Mzimu wa EPA waendelea kuitesa BOT

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,316
33,112
Monday, 05 December 2011 21:07

ndullu.jpg
Gavana wa BoT, Profesa Benno Ndulu​
Ramadhan Semtawa
BENKI Kuu Tanzania (BoT) imesema haitakurupuka kuamua kulipa au kutolipa madeni yaliyopo katika Akaunti ya malipo ya fedha za Kigeni (EPA) ili kuepuka uwezekano wa kutokea wizi mwingine kama uliotokea awali.

Tahadhari hiyo inachukuliwa baada ya kutokea wizi katika akaunti ya EPA ambao ulibainika katika hesabu za BoT za mwaka 2005/06, uliofanywa na Kampuni ya Ernst&Young baada ya kutokea mvutano kati ya mkaguzi wa awali Deloitte&Touche ya Afrika Kusini na Serikali ya Tanzania.

Akizungumza na gazeti hili jana Gavana wa BoT, Profesa Benno Ndulu, alisema benki hiyo haitakurupuka kuanza kulipa au kuamua kutolipa madeni licha ya muda wa mchakato wa ukaguzi maalumu unaofanywa na Kampuni ya Lazard ya Ufaransa kumalizika. Lengo la ukaguzi huo lilikuwa kubaini kama kuna uhalali wa kulipa deni hilo au kutolipa.

Lazard ilipewa miezi tisa kuanzia mwaka 2009 kufanya kazi ya ukaguzi na uchunguzi katika akaunti ya EPA na kuishauri BoT kama kuna madeni yanayostahili kulipwa au kutolipwa na athari zake kisheria kama yatalipwa au kutolipwa.

Akizungumzia sababu za kutoanza kuchukuza hatua licha ya muda wa uchunguzi kumalizika, Gavana Ndullu alisema; "Ni kweli muda wa awali wa ukaguzi ulimalizika. Lakini kazi haijamalizika kwani hata ripoti haijatoka. kutokana na unyeti wa jambo lenyewe tumeona tuangalie kwanza kwa makini ili waongezewe muda."

Profesa Ndulu, alisema kutokana na kuwepo baadhi ya vitu ambavyo vinahitaji kuendelea kufanyiwa kazi, Lazard itaongezewa muda kidogo ikamilishe mchakato huo kwa umakini mkubwa.

Alifafanua kwamba, Benki ya Dunia (WB) ambayo inasimamia maboresho hayo ya kimfumo, ndiyo ambayo itapaswa kuangalia namna ya kuongeza muda wa kazi wa Lazard, ili kuzuia uwezekano wa kutokea mambo kama ya mwaka 2005.

"Hili jambo linahusu mambo mbalimbali zikiwemo sheria za kimataifa, hivyo hatuwezi kufanya haraka bila kuweka mambo sawa. Kuna mambo ambayo Lazard na Benki ya Dunia watazungumza ili kuongeza muda wa kuyaangalia kwa kina," alifafanua gavana Ndulu.

Alisema Lazard ni kampuni ya kimataifa yenye ujuzi na uzoefu wa kazi za ukaguzi, hivyo hata ripoti yake ya mwisho inatarajiwa kutoa dira ya kisheria ya jinsi BoT itapaswa kufanya kuhusu deni hilo la EPA.

Alisema BoT itakurupuka kuzuia malipo kwa wadai halali na ikithibitika inaweza kupata matatizo ya kisheria na ikiamua kulipa itapaswa kuangalia na kufuata utaratibu wa ushauri wa kitaalamu kutoka Lazard ambao utaepusha matukio kama ya EPA.

Ukaguzi wa deni hilo la EPA ni miongoni mwa hatua ambazo Gavana Ndulu alizitangaza kuzichukua mara tu baada ya kuteuliwa kushika wadhifa huo mwaka 2007 baada ya Daud Balali kuwa nje kwa matibabu.

Hatua nyingine ilikuwa yeye kama gavana wa BoT kujiondoa katika nafasi ya mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi ya BoT ili kuondoa mgongano wa kimaslahi.

Kwa mujibu wa takwimu za Serikali, deni la EPA hadi mwaka 1999 lilifikia dola 623 milioni za Marekani, ambazo kati ya hizo, 325 milioni zilikuwa ni deni la msingi na 298 riba na kuongezeka hadi kufikia 677 milioni.

Hata hivyo, kulikuwa na Mpango wa Kununua Madeni (Debt Buy Back Scheme) wa mwaka 1994 kati ya Serikali na WB, ambao waliokuwa wakidai BoT waliombwa wakubali kulipwa sehemu tu ya fedha wanazodai.

Katika mpango huo, wapo waliokubali na wengine kukataa. Taarifa zinaonyesha kuwa hadi mwaka 2004, dola za Marekani 228 milioni, zililipwa chini ya mpango huo.

Utaratibu huo ndiyo ulileta matatizo ambayo yalibainika katika Ukaguzi wa Hesabu za BoT za mwaka 2005/06 uliyofanyika Agosti mwaka 2005 na kuonyesha matatizo katika ulipaji wa madeni kwa utaratibu huo wa idhini ya kulipwa wakala wa mdai katika akaunti ya EPA.

Baada ya hapo, kulitokea hali ya kutoelewana kati ya BoT na Mkaguzi Kampuni ya Deloitte & Touche , aliyegundua tatizo katika fedha sh 40bilioni zilizolipwa kwa kampuni ya Kagoda Agriculture, lakini Serikali iliingilia kati na Desemba 4, 2006 ilimwagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kuhakikisha ukaguzi huo unafanyika kwa uhakika.

Ukaguzi huo, uliofanywa na Ernst&Young ulibaini ufisadi wa zaidi ya Sh133bilioni ambazo zililipwa kwa makampuni 22 kiholela.

Kufuatia ufisadi huo, Januari 9, mwaka 2008 Rais Jakaya Kikwete, aliunda Kikosi Kazi (Task Force) chini ya aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Johnson Mwanyika, kuchunguza, kukamata na kufungua mashitaka dhidi ya waliohusika na ufisadi huo na tayari baadhi wako gerezani.

EPA ni akaunti ya madeni ya nje ambayo ilitumika wakati wa Mfumo wa Ujamaa. Awali ilikuwa katika iliyokuwa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), chini ya usimamizi wa BoT ikahamishiwa BoT mwaka 1985.
chanzo. Gazeti la Mwananchi
 
Back
Top Bottom