Migodi yakwepa kodi Sh.bil. 40

armanisankara

JF-Expert Member
Jul 15, 2011
283
49
Zaidi ya Sh. Bilioni 40 za sekta ya madini zilizotakiwa kuwanufaisha wananchi wanaoishi jirani na migodi mikubwa nchini zimepotea baada ya kampuni za madini kukwepa kulipa kodi ambayo ingetumika kuwaletea maendeleo wananchi hao.

Wananchi hao wanaishi katika lindi la umasikini kwa kukosa ajira, ardhi na fursa za kufanya biashara.

Kila kukicha wamekuwa wakishuhudia ndege zikitua na kupaa, zikiwa na kazi moja tu ya kusafirisha madini kuelekea Ughaibuni.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa migodi mikubwa iliyopo kwenye mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Tabora, Simiyu, Geita na Mara inadaiwa zaidi ya Sh. bilioni 5 baada ya kukwepa kodi kwa kipindi cha miaka saba.

Siri ya ukwepaji kodi imeibuka baada ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, kwa kushirikiana na Naibu wake anayeshughulikia madini, Stephen Masele, kuanza kazi ya kusafisha uozo ndani ya sekta ya madini.

Habari zilizoifikia NIPASHE Jumapili zinasema tayari wawekezaji hao wameanza kubanwa ili kulipa kodi hizo.

Imebainika kuwa huko nyuma wawekezaji hao walikuwa wakijipangia kiasi cha kodi wanachotaka kulipa kwa Halmashauri na mrahaba.

Kimsingi migodi hiyo ilikuwa ikilipa fedha hizo kwa serikali kama ruzuku tu, sio kwa kufuata sheria.

Wawekezaji hao wamekuwa kama miungu watu wanapofika wizarani hapo kwani kila wanachokifanya hakuna kiongozi aliyethubutu kuwagusa, kuwakemea na hata kusema neno hapana.

Chanzo chetu cha habari kimesema kuwa baada ya kuingia kwa mawaziri hao kazi waliyoanza nayo ni kuwalazimisha wawekezaji wa migodi hiyo kuzilipa Halmashauri kodi ya asilimia 0.3 ya uzalishaji wote kila mwaka kama kodi ya huduma.

Awali migodi hiyo ilikuwa ikilipa Dola za Kimarekani 200,000 kila mwaka kinyume na sheria.

Imebainika kuwa kama migodi hiyo ingelipa kodi ya huduma kwa kipindi chote tangu waanze uchimbaji mwaka 1997, Halmashauri zote zenye migodi zingeweza kujinunulia madawati, kuchimba visima vya maji na kuanzisha miradi ya mingi ya maendeleo bila kutegemea serikali kuu.

Kodi nyingine ambayo wawekezaji hao walitakiwa kulipa mara moja ni ile ya kuilipa serikali asilimia nne (4%) ya mrahaba, baada ya migodi hiyo kuendelea kulipa asilimia 3 tu licha ya mikataba yao kufanyiwa marekebisho ili ilingane na sheria.

MIGODI YAPEWA MASHARTI

Taarifa zilizopatikana kutoka ndani ya wizara hiyo zinaeleza mara baada Profesa Muhongo na Masele kuanza kazi, waliitwa wamiliki wa migodi mikubwa jijini Dar es Salam na kuwataka kuacha kutoa visingizio vya kukwepa kulipa kodi.

Waziri alisisitiza kuwa wizara hiyo itasimamia utekelezaji wote wa kisheria, kinachotakiwa wafuate sheria ya nchi kwa kulipa malimbikizo yote ya kodi.

Aidha, walielezwa kuwa suala la madini litafanywa na Masele na hakuna haja ya kumuona Profesa Muhongo labda kwa jambo la dharura.

Walielezwa kuwa kama mgodi hautalipa kodi hizo ikiwemo ya mrahaba hakutatolewa kibali cha aina yoyote ya kusafirisha madini nje.

MGOMO BARIDI WASHINDWA

Baada ya kufanyika kwa mkutano huo, imedaiwa baadhi ya wawekezaji wa migodi hiyo walionyesha jeuri kwa kukataa kulipa kodi hizo, ndipo mawaziri hao walipokataa kutoa vibali vya kusafirisha madini nje.

"Baadhi ya wamiliki wa migodi walifanya mgomo wa kulipa kodi, wakisema hawaitambui, lakini walinyimwa kibali, kitu ambacho waliona hapa hakuna utani," Kilisema chanzo hicho.

Baada ya kuona msimamo wa mawaziri hao umekuwa mkali, walirudi nyuma na kukubali kulipa madeni hayo, lakini waliiomba wizara waanze kulipa malimbikizo ya kodi kuanzia mwaka 2005 hado Julai mwaka huu.

NZEGA YAPEWA BILIONI 2.3 ZA MALIMBIKIZO

Mgodi wa Resolite ulikubali kuanza kulipa halmashauri ya Wilaya ya Nzega Sh. bilioni 2.3 ya malibikizo ya kodi kati ya Sh. bilioni 5.6 walizokuwa wakidaiwa.

Katika ripoti ya uzalishaji kwenye mgodi wa Resolute unaozalisha dhahabu na Fedha, inaonyesha kwa miaka saba kuanzia 2005 hadi Julai mwaka huu, uzalishaji wa madini hayo ulikuwa na thamani ya Dola bilioni 896,826,575, kodi ya huduma kwa Halmashauri ya Nzega ilitakiwa kulipwa Dola 2,690,480.

Hata hivyo, kutokana mgodi huo kujipangia kulipa Dola 200,000 ya kila mwaka, Halmashauri hiyo ilipata Dola 1,200,000 pekee huku fedha nyingine Dola 1,490,480 sawa na Sh. bilioni 5.6, mgodi huo ulikataa kulipa.

Wakati wa kukabidhi fedha hizo hivi karibuni, Naibu Waziri Masele, alisema kuanza kulipwa fedha hizo kwa Halmashauri ya Wilaya ya Nzega ni mwanzo wa Halmashauri zinginne kulipwa malimbikizo yao.

Alisema kiujumla wamejipanga kuhakikisha migodi yote inaanza kufuata sheria kwa kulipa kodi kama inavyotakiwa kwa ajili ya maslahi ya Watanzania.

Masele alisema baada ya Resolute, migodi mingine kama Bulyahulu, Buzwagi, Kahama Gold Mining, Geita na North Mara itafuata utaratibu huo haraka.

"Tunachozungumzia hapa ni maslahi ya Taifa, migodi hii inatoa dhahabu na wanawajibika kulipa kodi ya kisheria ili kuinua uchumi wa nchi, tunaapa hatutakuwa tayari kuona hali ya nyuma inajirudia tena," alisema Masele.

Makabidhiano hayo yalishuhudiwa na baadhi ya madiwani, wabunge na Mkurugenzi Mtendaji wa mgodi huo Don Mcleod.

Baadhi ya wabunge kutoka mikoa hiyo, Suleimani Zed na Abdallah Kigwangallah, walisema wanawapongeza mawaziri hao kufanya mambo ambayo mawaziri wengine walishindwa.

Walisema kitendo cha migodi hiyo kuonekana kukubali kulipa kodi hizo ni ishara kuwa kuna kazi kubwa imefanyika kwa kipindi kifupi. “Tulijitahidi kwa muda mrefu kupigania haki yetu na Taifa kwa ujumla, lakini tulishindwa lakini kwa muda mfupi wa mawaziri hawa tumeshuhudia mageuzi makubwa katika sekta ya madini,” alisema Kigwangallah.





CHANZO: NIPASHE

 
  • Thanks
Reactions: BAK
kwa wenzetu hakuna kosa kubwa kama kukwepa kulipa kodi na kwa sababu wamebainika wamekwepa kulipa kodi inabidi walipe na faini juu sio kulipa malimbikizo hiyo itawafanya wasirudie ukwepaji wa kodi
 
Back
Top Bottom