Mpiga Debe anapoongea Kiingereza: Baada ya kudhalilishwa kuwa hajasoma..

TANMO

JF-Expert Member
Apr 12, 2008
11,513
11,276
Wakuu hii habari nimeikuta kwenye Blog ya Da' Koero mkundi (Vukani)

Nanukuu maneno yake:


"Leo asubuhi nimekutana na kituko cha mwaka, naomba nikiri kwamba hata mimi nilikuwa ni mjinga kwani sikutarajia kwamba jambo hilo nililolishuhudia linawezekana. Naomba nikiri kuwa hata mie nilikuwa nawapa watu hawa mtazamo tofauti kabisa nikidhani labda mie ni mjanja kuliko wao, lakini hili nililolishuhudia asubuhi ya leo, nimenifunza jambo moja muhimu sana maishani, kwamba kamwe usimhukumu mtu kutokana na muonekano wake.
Ilikuwa ni majira ya saa kumi na mbili alfajiri, niko maeneo ya Msasani, nikisubiri daladala la kuelekea Kariakoo, mara likaja basi moja hivi aina ya Toyota Coster. Kama kawaida abiria wakiwemo wanafunzi tulilikimbilia na kuanza kugombea kupanda kila mtu akijaribu kuwahi kiti. Japokuwa hatukuwa wengi, lakini nilishangazwa na jinsi abiria walivyokuwa wakigombea kupanda utadhani watakosa nafasi ya kukaa. Lakini cha kushangaza ni kwamba vurugu zote zile ilikuwa ni ili kuwahi viti vya Dirishani!

Pale mlangoni alisimama mpiga debe mmoja ambapo kwa hapa Dar hujulikana kama Mateja, yaani watumia madawa ya kulevya, ambaye alikuwa amevaa nguo kuu kuu na zilikuwa chafu ajabu. Alikuwa pale mlangoni kuzuia wanafunzi wasipande. Kwa hapa Dar ni jambo la kawaida wanafunzi kuzuiwa wasipande kwenye basi na abiria wakabaki wakiangalia tu, kama vile haiwahusu. Kule Arusha mambo ni tofauti kidogo, wanafunzi huwa hawaachwi, tena kama hajavuka barabara, hasa watoto wadogo, kondakta anamfuata na kumvusha ili apande kwenye basi, kwa kweli nilishangazwa na ustaarabu wa makondakta wa daladala za Arusha.

Baada ya abiria wote kupanda, yule mpiga debe aliwaambia wale wanafunzi kuwa atachukua wanafunzi sita tu, wengine waende kwenye mabasi mengine. Pale chini kulikuwa na wanafunzi zaidi ya kumi na tano hivi na wote walionekana wakitaka kupanda kwenye hilo basi ili kuwahi shule. Yule kijana mpiga debe aliongea kwa usataarabu akiwaelewesha wale wanafunzi, akiwaambia kuwa hata yeye anajua adha ya usafiri kwa wanafunzi lakini ile gari ina Hesabu, yaani wanatakiwa wafikishe kiwango fulani cha hela kwa mwenye gari na wao wabaki na chochote, na kwa kuzingatia kuwa leo ni Jumamosi, ni ngumu sana kupata hesabu ya tajiri.

Lakini kulitokea kutoelewana kati ya wale wanafunzi na yule mpiga debe, wanafunzi walimjia juu wakimwambia aache siasa, wao wanataka kuwahi shule na hawahitaji Lecture pale. Kulitokea kutoelewana, lakini yule mpiga debe alisisitiza msimamo wake wakutaka wapande wanafunzi sita tu. Ni kweli walipopanda wanafunzi sita, aliwazuia wengine wasipande na kuruhusu dereva aondoe gari. Baadhi ya wanafunzi walioachwa pale chini walilazimisha kuning'inia mlangoni, lakini yule mpiga debe aliendelea kuwazuia huku gari likianza kuondoka mdogo mdogo..

Wakati zogo kati ya wanafunzi na yule mpiga debe likiendelea, ghafla akaibuka abiria mmoja, akaanza kumfokea yule mpiga debe, akimuonya kwamba kama hatawaruhusu wale wanafunzi wapande basi atalipeleka basi lile Polisi, yule Mpiga debe hakumjibu alikuwa akiendelea kuzozana na wanafunzi.

Yule abiria alianza kumtolea yule mpiga debe maneno ya kashfa huku akimtisha kuwa atampiga. Basi liliondoka na baadhi ya wanafunzi waliachwa pale kituoni, ndipo yule mpiga debe akamgeukia yule abiria na kumuuliza kisa cha kumkashifu wakati yuko kazini.

Yule abiria akawa kama amechokozwa, alimshambulia yule mpiga debe kwa maneno makali na kumkashifu kuwa hajasoma na ni mvuta unga tu na kibaka wa mtaani.

Yule mpiga debe akamwambia, ni kweli hajasoma, kwa sababu ingekuwa ni jambo la kustaajabisha kukuta mpiga debe msomi, hata hivyo hakuishia hapo, akamtupia swali yule abiria………

"inaonekana mwenzangu umesoma sana eh!….. hivi una degree ngapi mpaka sasa, au una masters?" Yule abiria aliendelea kumtolea maneno ya kashfa yule mpiga debe huku akisisitiza kuwa hajasoma na ni mjinga tu.

Yule Mpiga debe akaonekana kukerwa na yale maneno kutoka kwa abiria mkorofi, akamgeukia na kumwambia, kwa kiingereza, ngoja nimnukuu hapa……..

"Listen my friend, don't judge me because of what I am doing, I have good education background than you. To be a Daladala tout does not justify that I am ignorant. For your information, I am educated enough to work for a white-collarjob. I am here because of frustration, after being fired from my job; I had a nice job with a lot of benefits and privileges, I am not a fool ok!"

Wakati anamwaga kiingereza, kwanza abiria walishikwa na butwaa, na baadae wakaanza kumshangilia wakiwemo wale wanafunzi waliokuwa wakitetewa na yule abiria mkorofi. Hata hivyo yule abiria aliposikia jamaa anamwaga kiingeza, alikaa kimya asiamini masikio yake,hakujibu kitu.

Abiria waliendelea kumchagiza mpiga debe aendelee kutoa dozi kwa mshkaji, na yeye ili kupata ujiko zaidi akaendelea kumwaga ma-vitu, palikuwa ni patamu hapo…….

"You know sometimes people think all daldala touts are drug users and they are not educated ……..… No, you are totally wrong my friend, for this job I am earning more than enough, I can make your salary which you get from you Boss Indians for 10 days. Although I have been fired but I decided to work as a daladala touts rather than stealing someone's money."

Kisha akaendelea…..

"Why you are quiet, talk now Mr. Educated" ………… "You see," akatugeukia sisi abiria na kutuambia ……….. "Mr. Educated have failed to speak even two English words"

Jamaa akajikakamua na kumjibu,

"Hebu ondoka na kiingereza chako cha kuombea maji, mwenyewe unajiona umeongea kiingereza hapo, hamna kitu,unachapia tu"

Mpiga debe hakumkawiza akamjibu…….

"Ok, my English is just for begging water, where is yours, if you can speak only two English words, I will give you ten thousand, right now, in front of passengers, I am not joking"

Yule mpiga debe akatoa elfu kumi na kumpa abiria mwingine aishike, ili kuthibitisha kuwa hatanii. Kumbe jamaa alikuwa ni mweupe, hajui Ngeli, yaani ilikuwa ni aibu, karibu abiria wote wakawa wana mzodoa kwa maneno ya kejeli.

Tulipofika kituo cha Namanga jamaa akashuka kwa aibu na ninadhani alikuwa hajafika safari yake, naona alishuka ili kujisitiri na aibu iliyomkumba mle ndani ya basi.

Nakwambia ilikuwa ni gumzo ndani ya basi lile kila mtu akisema lake wapo waliosema kuwa yule mpiga debe ni mpelelezi wa Polisi, wapo waliosema ni shushushu yaani anafanya kazi usalama wa Taifa. Na hilo ndilo tatizo tulilonalo Watanzania, yaani mtu akijibainisha tofauti na muonekano wake basi ataitwa shushushu…….. Basi na yule mpiga debe akapewa cheo cha ushushushu pale pale, kisa kaongea Kiingereza, kuna wengine walisema sio Mtanzania bali ni Mkenya, kwa kuwa hakuna Mtanzania anayejua Kiingereza kama vile halafu afanye kazi ya kupiga debe, ili mradi kila mtu alisema lake.

Tulifika Kariakoo kilamtu akashika hamsini zake, nimerejea nyumbani jioni hii nikaona niwashirikishe wasomaji wangu katika kisa hiki ambacho hata mie kiliniacha mdomo wazi."


Mwisho wa kunukuu.
Source: Vukani Blog


Mytake: Nadhani wakati mwingine hawa wapiga Debe na Makondakta wanakuwa wakorofi kutokana na wao kufahamu wazi kuwa jamii inawadharau na inadharau kazi ya daladala. Hivyo wanaamua kuwa wavuta bangi au walevi ili kuweza ku-cope na stress za kila siku kutoka kwa abiria wenye dharau.. Hii story imenifurahisha sana na nadhani tukiitumia kujifunza na kubadili mtazamo wetu kwa hawa ndugu zetu, basi nao wanaweza kubadili baadhi ya tabia zao... When you start treating People like People, they become People....

watch




 
Aisee, hii nimeipenda.
Kweli watanzania tuna tabia ya kujidharau wenyewe hata kama tunaweza watu wanaibuka na hisia za kimtazamo wa kifikra na sio hali halisi.
 
Aisee, hii nimeipenda.
Kweli watanzania tuna tabia ya kujidharau wenyewe hata kama tunaweza watu wanaibuka na hisia za kimtazamo wa kifikra na sio hali halisi.

Anyway,kazi kazi ilimradi iwe halali,lakini kwa mtizamo wa haraka haraka ulishawahi kuona makonda wa mabasi makubwa wanadharauliwa?mi nadhani hawa makonda wa daladala nao wamejisahau,angalia baadhi yao wana sare chafu sana,sasa kuna watu wanamdharau mtu kwa kuona haiba yake ya nje tu(personality).kwa ushahidi wa tafiti nilizowahi kufanya kwa kuwahoji baadhi ya makonda,wanapat kati ya sh 15 -20 kwa siku,sasa huoni mshahara wa bachelor holder?kwa nini hawazithamini kazi zao?

TABIA YAO YA KUJIWEKA VIBAYA NDO KIINI CHA MATATIZO,INGAWA KILA ABIRIA ANA TABIA YAKE NA ANAVYOCHUKULIA MAMBO.

HIVI KONDA AKIVAA VIZURI KWANI ABRIA HAWATATOA PESA?
 
Ahh!Kweli huyo abiria katolewa nishai..kwasababu tu kavaa nguo safi na amekaa kwenye dalala na nauli analipa badala ya kukusanya basi anajiona bora zaidi!Nimefurahi kwamba huyo konda alimpa somo la kubaki nae maisha!Usidharau usiemjua!
 
Du,hakika usilolijua ni kama usiku wa giza!mie mwenyewe siwapendi makonda wasiowachukua wanafunzi hasa yule mwanafunzi ambaye keshapanda konda analazimisha kumshusha,huwa napata hasira huanza kubishana nao ila thanx God huwa siwatukani wala kuwadharau. ,tunarud pale pale. ULIMI ni kiungo kidogo LAKINi.............
 
Stori nzuri sana na imetufundisha mengi hapo,kwa sababu kuna watu wanadharau kazi za wengine.
 
Nice story, BUT kujua kiingereza sio kwamba ndio educated, nina mtoto wa dada yangu anaongea Kiingereza ila bado hajaanza kwenda shule.
Kiingereza ni kama lugha nyengine tu.
Kwahiyo kujua hicho kiingereza isiwe kigezo eti cha mtu ndio educated.
 
Nice story, BUT kujua kiingereza sio kwamba ndio educated, nina mtoto wa dada yangu anaongea Kiingereza ila bado hajaanza kwenda shule.
Kiingereza ni kama lugha nyengine tu.
Kwahiyo kujua hicho kiingereza isiwe kigezo eti cha mtu ndio educated.

ulikuwa wewe nini? Teh teh pole.
Me nimeachwa hoi na jinsi wanafunzi waliokuwa wanatetewa walivyomgeuka jamaaa
 
ulikuwa wewe nini? Teh teh pole.
Me nimeachwa hoi na jinsi wanafunzi waliokuwa wanatetewa walivyomgeuka jamaaa

Im far far away from bongo land. nikujulishe kwamba kutokujua hicho kiingereza sio kwamba jamaa ni mbumbumbuu, kutoweza kujitetea kwa watanzania ndio kunakowafanya wakenya waje kuchukua nafasi zenu za kazi.
yeye akikuzidi kwa kiingereza na wewe mzidi kwa kiswahili.
 
Abiria kaipata komesha mana siyo sabuni ya mbuni!!..bravo mpiga debe!!..
Katika kitu ambacho najivunia maishani ni kutokudharau mtu yoyote kwa maisha yake anayoishi...Wote tunahangaika duniani!!

kweli kabisa huko nje kuna kila watu wa kila aina. Usimdharau mtu kisa umemkuta barabarani anaomba nauli ukadhani ww ndiye mwenye maisha bora. Huwezi jua pengine kaibiwa, ama ni maswahiba ya siku moja tuu yamemkuta. Au usione mtu anamiliki gari basi ukaona ni tajiri. Unaweza kukuta hana hata pa kulala. Maisha ni mzunguko, heshimu kila unayemuona maana hujui ni kwa nini Mungu amekukutanisha naye siku hiyo.
 
Nice story, BUT kujua kiingereza sio kwamba ndio educated, nina mtoto wa dada yangu anaongea Kiingereza ila bado hajaanza kwenda shule.
Kiingereza ni kama lugha nyengine tu.
Kwahiyo kujua hicho kiingereza isiwe kigezo eti cha mtu ndio educated.

Una sema kweli lakini tuludi nyuma, Daradara ni biashara sidhani kama utapenda ufanye biashara kila siku upate hasara. Kwa ustaarabu wa huyo konda wa kuchukua wanafunzi sita alionyesha utu kabisa, kuliko wale ambao huwa wanawagomea wanafunzi kabisa. Kama utakuwa unafanya biashara utanielewa nina maana gani. Jioni huyo konda atatakiwa apeleke marejesho ili atetee kibarua chake. Lakini kuna watu mjini huwa wanadhani hizo daradara zinatolewa rudhuku na serikali. Akipakia wanafunzi wachache basi na daradara nyingine nayo ije ichukuwe wengine kuliko wote kulundikana kwenye gari moja kama vile imegeuzwa school bus.
 
Hiyo imekaa vizuri, haitakiwi kumdharau mtu kwa namna yeyote ile. Hao wenye dharau wakikabidhiwa ofisi za serikali kwa sababu ana degree ataendeleza dharau zake kwa wananchi wa kawaida bila kujali kuwa hao wananchi ndo wanao mlipa mshahara. Mpiga debe alimkomesha.
 
Mimi sidharau kazi ya dala dala, namfahamu jamaa mmoja alikuwa dereva wa waziri fulani baadae akapunguzwa kazi pale wizarani. Pesa aliyolipwa na serikali akaamua kununua daladala na yeye mwenyewe ndio dereva. Huwezi amini jamaa kajenga kibanda chake cha kuishi na anasomesha wanae na maisha ni mazuri kuliko alivokuwa dereva wa pale wizarani.

Watanzania tumeathirika na white colar job na tutakufa maskinikwa kudharau badhi ya kazi za watu kama huyo jamaa wa kwenye hilo daladala.
 
Back
Top Bottom