Elections 2010 Mwongozo wa uchaguzi mkuu - mwaka 2010 kwa vijana Wa tanzania

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,299
33,082
Mwongozo huu unalenga kuwaandaa vijana kuwa mstari wa mbele katika kufanikisha shughuli zote za uchaguzi mkuu ujao

Nia na madhumuni yakuwalenga vijana ni haya yafuatayo;


Ø Vijana ndio wapiga kura waliowengi kuliko rika lolote lile

Ø Vijana ndio taifa la leo na la kesho kwa hiyo maamuzi ya leo ni muhimu kwao kwa maisha yao ya sasa, baadaye nay ale ya vizazi vijavyo.

Ø Wana akili mpya zenye kufanya maamuzi sahihi endapo wataongozwa vyema

Ø Wana dira nzuri kwa ajili ya mema ya taifa lao


Ø Vijana ni wakala wakuu wa mabadiliko katika kila jamii

Ø Wanaweza kuepuka kutumiwa na watu wenye nia mbaya ya kuchochea vurugu.

Ø Ubunifu, nguvu na uwezo vimo ndani ya vijana na nijukumu lao kuvitumia ili waweze kuishi vyema kwa kuchagua na kuchaguliwa

Ø Vijana wanapaswa kuwa mstari wa mbele kupiga kura kama Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inavyosema katika ibara ya 5(1) Kila raia wa Tanzania aliyetimiza umri wa miaka kumi na minane anayo haki ya kupiga kura katika uchaguzi unaofanywa Tanzania na wananchi.

Ø Vijana wanakumbushwa kuwa uhuru wa kuchagua utanguliwa na utashi amabapo utashi huo utanguliwa na ukweli juu ya jambo hilo.



(…..wale wenye wajibu wa kufanya kazi na vijana wa umri mdogo wana nguvu kubwa zisizozidiwa na nguvu za yeyote yule kwa kutilia maanani hali ya baaadaye katika jamii yetu... (Mwl. JK Nyerere, The Power of Teachers, 27 Agosti 1966)
 
Katika Uchaguzi Mkuu ujao, Vijana wanashauriwa kufanya mambo yafuatayo:



  1. Kujitokeza kujiandikisha kwa wingi ili kuweza kupiga kura

Bila kujiandinkisha kupiga kura itakuwa ni vigumu kwa kijana yeyote kupiga kura na hivyo kutimiza haki yake ya msingi na kikatiba ya kuchangua kiongozi amtakaye. Hivyo Vijana wanahimizwa kujiandikisha kwa wingi ilikuhakikisha kuwa lengo letu la kuwaweka madarakani viongozi walio bora na siyo bora viongozi linatimia.


  1. Kujitokeza kupiga kura na kugombea nafasi za uongozi

Kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi mbali mbali za uongozi ili kujiletea na kusimamia mabadiliko chanya ya kijamii, kisiasa na kiuchumi. Ushahidi unaonyesha ni kwa kiasi gani vijana wanaweza kuitumikia jamii kwa akili, wema na unyenyekevu wa kutosha ili kuiendeleza jamii. Baba wa Taifa Mwalimu Julius K Nyerere alianza vugu vugu la mabadiliko na kufanikiwa kuikomboa nchi na kuiongoza akiwa kijana mwenye umri mdogo. Wapigania uhuru na haki wengi ni vijana. Hata waleta mabadiliko katika ulimwengu huu ni vijana wenyewe.
Hivyo basi, vijana wanashauriwa kujitokeza na kuwashawishi wenzao kugombea nafasi za uongozi waonapo inafaa ili kujenga uwakilishi imara katika vyombo vya kutoa maamuzi.

Vijana wanashauriwa kujitokeza na kuhudhuria mikutano ya kampeni ya wagombea mbali mbali ili kuzisikiliza sera zao na ahadi zao ili waweze kujua nani bora badala ya kuongozwa na ushabiki wa vyama vya kisiasa pekee usioleta tija.


  1. Kuepuka Ubaguzi wa Rangi, Udini na Ukabila

Vijana wanashauriwa kujiunga pamoja ili kuchagua viongozi wa kuwafaa.
Katika uchaguzi huu, vijana wajitenge na ubaguzi wa aina yeyote ile ukiwemo ule wa Rangi, ukabila, ukanda na udini. Vijana wajue kuwa Tanzania yetu ni moja, tu wamoja na ni katika umoja ndipo tunapoweza kujenga jamii endelevu na sio katika kubaguana kwa misingi yoyote ile. Kwa kufanya hivyo tutaweza kuwa na malengo mazuri ya sasa na ya baadaye. Kumbuka wahenga walisema: 'umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu'.

Vijana wanapaswa kushirikiana na kuepukana na udini. Tumeona baadhi ya dini zetu zikitoa barua na nyaraka zinazolenga kuwafanya watanzania waone jinsi dini zao zinavyowapenda na kuwajali na hivyo kuchagua viongozi wanaoendana na sifa zipendekezwazo na dini hizo. Viongozi wa dini zetu pia wanajua nani ni chaguo la Mungu kufuatana na dini waziongozao.

Hata kama wengi wa vijana ni wafuasi wa dini hizi, ni wajibu wao kuhakikisha
 
hawagawanyiki wala kujitenga kuchagua viongozi kwa sababu tu ni wafuasi wa dini fulani. Vijana wanashauriwa kuwa makini na baadhi ya maamuzi ya dini hizi na hasa likija suala la Uongozi. Historia inaonyesha kuwa Migogoro mingi na mikubwa duniani machafuko na umwagaji damu kwa kiasi kukubwa husababishwa au huchochewa na dini hizi zinazojigamba kuleta amani.

Mfano mapigano kati ya Israel na Palestina, ni ya kidini zaidi. Hata baadhi ya viongozi madikteta wa ulimwengu huu kwa kiasi kikubwa walitumia misahafu kuingia madarakani au walipigiwa kampeni na viongozi wa dini hizo. Mfano ni Adolf Hitler, Saddam Husein na wengine.

Je kuna tofauti gani kati ya maisha wanayoishi viongozi wa dini hizi na viongozi wa kisiasa? Wote si wanaishi kwenye majumba ya anasa na kukendesha magari ya gharama na ulinzi mkubwa dhidi ya vijana watukutu wasio na ajira? Si wanasomesha watoto wao ughaibuni au shule maalumu na sio zile za kata?

Hata kama vijana ni wafusi wa dini hizi, bado wanashauriwa kuepuka dini katika kuchagua uongozi wa taifa lao na badala yake watangulize maslahi na umoja wa kitaifa zaidi.


  1. Aina ya Viongozi wa kupigiwa kura
Ni jukumu la vijana kuwa makini na wagombea waliostaafu kazi. Uongozi uwe wa kuleta maendeleo na mabadiliko ya kweli. Nafazi za uongozi zisigeuzwe kuwa pahala pa kutunzia wastaafu. Tumeona wastaafu walioitumikia serikali katika nyanja mbali mbali kama vile mashirika ya umma na majeshi ya ulinzi wakigombea nafasi za uongozi, badala ya kututumikia vyema zaidi wamekuwa wazembe wa kukubali kila jambo ili mradi tu siku ziende.

Hata hivyo wapo wastaafu waliofanya makuu katika umri wao huo mkubwa na ndio maana vijana wanashauriwa kuwa makini juu ya ni mstaafu yupi anagombea. Hata hivyo ni vigumu sana kwa kiongozi mwenye umri mkubwa kuweka mipango makini ya maisha ya baadaye na hasa ikizingatiwa kuwa uwezekano wake wa kuwa ameondoka duniani ni mkubwa mno kuliko ule wa kuwepo.

Pamoja na kunusuru ngazi za maamuzi zisiwe vituo vya kulelea wastaafu, vijana tunapaswa kuwasikiliza wazee ili tuchukue busara kidogo walizonazo na kuweza kuendeleza ushindani wenye tija katika ulimwengu huu unaoenda kwa kasi na mikiki mikiki ya kila aina. Mikataba mingi ya hovyo imeingiwa kutokana na wazee wetu kuzidiwa ujanja. Ni viongozi vijana watakaoweza kupambana na kasi ya ulimwengu wa sasa.

Pia wazee kufia madarakani ni hatari kwani huacha vijana tukitapatapa bila kujua tushike lipi tuache lipi na hivyo ni vyema kurithi / kushika madaraka wazee wetu wakiwa bado hai na nguvu za kutushauri.

Vijana wanaoitwa 'Watoto wa Wakubwa´ waangaliwe kwa umakini mkubwa. Wengi wao hawana uwezo wa kuongoza na tusiwachague eti kwa sababu
 
wanapesa au majina makubwa. Wamesoma elimu za nje na ni vigumu kwao kujua maisha halisi ya vijana Watanzania. Hata hivyo ni vyema kufikiri vizuri kabla ya kuwapatia nafasi za kuongoza. Baadhi wamesoma elimu za nje na hivyo hawaijui vyema nchi yetu wanayotaka kuiongoza.



  1. Uchumi na Utamaduni
Vijana wanashauriwa kuchagua viongozi wa kwetu, yaani Watanzania halisi, wanaoutukuza na kuuishi Utanzania wetu. Viongozi wanaoweza kuwasiliana kwa lugha yetu adhimu ya Kiswahili na wanaotumia bidhaa zetu katika kujenga uchumi wa taifa hili. Viongozi walio tayari kuvaa mavazi ya kitamaduni ili kukuza utamaduni wetu na kupatia soko bidhaa zizalishwazo na wajasiriamali wetu badala ya wanaoutukuza bidhaa na utamaduni wa kigeni.

Viongozi watakaothamini na kusaidia shughuli za vijana ili ziendelee badala ya kuwatungia sera mbovu za kuwapiga na kuwatawanya eti wanachafua miji au ni wazururaji wakati wanahangahika kujitafutia riziki na kujenga uchumi wa taifa kwa kutumia walicho nacho (nguvu zao). Tunahitaji viongozi wa kujenga sera rafiki zinazoendana na vijana ili wachape kazi kwa bidii.

Ni vyema tukichagua viongozi wanaoishi katika mazingira yetu ya Tanzania na hata majimboni kwetu. Viongozi wanaoishi maisha ya kawaida ya Watanzania watasaidia sana katika kutunga sera zinazoendana na maisha yetu halisi badala ya wale wasiojua maisha halisi ya Mtanzania wanayemuongoza. Viongozi wanaosomesha watoto wao katika shule zetu za kata wataweza kuchochea maendeleo na wanaopata huduma za afya katika vituo vyetu vya afya (na siyo kutibiwa nje ya nchi) ili waweze kushiriki vyema katika kuboresha afya za Watanzania.

Kwa upande wa wabunge au wawakilishi, tuchague wabunge ambao ni wakazi halisi wa majimbo yetu na sio wakazi wa miji mikubwa eti kwa kuwa tu wana asili ya majimboni kwetu. Ni bora kumchagua mbunge au diwani asiye na asili ya majimbo yetu lakini anayeishi katika jimbo letu kuliko kuwachagua wenye asili ya majimbo yetu wanaoishi mijini. Hawa watakuwa ni watalii wasiojua wanayemuongoza na hivyo hawawezi kuchochea sera makini za maendeleo ya majimbo yetu kwani hawayajui na hawajui lipi ni jema kwetu kwa kuwa wao sio sehemu yetu ya jamii.

Hata hivyo vijana wanashauriwa kujihadhari sana na wanasiasa wanaotoa hongo na takrima ili wachaguliwe. Viongozi wa aina hii hawana uzalendo wa kweli na watatupeleka pabaya kwani zawadi zao zitageuka kuwa mwiba kwetu na hivyo tuwaepuke kwa nguvu zote kama tunataka mabadiliko ya kweli. Wanasiasa wanaowekeza katika kampeni watageuka na kuchukua baada ya kushika nafasi za uongozi.



(Ukichukua hongo ama taktrima ili umchague huyo akupaye unauza haki yako ya msingi. Kabla ya kuchukua uamuzi, fanya mahesabu ya thamani ya hongo aliokupa uilinganishe na thamani yako na thamani ya maisha yako kwa muda wa miaka mitano ijayo)
 
Tuchague viongozi makini, sio wanaotuomba kura na baada ya kuingia madarakani wanaongea na wazee na sio vijana tena, wakitaka kuongelea masuala ya wafanyakazi wanaongea na wazee wasioweza kuzalisha badala ya vijana ambo ndio nguvu kazi ya taifa. Tujihadhari dhidi ya kuwa na serikali masikini inayoongozwa na wanasiasa matajiri katika nchi (Tanzania) iliyojaa rasilimali kibao yenye wananchi wanaoishi katika lindi la umasikini

Je! Ni lini mfanyabiashara akawatetea watu ambao anawanyonya? Ni lini mkazi wa mjini akawatetea wakazi wa vijijini? Aau ni lini tajiri akamtetea masikini?



  1. Jinsia
Ni jukumu la vijana kuwaepusha akina mama na watoto dhidi ya athari za machafuko yatokanayo na ushawishi wa watu wenye nia mbaya. Vijana wawe mstari wa nyuma kujiingiza katika vurugu hizo kwani wanawake na watoto ndio waathirika wakuu hata kama hawana hatia. Pia kwa kuchagua viongozi makini kutawaepusha mama zetu dhidi ya sera mbovu na kandamizi zinazoleta umaskini na kukuza pengo kati ya matajiri na maskini.

Vijana wa kike wanashauriwa kuwa mstari wa mbele katika kugombea nafasi mbali mbali. Katiba ya Jamhuri ya Muugano wa Tanzania Kifungu 78 ibara ya (1)inasisitiza juu ya umuhimu wa vyama vya siasa vinavyoshiriki katika uchaguzi mkuu kuwa na nafasi maalumu kwa ajili ya wanawake. Vijana wa kike wanashauriwa kutokubweteka kwa kusubiria nafasi maalum ili kuongeza idadi ya wanawake bungeni na kuleta ushindani makini.


  1. Mazingira.

Uchafuzi wa mazingira ni hatari kwa maisha yetu, wadudu, wanyama na viumbe hai wengine. Tunashuhudia vyanzo vya maji vikikauka na vingine kuharibiwa kwa viwanda na migodi kutupa taka hatari kwa afya ya watu, wanyama na ekolojia; barafu ya mlima Kilimanjaro ikizidi kuyeyuka na kina cha maji Ziwa Victoria kikizidi kushuka. Pamoja na sababu za kimataifa, mazingira yetu yanazidi kuharibiwa kutokana na sera na sheria mbovu na baadhi ya wanasiasa wenye ubinafsi na wasiokuwa na dira kutotekeleza wajibu wao kwa mujibu wa sheria zilizopo.

Vijana wanashauriwa kuwa makini na kuchagua viongozi wanaharakati watakaohakikisha wanalinda mazingira na raslimali zetu kwa ajili yetu na kwa ajiri ya vizazi vijavyo na wale watakaohakikisha mgawanyo chanya wa mazao ya rasilimali lukuki tulizo nazo hapa Tanzania. Tuwaepushe akina mama dhidi ya athari za uchafuzi wa mazingira huku tukijiandaa kuwarithisha wadogo zetu na watoto wetu nchi nzuri ya baadaye. Hili litawezekana pekee kwa kuchagua uongozi makini kwa ajili yetu.


  1. Ulinzi na usalama.

Vijana walioko katika vyombo vya ulinzi na usalama, wanashauriwa kuwa makini na kutetea maslahi ya umma. Badala ya kuwanyanyasa watu wengi kwa
 
  1. Ulinzi na usalama.

Vijana walioko katika vyombo vya ulinzi na usalama, wanashauriwa kuwa makini na kutetea maslahi ya umma. Badala ya kuwanyanyasa watu wengi kwa ajili ya kulinda wanasiasa wachache kama ilivyotokea katika uchaguzi mkuu nchini Kenya mwaka 2007, vijana hawa wanashauriwa kulinda na kujali maslahi ya umma kwani wao ni sehemu ya umma huo na sera mbovu huwakandamiza wao pia na ni vyema hata mbele ya Muumba kuwatumikia wengi kuliko wachache na hata waswahili husema ‘wengi wape’.

Sera za ulinzi juu ya vijana walioko vifungoni iwe ni kuwaelimisha na kuwasaidia ili waje kuwa raia wema badala ya kuwapa adhabu kali za kuwanyanyasa na kuwaotesha usugu ili wakirudi uraiani wawe wema badala ya kuendeleza uhalifu uliokubuhu. Haya yatafanywa na uongozi makini uliochaguliwa na vijana makini kwa faida yao na jamii nzima

Ulevi wa kupindukia, ongezeko la matumizi ya bangi na madawa ya kulevya miongoni mwa vijana ni matokeo ya kukata tama mioyoni mwmao na sera mbovu za kutokushirikishwa katika uundaji na utekelezaji wa sera za nchi


  1. Hitimisho.

Vijana wakijitokeza kujiandikisha kwa wingi na kugombea nafasi mbali mbali za ngazi za chini na za juu, na pia wakijitokeza kufuatilia mikutano ya kampeni na kupiga kura na kushawishi watu makini wagombee uongozi. Huu utakuwa ni mwanzo mzuri wa kuwa na Tanzania endelevu na iliyo salama zaidi. Tutakuwa na uongozi unaoheshimu na kufuata matakwa ya vijana ambao ndio wengi na wenye nia ya mabadiliko ya kweli.

Kumbuka sera zetu zikiwaangalia kwa makini na kuwajali vijana wa kike na wa kiume tutajenga Tanzania imara iliyoendelea kijamii, kiikolojia, kiuchumi na kisiasa. Tutakuwa na kizazi chenye afya njema, kisichojihusisha matendo ya hovyo ya uvutaji bangi, ulevi, uzinzi na utumiaji wa madawa ya kulevya. Tutakuwa na taifa lenye kiu ya maendeleo na watu walio tayari kufanya kazi ili kujiletea maendeleo badala ya kutegemea kuletewa maendeleo.

Vijana wanashauriwa kujitafutia taarifa mbali mbali juu ya utendaji wa serikali ili waende na wakati na kuweza kujua serikali inafanya nini na jinsi ya kushirikiana nayo badala ya kuilaumu tu bila mabadiliko. Haya yatawezekana kwa kuwa tutakuwa tayari tumechagua serikali yetu inayotusikiliza sisi kwanza badala ya wengineo (wawekezaji na matajiri). Serikali itakayokuwa inaongozwa na watu wasiokuwa wabinafsi na wanaojua kuwa wapo madarakani kutumikia na sio kutumikiwa.

Tutakuwa na viongozi makini watakaoweza kupanga mipango madhubuti ya baadaye kwani wanauhakika wa kuwepo badala ya viongozi wenye hofu juu ya kifo au kuishiwa nguvu. Hapa nchini nguvu za vijana zinajidhirisha katika makampuni makubwa na yenye ushindani. Makampuni mengi yanayoonekana kufanya vizuri yanaongozwa na vijana, kwa nini sio serikali?

Kumbuka vijana wakijitoa na kupewa kipaumbele, ni sawa na kuisaidia jamii nzima kwani vijana ndio daraja liunganishalo kati ya watoto, wasiojiweza na wazee. Bila vijana makini jamii imara haiwezi kuwepo. Vijana wakiwa maskini basi jamii nzima itakuwa maskini. Kumbuka vijana ndio wazalishaji wakuu. Zaidi ya asilimia 60 ya nguvu kazi hutoka kwa vijana. Ni vigumu kwa nguvu kazi nyingine kuwa na tija bila kuwepo kwa vijana

Nchi yetu ina kila kitu inachohitaji ili kuendelea. Badala ya vijana kujiona kama wako katika mazingira hatari, tuchague viongozi bora kisha tufanye kazi kwa bidii, tuwe na uzalendo ili kujenga jamii imara na kuwa mfano kwa mataifa mengine. Mashujaa wa kizazi chetu wamo miongoni mwa vijana wa leo watakao kuwa makini kushika, kusikiliza, kujitokeza na kutumia sanduku la kura ili kuchagua viongozi makini.


Vijana tunaweza. Amani upendo na heshima kwa wote, wema na Umoja wa kitaifa na ufanyaji kazi kwa bidii ndio kauli mbiu yetu. Siasa za maneno matupu, utengano na ubaguzi zisiwe na nafasi katika uchaguzi ujao na katika maisha yetu yote. Kama mti mwema uzaavyo matunda mema, ndivyo vijana wema wawezavyo kuzaa uchaguzi mwema na uongozi mwema.

Katika hili hata Mungu yuko upande wetu. Asanteni.
 
Back
Top Bottom