Mgomo TUCTA: Serikali iliwatisha wafanyakazi kwa kuwasainisha

PELE

JF-Expert Member
Dec 23, 2009
229
12
Mwandishi Wetu
Raia Mwema
Mei 12, 2010

bul2.gif
Wakuu wa mikoa, wilaya wafanya mikakati ya siri
bul2.gif
Wafanyakazi serikalini, sekta nyeti wakosa morali


SERIKALI haikujiandaa kupata wafanyakazi mbadala kama wafanyakazi wa sasa wangeshiriki mgomo uliotishwa na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA) na wakafukuzwa kama ambavyo Rais Jakaya Kikwete alivyotishia kwenye hotuba yake kwa Wazee wa Dar es Salaam wiki iliyopita, Raia Mwema limebaini.

Kwa sababu ya kutojiandaa huko kupata wafanyakazi mbadala, Serikali iliibuka na mkakati wa kuwatisha baadhi ya waliopo waamue kuhusu mgomo kwa kusaini vitabu vya mahudhurio ofisini kwao.


Kwa mujibu wa vyanzo huru vya habari serikalini, siku moja kabla ya mgomo kuanza sehemu kubwa ya wafanyakazi serikalini walilazimishwa kutia saini kama watashiriki mgomo huo au la na zaidi, ikibainika kuwa kazi hiyo ilikuwa ikifanywa na viongozi wa mikoa na wilaya kwa maelekezo maalumu.


Uchunguzi wa Raia Mwema umethibitisha kwamba wakuu wa mikoa walitoa maelekezo ya siri kwa wakuu wa wilaya wakiwataka kuwatisha wafanyakazi wao wasishiriki mgomo huo uliokuwa umeandaliwa na TUCTA.


Mmoja wa viongozi hao, Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Dk. Christine Ishengoma, amethibitika kuwaandikia waraka wa siri wakuu wa wilaya mkoani kwake ili kuzima maadhimisho ya Mei Mosi, mkoani humo.


Taarifa zilizopo zinabainisha kuwa hata baadhi ya watendaji waandamizi serikalini walishtushwa na kauli ya Rais Kikwete kuwa wasiotaka kufanya kazi watachukuliwa hatua ikiwa ni pamoja na kufukuzwa. Kushtushwa kwa watendaji hao waandamizi kunatokana na ufahamu wao kuhusu masuala ya Serikali na kwamba wakati Rais anatoa kauli hiyo, hapakuwa na maandalizi yoyote ya utekelezaji endapo wafanyakazi wote wangetimka.


"Haiwezekani kufukuza wafanyakazi wote hata kama wangeshiriki mgomo…fikiria umemfundisha daktari kwa miaka mitano, amehitimu na kuwa na uzoefu wa miaka mingine mitano au zaidi. Hawa uwafukuze halafu utarajie kupata wengine ili mambo yaende kama kawaida…hapana ni suala lisilowezekana.


"Au unao wahandisi na watumishi wengine wenye kujua utekelezaji wa mipango mbalimbali ya Serikali na hata mikataba ya miradi mikubwa na midogo yenye manufaa ya umma, kuanzia kwenye halmashauri hadi Serikali Kuu..uwafukuze…hii haipo kabisa…tamko la Mkuu (Rais) lilikuwa la kisiasa tu," alisema mmoja wa maofisa waandamizi Menejimenti ya Utumishi wa Umma akiongeza ya kuwa zingeweza tu kuchukuliwa hatua nyingine za kinidhamu na si kuwafukuza wafanyakazi ovyo.


Kauli hiyo inaungwa mkono na Naibu Katibu Mkuu wa TUCTA, ambaye kwa sasa anakaimu nafasi ya Katibu Mkuu wa shirikisho hilo, Nocholaus Mgaya, akisema: "Hata kama Serikali ingeomba msaada wa watalaamu kutoka nchi nyingi ni dhahiri kuwa utendaji ungeyumba kwa kuwa mazingira ya ufanyaji kazi kati ya nchi moja na nyingine ni tofauti."


Uchunguzi wa Raia Mwema katika ofisi nyingi za Serikali unaohusisha mazungumzo na baadhi ya maofisa katika idara mbalimbali za serikali, manispaa na halmashauri za miji na vijiji umebaini kuwa palikuwapo shinikizo la kuwataka wafanyakazi kusaini tamko la kutoshiriki mgomo.


Uamuzi huo wa kuwashinikiza watumishi kutia saini tamko la kushiriki au kutoshiriki mgomo ulifanyika siku moja baada ya Rais Kikwete kutoa hotuba yake iliyokuwa inatishia kuwa watakaoshiriki mgomo watachukuliwa hatua.

Raia Mwema iliwasiliana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Hawa Ghasia, jana Jumanne kutaka kujua utayari wa Serikali kama wafanyakazi wangegoma bila mafanikio kutokana na simu yake kuwa nje ya mtandao.

Mbali na Waziri Ghasia, gazeti hili pia liliwasiliana bila mafanikio pia na Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Profesa Juma Kapuya ambaye naye simu zake hazikupatikana.


Hata hivyo, uchunguzi zaidi umebaini kuwa utendaji katika baadhi ya ofisi za Serikali umekuwa wa kusuasua na morali ya kazi ikiwa inazidi kushuka kwenye baadhi ya wizara huku mawaziri wakiwa majimboni kujipanga ili kurejea bungeni.


Katika baadhi ya wizara, mikoa na wilaya, wakuu wa maeneo hayo pia wamekimbilia kwenye majimbo ya uchaguzi kuhakikisha wanateuliwa kugombea ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).


Taarifa za uhakika kutoka mkoani Ruvuma zinamhusisha Mkuu wa Mkoa huo, Dk. Ishengoma na harakati za kuzima wafanyakazi hasa wa halmashauri kwa kutoa maagizo maalumu kwa wakuu wa wilaya za mkoani humo ili kukabili maadhimisho ya Mei Mosi, yaliyokuwa yamegubikwa na harakati za mgomo.


Katika maagizo yake, Dk. Ishengoma aliwataka wakuu wa wilaya kuhakikisha sherehe hizo za Mei Mosi, hazifanyiki. Hata hivyo, wawakilishi wa wafanyakazi mkoani Ruvuma waliwasiliana na wenzao wa TUCTA Makao Makuu na kuwatumia kwa nukushi (fax) barua ya Mkuu huyo wa Mkoa yenye maagizo hayo.


Taarifa za uhakika zinabainisha kuwa TUCTA walilazimika kuwasiliana na Mkuu huyo wa Mkoa kwa barua na kumkumbusha kuwa hatua yake hiyo ni kinyume cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kutokana na uamuzi huo wa TUCTA Makao Makuu, Mkuu huyo wa Mkoa alifuta mkakati wake huo.


TUCTA wameitisha mgomo wa wafanyakazi wote kutokana na madai matatu. Kwanza ni nyongeza ya mishara; pili kodi kubwa katika mishahara na tatu ni mafao kwa wastaafu yatolewe kwa uwiano sahihi miongoni mwa wafanyakazi tofauti na sasa kwa kuwa wapo wanaolipwa mafao makubwa zaidi ya wengine licha ya kufanana sifa na vigezo vya utumishi.


Mgomo huo uliahirishwa na viongozi wa TUTCA baada ya Rais Kikwete kutoa hotuba yenye vitisho dhidi ya watakaogoma huku akiwashangaa viongozi hao kuitisha mgomo wakati mazungumzo kati yao na Serikali yakiendelea, mazungumzo yaliyokuwa yamepangwa kufanyika Mei 8, mwaka huu.


Hata hivyo, TUCTA wamelazimika kusogeza tena mbele mgomo huo kwa mwezi mmoja. Kwa mujibu wa Mgaya, sasa wanasubiri siku 21 ambazo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, anatakiwa kutamka juu ya makubaliano yaliyofikiwa kuhusu maslahi ya wafanyakazi serikalini.


Katika mazungumzo yake na baadhi ya vyombo vya habari mapema wiki hii, Mgaya alisema ingawa wanasubiri tamko la Waziri bado wanaendelea na mchakato wa mgomo huo. Tamko hilo la Waziri ndilo litakaloipa TUCTA kufikia uamuzi wa kugoma au la.


Kwa mujibu wa Mgaya, mchakato wa kuandaa mgomo unaendelea kwa viongozi wa shirikisho hilo kufanya ziara za kuelimisha wafanyakazi wake mikoani na tayari mikoa ya Pwani, Morogoro na Dodoma imehusika.


Kuna dalili kuwa kama wito wa mgomo utatolewa tena wafanyakazi katika sekta mbalimbali za umma wanaweza kuunga mkono bila kujali athari zake kwa uchumi na watu, wakisisitiza kwamba atakayebeba lawama zote ni Serikali.


Kwa upande mwingine, TUCTA wamejipanga kukutana na wanasheria ili kujadili tangazo namba 172 la Serikali linalohusu kupandisha mishahara katika sekta ya umma linalotajwa kuwa na upungufu mkubwa kisheria.


Tangazo hilo namba 172 linatajwa kufuta tangazo jingine namba 233 la mwaka 2007 kwa kupunguza viwango vya mshahara badala ya kuvipandisha. Pia tangazo hilo linatajwa kufuta baadhi ya marupurupu kwa watumishi, kama likizo, usafiri na kodi ya nyumba.


Kwa mujibu wa Mgaya, kwa mfano, tangazo la Serikali namba 233 linataka mfanyakazi wa sekta ya viwanda na biashara alipwe kima cha chini cha Sh 150,000 wakati tangazo 172 limepunguza kiwango hadi Sh 80,000.
 
Kutisha ndicho kitu kikubwa serikali hii ya JK inachokijuwa badala ya hoja. Serikali hii imekaa kama vile ya kidikteta vile......haijui diplomacy wala ustahimilivu. Haijui mazungumzo ya kulenga upatikanaji wa mwafaka wala kujua imekaa vipi na wananchi wake. Kwake uwongo ndiyo imekuwa ibada!
 
wafanyakazi wanatakiwa kujua hakuna mwajiri duniani atayewaruhusu kugoma.
au kuwapa maslahi mazuri bila ya wao kudai haki yao kwa hiyo basi wachague moja
kati ya kudai mafao au wanyamaze waendelee na kazi kwani maneno maneno sasa
basi tufanye kazi kwani ni ulimwengu wa vitendo na si maneno matupu
 
Back
Top Bottom