nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
- Friday, July 8, 2011, 11:05
- Habari kuu, Mtanzania
*Lissu asema haukuridhiwa na Wazanzibari wote
*Adai Mwalimu Nyerere alimzidi ujanja Karume
*Mnyaa ahoji Karume kutochanganya udongo
Na Maregesi Paul, Dodoma
HOJA ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uliozaa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, juzi iliibuka bungeni baada ya baadhi ya wabunge kuhoji uhalali na muundo wake.
Hali hiyo ilijitokeza juzi jioni wakati wabunge walipokuwa wakichangia Makadirio ya Bajeti ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais kwa mwaka wa fedha wa 2011/2012 iliyowasilishwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan.
Aliyekuwa wa kwanza kuchokonoa Muungano ni Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), ambaye alisema kuna haja kwa Watanzania waliokuwapo wakati wa kuanzishwa Muuungano kuuleza umma ni kwa nini Tanganyika na Zanzibar ziliungana.
"Kuna siri kubwa sana kuhusu Muungano wetu, kuna haja sasa walioushuhudia kuueleza umma wa Watanzania ni kwa nini ulianzishwa kwa sababu Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA) tayari limeshaanza kuweka wazi baadhi ya mambo huku likieleza jinsi Balozi wa Marekani alivyoshiriki.
"Kama taarifa hizo zitatolewa, zitawasaidia Watanzania kujua ni muundo gani wa Muungano wanaotakiwa kuwa nao tofauti na ilivyo sasa ambapo watu hawajui ni muundo upi wa muungano unaowafaa," alisema Mnyika.
Mwingine aliyezungumzia hoja hiyo ni Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (CHADEMA) ambaye alisema kuna kila sababu muundo wa muungano huo kuangaliwa upya kwa kuwa kuna kasoro nyingi zinazoonekana kuwakwaza baadhi ya Watanzania.
"Hili suala la Muungano linahusu uhai wetu kama nchi na kama taifa na suala la mazingira ambalo nalo waziri alipowasilisha bajeti yake aliligusia, linahusu uhai wetu kama binadamu.
"Kwa leo sitagusia mazingira kwa sababu naandaa mchango wangu kwa maandishi na nimeanza kuuandaa tangu juzi, ila nitazungumzia muungano na ninataka kujua ni kitu gani kilichotufanya tuungane ingawa hakijaelezwa kwa miaka 47 sasa.
"Muungano ulizaliwa katika mazingira ya siri, ulianzishwa kwa kuwaficha baadhi ya viongozi waliokuwapo enzi hizo, kwa nini hali ilikuwa hivyo.
"Asili ya muungano ni vita baridi iliyokuwapo wakati huo na lengo la huu muungano lilikuwa ni kuwadhibiti watu waliokuwa maarufu kisiasa wakiwamo akina marehemu Mohamed Babu na Kassim Hanga, hii ndiyo hali halisi ya huu muungano tulionao sasa.
"Nawaambia, April 1964 ile hati ya muungano iliyosainiwa kati ya Hayati Nyerere na Karume ilisainiwa kimya kimya bila Aboud Jumbe kulishirikisha Baraza la Mapinduzi Zanzibar, Zanzibar hawakuridhia muungano kwa mujibu wa nyaraka zilizopo na ndiyo maana kila mara wanalalamika.
"Juni 10 mwaka 1965 masuala ya fedha yaliingizwa katika muungano kwa ujanja ujanja kwa kutumia hati ya dharura na mengine yakaja kuingizwa bila Wazanzibari kushirikishwa, mambo hayo ndiyo sasa yanawafanya watu waanze kuhoji muundo wa huu muuungano," alisema Lissu.
Katika mazungumzo yake, mwanasiasa huyo alisema pamoja na kwamba baadhi ya Watanzania wanataka muungano uendelee kuwapo, umefika wakati sasa kila mmoja kujiuliza maswali mawili ya msingi kuhusu muungano huo.
Aliyataja maswali hayo kuwa ni je, Tanzania Bara na Visiwani wanautaka muungano na je ni muungano upi unaotakiwa na wananchi wa pande hizo mbili.
Kwa mujibu wa Lissu, baada ya maswali hayo kujibiwa Watanzania wanatakiwa kukaa na kujadili upya muundo wa muungano huo ili kuondoa malalamiko yaliyopo.
"Hayo ndiyo maswali ya msingi kujiuliza, muungano wetu unahitaji ridhaa ya pande zote mbili, kuna watu wakikuona unahoji muungano wanakuona kama unataka kumtukana Nyerere, jamani haya siyo mambo ya Mungu.
"Haya ni mambo ya Kaisari, lazima tuyahoji, lazima tujue kilichopo nyuma ya pazia, lazima tujue huu muungano ulianzishwa kwa sababu zipi kwani wakati unaanzishwa Karume hakuwashirikisha wanasheria, alizidiwa ujanja na Nyerere, jamani hata ndoa huvunjika, tumechoshwa na propaganda," alisema.
Naye Mbunge wa Mkanyageni, Mohamed Habib Mnyaa (CUF), aliungana na wabunge hao wawili na kusema kuwa hajui ni kwa nini wakati wa kuchanganya udongo wa Tanganyika na Zanzibar, Hayati Karume hakushirikishwa.
"Kuna swali moja huwa ananiuliza mtoto wangu mdogo, kwamba Baba kila siku ya muungano tunaonyeshwa picha ya Nyerere akichanganya udongo peke yake, mbona Karume huwa hatumuoni akichanganya udongo?.
"Mwanangu huyo huwa ananiuliza, hivi huu ni muungano gani huu, hili swali huwa nashindwa kumjibu na kama mnabisha, angalieni hiyo siku ya muungano mtamuona Nyerere akichanganya udongo peke yake bila Karume.
"Kutokana na hali hii, lazima muundo wa muungano uangaliwe upya kwa sababu kitendo cha Zanzibar kutokuwa na mamlaka ya kukopa fedha nje bila ridhaa ya SMT( Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ) siyo sahihi kabisa na pia hili neno kero za muungano siyo sahihi bali usahihi ni matatizo ya muungano," alisema Mnyaa.
Katika hatua nyingine, alisema kuna haja kwa Serikali kukubaliana na mapendekezo yaliyowahi kutolewa na baadhi ya tume zilizoundwa kwa ajili yakuangalia muungano huo zikiwamo Tume ya Nyalali na Tume ya Kisanga ambazo kwa nyakati tofauti zilipendekeza uwepo wa Serikali tatu.