Mume wa mtu uibe, haitoshi umtoe roho mwenzio……….!

Mtambuzi

Platinum Member
Oct 29, 2008
8,810
15,398

parameter.jpg
Sherri Dally

livsfarlig_kj_rligh_864167a.jpg
Michael Dally na Sherry siku ya ndoa yao

livsfarlig_kj_rligh_864166a.jpg
Michael Dally na Diana Haun

livsfarlig_kj_rligh_864176a.jpg
Diana, Michael na Sherry


Tokea mwanzo tangu taarifa za kupotea kwa Sherri Dally aliyekuwa na umri wa miaka 35 zilipofikishwa katika kituo cha Polisi zilianza kutiliwa mashaka. Taarifa hizo ziliripotiwa na mumewe aitwaye Michael Dally siku hiyo ya Mei 6, 1996 majira ya jioni baada ya kutoka kazini kwake kwenye duka la Vons Supermarket lililoko katika mji wa Oxnard katika jimbo la California ambako alikuwa akifanya kazi kama msimamizi mkuu wa makarani.

Michael Dally ndiyo alikuwa amerudi nyumbani kwake katika mji wa Ventura na kukuta nyumbani kwake hakuna dalili za kuwepo mkewe au hata watoto wake wawili, waliokuwa na umri wa miaka 6 na 8 ambao Sherri hakuwa amewafuata shuleni kitu ambacho si cha kawaida. Baadae watoto hao walikuja kupatikana wakiwa wamehifadhiwa na jirani wakiwa salama. Kwa upande wa Polisi, walidhani kuwa Sherri atakuwa amekwenda kuwatembelea marafiki zake bila kutoa taarifa kwa mtu yeyote au labda atakuwa ameamua kuwa peke yake kwa muda fulani, au ameamua kutoweka kwenda mahali kusikojulikana kwa sababu anazozijua yeye mwenyewe. "matukio kama haya huwa yanatokea mara nyingi." Alisema msemaji wa Polisi wakati akiongea na waandishi wa habari kuhusiana na kutoweka kwa Sheri Dally.

Kwa jinsi siku zilivyokuwa zikiyoyoma bila ya fununu za kuonekana kwa Sherri Dally au dalili za kujulikana mahali alipo, askari wa upelelezi waliokuwa na jukumu la kupeleleza kesi hiyo walianza kuwa na wasiwasi kama Sherri anaweza kupatikana akiwa hai, kwani tangu kutoweka kwa mama huyu wa watoto wawili ambaye alikuwa akifanya kazi katika kituo cha kulelea watoto, kulikuwa hakuna taarifa zozote zilizopatikana ambazo zingewawezesha Polisi kujua mahali alipo.

Marafiki na majirani zake walimuelezea Sherri kama mama aliyekuwa akiwajali sana watoto wake hivyo ilikuwa si rahisi yeye kuondoka na kuwatelekeza watoto wake bila ya kuwaaga. Hata hivyo Polisi walianza kupata fununu kuwa maisha ya ndoa kati ya Michael Dally na mkewe hayakuwa shwari, kwani walikuwa wakigombana mara kwa mara.Polisi wa Upelelezi walianza kufuatilia mizunguko ya Sherri siku ile aliyotoweka. Kwa haraka Polisi waligundua kuwa majira ya saa tatu na nusu asubuhi, Sherri alionekana akiendesha gari lake kuelekea kwenye eneo lenye maduka mengi kusini mwa mji wa Ventura. Shuhuda mmoja aliyekuwa kwenye eneo la kuegeshea magari aliwaambia Polisi kuwa aliona gari dogo la blue aina ya Nissan Altima ambalo lilikuwa likilifuata gari la Sherri kwa karibu na wakati Sherri anaegesha gari lake, gari hilo nalo liliegeshwa nyuma ya gari la Sherri kwa karibu.

Na mara aliteremka mwanamke mmoja ambaye alikuwa ni mrefu kiasi na mwembamba wa wastani, alikuwa amevaa wigi la rangi ya dhahabu na suti ya rangi ya kahawia. Mwanamke huyo alimfuata Sherri na kuongea naye mazungumzo mafupi kabla ya kuongozana naye hadi kwenye gari la mwanamke huyo na kumwelekeza akae kiti cha nyuma na kisha kuondoka naye. Na huo ukawa ndio mwisho wa Sherri Dally kuonekana akiwa hai.


Tukio zima halikuonyesha hali ya kugombana au kulazimishwa, na kwa jinsi walivyoonekana wakiongea, ilikuwa ni kama vile ni marafiki wawili wanaofahamiana. Pia baadhi ya mashuhuda wengine walikiri kwamba, walidhani mwanamke yule alikuwa ni mmoja wa walinzi katika eneo lile, kwani mavazi yake yalishabihiana kidogo na ya walinzi katika eneo lile.Siku 10 zilipita lakini kulikuwa hakuna dalili za Sherri Dally kunekana. Msemaji wa Polisi wa kituo kikuu cha Polisi katika mji wa Ventura, Luteni Don Arth akiongea na waandishi wa habari, alionesha wasiwasi wake juu ya kupotea kwa Sherri Dally katika mazingira hayo ya kutatanisha. "Ni zaidi ya wiki moja sasa tangu mama huyu atoweke, tuna wasiwasi sana sio tu kwa muda aliotoweka bali pia kwa lile tukio lililotokea katika eneo lile la kuegeshea magari. Kulingana na mashuhuda ambao walikuwepo kwenye eneo la tukio walidai kwamba hapakuwa na hali ya uhasama au kuashiria shari wakati anaingia kwenye gari la mwanamke huyo, hakuonekana kuwa na hasira wala kulia." Alisema Luteni Don Arth, kisha akaendelea. "Kwa upande mwingine unaweza ukashangaa, kwa nini aondoke na mwanamke huyo, wakati muda huo alitakiwa akawachukue wanae shuleni, na hata muda wa kuingia kazini kwake ulikuwa unakaribia. Ni lazima ushangae ni kitu gani kinaendelea." Alisema.

Msemaji huyo aliendelea kubainisha kwamba, mpaka kufikia wakati ule Polisi walikuwa hawana ushahidi madhubuti wa kuthibitisha kwamba kulikuwa na mchezo mchafu,a lakini pia walishangaa kugundua kwamba Sherri aliacha funguo za gari, pochi yake, pamoja na leseni yake ya kuendeshea gari ndani ya gari lake. "Bado tunaifanyia kazi kesi hii yenye kushangaza. Tunafanya kazi kwa juhudi kubwa na sisi kama Polisi tuna dhima ya kuhakikisha tunafumbua kitendawili hiki. Tumeshatoa taarifa kwa wenzetu wa Patrol, lakini mpaka sasa hakuna taarifa ambazo zimeshapatikana zinazoweza kutusaidia."

Msemaji huyo aliendelea kusema kwamba, Michael Dally akishirikiana na ndugu wa Sherri Dally wamekutana kwa pamoja na kuandaa matangazo yenye picha za Sherri Dally na ahadi ya fedha kwa yeyote atakaye toa taarifa zatakazofanikisha kupatikana kwa mama huyo. Hata hivyo Luteni Arth hakuweka bayana habari zilizovuja kwamba Michael Dally alikuwa na mahusiano nje ya ndoa yake na mfanyakazi mwenzie aitwae Diana Haun aliyekuwa na umri wa miaka 35 na kwamba kupotea kwa Sherri Dally kulihusishwa na mwanamke huyo. Ukweli ni kwamba wapelelezi wa shauri hilo walikuwa kwenye hatua za mwisho za kuunganisha ushahidi ili kuthibitisha nadharia waliyoijenga kwamba Diana Haun ndiye aliyemteka nyara Sherri katika eneo la kuegeshea magari siku hiyo aliyotoweka.

Mnamo Mei 18, 1996 ikiwa ni siku tatu baada ya msemaji wa Polisi kuzungumza na wandishi wa habari, mkuu wa timu ya askari wa upelelezi katika kesi hiyo Luteni Carl Handy wa kituo cha Polisi cha Ventura alitangaza rasmi kwamba Diana Haun mkazi wa mji wa Port Hueneme amekamatwa akihusishwa na makosa ya kuteka nyara na kuua kwa kukusudia. Hata hivyo, Luteni Handy alisema kuwa, ingawa mwili wa Sherri Dally haujapatikana, lakini askari wa upelelezi wanalazimika kuamini kuwa Sherri ameuawa, na muuaji wake ni Diana ambapo inaonekana hakuwa peke yake, hivyo huenda watuhumiwa wengine wakatiwa mbaroni. Alipoulizwa na waandishi wa habari kuhusu uvumi kuwa Michael Dally alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na Diana, msemaji huyo alikataa kuzungumzia jambo hilo. Hata hivyo wafanyakazi wenzake na Michael Dally pamoja na Diana Haun walikiri kuwa ni kweli walikuwa na uhusiano ingawa walikataa kutaja majina yao katika vyombo vya habari.Naye Michael alipoulizwa kuhusu jambo hilo, alikanusha kabisa kuwa na uhusiano wa kimapenzi na Diana, lakini alikiri kuwa na urafiki wa kawaida na Diana na si zaidi ya hapo. Akionekana kumtetea Diana, Michael alisema, "Itakuwa ni vigumu sana kuamini kuwa Diana, mtu tunayeheshimiana sana anahusishwa kwa namna yoyote na kutoweka kwa mke wangu!"

Kwa upande wa familia ya Sherri, walikiri kusikia uvumi kuwa Michael alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na mfanyakazi mwenzie, lakini walikiri kutolijua jina lake. Alibainisha bibi yake Sherri aitwaye Claris Guess aliyekuwa na umri wa miaka 83 wakati huo.
Pamoja na Polisi kuongeza juhudi za ziada katika kumtafuta Sheri, lakini mama yake Sherri, Karlyne Guess akishirikiana na familia yake waliandaa vipepezushi vilivyokuwa vikitangaza zawadi ya dola 4,000 kwa mtu nyeyote atakayetoa taarifa zitakazosaidia kupatikana kwa mtoto wao. Akiongea na waandishi wa habari mama huyo alisema. "Tunachoamini ni kwamba, mahali fulani, mtu fulani, anafahamu ni nini kilichompata binti yetu, lakini kama familia, bado tunayo matumaini makubwa kwamba, binti yetu yuko hai" Mama huyo alikiri kusikia jina la Diana Haun likitajwa tajwa kuhusishwa na kutoweka kwa mwanaye, lakini alionyesha wasiwasi juu ya Polisi kutoweka bayana maendeleo ya upelelezi wa kesi hiyo.

Mara baada ya Diana Haun kufikishwa mahakamani na kusomewa mashtaka, msemaji wa Polisi, Luteni Handy aliwaambia waandishi wa habari kuwa Polisi wameamua kuomba msaada kutoka kitengo cha ulinzi wa jamii katika kuutafuta mwili wa Sherri Dally, hivyo kitengo hicho kimetoa helikopta ambayo itazunguka katika maeneo mbalimbali yasiyofikika kirahisi nje ya mji huo wa Ventura. Aliongeza kwamba, kazi hiyo ni ngumu kwa sababu Polisi hawana taarifa zozote kuhusu mahali mwili huo ulipo na maeneo ya kuchunguza ni mengi. Pia alibainisha kwamba kikundi cha kujitolea cha vijana kitajiunga na kazi hiyo.

Siku iliyofuata, msemaji huyo alikanusha habari kuwa Michael Dally ni miongoni mwa watu wanaochunguzwa na wapelelezi wa Polisi. Lakini hata hivyo ziliibuka habari kwamba Michael Dally aliwachukua watoto wake wawili wa kiume na kuondoka nao kwenda mapumzikoni kwa kutwa moja nje ya mji wa Ventura. Mpwa wake aitwae Hannah Murray anayeishi na Michael Dally tangu kutoweka kwa Sherri alitetea uamuzi wa Michael kwenda kwenye mapumziko na watoto wake, "Amekuwa mpweke na anaonekana kuchanganyikiwa." alisema Hannah kisha akaendelea. "Kwa sasa anachofanya ni kuiweka familia yake pamoja." Alimaliza kusema binti huyo.

Kutokana na kutopatikana kwa mwili wa Sherri Dally mpaka kufikia Mei 23, 1996, ilimlazimu mwendesha mashtaka kumuachia huru Diana Haun kutokana na kutopatikana kwa ushahidi wa kina wa kumfungulia mashtaka. Mnamo Juni 1, 1996, majira ya saa kumi na moja jioni ikiwa zimepita siku 26 tangu Sherri atoweke, kundi la vijana waliojitolea kwa kazi ya kuutafuta mwili huo waligundua mabaki ya mifupa ya mwanamke Magharibi mwa mji wa Ventura. Vijana hao waliwafahamisha Polisi na haukupita muda Polisi walifika wakiwa na mtaalamu wa kuchunguza maiti aitwae Dr. Ronald O'Halloran.

Walipofika katika eneo hilo, walikuta baadhi ya mifupa ikiwa imetawanyika na hata fuvu la kichwa lilikuwa mbali kidogo. Kwa upande wa uti wa mgongo wa mabaki yale kulionekana alama kama ya kuchomwa kisu. Dr. O'Halloran aliwaeleza waandishi wa habari wachache waliofika katika eneo hilo kwamba hawezi kuelezea hali hiyo ya fuvu la kichwa kukutwa mbali na yalipo mabaki mengine ya mifupa kama mhusika alichinjwa au ilitokana na shambulio lingine la wanyama wakali kwamba ndio waliotengenisha kichwa hicho na mwili baada ya mhusika kuuawa na mwili wake kutelekezwa pale. Baada ya kufanya uchunguzi wa awali, mabaki yale yalichukuliwa na kupelekwa hospitalini kwa uchunguzi zaidi.

Siku iliyofuata baada ya Dr. O'Halloran kufanya uchunguzi kamili, alitangaza rasmi kuwa mabaki yale yalikuwa ni ya mwili wa Sherri Dally, na uchunguzi ulionesha kwamba aliuawa kwa kupigwa na kuchomwa kisu na mtu au watu fulani.Pamoja na taarifa ile ya daktari, Polisi hawakutoa maoni yoyote kuhusiana na kumhusisha Diana Haun na kesi ile, na hiyo ilitokana na ushahidi finyu waliokuwa nao. Mnamo Juni 6, 1996 askari wa upelelezi walitembelea duka la kuuza mawigi liitwalo, Oxnard Discount Wigs and Beauty Supplies ambapo mmoja wa wafanyakazi anayeuza duka hilo aitwae Sandra Acevedo alithibitisha kwamba Diana Haun aliwahi kununua wigi la rangi ya dhahabu katika duka hilo siku chache kabla ya Sherri kutoweka.

Baadaye askari hao wa upelelezi walipiga simu katika kampuni moja ya kukodisha magari iitwayo Budget Car & Truck Rental ambayo ofisi zake zipo katika uwanja wa ndege wa Oxnard ambapo walipata ushahidi mwingine kuwa mnamo Mei 5, 1996 ikiwa ni siku moja kabla ya sherri kutoweka, Diana Haun au mtu mwingine alitumia kitambulisho chake kukodi gari dogo aina ya Nissan Altima.Mtu huyo aliyekodi gari hilo alilirudisha siku mbili baadae likiwa limetembea umbali wa maili 126 sawa na kilomita 202, na kwenye kiti cha nyuma cha gari hilo kulionekana kuwa na matone ya damu.

Kuanzia hapo askari wa upelelezi wakawa na uhakika kuwa wanao ushahidi wa kutosha kabisa kumtia hatiani Diana Haun kwa mauaji ya Sherri Dally. Wiki mbili baadae askari hao wa upelelezi walichukua kibali cha kuchunguza nyumbani kwa Diana Haun pamoja na nyumbani kwa dada yake aitwae Mary na mumewe aitwae Gilberto Oliver. Siku iliyofuata walikwenda kuchunguza nyumbani kwa Michael Dally.
Majira ya mchana Michael Dally na Diana Haun walichukuliwa hadi kituo cha Polisi kwa ajili ya kuhojiwa. Hata hivyo baadae jioni waliachiwa wote wawili bila kufunguliwa mashtaka. Nje ya kituo cha Polisi Diana Haun kwa mara ya kwanza aliongea na waandishi wa habari juu ya tuhuma za mauaji zinazomkabili. Alisema, tuhuma hizo ni uongo uliotungwa ili kumdhalilisha, na Polisi wamemsababishia maisha yake na familia yake kuwa kama Jehanam.

Hatimaye mnamo Agost 1, 1996, Polisi walikuwa tayari wameandaa hati ya mashtaka dhidi ya Diana Haun na siku hiyo hiyo Polisi walimkamata kwa tuhuma za utekeji nyara na mauaji. Diana aliwekwa ndani bila uwezekano wa kuachiwa kwa dhamana kwa muda wa miezi mitatu hadi Novemba 15, 1996 alipokamatwa Michael Dally na kuunganishwa naye na kufunguliwa mashtaka mapya wote wawili ya kuhusika na makosa ya utekeji nyara na mauaji pamoja na makosa hayo pia paliunganishwa kipengele kingine cha kutaka kunufaka kifedha.

Wakati miezi ikizidi kwenda kabla ya kesi ya Dally na Haun kuanza kusikilizwa, kwa pamoja Polisi wa Kituo kikuu cha Ventura pamoja na ofisi ya mwanasheria wa wilaya walijaribu kutovujisha kile kinachoendelea kabla ya kusikilizwa kwa kesi hiyo, lakini hilo halikuwezekana, kwani huko mitaani kesi hiyo ilikuwa ikizungumziwa kila kona na kila mtu alikuwa akisema lake. Profesa mmoja ambaye aliwahi kuwa Polisi huko nyuma ambaye anafundisha Chuo kikuu cha California, akizungumzia kesi hiyo alisema, "Kesi hii ni miongoni mwa yale yanayozikabili familia nyingi, matatizo ya kifedha na matatizo ya kutoka nje ya ndoa. Na mke huyu alikuwa anajitahidi kuinusuru ndoa yake ambayo ilikuwa inaenda harijojo. Ndoa nyingi zinakabiliwa na changamoto hizo."

Vyombo ya habari navyo havikubaki nyuma, kila siku ziliibuka habari za kushangaza juu ya kesi hiyo, ambapo wapo waliojitokeza na kudai kwamba Michael Dally aliwahi kukiri mbele yao kwamba hawara yake ndiye aliyemuua mkewe. Mwanamke mwingine alidai kwamba Dally na Haun walikuwa wakijihusisha na ulozi (Black Megic), na aliongeza kwamba kuna siku alimuona Dally akimng'ata Haun shingoni na kisha kumnyonya damu. Pia alibainisha kwamba Dally na Haun walikuwa wanatumia namba ya mwito ya 666 katika viitio vyao (Pagers), namba ambazo zinahusishwa na dini za Kishetani.

Hata hivyo wakili wa washtakiwa walikuwa na ombi maalum la kutaka kesi hiyo ihamishiwe nje ya mji wa Ventura kutokana na kutokuwa na imani na jinsi kesi hiyo ilivyokuwa ikizungumziwa katika mji huo. Naye wakili wa Dally aliomba kesi ya Dally itengenishwe na ile ya Haun kwa madai kwamba kuna uwezekanao wa muingiliano wa mashahidi katika shauri hilo jambo ambalo linaweza likakandamiza haki ya mwingine.

"Itakuwa si haki kuwa na kesi inayounganisha watu wawili, ambapo ushahidi unaotolewa dhidi ya mshitakiwa mmoja unaweza kutafsiriwa kumlenga mshitakiwa mwingine." Alisema mwanasheria huyo. Pamoja na mwendesha mashtaka kupinga jambo hilo, lakini Jaji aliyekuwa akisikiliza kesi hiyo Fredrick Jones alikubali ombi hilo la kutengenishwa kwa washtakiwa hao lakini alipinga shauri hilo kusikilizwa mahali pengine na akasisitiza kwamba kesi hiyo itaendelea kusikilizwa katika mji huo wa Ventura, lakini jopo la washauri watakaosikiliza kesi hiyo watatoka katika maeneo mengine.

Hatimaye kesi hiyo ilianza kusikilizwa rasmi hapo mnamo Agost 4, 1997 ikiwa ni zaidi ya mwaka mmoja tangu kukamatwa kwao. Kesi hiyo ilisikilizwa kwa muda wa wiki sita huku upande wa mshtaka ukiita mashahidi zaidi ya 100 ambao walikuja kutoa ushahidi wao dhidi ya Michael Dally na Diana Haun. Mnamo Septemba 22, 1997 kesi hiyo iliisha kusikilizwa na Jaji pamoja na baraza lake la washauri walikaa kwa siku nne wakijadili kesi hiyo dhidi ya watuhumiwa.

Baada ya mjadala huo mzito hapo mnamo Septemba 28, 1997 Diana alipatikana na hatia nya kuhusika na utekaji nyara na mauaji ya kukusudia ili kujinufaisha kifedha kupitia fedha za bima pamoja na pensheni ya Sherri Dally. Hukumu pekee kwa makosa ya aina hiyo ni kifo. Lakini Jaji Fredrick Jones, hakutoa uamuzi wa haraka, kumhukumu Diana Haun, kifo. Badala yake akaliita baraza lile lile lililosikiliza kesi ile ili kuamua kama Diana anastahili hukumu ya kifo kama ilivyoainishwa katika hukumu ya makosa ya aina hiyo au kifungo cha maisha kama pendekezo la pili.

Baada ya baraza hilo kupitia kesi hiyo hatimaye walikubaliana kwa pamoja kuwa Diana anastahili kuhukumiwa kifungo cha maisha bila uwezekano wa kifungo cha nje (Parole).

Siku hiyo hiyo Jaji Jones alianza maandalizi ya kusikiliza kesi dhidi ya Michael Dally. Kesi ambayo hata hivyo alidai kwamba yeye tayari amepoteza sifa ya kuisikiliza kutokana na mfumo wa sheria wa nchi hiyo, hivyo alibainisha kwamba amekubaliana na mahakama ya wilaya ya Santa Barbara kuteua baraza la kusikiliza kesi hiyo, na yeye aliahidi kushirikiana kwa karibu na Jaji Robert C. Bradley aliyeteuliwa kuendelea na kesi hiyo.

Kesi ya Michael Dally iliibua mengi yaliyojificha, kashfa ya kupenda Malaya na matumizi ya madawa ya kulevya ziliibuliwa pale mahakamani dhidi ya Michael Dally na miongoni mwa watu walioitwa kutoa ushahidi, ni wale aliokuwa akishirikiana nao kuvuta unga na pia hata Malaya aliowahi kutoka nao.


Mnamo Juni 9, 1998 kama Diana Haun, Michael Dally naye akakutwa na hatia ya kuhusika na mauaji ya mkewe na hivyo kuhukumiwa kifungo sha maisha bila uwezekano wa kifungo cha nje (Parole) na pia aliamriwa ailipe fidia ya kiasi cha dola 15,000 familia ya Sherry Dally.
 
Mtambuzi heading imenipa shock
Hebu ngoja nisome kisa na mkasa
jamani ulisahau kuwa mie ni mtu wa visa na mikasa!
Huu mkasa umeshatengenezewa Tamthilia kule Hollywood nchini Marekani na pia niliwahi kusikia kuwa kuna Movie imetengenezwa ikizungumzia mkasa huu. Bado najitahidi kuperuzi mtandano kujariibu kama nitapata link ya Youtube ya tamthilia hiyo ili niweke hapa.

Wiki ijayo nitajivinjari na mkasa wa hapa Afrika Mashariki-Stay Tune

 
khaaaaaaa! anyway tutafika tu. kweli nakwambia wengine wataishia kuwa kuni zenye moto mkali mithili ya moto wa mpingo huko akhera!
 
Kuna mambo mengi ya kujifunza kwenye hii thread, yani tusipende malaya zaidi ya wake zetu.

Ndefu lakini nimeisoma.
 
Mtambuzi heading imenipa shock
Hebu ngoja nisome kisa na mkasa
FistLady, hata mimi nilipoona nilidhani ni kisa chetu cha mume wa mtu hapa nyumbani!. Kumbe Marekani!.

Mtambuzi, tafuta kisa Asha Mkwizu Dyauli alimchinja kimada wa mume wake na kumkata kata vipande vipande na kumuweka kwenye gunia, akamiminia mafuta ya taa na kumchoma, mabaki akayaweka stoo pale maghorofa ya Muhimbili, harufu ndiyo iliyowastua majirani!.
 
Gustavo wa fridays!
Nimetafuta wapi mreno jana?
Nakusoma mkuu hongera nimekuwa teja wa simulizi zako
 
jamani ulisahau kuwa mie ni mtu wa visa na mikasa!
Huu mkasa umeshatengenezewa Tamthilia kule Hollywood nchini Marekani na pia niliwahi kusikia kuwa kuna Movie imetengenezwa ikizungumzia mkasa huu. Bado najitahidi kuperuzi mtandano kujariibu kama nitapata link ya Youtube ya tamthilia hiyo ili niweke hapa.

Wiki ijayo nitajivinjari na mkasa wa hapa Afrika Mashariki-Stay Tune


Tuchambulie na za siasa.e.g assasin of John Kennedy
 
FistLady, hata mimi nilipoona nilidhani ni kisa chetu cha mume wa mtu hapa nyumbani!. Kumbe Marekani!.

Mtambuzi, tafuta kisa Asha Mkwizu Dyauli alimchinja kimada wa mume wake na kumkata kata vipande vipande na kumuweka kwenye gunia, akamiminia mafuta ya taa na kumchoma, mabaki akayaweka stoo pale maghorofa ya Muhimbili, harufu ndiyo iliyowastua majirani!.

Ahsante kwa ushauri wako mzuri..........Nimeshaiandika hiyo kesi ya Asha Mkwizu, lakini jinsi mauaji yalivyofanyika si kama ulivyoeleza................. Hakumuua kwa staili hiyo na wala hakumkatakata na kumuweka kwenye gunia na kumhifadhi stoo, labda kama Mahakama na Polisi walidanganywa, na siamini kama hilo linaweza kutokea.

Na alikuwa haitwi Asha Mkwizu Dyauli jina llilotumika pale mahakamani ni Asha Mkwizu Hauli

Wiki zijazo panapo majaaliwa nitaiweka hiyo kesi hapa. Stay Tune!
 
Gustavo wa fridays!
Nimetafuta wapi mreno jana?
Nakusoma mkuu hongera nimekuwa teja wa simulizi zako
Ahsante sana kwa kunipa hamasa, nitajitahidi pia kuwaletea kesi za kushangaza zilizotokea hapa Afrika kwa ujumla wiki ijayo nitajivinjari Afrika Mashariki.
 
FistLady, hata mimi nilipoona nilidhani ni kisa chetu cha mume wa mtu hapa nyumbani!. Kumbe Marekani!.

Mtambuzi, tafuta kisa Asha Mkwizu Dyauli alimchinja kimada wa mume wake na kumkata kata vipande vipande na kumuweka kwenye gunia, akamiminia mafuta ya taa na kumchoma, mabaki akayaweka stoo pale maghorofa ya Muhimbili, harufu ndiyo iliyowastua majirani!.
Pasco ngoja nikuchokoze kidogo, hivi kesi hiyo ya Asha Mkwizu ikiunguruma pale Mahakama Kuu jiji Dar ulikuwa na umri gani?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom