Mpango wa CCM kuhusu Kigamboni una walakini wa maono!

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,475
39,991
Na Lula wa Ndali Mwananzela (Raia Mwema - Jumatano)

MOJAWAPO ya mipango mikubwa ya ujenzi wa jiji la kisasa, ni ule wa ujenzi wa Kigamboni kuwa jiji jipya la kisasa uliobuniwa na ambao unatarajiwa kutekelezwa chini ya Serikali ya CCM.

Mpango huu mkubwa una lengo la kubadilisha eneo la Kigamboni kuwa jiji la kisasa kabisa likiwa na barabara kubwa za kila aina, majengo makubwa na maeneo ya makazi ambayo yataweza kuchukua karibu watu laki tano.

Mradi huu mkubwa umetengenezewa hadi video ya kuupigia debe kwa wafadhili; huku ukionyesha mji wa ‘njozi" ambao unatakiwa kujengwa huko Kigamboni.

Kwa watu wanaopenda njozi, mpango wa kuijenga Kigamboni kwa kiasi hicho unavutia hisia, unaburudisha vionjo na unachochea matamanio ya ‘Paradiso ya Bongo'.

Kwa mtu yeyote ambaye amefuatilia kile kinachoitwa "Kigamboni New City Master Plan" anaweza kuona jinsi ambavyo watawala wetu walioshindwa wamejaribu kubuni kitu ambacho masikioni mwa watu kinasikika kuwa ni kizuri na ambacho jiji la Dar linakihitaji; yaani kulihahimisha jiji la Dar lilivyoborongwa sasa na kwenda kuanza kujenga upya ng'ambo ya Kigamboni.

Katika mipango yao wanataka kuona kuwa Kigamboni ndio panakuwa kitovu cha maisha ya kisasa. Sasa hivi Kigamboni ina wakazi wapatao zaidi kidogo ya 80,000 na mradi huu mkubwa ukikamilika Kigamboni itakuwa na watu wapatao 500,000 ikiwa ni mji unaojitegemea ukihusisha maeneo ya viwanda, maofisi, makazi na maeneo wazi. Ni mpango ambao ukiangalia kwa haraka unaweza kuamini kuwa umefikiriwa kwa kina na utakuwa ni suluhisho la tatizo la jiji la Dar la sasa.

Ndugu zangu, lengo kubwa lisilosemwa la kujenga hilo jiji jipya la Kigamboni ni kukubali kuwa watawala wetu wa leo wameshindwa kuboresha na kujenga jiji la Dar la sasa. Ni kukubali kuwa kufanya jiji la Dar la sasa kuwa la kisasa kumewashinda sasa wanataka kujaribu eneo jipya wakiamini kuwa wataweza.

Gharama zake kwa muda mrefu zitazidi kwa mara mia nyingi sana gharama za kuwapatia watoto wa Kitanzania elimu ya bure kuanzia msingi hadi Chuo Kikuu kwa miaka mingi ijayo! Ukiwauliza Wizara ya Ardhi na wale wenye kuupigia debe ujenzi huu watuambie gharama zake ni kiasi gani, hakuna hata mmoja anayeweza kutuambia kwa sababu ni mji wa njozi ambao hauwezi kujengwa kama kwa kutengeneza kwa kompyuta. Miji haishushwi kama Yerusalemu ya Kitabu cha Ufunuo, hujengwa kwa jasho na kwa damu!

Watawala wetu wa sasa walioshindwa wanataka wananchi wa Kigamboni na Jiji la Dar kuanza kufikiria kuwa Kigamboni itageuka kuwa mji wa njozi miaka michache ijayo. Kama miaka hamsini iliyopita tukiwa na "master plan" ya Jiji la Dar wameweza kuiboronga na kuharibu jiji hili lililochorwa tangu zamani kwa nini tunafikiria watu wale wale wataweza kujenga jiji jipya la kisasa pembeni?

Ati wanapita na kuomba kura wakiwashawishi wananchi kuwa Kigamboni litakuwa jiji la kisasa! Na wapo wananchi ambao wameshasahau kujenga hilo daraja la Kigamboni tu ni karibu miaka 30 sasa tangu wazo lake lianze!

Ninachosema ni kuwa mpango huu wa Serikali ya CCM kujenga Kigamboni kuwa jiji jipya una tatizo, na si tatizo dogo bali ni kubwa. Ni tatizo la maono, falsafa na la kimtazamo.

Kwanza, kwa sababu jiji la Dar la sasa halijashindikana kujengwa kuwa jiji la kisasa. Ninaamini kabisa Jiji la Dar likijengwa upya, miundombinu ya kisasa na mfumo mzuri wa matumizi ya ardhi bado lina uwezo wa kuhimili karibu watu milioni kumi hivi.

Kwa maneno mengine, ni kuwa jiji la Dar bado lina uwezo wa kutoa nafasi kwa yote yanayopendekezwa kufanyika Kigamboni ikiwemo ujenzi wa barabara za kisasa, maeneo mapya ya viwanda na ICT, na hata maeneo mapya ya makazi ya kisasa.

Bado jiji la Dar lilivyo sasa lina mojawapo ya matumizi mabaya kabisa ya ardhi katika nchi ya watu walio huru na wenye dalili ya kuwa na akili timamu!

Pili, waliobuni mpango huu wameshindwa kuelewa mojawapo ya matatizo makubwa ambayo yametokea mahali popote ambapo kuna tofauti kubwa ya kimaisha na kimaendeleo. Huwezi kuwa na eneo tajiri linaloishi karibu na eneo maskini bila kuwa na mvuto wa lazima kwa maskini kujitahidi kuhamia kwenye utajiri.

Ni kwa sababu hiyo wananchi maskini wa Mexico (iliyo Kusini mwa Marekani) wamekuwa wakijitahidi kuingia Marekani ili kutafuta maisha kwani Mexico ni maskini kulinganisha na Marekani. Lakini huwezi kuona wananchi wa Canada (iliyo Kaskazini ya Marekani) wakihangaika kuingia Marekani kwa wingi kwani Canada ina utajiri mkubwa kuweza kuhimili mvuto wa utajiri wa Marekani.

Huwezi kuwa na jiji jipya la kisasa Kilometa chache tu kutoka Manzese, Tandale, Magomeni na Dar ya zamani! Matajiri wa sasa wa Dar wakihamia Kigamboni mpya, maskani wa sasa wa Dar nao watahamia Kigamboni mpya!

Tatu, kutokana na mpango wa kujenga eneo la kisasa na lenye nafasi za utajiri hapo Kigamboni, tatizo lile lile lililoikuta Dar ya sasa litakuja Kigamboni na hapatakuwa na pa kukimbilia.

Kwa miaka mingi na toka enzi na enzi wananchi kutoka sehemu zote za Tanzania hata sehemu za nchi jirani wamekuwa wakikimbilia kuja Dar kutafuta maisha. Visa vimetungwa, hadithi zimesimuliwa na filamu zimetengenezwa juu ya jambo hili la eneo lililoendelea kuvuta maskini.

Matokeo yake tumeona kuwa jiji la Dar ambalo lilibuniwa kwa watu chini ya milioni moja likichukua karibu watu milioni nne sasa. Hiyo Kigamboni ambayo inafikiriwa itachukua watu laki tano ni kwenye makaratasi tu ifanya hivyo kwani kwanza itakomba mamilioni ya watu wa Dar (kama nilivyosema hapo juu) lakini vile vile itavuta kundi jipya la watu kutoka bara na maeneo mengine kuja "kutafuta maisha".

Hivyo, idadi kuwa jiji hili litakuwa ni la watu wapatao laki tano tu ni kudanganyana mchana kweupe; kwani hakuna jiji duniani lililowahi kujengwa likaweza kuwa na idadi ya watu waliokusudiwa tu. Si New York, si Tokyo na si Lagos au Kuala Lumpur. Majiji hayo yote yamejikuta yakitafuta njia na mbinu za kudhibiti msongamano wa watu.

Kwa nini basi kabla ya kuja na njozi ya Kigamboni Mpya wasituonyeshe kuwa wanaweza kukabiliana na ongezeko la watu kwenye jiji la Dar ya zamani?

Nne, ni kuwa huu ni mpango mbovu mno kwa sababu Kigamboni kama ilivyo Dar ni karibu na miji mikubwa mitatu ambayo bado haijajaa na inaweza kabisa kumeza idadi ya watu wa Dar na kuacha eneo la Kigamboni kuwa eneo la makazi na maeneo ya wazi ya wananchi wa jiji la Dar kupumzikia.

Kwanza, kuna Pwani (katika miji yake yote), ipo Tanga, na upo Morogoro. Kati ya maeneo hayo matatu ni eneo moja tu ambalo ninaamini, kama nilivyodokeza wiki iliyopita, laweza kujengwa kwa haraka zaidi, na likachukua nafasi ya jiji jipya nje ya Dar na ambalo halihitaji kuanzia sifuri kama wanavyotaka CCM huko Kigamboni.

Ninaamini ni jiji la Tanga tu ambalo lina sifa za kuweza kuwa eneo jipya la kibiashara na kiuchumi kuliko Kigamboni.

Kwanza, kwa sababu tayari lina miundo mbinu ya kuanzia na ambayo bado inaweza kuendelezwa kwa haraka zaidi kuliko kuanzia Kigamboni. Tanga kama mnavyojua ina umeme wa kudumu kutoka kwenye Gridi ya Taifa na vile vile una miji na mitaa ambayo tayari imepimwa na ambayo ni rahisi kuboreshwa au kupanuliwa.

Pili, mji wa Tanga tayari una bandari na eneo zuri kwa viwanda vya kisasa ukiwa na reli ambayo imeshaunganishwa kwenda sehemu yoyote ya Tanzania. Kwa maneno mengine, hata vikianza kujengwa viwanda kwa upya au mpango ambao niliudokeza wa CHADEMA kuhusu mambo ya TEKINOHAMA Tanga bado ina uwezo hata wa kuipiku Dar kuwa jiji la kisasa zaidi.

Tatu, Tanga ni mji ambao unaweza kufikika kiurahisi na kwa haraka kutokea Dar. Badala ya kuanza ujenzi mpya wa mabarabara ya kwenda ‘mbinguni' huko Dar au Kigamboni, kwa sasa inahitajika ujenzi wa barabara kubwa ya kisasa kuunganisha Tanga na Dar na hivyo kufanya usafiri kutoka Dar kuja Tanga kuwa ni wa muda mfupi zaidi.

Kwa hesabu za haraka haraka kama nilivyoonesha wiki iliyopita, treni la haraka (express) lisilotumia umeme laweza kufika Dar kutoka Tanga ndani ya saa moja na nusu. Ukijumlisha muda ambao watu wanatumia leo hii kutoka maeneo ya Dar kufika mjini utaona kuwa mtu anaweza kutoka Tanga akafika Dar mapema zaidi kuliko mtu anayetoka Mbezi ya Kimara kufika katikati ya jiji!

Hii ina maana tukiboresha usafiri wa treni kati ya miji hii miwili mtu anaweza kuishi Tanga na kufanya kazi Dar au kinyume chake!

Nne, wakati jiji la Dar lina ukubwa wa Kilomita za mraba 1590 (maili za mraba 614) mji wa Tanga una Kilomita za mraba zipatazo 1000 hivi (za jiji la sasa na ardhi). Idadi ya watu hata hivyo ina tofauti kubwa sana. Dar es Salaam inakaribia (au kupita kidogo) watu milioni 3 wakati mji wa Tanga una watu chini ya laki mbili na nusu.

Hii ina maana msongamano wa watu kwenye jiji la Tanga ni karibu watu 453/Km2 wakati jiji la Dar kwa Kilometa moja ya mraba ina watu 1760. Kwa maneno mengine, hata tukiongeza idadi ya watu 500,000 (wanaopendekezwa kuhamia Kigamboni) kwenye mji wa Tanga na kufanya idadi yake ya watu iwe 750,000 bado mji wa Tanga utakuwa na wastani wa watu 750 kwa kila Kilomita ya mraba!! Bado haitakuwa imefikia msongamano wa watu ulivyo sasa kwenye jiji la Dar! Sasa kwa nini tujenge Kigamboni?

Hapa ndipo ninapoona kuwa mpango huu wa CCM kama ulivyoanishwa katika Ilani yao 60:b(iv) una walakini - tena mkubwa. Wao wanasema wakichaguliwa mojawapo ya mpango wao ni "Kuanzisha mji wa kisasa wa Kigamboni ("Kigamboni New City)".


Hawatuambii watauanzisha lini, kwa gharama gani na fedha zitatoka wapi. Hawatuambii kuwa ni mpango utakaochukua miaka karibu themanini ijayo au mia moja au mitano ijayo na utawezekana vipi kama watendaji na wanasiasa ni wale wale!

Na utafanikiwa vipi hasa kama ufisadi ambalo ndilo tatizo kubwa zaidi la maendeleo yetu utaendelea kuhofiwa hata kutajwa kwa jina kwenye kampeni zao.

Sasa watu wa Dar wamepewa uchaguzi wa wazi. Jiji la Dar linahitaji mabadiliko tena ya haraka. Kigamboni kunahitaji kuendelezwa na kuwa ni eneo la kisasa. Ni vizuri wananchi wa Dar wawaulize wagombea wa vyama vingine kuhusu jinsi gani wataliboresha jiji la Dar na jinsi gani eneo la Kigamboni litaendelezwa.

Natumaini mojawapo ya vyama vya upinzani vitaweza kuangalia wazo langu la kuiendeleza Tanga na kuufutilia mbali mpango wao wa mji wa njozini wa Kigamboni. Na mkumbuke nimeelezea upande wa Tanga tu sijagusa ile miji mingine ya karibu ya Morogoro na maeneo ya Pwani!

Waliobuni na wanaoutetea mpango wa Kigamboni ni watu waliokosa fikra za utatuzi wa matatizo ya Jiji la Dar. Wanaoniudhi zaidi ni wananchi wa Jiji la Dar ambao wanapenda kugereshwa kirahisi na watasimama mistarini Oktoba 31 kuwachagua watu wale wale wenye fikra zile zile zilizoshindwa.
 
Mwanakijiji wanasema jiji litajengwa kwa miaka 20 kwa phases 3. Mradi wanasema utaanza 2011:confused2::becky: kwa awamu ya kwanza na kuendela kwa miaka hiyo 20.

Maswali yangu yote yanarudi pale pale kama hawa hawa walishindwa kuijenga Dodoma mpya na kila mara tumesikia promises tu wakati hawataki kutoka Dar kwenda huko Dodoma, nitawaaminije kwa mradi huu? Mi nadhani kuna tatizo. Kwani kila ifikapo uchaguzi tunaletewa ndoto na walioshindwa kufanya waliyoahidi miaka mitano iliyopita.

Lakini pia nimebaki najiuliza hata kama mradi huu utakuwepo ipo wapi policy ya kuwafanya wamiliki wa ardhi ya Kigamboni kunufaika kwa wao kuwa wamiliki bado wa ardhi yao na wawekezaji kuwa wakodishaji wa ardhi hiyo?

Mungu ibariki Tanzania na wabariki watu wake kweli.
 
Cha kushangaza zaid hii project yote ya Kigamboni ni kwa ajili ya kujenga mji wa watu 500,000 tu?
 
Cha kushangaza zaid hii project yote ya Kigamboni ni kwa ajili ya kujenga mji wa watu 500,000 tu?

Na Wakati kuna malaki ya Wanafunzi wanasugua Makalio kwenye sakafu, Maelfu ya Wamama wanajifungulia Chini!
 
CCM ni wapumbavu! Eti wanataka kujenga mji wa kisasa! Alafu? Yani hawa jamaa wanaboa sasa huwezi amini!
 
Mtazamo wangu ni kuwa muandishi ameandika makala kwa kutumia hisia zaidi ya uthibitisho. Kama anavyowakosoa CCM kwa kujenga hoja ya madi huu bila ya kutupa uthibitisho wa vyanzo vya pesa n.k, ndivyo yeye alivyoshindwa kutupa uthibitisho wa kwa nini mradi huu haufai.


Ndugu zangu, lengo kubwa lisilosemwa la kujenga hilo jiji jipya la Kigamboni ni kukubali kuwa watawala wetu wa leo wameshindwa kuboresha na kujenga jiji la Dar la sasa. Ni kukubali kuwa kufanya jiji la Dar la sasa kuwa la kisasa kumewashinda sasa wanataka kujaribu eneo jipya wakiamini kuwa wataweza.

Nna mashaka mengi na hili hitimisho alilolifikia mwandishi kuwa lengo kubwa lisilosemwa ni kuwa watawala wameshindwa kuboresha jiji la Dar kwa hiyo wameamua kujaribu kwengine. Mwandishi amefikia hitimisho hilo kama nani? Mtaalamu wa mipango miji? Mwandishi aliyetumia vielelezo au ni maoni binafsi yasiyofungamana na nukuu za kitaalamu?

Kwanza, kwa sababu jiji la Dar la sasa halijashindikana kujengwa kuwa jiji la kisasa. Ninaamini kabisa Jiji la Dar likijengwa upya, miundombinu ya kisasa na mfumo mzuri wa matumizi ya ardhi bado lina uwezo wa kuhimili karibu watu milioni kumi hivi.
Kwa maneno mengine, ni kuwa jiji la Dar bado lina uwezo wa kutoa nafasi kwa yote yanayopendekezwa kufanyika Kigamboni ikiwemo ujenzi wa barabara za kisasa, maeneo mapya ya viwanda na ICT, na hata maeneo mapya ya makazi ya kisasa.

Ninakubaliana na wewe kuwa jiji la Dar la sasa halijashindikana kujengwa kuwa la kisasa, lakini uboreshaji huo hauwezi kutokea kwa haraka na hata kwa gharama nafuu kama uanzishaji wa mji kutoka eneo ambalo bado halijaendelezwa sana.
Ujenzi wa kigamboni hakutakiwi kumaanisha kuwa jiji la Dar ndio litapuuzwa na kuachwa bila ya juhudi za kuboreshwa.

Pili, waliobuni mpango huu wameshindwa kuelewa mojawapo ya matatizo makubwa ambayo yametokea mahali popote ambapo kuna tofauti kubwa ya kimaisha na kimaendeleo. Huwezi kuwa na eneo tajiri linaloishi karibu na eneo maskini bila kuwa na mvuto wa lazima kwa maskini kujitahidi kuhamia kwenye utajiri.
Huwezi kuwa na jiji jipya la kisasa Kilometa chache tu kutoka Manzese, Tandale, Magomeni na Dar ya zamani! Matajiri wa sasa wa Dar wakihamia Kigamboni mpya, maskani wa sasa wa Dar nao watahamia Kigamboni mpya!

Na tatizo hapo ni lipi hasa?

Tatu, kutokana na mpango wa kujenga eneo la kisasa na lenye nafasi za utajiri hapo Kigamboni, tatizo lile lile lililoikuta Dar ya sasa litakuja Kigamboni na hapatakuwa na pa kukimbilia.
Kwa miaka mingi na toka enzi na enzi wananchi kutoka sehemu zote za Tanzania hata sehemu za nchi jirani wamekuwa wakikimbilia kuja Dar kutafuta maisha.
Matokeo yake tumeona kuwa jiji la Dar ambalo lilibuniwa kwa watu chini ya milioni moja likichukua karibu watu milioni nne sasa.
Hivyo, idadi kuwa jiji hili litakuwa ni la watu wapatao laki tano tu ni kudanganyana mchana kweupe; kwani hakuna jiji duniani lililowahi kujengwa likaweza kuwa na idadi ya watu waliokusudiwa tu. Si New York, si Tokyo na si Lagos au Kuala Lumpur. Majiji hayo yote yamejikuta yakitafuta njia na mbinu za kudhibiti msongamano wa watu.

Kama ulivyosema hakuna jiji duniani ambalo limewahi kukadiriwa wakazi na wakakaa wakazi hao hao, lakini taaluma ya mipango miji inalazimisha kufanyika kwa makadirio ya wakaazi watakaotarajiwa kuishi kwenye eneo husika. Kitaaluma watu wa mipango miji hufanya makadirio huku wakijumuisha idadi ya watu wanaotegemewa kuongezeka kulinganisha na wakati kutokanako na hali ya uchumi na projections nyengine.
Majiji makubwa uliyoyataja huchukua hatua kama hizo za kuanzisha miji karibu na miji mikubwa kama hatua za kukabiliana na msongomano wa watu mijini.
Tokyo imeanzisha Odaiba (ambayo kimuonekano iko kama Kigamboni), na serikali ikajenga madaraja na undersea tunnels, automatic trains, highways, artificial beach, ili kuhamishia maofisi, maeneo ya staarehe na masoko makubwa kwenye eneo hilo.
Malaysia imejenga Putrajaya eneo la utawala nje ya jiji la Kuala Lumpur ili kuepusha misongamano ya watu kwenye jiji kuu. China imejenga mpaka eco-cities karibu na mji mikubwa katika hatua za kupunguza msongamano na kunyanyua uchumi na hata Urussi kumekuwa na mipango ya miji mipya.

Kwa nini basi kabla ya kuja na njozi ya Kigamboni Mpya wasituonyeshe kuwa wanaweza kukabiliana na ongezeko la watu kwenye jiji la Dar ya zamani?

Hawawezi kuwaonyesha kuwa wanaweza kukabiliana na ongezeko la watu kwa sababu kitu hicho hakijaweza kufanikiwa na jiji lolote hadi sasa kama ulivyoeleza mwenyewe kwenye paragraph hii hii!

Nne, ni kuwa huu ni mpango mbovu mno kwa sababu Kigamboni kama ilivyo Dar ni karibu na miji mikubwa mitatu ambayo bado haijajaa na inaweza kabisa kumeza idadi ya watu wa Dar na kuacha eneo la Kigamboni kuwa eneo la makazi na maeneo ya wazi ya wananchi wa jiji la Dar kupumzikia.
Kwanza, kuna Pwani (katika miji yake yote), ipo Tanga, na upo Morogoro. Kati ya maeneo hayo matatu ni eneo moja tu ambalo ninaamini, kama nilivyodokeza wiki iliyopita, laweza kujengwa kwa haraka zaidi, na likachukua nafasi ya jiji jipya nje ya Dar na ambalo halihitaji kuanzia sifuri kama wanavyotaka CCM huko Kigamboni.
Ninaamini ni jiji la Tanga tu ambalo lina sifa za kuweza kuwa eneo jipya la kibiashara na kiuchumi kuliko Kigamboni.

Umezungumzia Kigamboni ‘kupelekwa' Tanga na kuchukulia kuwa mafanikio na makadirio yale yale ya kigamboni yatafanya kazi moja kwa moja kwa Tanga.
Taaluma ya mipango miji haikubaliani na mtazamo huo. Kigamboni kuna ‘upekee' wake ambao Tanga haupo (na kinyume chake ni sawa).
Pia muandishi hukutaka kutuonyesha faida hata moja au faida zinazodaiwa kuwepo kwa kuanzisha kwa mji Kigamboni na si sehemu nyengine ya Tanzania. Uwepo wa Kigamboni karibu na jiji la Dar pekee kunatoa faida kadhaa ambazo zimenukuliwa na waliobuni mpango huo wa Kigamboni.
Pia umetaka tuamini kuwa kwa kujengwa kwa mji mpya Kigamboni, jiji la Dar na miji mengine hayataboreshwa kabisa kabisa kitu ambacho ni dhahiri kuwa ni upotoshaji.

Hapa ndipo ninapoona kuwa mpango huu wa CCM kama ulivyoanishwa katika Ilani yao 60:b(iv) una walakini - tena mkubwa. Wao wanasema wakichaguliwa mojawapo ya mpango wao ni "Kuanzisha mji wa kisasa wa Kigamboni ("Kigamboni New City)".
Hawatuambii watauanzisha lini, kwa gharama gani na fedha zitatoka wapi. Hawatuambii kuwa ni mpango utakaochukua miaka karibu themanini ijayo au mia moja au mitano ijayo na utawezekana vipi kama watendaji na wanasiasa ni wale wale!

Hapa tuko pamoja mwandishi lakini sio kwa mujibu wa sababu zilizokosa jicho la kitaalamu ulizoziainisha.
 
Kuhusu Kigamboni naona kuna ukungu mkubwa sana ambao sote hatuuoni, kwanini daraja lisianze kwanza? kwanini miundo mbinu isipelekwe kabla ya hilo jiji? ni vipi Kigamboni kuwe Jiji zuri na kule Samora, Kariakoo, Kisutu etc.. kuwe Manzese ya jiji la Dar? bado ukiangalia kwa darubini ndogo tu utaona kuwa wakazi wa Kigamboni hawatakuwa na haki yoyote tena punde watakapokubali ardhi yao kuchukuliwa na kukabidhiwa mafisadi wachache ndani ya hao watu 500,000..bado pia ukiangalia vizuri utaona kwamba hakuna utaratibu unaojulikana wazi au wa kisheria kuwa wanakigamboni watalipwa vipi? watamiliki vipi? yote hayo hawajashirikishwa..kwa kifupi wajitayarishe kuumia kama wale wa uwanja wa ndege.., kwa ujumla hawa watu hawaaminiki na kila wanachokifanya wao basi hebu kwanza tuwafikirie kwa undani kwani waao siku zote wanaamini kuwa sisi watanzania ni wavivu wa kufikiri, tukumbuke ya Ndege ya Rais, Rada, Richmond, TICTS, Meremeta,waliyaanzisha hivihivi achilia mbali mvua za Lowassa ambazo tumshukuru Mungu pekee kutunusuru kwa hilo la sivyo wangeshachota na kujaza mifuko yao, tukubali tusikubali hawa jamaa wanaangalia kwa namna yoyote jinsi gani wapate fedha za kujaza mifuko yao,familia zao na au kusaidia uchaguzi utakaofuata (endapo watashinda uchaguzi huu..na wanaaamini hivyo)
 
Mchukia Fisadi:

Swala na Makao makuu ya nchi kuhamia Dodoma anaweza kukueleza vizuri nini kilitokea n "Sir" George Kahama - Chairman : Seacom (TZ)!

Mwanakijiji:

No Doubt - Mradi wa Kigamboni ni another "White Elephant"! Wa-Tanzania tumeshindwa kabisa kujifunza kutokana na historia na hili linaendelea kutugharimu sana - so sad
 
watu llaki tano ni wachache sana jamani. Kwanza mafisadi na ndugu zao na marafiki zao wanaweza kufika laki moja ,hujajumlisha wazungu ambao watatoa misaada,nao watataka appartment pale.he!!!
 
Boresha miundo mbinu katika jiji la sasa kwanza kuweza kuhudumia wakazi walio wengi.Acha mambo ya Abunuasi.Jifunze kujua na kufanya mambo ya msingi kwanza,kama vichwa vya kufikiri vimechoka achia ngazi,Tanzania ni ya wananchi wote.
 
Uo mradi kaka una utaratibu wake,na uyo jamaa apo aneitwa mchukia mafisadi kakujibu vizurina uo mradi si wa ccm pekee wala wa chama gani ni wetu sisi sote, na mradi uo pia wafadhili watatoa asilimia kubwa kuusu ilo shaka ondoa,upo apo mwanakijiji?
 
I think this is a good project if implemented accordingly... This is a world bank project, kama ile project ya Sinza, which failed during implementation. I think it is a good plan, with a good vision. Lets hope the implementation will also be as good.

Since the project is in three phases, lets wait and see the first phase. I think this project involved a lot of competitive analysts, city planners etc. Lets not discredit this one if we do not have a better clear alternative. Itakua mambo ya porojo tu! The good thing is that the project is out there for everyone to see, so if it does not go according to the plan...we can voice our opinions. If this is your area and you have a better plan, let us see it, or may be try to contact relevant bodies to include your views.
 
I think this is a good project if implemented accordingly... This is a world bank project, kama ile project ya Sinza, which failed during implementation. I think it is a good plan, with a good vision. Lets hope the implementation will also be as good.

Since the project is in three phases, lets wait and see the first phase. I think this project involved a lot of competitive analysts, city planners etc. Lets not discredit this one if we do not have a better clear alternative. Itakua mambo ya porojo tu! The good thing is that the project is out there for everyone to see, so if it does not go according to the plan...we can voice our opinions. If this is your area and you have a better plan, let us see it, or may be try to contact relevant bodies to include your views.

Mmh.. nadhani imeandikwa kwa nini wasijenge huo mji wa njozi Tanga ambapo tayari kuna miundo mbinu, eneo bado halijaendelea sana?
 
ivi tangu lini imekuwa kazi ya serikali kujenga mji?kwa nini wasiweke mazingira ya kuwezesha wananchi kujenga mji?au wanataka kuleta siasi ya ujamaa kwa mtazamo mpya?
 
ivi tangu lini imekuwa kazi ya serikali kujenga mji?kwa nini wasiweke mazingira ya kuwezesha wananchi kujenga mji?au wanataka kuleta siasi ya ujamaa kwa mtazamo mpya?

Ningewasifu sana kama hata hilo daraja lingekuwa linajengwa kwa sasa na baadhi ya miundombinu kama kuvuta maji toka mto rufiji imeanza, kuchonga barabara kwa kiwango cha kokoto, kutandaza mambomba ya maji safi na taka, pipes za gasi na umeme (underground) pamoja ya zile za mkongo wa mtandao (Internet fiber cables) . Haya nayo yanahitaji pesa toka World Bank? sisi tunaweza nini?

Na ningefarijika sana kama mradi huu ungehusisha wananchi wa eneo husika, isije ikawa mikataba ya ajabu ajabu kama ilivyo kawaida ya serikali yetu - Lakini when comes to ownership wanasema tu kiujumla wananchi watashirishwa but how? kwa sheria ipi ya ardhi? waeleze wananchi in details ili kila kitu kiwe wazi.

Leo hii ukifika Kigamboni wananchi wanaoishi maeneo yanayopitiwa na mradi huu hawajui chochote kinachoendelea na ndiyo maana mdau mmoja kasema watu wako negative, si hivyo bali they need to know how are they going to benefit when this project is implemented.

Huu mji wanajijengea wao, sidhani kwa hali ya mtanzania wa kawaida ataweza kuishi kwenye hizo apartments, kwa maana nyingine ni kuwafukuza wananchi maskini walioishi kwenye maenneo haya toka miaka ya 60 wakati wa uhuru na kuwapeleka mbali, bila hata kuweka maeneo mbadala kwa ajili ya makazi yao. Mji huu wataishi hao naowaita wawekezaji uchwara wanaokwepa kulipa kodi na mikataba ya ulaghai waishi kwa raha na amani. Serikali isiyojali wananchi wake ni serikali hatari sana.
 
Ningewasifu sana kama hata hilo daraja lingekuwa linajengwa kwa sasa na baadhi ya miundombinu kama kuvuta maji toka mto rufiji imeanza, kuchonga barabara kwa kiwango cha kokoto, kutandaza mambomba ya maji safi na taka, pipes za gasi na umeme (underground) pamoja ya zile za mkongo wa mtandao (Internet fiber cables) . Haya nayo yanahitaji pesa toka World Bank? sisi tunaweza nini?

Na ningefarijika sana kama mradi huu ungehusisha wananchi wa eneo husika, isije ikawa mikataba ya ajabu ajabu kama ilivyo kawaida ya serikali yetu - Lakini when comes to ownership wanasema tu kiujumla wananchi watashirishwa but how? kwa sheria ipi ya ardhi? waeleze wananchi in details ili kila kitu kiwe wazi.

Leo hii ukifika Kigamboni wananchi wanaoishi maeneo yanayopitiwa na mradi huu hawajui chochote kinachoendelea na ndiyo maana mdau mmoja kasema watu wako negative, si hivyo bali they need to know how are they going to benefit when this project is implemented.

Huu mji wanajijengea wao, sidhani kwa hali ya mtanzania wa kawaida ataweza kuishi kwenye hizo apartments, kwa maana nyingine ni kuwafukuza wananchi maskini walioishi kwenye maenneo haya toka miaka ya 60 wakati wa uhuru na kuwapeleka mbali, bila hata kuweka maeneo mbadala kwa ajili ya makazi yao. Mji huu wataishi hao naowaita wawekezaji uchwara wanaokwepa kulipa kodi na mikataba ya ulaghai waishi kwa raha na amani. Serikali isiyojali wananchi wake ni serikali hatari sana.

si ndo hapo!in short...wanatudanganya!huwezi kujenga mji hata siku moja!!cities are built by people not govts!
 
Mmh.. nadhani imeandikwa kwa nini wasijenge huo mji wa njozi Tanga ambapo tayari kuna miundo mbinu, eneo bado halijaendelea sana?

Kigamboni imeuzwa kwa MAREKANI bwana si yetu wala ya selikali yetu hiii ngome ni ya marekani anaweka kambi ya jeshi hapo
 
Back
Top Bottom