X-PASTER
JF-Expert Member
- Feb 12, 2007
- 11,610
- 1,810
1
Ujana kitu kitamu, tena ni azizi sana
Maungoni mwangu humu, nilikuwa nao jana
Kwa wingi katika damu, tahamaki leo sina!
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
2
Kichwa kimejaa mvi, kinywani meno hamna
Nikenda kama mlevi, miguu nguvu haina
Kumbe ujana ni hivi, ukenda hauji tena!
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
3
Jua langu limekuchwa, na nyota nilizoona
Ukinitizama kichwa, nywele nyeusi hakina
Kama zilizofikichwa, zikang'olewa mashina
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
4
Natatizika kauli, midomo najitafuna
Nimekusanya adili, walakini hali sina
Dunia kitu bahili, hiki una kile huna!
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
5
Nilikuwa ni waridi, furaha ya wasichana
Neno hawakunirudi, wakati wa kukutana
Sasa nanuka baridi, wanionapo waguna
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
6
Walio wakinibusu, walikuwa wengi sana
Wanawake wenye busu, uzuri na usichana
Sasa sina hata nusu, ya wanitajao jina
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
7
Wazuri wenye uturi, na mikono yenye hina
Kila mtu mashuhuri, alipenda kuniona
Nilifaa kwa shauri, na sasa sauti sina
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
8
Dunia bibi arusi, kwa watu kila namna
Inapendeza nafsi, wakati wa kuiona
Na leo sina nafasi, kwa uzee kunibana
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
9
Kilichokuwa gizani, niliweza kukiona
Nikakijua thamani, sura yake hata jina
Sasa sijui ni nini, hata ikiwa mchana
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
10
Kilichotaka fikira, niliweza kukinena
Kwa mfano na kwa sura, mpaka kikafanana
Leo tazama hasara, nguvu hiyo sina tena
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
11
Kilichotaka mapimo, sikifahamu mapana
Marefu yake na kimo, siifahamu bayana
Nusu nimo nusu simo, duniani najiona
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
12
Hadumu nasikitika, rafiki yangu ujana
Machozi yamiminika, na la kutenda hapana
Ni wakati umefika, uzee dawa hauna
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
13
Hauna dawa uzee, mabega yamepetana
Anionaye ni"wee!, ondoka hapa laana"
Wanaposema na miye, niliyekuwa na jina!
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana.
14
Wakatabahu shairi, uchungu wanitafuna
Walakini nafikiri, twafuata Subuhana
Katika ile amri, ya"kuwa"na "kutengana"
Nasikitika hadumu, rafiki yangu ujana
By Shaaban Robert