Mgomo tishio kwa Kikwete

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
TUCTA sasa 'yaishika pabaya' Serikali
Yasema fedha zipo, zinaliwa na vigogo
Bilioni 113.4/- zalipa posho wakubwa tu
wa wafanyakazi nchini ambao unaelekea kuungwa mkono na sehemu kubwa ya vyama vya wafanyakazi nchini, umeelezwa kuwa tishio kubwa kwa Serikali ya Rais Jakaya Kikwete kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu kutokana na nguvu kubwa waliyonayo wafanyakazi walioenea sekta zote nchini zikiwamo za umma na binafsi, Raia Mwema limeelezwa.

Ofisa Mwandamizi wa Serikali aliyekaribu na vyombo vya dola, ameliambia Raia Mwema ya kuwa kwa sasa mgomo huo unaumiza vichwa vya watendaji wa vyombo vya dola kutokana na historia ya nguvu za wafanyakazi duniani hasa baada ya kudhihirika kwamba wengi wamekata tamaa ya maisha kutokana na kuzidi kupanuka kwa wigo wa mapato kati yao na wakubwa.

Tayari Rais Kikwete ameshitukia uzito wa mgomo huo akitumia sehemu ya hotuba yake ya mwisho wa mwezi uliopita kuwasihi wafanyakazi kutokugoma huku akigusia kuwa wafanyakazi wanaotakiwa kugoma baadhi ni wale wanaomzunguka serikalini na hata katika sekta ya huduma za umma.

Wafanyakazi hao wanapanga kugoma wakidai nyongeza stahili ya mshahara, punguzo la kodi na mafao bora, hoja ambazo Serikali imekuwa ikisema kwamba haiwezi kuzimudu kwa vile haina fedha.

Serikali yashikwa pabaya

Lakini pamoja na Serikali kusema haina fedha, utafiti mpya uliohusisha wachumi bingwa wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi nchini (TUCTA) unabainisha ya kuwa uchumi unamudu madai hayo, kama matumizi mabaya ya fedha miongoni mwa vigogo yatakomeshwa, ikifichuliwa kuwa, mwaka 2006/2007 pekee, Sh bilioni 113.4 ‘zilitafunwa’ kwa posho.

Kwa mujibu wa utafiti huo uliogharimiwa na TUCTA na unaotarajiwa kuwekwa hadharani kwa waandishi wa habari wakati wowote wiki hii, kama asilimia takriban 60 pekee ya kiwango hicho cha posho kingebanwa kila bajeti, ambayo ni takriban Sh bilioni 67.91, wafanyakazi, na hasa wa kima cha chini, wangekuwa na maisha nafuu.

Raia Mwema imefanikiwa kuona sehemu ya ripoti ya utafiti huo ambao dhahiri ni changamoto mpya kwa Serikali katika kutuliza wafanyakazi nchini kutokana na ukweli kwamba, ni utafiti unaoainisha vyanzo vya mapato na kiasi kinachopotea kutokana na kile kinachoweza kuelezwa kuwa ni uzembe wa Serikali kujipanga kukusanya kodi na kudhibiti matumizi yake ya anasa.

Sehemu ya matumizi ya anasa yanayoanishwa katika ripoti hiyo ni pamoja na matumizi ya magari ya kifahari, katika miji mikubwa yenye barabara za lami kama Dar es Salaam, ambako wakurugenzi na maofisa wengine wa wizara na idara za Serikali wanatumia magari aina ya Toyota Landcruiser VX, yanayotajwa kuwa na ghali na yana gharama kubwa za matunzo hali ambayo pia imewahi kulalamikiwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, akiishia kusitisha manunuzi ya magari hayo.

Kwa mujibu wa utafiti huo wa TUCTA imebainika kuwa takriban asilimia saba ya mapato ya ndani hutumika katika kulipana posho za semina za viongozi waandamizi wakiwamo mawaziri, naibu mawaziri, makatibu wakuu na wasaidizi wao.

Msimamo wa TUCTA kuhusu utafiti

Katibu Mkuu wa TUCTA, Nicholas Mgaya amethibitisha kuwapo kwa ripoti hiyo na akasisitiza kuwa wakati wowote wiki hii itatolewa kwa waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam.

“Ni kweli tumejiandaa vizuri katika kusindikiza hoja za madai yetu. Tumekuwa na timu ya wachumi waliobobea ambao wamechambua hali ya uchumi nchini, wameainisha vyanzo vya mapato lakini pia wameeleza namna Serikali inavyopoteza mapato yake bila sababu za msingi,” alisema Mgaya lakini akikataa kuzungumzia kilichomo kwenye ripoti hiyo yenye kurasa 37.

Hata hivyo, katika uchunguzi wake Raia Mwema imebaini kuwa kati ya mapendekezo yaliyomo kwenye ripoti hiyo ni pamoja na Serikali kutakiwa kupunguza matumizi yake ya anasa na sehemu ya fedha kupelekwa kwa wafanyakazi. Sehemu ya takwimu katika ripoti hiyo zinabainisha kuwa kwa mwaka 2005/2006, ni asilimia 21 tu ya mapato ya ndani ndiyo yametumika kulipa mishahara na asilimia saba ya mapato hayo ikitumika kulipa posho.

Ripoti hiyo pia inaeleza kuwa Serikali kwa sasa inakabiliwa na pengo la makusanyo ya mapato na sehemu ya sababu za kuwapo kwa hali hiyo ni wigo mdogo wa kodi na wakati huo huo makusanyo ya kidogo kinachopatikana yanatumika vibaya, sambamba na mianya mingi ya uvujaji mapato, hasa eneo la Bandari ya Dar es Salaam. Pamoja na makusanyo madogo serikali imekiri kupitia Hazina kutumia mara mbili ya makusanyo.

Alipoulizwa kuhusu maelezo hayo kuwamo kwenye ripoti hiyo, Mgaya ingawa hakutaka kuzungumza kwa undani lakini alisema haingii akilini Serikali kutokutoza kodi kwa mfanyabiashara mwenye mtaji wa milioni 19 kurudi chini lakini wakati huo mfanyakazi mwenye mshahara wa 500,000 au pungufu ya hapo akitozwa kodi kubwa.

“Serikali imeweka utaratibu mfanyabiashara anayepaswa kulipa kodi awe na biashara inayoanzia Sh milioni 20, pungufu ya hapo asitozwe kodi…haya hayaingii akilini,” alisema Mgaya na kuongeza kuwa “Tumebaini kuwa mchezo uliopo serikalini ni kwamba wanalipana posho zinazozidi viwango vya mshahara. Hizi posho hazitozwi kodi.”

Hoja nyingine zinazosindikiza mgomo wa wafanyakazi licha ya hiyo ya mishahara midogo ni kufutwa kwa mifuko mingi ya pensheni na kubakiza miwili au mmoja, ikielezwa kuwa kwa sasa mfuko wa PSPF unalipa fedha nyingi zaidi ya mifuko mingine ingawa viwango vya mshahara kati ya wafanyakazi walioingia kazini sawa, elimu sawa, vyeo sawa na kustaafu sawa vinatofautiana mmoja akilipwa Sh milioni 100 na mwingine milioni 16.

Aidha, katika ripoti hiyo nchi kadhaa za Scandinavia zinatajwa kama mifano katika harakati za kufikia kutoa maslahi bora kwa wafanyakazi kulingana na kiwango cha uchumi wa nchi hizo, lakini kwa upande mwingine Ugiriki ikionekana kama mfano wa nchi zilizoshindwa kukidhi maslahi ya wafanyakazi kutokana na kushindwa kukusanya kodi hasa kutoka kwa wafanyabiashara vigogo.

Ripoti hiyo inaanika udhaifu wa Serikali zilizotangulia baada ya ile ya Mwalimu Julius Nyerere inayotajwa wakati wote kuhakikisha katika kila nyongeza ya mshahara pengo kati ya mfanyakazi wa kima cha chini linapungua kwa kulinganisha na wafanyakazi wa kima cha juu. “Hali ni tofauti sasa, mfanyakazi wa chini anaweza kulipwa Sh 100,000 lakini bosi wake akilipwa Sh milioni mbili,” inasema taarifa hiyo.

Hata hivyo, wakati TUCTA ikiwa imejizatiti kuibana Serikali ili ijali maslahi ya wafanyakazi katika uwiano sahihi na uchumi wa Tanzania ambao kwa sasa inadaiwa unanufaisha kundi dogo la wanasiasa, wakiwamo wabunge ambao maslahi yao yameongezwa na idadi ya majimbo ya uchaguzi yakitarajiwa kuongezwa hali itakayozidisha gharama, tayari Chama Cha Waajiri Tanzania (ATE) wamepinga mgomo huo.

ATE ambao katika madai ya TUCTA nao ni sehemu ya waajiri wanaotuhumiwa kufinya maslahi ya wafanyakazi hasa wa kima cha chini, wamekutana na waandishi wa habari Aprili 5, wiki hii wakisema waajiri wanaweza kuwaadhibu wafanyakazi wao watakaogoma.

Katika hotuba yake katika kuwasihi wafanyakazi kutogoma, Rais Jakaya Kikwete alisema Serikali yake imekuwa ikikutana na viongozi wa wafanyakazi mara kwa mara kujadili masuala yao, kupitia kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na mawaziri, Juma Kapuya wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana na Hawa Ghasia ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma.

Hata hivyo, katika akizungumza na Raia Mwema ofisini kwake mwanzoni mwa wiki hii, Mgaya alisema walikutana rasmi Ikulu Mei 5, mwaka jana na kikao kilichofuata kilipaswa kufanyika Agosti, 2009, utaratibu ukiwa ni kila baada ya miezi mitatu lakini hakuna kikao chochote kilichofanyika katika mazingira na utaratibu huo rasmi.

“Waziri Kapuya na Hawa Ghasia walikuwapo katika kikao cha Ikulu, Mei 5, 2009 na ilikubalika kikao kingine kifanyike Agosti 2009, hakuna kilichofanyika. Mada kwa ajili ya kikao zilikwishakuwasilishwa kama inavyotakiwa kwenda kwa Waziri wa Kazi Kapuya, tumekuwa tukifuatilia majibu lakini muda wote huo Waziri amekuwa akisema yuko mbioni kutafuta mihadi (Ikulu).

“Mara ya mwisho tulikwenda kwake (Waziri Kapuya) kuulizia hiyo mihadi Desemba 2009, akatueleza ajenda (nyaraka za mada zilizowasilishwa kwake) hazioni na wakati huo tulikwishakutangaza notisi ya mgomo katika mkutano wetu mkuu wa kazi uliofanyika Arusha Oktoba 24 na 25, 2009,” alisema Mgaya akiongeza ya kuwa bado masuala yao ya msingi yamegawanyika katika maeneo matatu. Mosi, nyongeza ya mshahara; pili, kodi kubwa ya mishahara na tatu ni mafao duni.

Chanzo siasa mbovu, unyonyaji

Akizungumzia suala hilo, Mhadhiri wa Chuo Kikuu Dar es Salaam, Bashiru Ally alisema vyama vya wafanyakazi kwa mda mrefu vimedhoofika kiasi cha kutokuwa na nguvu ya kudai haki za wanachama wake hasa walioko serikalini na kwamba, udhaifu wa vyama hivyo umetokana na mabadiliko ya kiuchumi na kisiasa ambayo yamefinya wigo wa ajira za uhakika.

“Vyama vingi vina wanachama wachache sana na baadhi yake vimekumbwa na migogoro ya uongozi. Ingawa sheria mpya za kazi zimetungwa kuna kila dalili kwamba ama hazitekelezeki au shinikizo la vyama vya wafanyakazi ni dogo sana kiasi kwamba baadhi ya waajiri wanapata mwanya wa kuwanyonya wafanyakazi kinyume cha sheria. Lipo suala ambalo halizungumzwi sana nalo ni hili la kupishana sana kwa mishahara ya kima cha chini na kima cha juu.

“Hivi sasa kuna pengo kubwa katika viwango vya mishahara ya watumishi katika sekta zote ziwe za umma au binafsi. Mimi binafsi natishwa na namna ambavyo baadhi ya watumishi wanalipwa mishahara, marupurupu na pensheni kubwa wakati watumishi wengi wanaambulia malipo kidogo yasiokidhi mahitaji yao ya lazima. Hili ni tatizo la mfumo wa uchumi wetu ambao unawafukarisha wavuja jasho waliowengi na kuwanufaisha walajasho wachache.

“Tatizo hili haliwezi kumalizwa kwa mazungumzo baina ya vyama vya wafanyakazi na waajiri peke yao. Hili ni tatizo linalohitaji mjadala wa kitaifa juu ya hatima ya uchumi wetu. Mgogoro wa sasa baina ya vyama vya wafanyakazi na Serikali ni fursa nzuri kwa Watanzania kujiuliza ikiwa mfumo huu wa uchumi tunaoujenga ni muafaka na unakidhi haja na mahitaji yetu ya sasa na ya siku za usoni,” alisema Ally.

Aliweka bayana kuwa chanzo cha mgogoro huu ni udhaifu uliopo katika mfumo wa uchumi na siasa ambao msingi wake ni unyonyaji na si uzalishaji wenye tija.

“Hili si tatizo la wafanyakazi pekee, ni tatizo la kitaifa. Mazungumzo baina ya wafanyakazi na Serikali yanaweza kuwa na mafanikio ikiwa agenda ya mazungumzo hayo itaenda mbali zaidi ya nyongeza za mishahara. Yapo masuala kama vile uchumi huu tulionao ni wa kitaifa au si wa kitaifa, Je, kukua kwa tabaka la walionacho na wasionacho kunadhoofisha misingi ya utaifa na amani,” alihoji Ally.

Kauli hiyo ya msomi huyo inadhihirisha ukubwa wa tatizo na kwamba wafanyakazi watakaogoma wanaweza kuungwa mkono ama kusukumwa na familia zao na hata wanaharakati wengine wa haki za raia kutokana na ukataji tamaa kuenea katika sehemu kubwa ya wananchi huku kukiwa hakuna mwanga wala kundi linaloonekana kuwatetea.

“Tulikuwa tunategemea vyama vya upinzani na vyombo vya habari lakini vimeshashikwa na serikali na CCM (Chama cha Mapinduzi). Kwa sasa akitokea hata mwendawazimu anayeweza kutusaidia tutamuunga mkono,” anasema Ali Shaibuni wa Magomeni ambaye amesema kwa sasa hana ajira akiishi kwa kutegemea msaada wa ndugu na jamaa.
 
Back
Top Bottom