Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,316
- 33,125
GHARAMA za kupiga simu na matumizi ya intaneti yanatarajiwa kupungua kwa asilimia 50 na 80, baada ya kukamilika kwa mkongo wa taifa wa mawasiliano unaojengwa hivi sasa. Akitoa taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2005 katika wizara yake kwa kipindi cha miaka mitano, Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Profesa Peter
Msolla, alisema gharama hizo zitapungua kwa kuwa hakutakuwa na matumizi ya setelaiti, ambayo yana gharama kubwa. Profesa Msolla alisema kwa kutumia mawasiliano ya mkongo, gharama za simu zitapungua kwa asilimia 80, wakati zile za intaneti zitashuka kwa asilimia 50. Licha ya kwamba gharama zitashuka, hata muda wa kufungua mtandao utakuwa mfupi ikilinganishwa na sasa, ambapo mtu ataweza pia kufungua hata nyaraka ambazo zina ujazo mkubwa, alisema. Kuhusu usajili wa simu, Profesa Msolla alisisitiza simu ambazo zitakuwa hazijasajiliwa hadi Juni 30, mwaka huu, zitafungwa hivyo wamiliki hawatazitumia tena. Alisema baada ya muda huo, watu ambao watapoteza simu watapaswa kutoa ripoti mara moja kwa kuwa iwapo zitatumika katika matukio ya uhalifu, wanaweza kukamatwa na kuchukuliwa hatua. Katika hatua nyingine, Profesa Msolla alisema wizara kwa kushirikiana na taasisi zingine za serikali, zimeandaa mpango kamambe wa kudhibiti uingizwaji wa vifaa vya elektroniki, hasa simu na kompyuta ili kulinda afya za watumiaji na mazingira. Alisema kumekuwa na uingizaji holela wa simu na kompyuta, ambazo hutumika muda mfupi na kutupwa, hivyo umeandaliwa mpango wa kudhibiti ili kuhakikisha hazileti madhara kwa wananchi.
Mkongo wa taifa kupunguza gharama kwa asilimia 80