Elections 2010 Moto wawaka CCM:Shangingi la mbunge lachomwa moto

Mtaka Haki

JF-Expert Member
Oct 1, 2010
492
149
HUWEZI KUAMINI HABARI ZILIZOKO HAPA CHINI "KAMA ZILIVYO" NIMEZINAKILI KWENYE TOVUTI YA GAZETI LA MTANZANIA. NI VIZURI WASHINDANI WA CCM WAKAFUATILIA HILO LA MASHINE ZA KUCHAPISHA VITAMBULISHO VYA MPIGA KURA LILIISHIA WAPI? WENYE SIMU ZA VIONGOZI WA CHAMA TAWALA KINACHOTARAJIWA WAPIGIENI WAFUATILIE HABARI ZA CHAMA KINACHOTARAJIWA KUWA CHAMA KIKUU CHA UPINZANI HIVI KARIBUNI (CCM) SOMA ZILIVYO SIJAONGEZA WALA KUPUNGUZA TOKA KWENYE TOVUTI. NYINGINE NI ZA ZAMANI LAKINI NI ISSUES ZA KUFUATILIA.


*Viongozi watano CCM wasimamishwa
*Mtambo wa kufyatua kadi wakamatwa
*Wabunge 8 Mwanza wapumulia mashine
*Shy-Rose ampeleka puta Azzan Kinondoni
*Makalla, Murad moto, Ubungo ni kizaazaa

Waandishi Wetu, mikoani na Dar

MOTO unazidi kuwaka ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambapo watu wawili wameuawa kwa kugongwa na gari la mbunge wa Musoma Vijijini aliyemaliza muda wake, Nimrod Mkono, katika eneo la Mkiringo, Barabara ya Musoma-Mwanza.

Kama kulipiza kisasi, kwa hasira wananchi waliofika eneo la tukio nao wameamua kulichoma moto shangingi la mbunge huyo na kuliteketeza kabisa.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, ACP Robert Boaz, alisema tukio hilo lilitokea saa 2 usiku. Gari lililohusika ni lenye namba T 173 AZW aina ya Nissan Patrol, lililokuwa likitoka Mjini Musoma kwenda kijijini Busegwe ambako ndiko nyumbani kwa Mkono.

Alisema wakati wa tukio, Mkono hakuwamo kwenye gari hilo. Lilikuwa likiendeshwa na Petro Andrea (43).

Kamanda Boaz alisema waliokufa walikuwa katika pikipiki. Walitambuliwa kuwa ni Magori Magori (39), aliyekuwa akiendesha pikipiki na Wambura Kitongori (40). Wote ni wakazi wa Nyabange, wilayani Musoma.

Kamanda Boaz alisema baada ya ajali, wananchi walifika eneo la tukio na kuliteketeza kabisa gari hilo kwa moto. Dereva alinusurika baada ya kukimbia.

“Tunaendelea na uchunguzi wa ajali na wale waliohusika na tukio na watakaokamatwa katika kuhusika na tukio hilo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao kwani kuchoma moto gari hata kama limesababisha ajali ni kosa la jinai,”alisema.

Wakati huo huo, kijana aliyejulikana kwa jina la Mohamed Nyanganira alikamatwa juzi saa 6: 45 usiku akituhumiwa kuchoma mlango wa nyumba inayomilikiwa na Richard Moris (29).

Musoma

Chama Cha Mapinduzi, Wilaya ya Musoma Vijijini mkoani Mara, kimewasimamisha uongozi viongozi watano kwa kukiuka taratibu za uchaguzi ndani ya chama hicho kwa tuhuma za kuwafanyia kampeni baadhi ya wagombea ubunge.

Viongozi watatu kati ya hao ni wa ngazi ya kata na mmoja ni wa tawi ambao wanatuhumiwa kuwapigia kampeni baadhi ya wagombea, huku wakitumia ukabila.

Katibu wa CCM Wilaya ya Musoma Vijijini, Ferouz Bhano, alisema jana kuwa uamuzi wa kusimamishwa kwa viongozi hao ulifikiwa juzi jioni na Kamati ya Siasa ya Wilaya.

Alisema katika kikao hicho wajumbe baada kujadili kwa kina tuhuma za viongozi hao walibaini kuhusika kwao na vitendo hivyo vinavyokwenda kinyume na kanuni na maadili.

Waliosimamishwa ni Mwenyekiti wa CCM Kata ya Kyanyari, Elisha Magoma, Mwenyekiti CCM Kata ya Etaro, Edward Nyamarungu; Katibu Mwenezi Kata ya Etaro, Bwire Gibuma; Jackson Nyakia ambaye ni Katibu wa Tawi la Nyangoma katika Kata ya Mugango; na Elambika Mange ambaye ni Mwenyekiti wa Kata ya Mkirira.

Alisema baadhi ya wagombea na wapigadebe wao wamekuwa wakitumia ukabila na kutoa rushwa ya pombe, hasa katika Tarafa ya Nyanja.

Wakati huo huo, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani Mara inawashikilia wajumbe 11 wa wagombea ubunge wa Viti Maalumu kupitia Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT) kwa tuhuma za kutoa, kuomba na kupokea rushwa.

Kamanda wa Takukuru mkoani Mara, Elias Nyororo, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo.

Arusha

Takukuru mkoani Arusha inawashikilia watu watano baada ya kukutwa wakiwa na mtambo wa kuchapisha vitambulisho vya wapiga kura vinavyotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

Pamoja na vitambulisho, watuhumiwa hao walikamatwa wakiwa na kadi za CCM ambazo zinadaiwa kuwa ni batili.

Watu hao ambao Takukuru imehifadhi majina yao, walikamatwa jana asubuhi katika kata za Themi, Sokoni na Daraja Mbili. Miongoni mwa wanaoshikiliwa ni viongozi wa CCM wa matawi na kata.

Takukuru waliweka mtego kwa kumtumia mtu mmoja ambaye alipeleka picha na kutengenezwa kadi ya kupigia kura kwa masharti ya kumpigia kura mmoja wa waomba wa ubunge.

Pia kulikutwa orodha ya wanachama wa CCM ambao walitakiwa kupiga kura. Hadi jana mchana wanachama na viongozi wengine waandamizi wa CCM walikuwa wakitafutwa na Takukuru.

Chato

Aliyekuwa Diwani wa Kata ya Buselesele wilayani Chato, Crispine Kagoma, kupitia Chama cha Wananchi (CUF), amekihama chama hicho na kujiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Kagoma alitangaza uamuzi huo katika mkutano wa hadhara uliofanyika Buselesele. Baadaye yalifanyika maandamano ya kumpongeza kwa kutimiza miaka 10 ya udiwani. Kaimu Mwenyekiti wa CHADEMA Wilaya ya Chato, Paul Butondo, ameliambia gazeti hili kuwa chama chake kimepokea uamuzi huo kwa shangwe.

Mpanda

Watu zaidi ya 10 wamekamatwa na kuhojiwa na Takukuru, Wilaya ya Mpanda, Mkoa wa Katavi katika kampeni za kugombea Ubunge wa Viti Maalumu akiwamo Mgombea wa Ubunge.

Miongoni mwa waliokamatwa na kuhojiwa na Takukuru ni mtoto wa Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Asha Kapuya, anayegombea ubunge kupitia Viti Maalumu Mkoa wa Katavi. Pia yumo aliyeshinda kwenye kura za maoni nafasi ya udiwani Viti Maalumu katika uchaguzi uliofanyika wiki iliyopita Roda Mwakalenge.

Kamanda wa PCCB Wilaya ya Mpanda, Aron Misanga amesema watu hao walikamatwa juzi katika maeneo tofauti wakitoa pesa, vitenge, khanga, chakula na wengine wamewapangishia vyumba wapigakura katika nyumba za kulala wageni.

Mwanza

Zikiwa zimebaki siku tatu kwa CCM kupiga kura za maoni kupata wagombea wake, wabunge wanane kati ya 14 wa mkoa wa Mwanza wamekabwa kooni, kwa kiwango kinachoweza kutajwa kuwa wanapumulia mashine.

Taarifa kutoka katika majimbo ya Mkoa wa Mwanza zimeeleza kuwa wabunge hao wamekuwa wakikabiliwa na wakati mgumu kutokana na kushutumiwa katika mikutano ya kampeni kuwa wametekeleza majimbo yao kwa muda mrefu na hakuna kitu chochote cha maana ambacho wamekifanya wakiwa madarakani.

Wabunge waliokaliwa kooni na wapinzani wao katika kampeni za kuwania ndani ya CCM na majina ya majimbo yao kwenye mabano ni Jacob Shibiliti (Misungwi), Dk. Festus Limbu (Magu), Getruda Mongela (Ukerewe), Ernest Mabina (Geita) Samwel Chitalilo (Buchosa), James Msalika (Nyang'hwale), Bujiku Sakila (Kwimba) na Richard Ndassa (Sumve).

Kutokana na upepo jinsi unavyovuma kwa sasa, majina ya washindani wa waliokabwa koo yamehifadhiwa, kwa nia ya kuruhusu uwanja sawa wa ushindani.

Mbunge wa Jimbo la Nyamagana anayemaliza muda, Lawrence Masha, sasa amepata nafuu baada ya CCM kukemea vikali watu wanaopita nyumba hadi nyumba wakieneza ukabila na wengine kufanya ushirikina.

Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Dodoma anayemalizia muda wake, Mariamu Mfaki, jana aliwapigia magoti wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoani hapa kuwaomba kura.

Mfaki alipiga magoti alipopewa nafasi kwa mara ya mwisho kuomba kura muda mfupi kabla ya uchaguzi kuanza ambao ulikuwa unafanyika katika Ukumbi wa Kilimani mjini hapa.

Alisema anapiga magoti kwa mara ya mwisho kuomba kura kwa kuwa hatasimama tena mbele ya wajumbe hao kuomba kura katika uchaguzi ujao wa Mwaka 2015.

Kinondoni

Kisulisuli cha kisiasa kimeanza kumvumia Mbunge wa Kinondoni anayemaliza muda wake, Iddi Azan, baada ya kundi kubwa la wanawake kuamua kuwa zamu hii wanamchangua Shy-Rose Bhanji mwanamke mwenzao.

Upepo kwa kisiasa maeneo ya Kinondoni, katika vikao mbalimbali kwa sasa unaonyesha kuwa ushindani umebaki kwa watu wawili, ambao ni Azan na Shy-Rose, na katika hali inayoonyesha kuwa Azan ameanza kusikia joto, kwenye mikutano ya juzi aliwaomba wananchi wasikumbatie wasomi.

Kauli hii inaashiria kuwa Azan amekwishaona ukali wa washindani wake, hivyo anafanya kila mbinu kepusha kupoteza fursa hiyo. “Hata wanaume, wanasema wanawake wagombea wako saba, kazi imebaki kwenu kumuunga mkono mwenzenu au kumtupa mkono. Fainali ni Jumapili,” alisema Hassan Hassan, aliyezungumza na Mtanzania jana.

Mvomero

Wakati wagombea wanaotaka kuwania nafazi za ubunge kupitia CCM wakiendelea kufanya kampeni kwa ajili ya kuomba kura za maoni nchini, hali inazidi kuwa mbaya katika Jimbo la Mvomero kutokana na wagombea wa chama hicho tawala kufanya kampeni kwa mabavu.

Hali hiyo inaendelea kutishia amani katika Jimbo hilo kutokana na wagombea wake wawili ambao walianza uhasimu muda mrefu kufikia hatua ya kutaka kuchapana makonde wakati msafara wa kuwapeleka wanakojinadi na kuomba kura.

Bila kuficha chuki na hasira zao za muda mrefu wagombea hao ambao ni Mweka Hazina wa CCM Taifa, Amos Makalla na mbunge aliyemaliza muda, Sadiq Murad walifikia hatua hiyo pale, Makalla alipodai kuwa anapigwa madongo kwenye kampeni hizo na wagombea wenzake.

Tukio hilo lililowashangaza wananchi walio wengi lilitokea juzi wakati wagombea hao wakiwa kwenye gari la pamoja walipokuwa wakifanya kampeni katika Kata ya Mvomero iliyopo ndani ya Tarafa ya Mama ya Mvomero ambapo wagombea wenzao waliokuwepo kwenye msafara huo walifanya kazi ya ziada ya kuwaamulia na kutuliza ghasia.

Wakati huo huo, wananchi wa Kijiji cha Maharaka katika Kata ya Doma, juzi walimbeba juu juu Amos Makalla na wakishangilia, huku wakimwimbia nyimbo za pongezi kuwa tayari ndiye mbunge wa Jimbo hilo.

Kundi la vijana liliibuka wakiwa wanapuliza mavuvuzela na vipeperushi katikati ya mkutano huo baada ya ya kujieleza.

Askofu ataka mdahalo

Askofu Mkuu wa Makanisa ya Calvary Assemblies of God Tanzania, Dunstan Maboya, ametoa wito wa kuandaliwa kwa mdahalo wa wazi utakaowakutanisha wagombea wote wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, bila kutuma wawakilishi.

Pia ameitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC), kulionea huruma taifa kwa kutenda haki kwa vyama vyote ya siasa hususan vinavyoshiriki Uchaguzi Mkuu wa Mwaka huu ili uwe wa amani na utulivu.

Alitoa rai hiyo katika semina ya siku moja iliyoandaliwa na Jeshi la Polisi ikiwashirikisha viongozi wa dini na madhehebu mbalimbali. Mada kuu ilikuwa umuhimu wa viongozi wa dini katika kudumisha amani, usalama na utulivu katika Uchaguzi Mkuu.
Baadhi wa waliojitokeza kugombea ni Dk. Wilbrod Slaa (CHADEMA), Profesa Ibrahim Lipumba (CUF), Hashim Rungwe (NCCR-Mageuzi), Mutamwega Mgaywa (TLP) na Dk. Rais Jakaya Kikwete (CCM).

Sheikh Abdallah Swalehe Ndauga alisema ili kuimarisha amani katika mchakato wa Uchaguzi Mkuu ujao, wagombea wa nafasi zote za uongozi hawana budi kupewa elimu sahihi ya uraia juu ya haki na wajibu wao.

Iramba

Mkandarasi Samweli Nakei, amewaomba wapiga kura katika Jimbo la Iramba Mashariki wampe kura za kutosha kumwezesha kuwa mbunge kwa madai anao wafadhili kutoka Japan ambao wamemwahidi kuboresha miundombinu ya barabara katika jimbo hilo.

"Ninyi wananchi wa Kijiji cha Mng'anda mko kisiwani. Hakuna barabara ya kuaminika ya kuwaunganisha na vijiji vingine, pia mnahitaji daraja la kuwawezesha kuvuka ili mwende katika kijiji jirani cha Nkungi mahali mnapoweza kupata matibabu ya hakika. Mkinichagua, haya yote nitayatafutia ufumbuzi wa kudumu," aliahidi Nakei.

Jimbo la Bagamoyo

Kampeni za kuwania kuteuliwa kugombea ubunge kupitia CCM, Jimbo la Bagamoyo jana ziliibu vituko vya mwaka baada ya mmoja ya wanaowania ubunge Andrew Kasambala, kubanwa aeleze na kumtaja mtu aliyempa ekari 30 za kujenga kituo na makazi ya yatima katika Kijiji cha Sanzale.

Mmoja wa wanachama wa CCM alimuuliza swali mgombea huyo na kumtaka aeleeze ni nani aliyempa hizo ekari 30 za kujenga kituo hicho wakati kijiji hicho hakina ardhi ya kutosha na kina migogoro ya ardhi.

Akijibu maswali ya wanachama hao, Kasambala ambaye alishindwa kukanusha azma ya kutumia mgongo wa yatima kama turufu ya kuwania nafasi hiyo ya uwakilishi bungeni alisema hawezi kumtaja mtu aliyempa eneo hilo la kujenga kituo cha yatima.

“Ndugu zangu siwezi kumtaja mtu aliyenipa eneo hilo kwa sababu za kisiasa, lakini nawaahidi kuwa nitaweza kujenga kituo hicho mara tu mkinichagua kuwa mwakilishi wenu,” alisema na kauli hiyo ilizua minon’gono na kelele za wananchi ambao walikuwa wakidai kuwa anawaongopea.

APPT- Maendeleo

Rais Mtendaji wa Chama cha African Progressive Party (APPT)-Maendeleo, Peter Kuga Mziray ameahidi kuwawekea pingamizi wagombea wa Ubunge na Udiwani CCM Jimbo la Same Mashariki kwa kufanya kampeni kabla ya muda uliopangwa kisheria.

Mziray alitoa kauli hiyo jana jijini Dar es Salaam Mbele ya Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Lewis Makame, wakati wa kusaini makubaliano ya kisheria ya kufuata maadili wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka huu, yaliyohusisha vyama vitano vya siasa ambavyo vilikuwa vimesalia baada ya vingine 13 kufanya hivyo hivi karibuni.

“Nasikitika kusema kuwa wakati sisi tunasaini makubaliano haya, wenzetu CCM wanaendelea kufanya kampeni na hapa nasaini haya makubaliano, lakini nitachukua hatua za kisheria kuweka pingamizi kwa wagombea wa CCM Jimbo la Same Mashariki kwa kutumia mwanya wa kampeni za maoni kufanya mikutano ya hadhara,’’ alisema.

Akizungumzia malalamiko hayo, Jaji Makame alisema kwa sasa NEC haina nguvu kisheria kuvichukulia hatua vyama vinavyokiuka maadili ya Uchaguzi mpaka Agosti 20, mwaka huu zitakapoanza kampeni rasmi.

“Kwa sasa NEC haina nguvu kisheria na haiwezi kufanya kazi ambayo haikupewa, hivyo itabaki kama mtazamaji tu isipokuwa kuanzia tarehe ya kuanza kampeni ndiyo tutakuwa na meno kisheria,” alisema.

Akizungumzia kauli hiyo Jaji Makame, Kaimu Katibu Mkuu wa UDP, John Nkoro, alisema NEC imekwepa majukumu yake kwa vile Sheria ya Maadili ya Uchaguzi inatakiwa kutumika kuanzia mwanzo wa mchakato wa kutafuta wagombea.

Vyama vilivyotia saini makubaliano hayo jana ni pamoja na APPT maendeleo kikiwakilishwa na Mziray, Chama cha Wananchi (CUF) kilichowakilishwa na Mkurugenzi wake wa Haki za Binadamu na Sheria, Julius Mtatero, na UDP kilichowakilishwa na John Nkoro. CHADEMA na DP bado havijasaini.

Jimbo la Ubungo

Wagombea 13 wa Jimbo la Ubungo wameendelea kuchuana vikali huku Nape Nnauye akisema yeye ni msema kweli daima, Hawa N’ghumbi akipiga magoti na Shamsa Mwangunga akiendeleza staili yake ya kutoa shikamoo kwa wapigakura, huku akisema yeye ni mzoefu hivyo wananchi wamchague atashirikiana nao kutatua kero zao kwani na yeye ni mkaazi wa jimbo hili na mzaliwa. Yote hayo yalitokea mbele ya Mlezi wa CCM Dar es Salaam, Abdulrahman Kinana.

Habari hizi zimeandikwa na Victor Bariety (Chato) Walter Mguluchuma (Mpanda), John Maduhu (Mwanza), Debora Sanja (Dodoma), Joseph Sabinus, Nathaniel Limu (Iramba), Patrick Mwillongo (Bagamoyo), Malela Kassim na Rose Mweko.
 
Mboni hii habari inaonyesha ni ya mwaka uliopita au miezi iliopita ka mitanu ?
 
aaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaah, what is this Mtaka haki? Nilisoma hii habari miezi mitatu iliyopita inakuwaje mkuu au ndo unataka tuumize kichwa, tupoteze muda kwa inshu ambayo tayari tulishazungumzia.
 
Back
Top Bottom