Mwanafunzi bora adai siri ya mafanikio yake ni kumwomba Mungu

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,956
22,138
Mwanafunzi bora adai siri ya mafanikio yake ni kumwomba MunguNa Joyce Mmasi

MWANAFUNZI aliyeongoza kwa kufanya vizuri katika mitihani ya kidato cha sita mwaka huu na kuwazidi wenzake 51,563, Aude Kileo amesema siri kubwa ya mafanikio yake ni kumwomba Mungu, ushirikiano na wanafunzi wenzake na bidii katika masomo.

Akizungumza katika mahoajiano maalum na Mwananchi Jumapili jana Kileo (pichani) alisema kuibuka kuwa mwanafunzi bora kumemfanya atimize ndoto yake ya siku nyingi.

"Siku zote nilikuwa nikiomba ili niwe mwanafunzi bora nchini, namshukuru Mungu kwani amesikia na ameyajibu maombi yangu, nimekuwa bora kweli," alisema Kileo huku akitabasamu.

Kileo ambaye ameshinda kwa kupata daraja la kwanza la pointi tatu katika mchepuo wa sayansi akiwa na alama A kwa masomo ya Fizikia, Kemia na Hisabati (PCM) alikuwa akisoma katika shule ya Sekondari ya Kibaha iliyopo mkoani Pwani.

"Katika maisha kila mtu anafurahia matokeo mazuri, na mimi nimefurahi sana," anasema.

Kileo ambaye ni mtoto wa Mchungaji Michael Kileo wa Kanisa la Kilutheri Tanzania (KKKT), Usharika wa Kashashi Wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro, anasema maombi ya wazazi wake na ushirikiano na wanafunzi wenzake ndio uliomuwezesha kufikia mafanikio hayo makubwa.

Anasema kuwa siri nyingine ya mafanikio yake ni kumuomba Mungu, kusoma kwa bidii, kuwa na adabu na utii sambamba na kushirikiana na wanafunzi wenzake.

"Unapokuwa na adabu na utii, unakuwa na nafasi kubwa sana ya kuepuka adhabu kutoka kwa walimu na kwa kawaida kitu kikubwa kinachopoteza muda wa kusoma kwa wanafunzi ni kutumikia adhabu anazopewa baada ya kufanya mambo kinyume na maelekezo ya walimu na walezi," alisema.

Kileo alisema pamoja na mafanikio hayo makubwa aliyoyapata, yeye na wanafunzi wenzake walikuwa wakikumbana na vikwazo vingi shuleni, ikiwamo ratiba ya shule kutoeleweka.

"Matatizo ya mashindano ya Umitashumta yaliyokuwa yakifanyika shuleni kwetu yalikuwa yakituharibia kwa kiasi kikubwa ratiba zetu za masomo," alisema.

Hata hivyo, alisema pamoja na msaada mkubwa wa walimu, ushirikiano wa wanafunzi wenyewe kwa wenyewe nao umechangia mafanikio yake na wanafunzi wenzake.

"Wanafunzi wenyewe tumekuwa pamoja, tukishirikiana kusoma na hata kutafuta material (vitu vya kusoma)," alisema.

Kijana huyo alisema ndoto yake ni kuwa mhandisi wa mawasiliano (telecommunication enginier) ambapo anasema malengo yake ni kumiliki kampuni yake binafsi ya mawasiliano.

Wanafunzi 10 bora kwa jumla kitaifa wanatoka shule za sekondari za Kibaha, Tabora Boys, Ilboru na Mzumbe.

Wanafunzi wengine katika kundi hilo ni Raymond Aidan (Kibaha Sekondari), Frank Shega (Tabora Boys), Charles Simkonda (Ilboru Sekondari), Maclean Mwaijonga (Feza Boy's), Sophia Nahoza (Marian Girls), Atupele Kilindu (Mzumbe Sekondari), Athuman Juma (Ilboru Sekondari), Dickson Mutegeki (Tabora Boys) na Michael Andrew (Ilboru Sekondari). Akitangaza matokeo hayo jijini Dar es Salaam juzi, Katibu Mtendaji wa Necta Dk Joyce Ndalichako alisema wanafunzi kutoka shule za serikali wameongoza katika watahiniwa 10 bora kwa jumla kitaifa akiwemo msichana mmoja tu katika kundi hilo na wote walioshika nafasi hizo walikuwa wakisoma masomo ya mchepuo wa sayansi (PCM).
 
Kaza buti Kileo, Kazi bado kamata u profesa Kabisa. Usilewe sifa ukaona umefika. Best student wengi wakifika vyuoni huwa wanachemsha sana kwa kujiona kwamba wanajua kila kitu.
 
Back
Top Bottom