzibar.
Ndipo mwaka 1964 watawala wetu shupavu (!?) kwa jeuri zote wakaamua kurejesha na kuziunganisha nchi hizo na kufanya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, na nchi hizo zikajipatia jina maarufu la Tanzania.
Watawala hawakuishi hapo, maana maazimio yao yalikuwa mengi sana miaka mitatu baadae wakaona si vibaya kuchukuwa kwa nguvu mali, majumba, mashamba na mashirika waliyo yakuta na kuyafanya kuwa ni mali ya Umma (!?) kwa ufupi walitaifisha mali za watu binafsi na kuzifanya za taifa (sina uhakika hapa kama kweli zilikuja kuwa mali za umma au za viongozi wachache). Mambo hayo yalijiri mwaka sitini na saba (1967) na tukaipa jina - Azimio la Arusha.
Hawakuishia hapo fikra zao sahihi zikapelekea azimio lingine la madaraka mikoani hii ilikuwa mwaka1971 (siyasa hii ilikuja baadae kuuwa co-operatives zote zilizo anzishwa na wananchi, usiniulize tafadhali ilikuwaje kuwaje sitaki udaku).
Bila kuwachosha wengi wetu wanakumbuka sana kipindi ambacho wanafunzi waliomaliza darasa la saba na kuingia kwenye ualimu (U.P.E) (nahisi hapa ndipo ile graph ya elimu ilipoanza kushuka kwa kasi sana ) Bila kusahau mambo ya vijiji vya ujamaa, kama bado unakumbuka maduka ya kaya, elimu bure, kutaifisha majumba, mashamba na kila dhahma ambayo sijaiweka hapa.
Makada nao hawakuwa nyuma maana nyimbo nyingi zilitungwa kupongeza kila hatua iliyochukuliwa. Kwa bahati nzuri miaka yote ya sitini na sabini iliwashuhudia Watanzania chini ya utamaduni wa kuheshimu na kuthamini sana viongozi wao, hivyo moyo wa uzalendo ulijitokeza wazi wazi. Kwa hakika tulizitimiza na kuzifanyia kazi Fikra sahihi za Mwenyekiti !
Hali hii ilijitokeza hasa pale wananchi walivyozitii hata amri ambazo ziliwaletea maafa na taabu za kimaisha maana hata serikali iliona tabu kuzitekeleza, mfano kuanzishwa vijiji vya ujamaa, kutaifisha majumba na mashamba n.k.
Watawala hawakuishia hapo Wakatuambia nasi tukaamini kuwa Tanzania haiwezi kuwa huru hadi Afrika yote iwe huru (Fikra nzuri eeh?). Tulitumia kila tulichoweza kufikia lengo hili. Tukawasaidi wale tulio waita ndugu zetu kusini mwa bara la Afrika vyama kama ANC, SWAPO, MPLA na FRELIMO na kule Biafra Nigeria Hakika walifaidi sana msimamo wetu huo.
Kwa kweli watawala hawakuchoka, maana ile siyasa ya ujamaa na kujitegemea ilikuwa imeshika kani kweli kweli tulifunzwa mbinu nyingi ikiwemo jinsi ya kufanya propaganda za kisiyasa, na haswa kipindi kile ambacho tuliambiwa kuwa Idd Amin ni nduli tena Joka Kuu, ambalo linatumiwa na mabwana zake ili kuzorotesha harakati za ukombozi wa Afrika. Na lipo tayari kulimeza Bara lote la Afrika... loh! Wananchi tukataharuki... Maana limesha anza kuimeza Kagera yetu na kiwanda chetu cha sukari guru kimeliwa na Joka hilo... Tulilikubali hili watu walitoa mali na roho zao kuikomboa (!?) ardhi ya majirani zetu na Kagera yetu, kisha tukampa adhabu kidogo sana ndani ya mipaka ya nchi yake. Tukamweka yule tuliye mtaka . Nina maanisha aliyetakiwa na mtawala wetu.
Mambo yote haya yalifanyika bila mtu yeyote kuhoji kwa vile wengi walidhani kufanya vile ni katika harakati zile zile za kutuletea maendeleo.
Leo hii ni miaka miaka 48 kasoro mwezi mmoja maana desemba hiyo yaja ., wale waliojaliwa umri na wale waliozaliwa nyuma tunalazimika kujiuliza ikiwa ndoto zetu juu ya faida za uhuru zilikuwa kweli.
Wazalendo wale ambao enzi zile walijulikana kama Makabwela, yaani watu wa kipato cha chini, leo hii tunajulikana kwa jina la Walala Hoi, na haswa wanaoishi mikoani wanaweza zaidi kuona kile ninacho kizungumza (Kama nao wanapitia JF subutuuu).
Ni matarajio ya kila binadamu anayeishi kwa kupambana na maisha kumwona mwanaye akilala katika nyumba bora zaidi kuliko ile yake, akila chakula bora zaidi na kuvaa mavazi bora zaidi. Kwa kweli hali ni kinyume kabisa kwa wale tunao itwa Walala hoi.
Si ajabu uko mikoani na haswa ukitembea siku ya gulio ukamwona dalali akiuza kitanda cha kamba... (bado kuna uwezekano wa kumpata mtu anayelalia kitanda cha kamba au telemka tukaze) karne hii.
Mimi bado najiuliza sababu ya huu umasikini ni nini haswa. Tulikuwa tunaambia kuwa ili nchi iendelee tunaitaji mambo manne, Ardhi, watu, siyasa safi na uongozi bora Je hivi vyote kweli hatuna hata kimoja !?
Kuna siku katika kupita pita zangu mitaani, nilipita kwenye kigenge cha kahawa, kulikuwa na mkusanyiko wa vijana na wazee walikuwa wakijadili mambo ya kimaisha na pembeni yake kulikuwa na muuza magazeti, japo mengine yalikuwa yameshachakaa nikaamua kukaa na kuagiza kahawa ili nipate mawili matatu, hakika sikuwaruhsu wafahamu kuwa nilikuwa ninawasikiliza. Mzee mmoja wa makamo aliyeonekana kama mtu wa kijiweni alikuwa amevalia kaunda suti yake ya kijivu iliyo chakaa na kuweka vilaka vya rangi mbali mbali, alitoa hoja zilizonisisimua na kunifanya niamini kuwa alikuwa ni afisa wa serikali ya ujamaa na kujitegemea aliyestaafu.
Kimsingi haiba yake haiwezi kumtofautisha na mtu wa mtaani bali hoja zake zilimtofautisha.
Yeye alidai kuwa uvivu wa Watanzania umeanzia kwenye vijiji vya ujamaa na utaifishaji mali za watu uliofuatia Azimio la Arusha . Anasema mtu anahamishwa kwenye eneo lake lililo karibu na shamba lake halafu anahamia mbali na shamba lake vipi tena aweze kurudi kulihudumia?
Serikali ilipoamua kuzuia umilikaji mali binafsi na kutilia mkazo mali kuwa ya wote, au ya mtu kufanya kazi tena kwa nia ya kujipatia mali watu wengi wakaogopa kutafuta mali na kutegeana kwenye mambo ya ushirika.
Akaongeza kuwa watu waliokuwa na majumba ya ghorofa waliponyang'anywa walio baki wakaamua kuamisha mali zao kisiri siri Zikapelekwa Canada na Uingereza.
Kuna mameneja na wakurugenzi ambao walikuwa wakiharibu hapa wanapelekwa pale, nayo hii iliuwa hali ya walalahoi kujituma kwenye uzalishaji mali viwandani na maofisini !
Kuhusu mazao ya biashara kama korosho, pamba na mengineyo ambayo serikali imeshindwa kuyapatia masoko na dhurma imeamua kulipiza kisasi kiasi ambacho hata wananchi wakaona kuwa ni kazi bure kuingia kwenye kilimo cha mazao ya biashara, kwani hayana masoko uko nje au watawala wanawaibia wakulima kwa kuwalipa kidogo sana kiasi wakashindwa hata kununua pembejeo, kazi kila msimu ni kukopa tena na tena.
Mstaafu huyo wa serikali ya ujamaa alionyesha kuwa huenda mazao ya Biashara yamehujumiwa na wale ambao tulio wadhurumu kipindi kile cha Azimio la Arusha Nasikia India ndio ilikuwa mnunuzi mkubwa wa korosho ya Tanzania.
Pia alidai kuwa viwanda vingi vilivyotapakaa kuanzia Kibaha, barabara ya Nyerere, Barabara ya Kilwa, na uko mikoani vilijengwa bila kuzingatia utafiti wa kitaalamu juu ya uwezo wetu wa uzalishaji. Na vile tulivyo virithi toka mkoloni tuliwapatia watendaji wasio na uwezo wala ubunifu wa kuendeleza viwanda.
Alihitimisha kwamba maamuzi ya kisiyasa yaliyofanywa na watawala wetu bila kuzingatia ushauri wa kitaalamu ndiyo sababu ya kukata tamaa kwa Watanzania na hivyo kuwa wavivu. Watawala walikuwa Hawa-Hambiliki
Lakini cha ajabu leo hii kuna matajiri wakubwa kupindukia kiasi ya kwamba nafasi kati ya walio nacho na wasio nacho ni kubwa sana !
Nilipo angalia muda nikaona umeyoyoma, nikanyayuka na kuelekea zangu nyumbani uku nikiyatafakari maneno ya mzee yule mstaafu... Nikawa najiuliza Natamani nami nikagombee japo Ubunge, lakini nashindwa ni ahadi au matumaini gani niwape watu hao.... Utashangaa zaidi ukianza kufikiri kuwa watu hawa wamekuwa wakishiriki uchaguzi wa wabunge na Rais kama mara nane sasa tangu tupate uhuru, na hasa nashindwa kujua ikiwa wengi wao wanafahamu uhusiano uliopo baina ya thamani ya kura zao na hali yao duni ya maisha....!
Nakumbuka kuna wakati ilisemekana kuwa baadhi ya wabunge wa kusini waliona ni heri kujitenga na kujiunga na Msumbiji. Kipindi kile tuliwaona kuwa hawa wabunge wamekosa uzalendo au wamekosa la kuongea bungeni.
Hata mie nilidhani hivyo hivyo, lakini sasa nimeona mantiki ya tamko lile. Kwanza wenzetu wa Msumbiji wanasababu ya kuwa masikini. Uhuru wao wote, wameishi katika vita vya wenyewe kwa wenyewe. Lakini sisi tunajivunia amani na utulivu hali yetu shwari kabisa, "Mchawi" wetu ni nani?
Wako watu ambao tayari walishaanza kushtuka mapema... Lakini pia wako wapiga kura walioanza kujua chanzo cha matatizo yao na kutumia kura zao vema. Wako wale ambao wanadhani hali yao ya maisha inatokana na kudura za Mungu na hawaitaji mabadiriko maana kila kiongozi ni chaguo la mungu.
Palipo na matatizo watu uja na njia na mbinu mbalimbali za namna ya kutatua tatizo. Kwa wale wenye mtazamo wa kisiyasa kama mimi na wewe huenda watu hawa wanahitaji msaada wa kisiyasa, katika zama hizi za uwazi na ukweli ni vyema wakazifahamu haki zao za kiraiya, wakajua kutofautisha kati ya mwananchi na raia. Na kufahamu thamani ya kura zao.
Wakijua hili ni rahisi kujua kuwa kura yao ndiyo itakayochagua aina ya maisha watakayoishi miaka 10 ijayo. Baada ya hapo watampima muombaji kwa kile atakachowafanyia, watamtazama endapo hana uhusiano na hao waliowadumaza.
Kwa wale walio katika madaraka njia hii huenda ikawa mbaya kwao endapo wananchi wakigundua kuwa ndiyo "wachawi" wao la sivyo ni njia nzuri ya kutofautisha wanasiyasa wa watu na wale wababaishaji.
Ni wazi pia kuwa wako wananchi ambao hawajui kuwa wanataabu kwa vile tu hawajawaona wenzao wenye afadhali. Pia wapo wanaojua wana taabu lakini hawajui wafanye nini.
Cha msingi ni kwamba wote tunao tegemea maisha ndani ya Tanzania yawe bora kuliko yale ya Tanganyika, hatukutegemea kuishi ndani ya "Tanganyika" hadi leo hii miaka inakaribia hamsini (50) baada ya uhuru.
Hata Mlalahoi naye ana hadhi yake na haki zake zinazoandamana na hadhi hiyo. Tanzania bado kuna hukumu ya kifo na nina uhakika kabisa Walalahoi wote tumekwisha hukumiwa kifo tayari, japokuwa si kwenye mahakama rasmi, lakini tawala zetu zimesha tuhukumu... japokuwa si kile cha kunyongwa hadi kufa kwa kuning'inizwa kambani lakini cha moto tunakiona... Na tunakufa taratibu tukijiona na machozi yetu yenda na maji hakuna wa kuyaona.
Walalahoi tunajiuliza "Masihi Mkombozi" wetu atazaliwa lini? Au huenda baadhi yetu tunatamaa labda ndiye huyu au yule Maana zama hizi wapo wengi kweli kweli.
Ninachopenda kuwaambia ni kuwa maendeleo ya watu huletwa na watu wenyewe. Tuuzeni kura zenu kwa maendeleo Tusipapie tena pilau, vitenge na pesa za kula leo na tukabakia na njaa ya miaka kumi ijayo.
Nyie wanasiyasa mnao jiita wapinzani Masihi watarajiwa wa Kumkomboa Mtanzania mmefanya juhudi zipi kutuelimisha wapiga kura wenu ili tupate kuwachagua ? Je ni kweli mpo tayari kutuletea maendeleo tukaishi Tanzania badala ya Tanganyika au ni sawa na kubadilisha mkono, leo kushoto kesho kulia....!?